MAONI YA BIBLIA
Feza
Feza ndizo zinaleta mambo yote mabaya?
“Kupenda [feza] ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote.”—1 Timotheo 6:10.
MAMBO WATU FULANI WANASEMA:
Feza ndizo zinaleta mambo yote mabaya.
MAMBO BIBLIA INASEMA:
Ni “kupenda [feza]” ndiko kunaleta “mambo mabaya,” wala si feza zenyewe. Katika Biblia, Mufalme Sulemani aliyekuwa tajiri sana, alionyesha mambo tatu mabaya yanayopata watu wanaopenda feza. Jambo la 1, woga: ‘Wingi alio nao tajiri haumuruhusu kulala.’ (Mhubiri 5:12) Jambo la 2, kukosa kutosheka: ‘Anayependa feza hatatosheka na feza, wala anayependa mali hatatosheka na mapato.’ (Mhubiri 5:10) Jambo la 3, kishawishi cha kuvunja sheria: “Yeye anayefanya haraka kupata utajiri hatabaki pasipo hatia.”—Methali 28:20.
Feza zinasaidia watu namna gani?
“[Feza] ni ulinzi.”—Mhubiri 7:12.
MAMBO WATU FULANI WANASEMA:
Feza zinamufanya mutu kuwa salama na zinamuletea furaha.
MAMBO BIBLIA INASEMA:
Wazo la kwamba feza zinanunua furaha na usalama ni sehemu ya “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Hata hivyo, ‘[feza] zinatokeza jibu katika mambo yote.’ (Mhubiri 10:19) Kwa mufano, feza zinaweza kununua vitu ambavyo mutu anahitaji ili aendelee kuishi, vitu kama vile chakula na dawa.—2 Wathesalonike 3:12.
Feza zinamusaidia pia mutu kutunza familia yake. Kwa kweli, Biblia inasema hivi: ‘Ikiwa yeyote hawaandalie mahitaji wale walio wake mwenyewe, na hasa wale walio washiriki wa nyumba yake, ameikana imani.’—1 Timotheo 5:8.
Namna gani unaweza kutumia feza kwa hekima?
‘Uketi kwanza na uhesabu garama.’—Luka 14:28.
MAMBO BIBLIA INASEMA:
Utumie feza kwa njia ambayo Mungu anakubali. (Luka 16:9) Ni jambo la hekima kutumia feza vizuri na kwa njia ya haki. (Waebrania 13:18) Ili kuepuka muzigo wa kutumia feza nyingi zaidi ya zile unazopata, ufanye ‘namna yako ya maisha iwe bila upendo wa [feza].’—Waebrania 13:5.
Hata ikiwa Biblia haikataze kuomba deni, inaonya hivi: ‘Mukopaji ni mutumishi wa mutu anayemukopesha.’ (Methali 22:7) Epuka kununua vitu bila mupango, kwa sababu ‘kila mutu anayetenda haraka-haraka bila shaka anaelekea uhitaji.’ (Methali 21:5) Lakini, ‘weka kando kitu fulani katika akiba kulingana na unavyofanikiwa,’ na uweke feza juu ya mambo yaliyo ya maana kwako.—1 Wakorintho 16:2.
Biblia inatutia moyo ‘tuwe na mazoea ya kuwapa watu.’ (Luka 6:38) Watu wanaotaka kumupendeza Mungu wana sababu nzuri ya kuwa wakarimu, kwa kuwa ‘Mungu anamupenda mutoaji muchangamufu.’ (2 Wakorintho 9:7) Kwa hiyo, ‘musisahau kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine, kwa maana Mungu anapendezwa vema na zabihu za namna hiyo.’—Waebrania 13:16.