Jumatano, Septemba 3
Yosefu akaamka . . . na kufanya kama alivyoambiwa na malaika wa Yehova, akampeleka mke wake nyumbani.—Mt. 1:24.
Yosefu alikuwa tayari kufuata mwongozo wa Yehova, na hilo lilimfanya awe mume mzuri. Katika pindi tatu tofauti, alipata mwongozo kutoka kwa Yehova kuhusu familia yake. Kila mara, alitii bila kusita, hata ilipomaanisha kufanya mabadiliko makubwa. (Mt. 1:20; 2:13-15, 19-21) Kwa kufuata mwongozo wa Yehova, Yosefu alimlinda Maria, akamtegemeza, na kumwandalia mahitaji yake. Wazia jinsi matendo ya Yosefu yalivyomfanya Maria ampende na kumheshimu hata zaidi! Waume, mnaweza kumwiga Yosefu kwa kutafuta ushauri katika Biblia kuhusu jinsi ya kutunza familia zenu. Unapofuata ushauri huo, hata ikimaanisha kufanya mabadiliko fulani, unaonyesha kwamba unampenda mke wako na unaimarisha ndoa yenu. Dada mmoja nchini Vanuatu ambaye amefunga ndoa kwa zaidi ya miaka 20 anasema hivi: “Mume wangu anapotafuta na kufuata mwongozo wa Yehova, ninamheshimu hata zaidi. Ninajihisi salama, na nina uhakika katika maamuzi anayofanya.” w23.05 21 ¶5
Alhamisi, Septemba 4
Huko kutakuwa na barabara kuu, naam, njia inayoitwa Njia ya Utakatifu.—Isa. 35:8.
Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni walipaswa kuwa “watu watakatifu” kwa Mungu wao. (Kum. 7:6) Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba hawakuhitaji kufanya mabadiliko ili kumfurahisha Yehova. Wayahudi wengi waliozaliwa huko Babiloni walikuwa wameathiriwa na njia ya kufikiri na mazoea ya Wababiloni. Miaka mingi baada ya kikundi cha kwanza cha Wayahudi kurudi Israeli, Gavana Nehemia alishangaa alipotambua kwamba watoto ambao walikuwa wamezaliwa huko Israeli, hata hawakuwa wamejifunza lugha ya Kiyahudi. (Kum. 6:6, 7; Neh. 13:23, 24) Watoto hao wangewezaje kujifunza kumpenda na kumwabudu Yehova ikiwa hawangeweza kuelewa Kiebrania—lugha kuu ambayo ilitumiwa kuandika Neno la Mungu? (Ezra 10:3, 44) Basi, Wayahudi hao walihitaji kufanya mabadiliko makubwa, lakini ingekuwa rahisi zaidi kwao kufanya mabadiliko hayo wakiwa huko Israeli, ambako ibada safi ilikuwa inarudishwa hatua kwa hatua.—Neh. 8:8, 9. w23.05 15 ¶6-7
Ijumaa, Septemba 5
Yehova huwategemeza wote wanaoanguka na kuwainua juu wote walioinama chini.—Zab. 145:14.
Inasikitisha kwamba hata tuwe tumechochewa au tuna nidhamu kadiri gani, bado huenda tutakabili vipingamizi vinavyofanya iwe vigumu kufikia malengo yetu. Kwa mfano, “matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kuchukua muda tunaohitaji ili tufanyie kazi lengo letu. (Mhu. 9:11) Huenda tukakabili hali ngumu ambayo itatuacha tukiwa tumevunjika moyo na kuishiwa nguvu. (Met. 24:10) Kwa kuwa hatujakamilika, huenda tukafanya makosa ambayo yatafanya iwe vigumu kutimiza lengo letu. (Rom. 7:23) Au huenda tukahisi tu kwamba tumechoka. (Mt. 26:43) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda vipingamizi au hali ngumu? Kumbuka, kipingamizi hakimaanishi kwamba umeshindwa. Biblia inasema kwamba huenda tukakabili tena na tena matatizo au hali ngumu. Hata hivyo, pia inataja wazi kwamba tunaweza kusimama tena. Naam, ukisonga mbele licha ya vipingamizi, unamthibitishia Yehova kwamba unataka kumfurahisha. Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona ukijitahidi kutimiza lengo lako! w23.05 30 ¶14-15