Ijumaa, Septemba 5
Yehova huwategemeza wote wanaoanguka na kuwainua juu wote walioinama chini.—Zab. 145:14.
Inasikitisha kwamba hata tuwe tumechochewa au tuna nidhamu kadiri gani, bado huenda tutakabili vipingamizi vinavyofanya iwe vigumu kufikia malengo yetu. Kwa mfano, “matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kuchukua muda tunaohitaji ili tufanyie kazi lengo letu. (Mhu. 9:11) Huenda tukakabili hali ngumu ambayo itatuacha tukiwa tumevunjika moyo na kuishiwa nguvu. (Met. 24:10) Kwa kuwa hatujakamilika, huenda tukafanya makosa ambayo yatafanya iwe vigumu kutimiza lengo letu. (Rom. 7:23) Au huenda tukahisi tu kwamba tumechoka. (Mt. 26:43) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda vipingamizi au hali ngumu? Kumbuka, kipingamizi hakimaanishi kwamba umeshindwa. Biblia inasema kwamba huenda tukakabili tena na tena matatizo au hali ngumu. Hata hivyo, pia inataja wazi kwamba tunaweza kusimama tena. Naam, ukisonga mbele licha ya vipingamizi, unamthibitishia Yehova kwamba unataka kumfurahisha. Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona ukijitahidi kutimiza lengo lako! w23.05 30 ¶14-15
Jumamosi, Septemba 6
[Iweni] vielelezo kwa kundi.—1 Pet. 5:3.
Upainia unamsaidia mwanamume kijana kujifunza jinsi ya kufanya kazi vizuri pamoja na watu mbalimbali. Pia, unamsaidia kupanga bajeti vizuri na kushikamana nayo. (Flp. 4:11-13) Njia nzuri ya kuanza utumishi wa wakati wote ni kufanya upainia msaidizi, jambo ambalo litakusaidia kuwa tayari kuanza upainia wa kawaida. Upainia unaweza kufungua mlango unaoongoza kwenye aina nyingine za utumishi wa wakati wote, kutia ndani kutumikia ukiwa mjenzi au Mwanabetheli. Wanaume Wakristo wanapaswa kuwa na lengo la kustahili kuwatumikia ndugu na dada zao wakiwa wazee wa kutaniko. Biblia inasema kwamba wanaume wanaojitahidi kufikia jukumu hilo ‘wanatamani kazi njema.’ (1 Tim. 3:1) Kwanza, ni lazima ndugu astahili kutumikia akiwa mtumishi wa huduma. Watumishi wa huduma wanawasaidia wazee kwa njia nyingi hususa. Wazee na watumishi wa huduma wanawatumikia kwa unyenyekevu ndugu na dada zao na kushiriki kwa bidii katika huduma. w23.12 28 ¶14-16
Jumapili, Septemba 7
Alipokuwa angali mvulana, alianza kumtafuta Mungu wa Daudi babu yake.—2 Nya. 34:3.
Mfalme Yosia alikuwa tineja alipoanza kumtafuta Yehova. Alitaka kujifunza kumhusu Yehova na kufanya mapenzi Yake. Hata hivyo, maisha hayakuwa rahisi kwa mfalme huyo kijana. Alihitaji kuchukua msimamo upande wa ibada safi wakati ambapo ibada ya uwongo ilikuwa imeenea. Na kwa kweli, alifanya hivyo! Kabla Yosia hajafikisha umri wa miaka 20, alianza kuondoa ibada ya uwongo katika taifa hilo. (2 Nya. 34:1, 2) Hata ikiwa wewe ni kijana, unaweza kuamua kumwiga Yosia kwa kumtafuta Yehova na kujifunza kuthamini sifa Zake. Ukifanya hivyo, utachochewa kujiweka wakfu kwake. Kujiweka wakfu kutaathirije maisha yako ya kila siku? Luke, ambaye alibatizwa akiwa na umri wa miaka 14, anasema hivi: “Kuanzia sasa na kuendelea, nitatanguliza kumtumikia Yehova maishani mwangu na nitajitahidi kumfurahisha.” (Marko 12:30) Wewe pia utapata baraka ikiwa unatamani kufanya hivyo! w23.09 11 ¶12-13