Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • es25 uku. 57-67
  • Mwezi wa 6

Hakuna video juu ya habari yenye umechagua.

Pole, kulikuwa kosa fulani wakati video ilikuwa inajaribu kusoma.

  • Mwezi wa 6
  • Tuchunguze Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa Vidogo
  • Siku ya Yenga, 1 Mwezi wa 6
  • Siku ya Kwanza, 2 Mwezi wa 6
  • Siku ya Pili, 3 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tatu, 4 Mwezi wa 6
  • Siku ya Ine, 5 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tano, 6 Mwezi wa 6
  • Siku ya Posho, 7 Mwezi wa 6
  • Siku ya Yenga, 8 Mwezi wa 6
  • Siku ya Kwanza, 9 Mwezi wa 6
  • Siku ya Pili, 10 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tatu, 11 Mwezi wa 6
  • Siku ya Ine, 12 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tano, 13 Mwezi wa 6
  • Siku ya Posho, 14 Mwezi wa 6
  • Siku ya Yenga, 15 Mwezi wa 6
  • Siku ya Kwanza, 16 Mwezi wa 6
  • Siku ya Pili, 17 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tatu, 18 Mwezi wa 6
  • Siku ya Ine, 19 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tano, 20 Mwezi wa 6
  • Siku ya Posho, 21 Mwezi wa 6
  • Siku ya Yenga, 22 Mwezi wa 6
  • Siku ya Kwanza, 23 Mwezi wa 6
  • Siku ya Pili, 24 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tatu, 25 Mwezi wa 6
  • Siku ya Ine, 26 Mwezi wa 6
  • Siku ya Tano, 27 Mwezi wa 6
  • Siku ya Posho, 28 Mwezi wa 6
  • Siku ya Yenga, 29 Mwezi wa 6
  • Siku ya Kwanza, 30 Mwezi wa 6
Tuchunguze Maandiko Kila Siku—2025
es25 uku. 57-67

Mwezi wa 6

Siku ya Yenga, 1 Mwezi wa 6

Lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia taabu nyingi.​—Mdo. 14:22.

Yehova alibariki Wakristo wa karne ya kwanza juu walijipatanisha na hali. Waliteswa mara mingi, wakati fulani, pengine ile iliwafikia bila kutazamia. Fikiria mambo yenye ilifikia Barnaba na mutume Paulo wakati walikuwa nahubiri mu eneo ya Lystra. Ku mwanzo, wale wenye waliwasikiliza waliwakaribisha kwa uchangamufu. Kisha, watu wenye kuwapinga “wakashawishi watu wengi,” na wamoja kati ya walewale watu wakamupiga Paulo majiwe na kumuacha inje kwa kuwaza kama anakufa. (Mdo. 14:19) Lakini, Barnaba na Paulo waliendelea kuhubiri fasi ingine. Walipata matokeo gani? Walifanya “watu wengi kuwa wanafunzi.” Tena, maneno na mufano wao ilitia nguvu waamini wenzao. (Mdo. 14:21, 22) Watu wengi walipata faida juu Barnaba na Paulo hawakuacha kuhubiri hata kama walipata mateso bila kutazamia. Na siye, Yehova atatubariki kama hatuache kumutumikia. w23.04 16-17 fu. 13-14

Siku ya Kwanza, 2 Mwezi wa 6

Ee Yehova, sikiliza sala yangu; na usikilize vilio vyangu vya kuomba musaada. Ninakuitia katika siku ya taabu yangu, kwa maana utanijibu.​—Zb. 86:6, 7.

Mufalme Daudi alikuwa na maadui wengi hatari mu maisha yake, na kila mara alikuwa namuo-mba Yehova musaada. Daudi alikuwa hakika kama Yehova alisikia na kujibia sala zake. Na weye ukuwe hakika kama Yehova atafanya vile. Biblia inatuhakikishia kama Yehova anaweza kutupatia hekima na nguvu yenye tuko nayo lazima ili kuvumilia. Anaweza kutumia ndugu na dada zetu ao hata wale wenye hawamuabudu kwa sasa ili kutusaidia mu njia fulani. Pengine Yehova hatajibia sala zetu mu njia yenye tunatazamia, hata vile tunajua kama atazijibia. Atatupatia mambo yenye tuko nayo lazima kabisa wakati wenye tuko nayo lazima. Kwa hiyo, uendelee kusali na kuamini kama Yehova atakusikia, ukuwe hakika kama atakuhangaikia sasa, na kama “atatimiza tamaa ya kila kitu chenye uzima” mu dunia mupya.​—Zb. 145:16. w23.05 8 fu. 4; 13 fu. 17-18

Siku ya Pili, 3 Mwezi wa 6

Nitamulipa Yehova nini kwa mema yote yenye amenitendea?​—Zb. 116:12.

Ni muzuri kukaza akili juu ya baraka zenye utapata wakati unafikia muradi fulani. Unapaswa kukaza akili juu ya baraka gani? Kama muradi wako ni wa kusoma Biblia ao kusali, fikiria namna ile inaweza kufanya urafiki wako na Yehova ukuwe nguvu zaidi. (Zb. 145:18, 19) Kama muradi wako ni wa kukomalisha sifa fulani ya kiroho, kaza akili juu ya namna ile itafanya uhusiano wako na wengine ukuwe muzuri zaidi. (Kol. 3:14) Unawaza nini kama unafanya liste ya sababu zenye zinafanya upende kufikia muradi wako? Kila mara ukuwe nachunguza ile liste. Tena, upitishe wakati pamoya na wale wenye watakuchochea kufikia muradi wako. (Mez. 13:20) Lakini, kusema kweli, wakati fulani inawezekana tusikuwe na hamu ya kufikia muradi wetu. Ile inamaanisha kama hatupaswe kuendelea kujikaza? Hapana. Tunaweza pia kujikaza kufikia muradi wetu hata kama hatuna hamu ya kufanya vile. Kusema kweli, haiko mwepesi; lakini kama tunaufikia, tutakuwa na furaha. w23.05 27-28 fu. 5-8

Siku ya Tatu, 4 Mwezi wa 6

Kitu chochote chenye mutu anapanda, ni kile atavuna pia.​—Gal. 6:7.

Kujua kama tunapaswa kukubali matokeo ya maamuzi yetu, kunaweza kutuchochea tutubu zambi zetu, kurekebisha makosa yetu, na kuepuka kuirudilia. Kama tunafanya vile, tunaweza kuendelea mu mbio ya uzima. Kama hauwezi kubadilisha uamuzi wa mubaya wenye ulikamataka, ukubali matokeo yake. Usipoteze wakati na nguvu yako bure kwa kutafuta kuonyesha kama haukukosea ao kwa kulaumu wengine. Kuliko kufanya vile, ukubali makosa yako na ujikaze sasa kufanya mambo ya muzuri. Kama uko najihukumu juu ya jambo fulani ya mubaya yenye ulifanyaka, usali Yehova kwa unyenyekevu, ukubali kosa yako, na umuombe akusamehe. (Zb. 25:11; 51:3, 4) Uombe musamaha kwa wale wenye ulikoseaka na kama ni lazima utafute musaada kwa wazee. (Yak. 5:14, 15) Ujifunze kupitia makosa yako na ufanye yako yote juu usiirudilie tena. Kama unafanya vile, unaweza kuwa hakika kama Yehova atakuonyesha rehema yake na atakutegemeza.​—Zb. 103:8-13. w23.08 28-29 fu. 8-9

Siku ya Ine, 5 Mwezi wa 6

Yehoashi aliendelea kufanya mambo yenye yalikuwa sawa mbele ya macho ya Yehova siku zote zenye Yehoyada kuhani alimufundisha.​—2 Fa. 12:2.

Yehoyada alimusaidia Mufalme Yehoashi kuwa mutu muzuri. Ile ilifanya kijana Yehoashi apende kumufurahisha Yehova. Lakini kisha kifo ya Yehoyada, Yehoashi alianza kusikiliza wakubwa wenye walikuwa waasi-imani. (2 Ny. 24:4, 17, 18) Hata kama Yehova alikasirika sana juu ya ile, “aliendelea kutuma manabii kati yao ili kuwarudisha . . . , lakini walikataa kusikiliza.” Hawakumusikiliza hata Zekaria, mutoto wa Yehoyada, mwenye alikuwa nabii wa Yehova na kuhani, lakini pia binamu (cousin) wa Yehoashi. Jambo ya kuhuzunisha, Mufalme Yehoashi alimuua Zekaria. (2 Ny. 22:11; 24:19-22) Yehoashi hakuendelea kumuogopa Yehova mu njia yenye kufaa. Yehova alisemaka hivi: “Wale wenye kunizarau watazarauliwa.” (1 Sa. 2:30) Kisha, jeshi kidogo ya Siria ilishambulia “jeshi kubwa sana” ya Yehoashi na “kumuumiza sana.” (2 Ny. 24:24, 25) watumishi wa Yehoashi walimuua juu naye aliuaka Zekaria. w23.06 18-19 fu. 16-17

Siku ya Tano, 6 Mwezi wa 6

Wakati fulani mulikuwa giza, lakini sasa ninyi ni mwangaza.​—Efe. 5:8.

Mutume Paulo alipitisha wakati fulani Efeso, alikuwa anahubiri na kufundisha kuhusu habari njema. (Mdo. 19:1, 8-10; 20:20, 21) Alipenda ndugu zake sana na alipenda kuwasaidia wabakie waaminifu kwa Yehova. Waefeso wenye Paulo alizungumuzia walikuwa wakati fulani watumwa wa dini ya uongo na waliamini mambo ya uchawi. Watu wa Efeso walikuwa na mwenendo muchafu sana na wa bila haya. Walisema maneno machafu mu majumba yao ya maonyesho na hata mu sherehe zao za kidini. (Efe. 5:3) Watu wengi wenye walikuwa wanaishi Efeso walikuwa ‘wameishiwa na ufahamu wote wa mambo yenye kuwa sawa.’ Ile maneno inamaanisha neno kwa neno “hawakukuwa wanasikia tena maumivu.” (Efe. 4:17-19) Mbele ya kujua mambo yenye kuwa ya muzuri na yenye kuwa makosa, Waefeso hawakusumbuliwa na zamiri. Njo maana Paulo alisema kama walikuwa “katika giza kiakili, na wametenganishwa na uzima wenye kuwa wa Mungu.” Lakini, Waefeso fulani hawakubakia mu giza. w24.03 20 fu. 2, 4; 21 fu. 5-6

Siku ya Posho, 7 Mwezi wa 6

Wale wenye kumutumainia Yehova watapata nguvu tena . . . hawatachoka.​—Isa. 40:31.

Juu Gideoni alikuwa muamuzi, iliomba atumike sana. Wakati Wamidiani walikimbia kutoka ku vita katikati ya usiku, Gideoni aliwafuatilia kuanzia mu bonde ya Yezreeli mupaka ku Muto Yordani. (Amu. 7:22) Gideoni aliishia tu pale ku Muto Yordani? Hapana! Hata kama yeye na wanaume 300 wenye alikuwa nao walikuwa walishachoka, waliendelea tu kuwafuatilia. Ku mwisho, waliwakuta na kuwashinda. (Amu. 8:4-12) Gideoni alikuwa hakika kama Yehova atamupatia nguvu, na hakuvunjika moyo. (Amu. 6:14, 34) Wakati fulani, Gideoni na jeshi yake walifuatilia kwa muguu wafalme wawili Wamidiani wenye pengine walikuwa ku ngamia wao. (Amu. 8:12, 21) Hata vile, Mungu alisaidia Waisraeli wawakamate na kuwashinda. Wazee pia wanaweza kumutegemea Yehova, mwenye “hachokake wala kuishiwa nguvu.” Atawapatia nguvu wakati wako nayo lazima.​—Isa. 40:28, 29. w23.06 6 fu. 14, 16

Siku ya Yenga, 8 Mwezi wa 6

[Yehova] hatakutupa wala kukuacha.​—Kum. 31:6.

Hata ikiwa tunapambana na majaribu ya namna gani, tunaweza kuwa na moyo wenye kuwa imara. Kwa hiyo tumutegemee Yehova. Ona namna Baraka alipata ushindi juu alitegemea muongozo wa Yehova. Hata kama Waisraeli hawakukuwa na ngao wala mukuki, Yehova alimuambia Baraka aende kupigana na Sisera, mwenye alikuwa mukubwa wa jeshi ya Wakanaani, na jeshi yake, wenye walikuwa na silaha mingi kwa ajili ya vita. (Amu. 5:8) Nabii mwanamuke Debora alimupatia Baraka muongozo wa kuenda mu bonde ili kupigana na Sisera na jeshi yake yenye ilikuwa na magari ya vita 900. Mu ile bonde, ingekuwa nguvu kwa Waisraeli kupigana na ile jeshi juu ile magari ya vita ilikuwa nakimbia sana. Hata kama Baraka alijua vile, alitii. Wakati maaskari walikuwa nashuka Mulima Tabori, Yehova alinyeshesha mvula kubwa sana. Magari ya Sisera ilianza kuzama mu matope na Yehova alimupatia Baraka ushindi. (Amu. 4:1-7, 10, 13-16) Vilevile, Yehova atatupatia ushindi kama tunamutegemea na kama tunategemea muongozo wenye anatupatia kupitia wale wenye kumuwakilisha. w23.07 19 fu. 17-18

Siku ya Kwanza, 9 Mwezi wa 6

Ule mwenye atavumilia mupaka mwisho ataokolewa.​—Mt. 24:13.

Kama tuko na uvumilivu, tutaokolewa. Sawa vile watumishi waaminifu wa zamani, tunapaswa kungoya kwa uvumilivu Mungu atimize ahadi zake. (Ebr. 6:11, 12) Biblia inalinganisha hali yetu na hali ya mulimaji. (Yak. 5:7, 8) Mulimaji anatumikaka sana juu ya kupanda mbegu na kuimwangia maji, lakini hajuake kabisa ni wakati gani itaota. Kwa hiyo, anangoyaka kwa uvumilivu na anakuwaka hakika kama ile mbegu itaota. Vilevile, na siye tunafanyaka kazi ya kiroho kwa bidii, hata kama “hatujue Bwana [wetu] atakuja siku gani.” (Mt. 24:42) Tunangoyaka kwa uvumilivu na tunakuwaka hakika kama kwa wakati wenye kufaa Yehova atatimiza ahadi zake zote. Kama hatufanye vile, tunaweza kuchoka kungoya na kuacha kweli pole kwa pole. Tunaweza hata kuanza kutafuta vitu vyenye tunaweza kuwaza kama vitafanya tukuwe na furaha palepale. Lakini kama tuko na uvumilivu, tunaweza kuvumilia mupaka mwisho na kuokolewa.​—Mik. 7:7. w23.08 22 fu. 7

Siku ya Pili, 10 Mwezi wa 6

Vidole vya miguu vilikuwa sehemu moja chuma na sehemu ingine udongo.​—Da. 2:42.

Kwa kulinganisha unabii wenye kuwa mu Danieli 2:41-43 na maunabii ingine yenye kuwa mu kitabu ya Danieli na Ufunuo, tunaelewa kama vile vikanyangio vinafananisha Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika yenye iko na nguvu sana na yenye iko natawala ulimwengu leo. Danieli alisema hivi kuhusu ile serikali: “Ufalme huo utakuwa wenye nguvu sehemu moja na zaifu sehemu ile ingine.” Juu ya nini sehemu moya iko zaifu? Ni juu watu wa kawaida wenye kufananishwa na udongo wa teketeke wanafanya uwezo wake wa kutenda kwa nguvu sawa vile chuma ukuwe zaifu. Tunajifunza kweli fulani za maana kupitia ndoto ya sanamu kubwa yenye Danieli alifasiria. Siku ya Kwanza, Serikali Kubwa ya Ulimwengu ya Uingereza na Amerika ilionyesha kama iko na nguvu mu njia mbalimbali. Kwa mufano, ilikuwa kati ya mataifa yenye ilipata ushindi mu Vita ya Siku ya Kwanza ya Ulimwengu na Vita ya Pili ya Ulimwengu. Hata vile, ile serikali iko zaifu na itaendelea kufanywa kuwa zaifu na raia wake wenye hawaelewane kati yao. Pili, ile serikali njo itakuwa ya mwisho kutawala wanadamu mbele Ufalme wa Mungu ukuye kutosha serikali zote za wanadamu. w23.08 10-11 fu. 12-13

Siku ya Tatu, 11 Mwezi wa 6

Katika taabu yangu nilimuitia Yehova, niliendelea kumulilia Mungu wangu anisaidie. Akiwa katika hekalu lake akasikia sauti yangu.​—Zb. 18:6.

Wakati fulani, Daudi alihuzunika kwa sababu ya majaribu na magumu yenye alikuwa napambana nayo. (Zb. 18:4, 5 ) Lakini, kwa sababu Yehova alimuonyesha upendo mwingi na kumuhangaikia, Daudi aliburudishwa ao alijisikia muzuri. Yehova aliongoza rafiki yake Daudi kwenye “malisho yenye majani mengi” na kwenye “nafasi za kupumuzikia zenye maji mengi.” Matokeo ilikuwa nini? Daudi alipata tena nguvu, na aliweza kuendelea kumutumikia Yehova. (Zb. 18:28-32; 23:2) Leo pia, “ni kwa sababu ya upendo mushikamanifu wa Yehova ndiyo maana hatuishe” wakati tunapambana na majaribu na magumu mu maisha yetu. (Omb. 3:22; Kol. 1:11) Uzima wa Daudi ulikuwa mu hatari mara mingi, na alikuwa na maadui wengi wenye nguvu. Lakini upendo wa Yehova ulimufanya ajisikie kuwa salama na mwenye kulindwa. Daudi alijisikia sawa vile Yehova alikuwa naye mu kila hali, na alikuwa anamutia moyo. Ndiyo sababu aliimba hivi: “[Yehova] aliniokoa katika mambo yote yenye kuniogopesha.” (Zb. 34:4) Ni kweli kwamba Daudi aliogopa, lakini upendo wa Yehova ulikuwa nguvu zaidi kupita woga wake. w24.01 30 fu. 15-17

Siku ya Ine, 12 Mwezi wa 6

Kama watenda-zambi wanajaribu kukushawishi, usikubali.​—Mez. 1:10.

Maamuzi ya mubaya ya Yehoashi ikufundishe. Kisha Kuhani Mukubwa Yehoyada kufa, Yehoashi alichagua marafiki wabaya. (2 Ny. 24:17, 18) Aliamua kusikiliza wakubwa wa Yuda wenye hawakumupenda Yehova. Hauone kama Yehoashi alipaswa kuepuka marafiki wa vile? (Mez. 1:10) Kuliko kufanya vile, aliwasikiliza. Na hata, wakati binamu yake Zekaria alijaribu kumurekebisha, Yehoashi aliamuru auawe. (2 Ny. 24:20, 21; Mt. 23:35) Ile ilikuwa tendo ya mubaya sana na ya upumbavu! Yehoashi alianza maisha yake muzuri. Lakini jambo ya kuhuzunisha ni kwamba, alifikia kuwa muuaji na muasi-imani. Ku mwisho, watumishi wake mwenyewe walimuua. (2 Ny. 24:22-25) Bila shaka, maisha yake ingekuwa tofauti kabisa kama angeendelea kumusikiliza Yehova na wale wenye kumupenda Yehova. w23.09 9 fu. 6

Siku ya Tano, 13 Mwezi wa 6

Acha kuogopa.​—Lu. 5:10.

Yesu alijua kama mutume Petro angeweza kubakia muaminifu. Kwa hiyo, Yesu alimuambia hivi kwa upendo: “Acha kuogopa.” Juu Yesu alimutumainia Petro, ile ilikuwa na matokeo makubwa sana mu maisha ya Petro. Kisha wakati fulani Petro na ndugu yake Andrea waliacha kazi yao ya kuvua samaki na wakakuwa wafuasi wa wakati wote wa Yesu. Ule uamuzi uliwaletea baraka mingi. (Mk. 1:16-18) Petro alijionea mambo mingi ya ajabu juu alikuwa mufuasi wa Yesu. Aliona vile Yesu aliponyesha wagonjwa, namna alifukuza pepo wachafu, na hata kufufua wafu. (Mt. 8:14-17; Mk. 5:37, 41, 42) Petro aliona pia katika maono utukufu wa Yesu mu Ufalme wake wa wakati wenye kuya, na aliendelea kukumbuka ile maono maisha yake yote. (Mk. 9:1-8; 2 Pe. 1:16-18) Kwa kweli, Petro aliona mambo yenye hangewaziaka. Bila shaka Petro alifurahi sana juu hakuruhusu ile mawazo ya kujiona kuwa hastahili imufanye akose zile baraka zote! w23.09 21 fu. 4-5

Siku ya Posho, 14 Mwezi wa 6

Yesu akamuambia: “Ninakuambia, hapana mupaka mara saba (7), lakini mupaka mara makumi saba na saba (77).”​—Mt. 18:22.

Mu barua yake ya kwanza, mutume Petro alitumia maneno “upendo mwingi.” Upendo wa vile unafunika, hapana tu makosa kidogo, lakini “zambi nyingi.” (1 Pe. 4:8) Pengine Petro alikumbuka mambo yenye Yesu alimufundisha kuhusu kusamehe miaka mingi mbele ya pale. Wakati fulani Petro aliwaza kama alikuwa mutu muzuri sana wakati alisema kama anaweza kusamehe ndugu yake “mupaka mara saba (7).” Lakini Yesu alimufundisha yeye, lakini pia siye, kusamehe “mupaka mara makumi saba na saba (77),” ni kusema bila mipaka. (Mt. 18:21) Kama unaona ni nguvu kutumikisha ile mashauri, usivunjike moyo! Wakati fulani inakuwaka nguvu kwa watumishi wote wa Yehova wenye hawakamilike kusamehe. Jambo ya maana ya kufanya sasa ni kukamata hatua ya kusamehe ndugu yako na kufanya amani pamoya naye. w23.09 29 fu. 12

Siku ya Yenga, 15 Mwezi wa 6

Nilimuita Yehova, naye akanijibu.​—Yon. 2:2.

Wakati alikuwa katika tumbo la samaki, Yona alikuwa hakika kama Yehova atasikiliza sala yake ya kutubu yenye alitoa kwa unyenyekevu, na kama Yehova angemusaidia. Kisha Yona alirudishwa ku inchi kavu na alikuwa tayari kukubali na kutimiza mugao wenye Yehova alimupatia (Yon. 2:10–3:4) Wakati wa magumu unahangaikaka sana mupaka unashindwa kusali waziwazi? Ao unajisikiaka kama hauna nguvu ya kujifunza? Kumbuka kama Yehova anaelewa muzuri sana hali yako. Kwa hiyo, hata wakati unasali kwa kutumia maneno kidogo, unaweza kuwa hakika kama atakupatia mambo yenye uko nayo lazima. (Efe. 3:20) Kama maumivu ya kimwili ao ya kihisia inafanya ikuwe nguvu kwako kusoma na kujifunza, unaweza kusikiliza Biblia yenye kurekodiwa ao vichapo vyenye kutegemea Biblia vyenye kurekodiwa. Kusikiliza nyimbo zetu ao kuangalia video ku jw.org, kunaweza pia kukusaidia. Wakati unasali kwa Yehova na unatumia mambo ya kiroho yenye anatutolea, unamupatia nafasi ya kukutia nguvu. w23.10 13 fu. 6; 14 fu. 9

Siku ya Kwanza, 16 Mwezi wa 6

Roho takatifu inafanya ikuwe wazi kwamba njia ya kuingia mahali patakatifu ilikuwa haijafunuliwa wakati ile hema ya zamani ilikuwa yenye kusimama.​—Ebr. 9:8.

Sehemu fulani zenye zilikuwa mu tabenakulo zilikuwa nafanana na sehemu fulani zenye zilikuwa mu hekalu yenye ilifikia kujengwa Yerusalemu. Ndani mulikuwa vyumba viwili, ni kusema, “Patakatifu” na “Patakatifu Zaidi,” vyenye vilitenganishwa na pazia. (Ebr. 9:2-5; Kut. 26:31-33) Ndani ya Patakatifu mulikuwa kinara cha taa cha zahabu, mazabahu ya kuchomea uvumba, na meza ya mikate ya wonyesho. “Makuhani wenye kutiwa mafuta” tu njo waliruhusiwa kuingia ndani ya Patakatifu ili kutimiza utumishi mutakatifu. (Hes. 3:3, 7, 10) Ndani ya Patakatifu Zaidi mulikuwa sanduku la agano la zahabu lenye lilifananisha kuwapo kwa Yehova. (Kut. 25:21, 22) Ni kuhani mukubwa tu njo mwenye aliruhusiwa kupita pazia na kuingia Patakatifu Zaidi mara moya ku mwaka, Siku ya Kufunika Zambi. (Law. 16:2, 17) Aliingia Patakatifu Zaidi ili kutoa damu ya wanyama juu zambi zake na zambi za taifa yote zifunikwe. Kisha wakati Yehova alionyesha wazi maana ya zile sehemu za tabenakulo.​—Ebr. 9:6, 7. w23.10 27 fu. 12

Siku ya Pili, 17 Mwezi wa 6

Mupendane.​—Yoh. 15:17.

Mu Neno ya Mungu tunapata tena na tena amri ya “kupendana.” (Yoh. 15:12; Ro. 13:8; 1 Te. 4:9; 1 Pe. 1:22; 1 Yo. 4:11) Lakini upendo ni sifa ya moyo ao sifa ya ndani, na hakuna mwanadamu mwenye anaweza kuona mambo yenye kuwa mu moyo wetu. Kwa hiyo, namna gani upendo wetu kwa wengine unaweza kuonekana? Kupitia maneno na matendo. Tunaweza kuonyesha ndugu na dada zetu upendo mu njia mbalimbali. Hapa kuko mifano fulani: “Museme kweli mumoja na mwingine.” (Zek. 8:16) “Muendelee kuwa na amani mumoja na mwingine.” (Mk. 9:50) Mukuwe wa Siku ya Kwanza “katika kuonyeshana heshima.” (Ro. 12:10) “Mukaribishane.” (Ro. 15:7) “Muendelee . . . kusameheana.” (Kol. 3:13) “Muendelee kubebeana mizigo mizito.” (Gal. 6:2) “Muendelee kufarijiana.” (1 Te. 4:18) “Muendelee . . . Kujengana.” (1 Te. 5:11) ‘Musali kwa ajili ya mutu na mwenzake.’​—Yak. 5:16. w23.11 9 fu. 7-8

Siku ya Tatu, 18 Mwezi wa 6

Mufurahi katika tumaini.​—Ro. 12:12.

Kila siku, tunakamataka maamuzi yenye inaomba imani ya nguvu. Kwa mufano, tunakamataka maamuzi kuhusu marafiki, mambo ya kujifurahisha, masomo, ndoa, watoto, na kazi ya kimwili. Ni muzuri tujiulize hii maulizo: ‘Mambo yenye nachagua kufanya, inaonyesha kabisa kama niko hakika kuwa hii dunia ni ya muda tu na kama hivi karibuni Mungu ataleta dunia mupya? Ao nachagua kufanya mambo sawa vile wale wenye hawaamini kama wanaweza kuishi milele?’ (Mt. 6:19, 20; Lu. 12:16-21) Ikiwa tunaamini kama dunia mupya iko karibu, tutakamata maamuzi ya muzuri sana.Tunapataka pia magumu fulani yenye inaomba imani ya nguvu. Inaweza kuwa mateso, magonjwa yenye inafanya miaka mingi, ao mambo ingine yenye inaweza kutuvunja moyo. Ku mwanzo, unaweza kujisikia sawa vile unaweza kuvumilia ile magumu. Lakini mara mingi magumu ya vile inakamataka wakati murefu. Njo maana, inaomba tukuwe na imani ya nguvu ili kuvumilia na kuendelea kumutumikia Yehova kwa furaha.​—1 Pe. 1:6, 7. w23.04 27 fu. 4-5

Siku ya Ine, 19 Mwezi wa 6

Musali bila kuacha.​—1 Te. 5:17.

Yehova anatazamia tutende kulingana na sala zetu. Kwa mufano, ndugu anaweza kumuomba Yehova amusaidie ili wamupatie siku fulani ku kazi juu aweze kuenda ku mukusanyiko wa eneo. Yehova anaweza kujibia ile sala namna gani? Anaweza kumupatia ule ndugu uhodari wenye iko nao lazima juu aweze kuzungumuza na mukubwa wake wa kazi. Lakini ule ndugu naye anapaswa kufanya jambo fulani; anapaswa kukamata hatua ya kuomba mukubwa wake wa kazi ruhusa. Pengine itaomba afanye vile tena na tena. Anaweza hata kukamata mipango ya kutafuta mufanyakazi mwenzake mwenye anaweza kutumika pa nafasi yake wakati ataenda ku mukusanyikoao kupendekeza wasimulipe ile wakati yenye hatatumika. Yehova anatazamia tusali tena na tena kuhusu mahangaiko yetu. Yesu alionyesha kama Mungu hatatupatia palepale mambo fulani yenye tunamuomba. (Lu. 11:9) Kwa hiyo, tusichoke! Tusali tena na tena kwa moyo wote. (Lu. 18:1-7) Wakati tunafanya vile, tunaonyesha Yehova kama tuko kabisa na lazima ya ile jambo. Tunaonyesha pia kama tuko na imani kuwa iko na uwezo wa kutusaidia. w23.11 22 fu. 10-11

Siku ya Tano, 20 Mwezi wa 6

Tumaini halikatishe tamaa.​—Ro. 5:5.

Yehova alimuahidi rafiki yake Abrahamu kama mataifa yote ya ku dunia itajibariki kupitia uzao wake. (Mwa. 15:5; 22:18) Juu Abrahamu alikuwa na imani ya nguvu kwa Mungu, alikuwa hakika kama ile ahadi ya Mungu itatimia. Hata vile, wakati Abrahamu alikuwa na miaka 100 na Sara miaka 90, wale bibi na bwana waaminifu walikuwa tu hawajapata mutoto. (Mwa. 21:1-7) Lakini Biblia inasema: “Kwa kutegemea tumaini, [Abrahamu] alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi kulingana na yale yenye yalikuwa yamesemwa.” (Ro. 4:18) Tunajua kama mambo yenye Abrahamu alitumainia ilitimia. Alifikia kuwa baba ya Isaka, mutoto mwenye kwa miaka mingi alitumaini kama atapata. Ni nini njo ilifanya Abrahamu akuwe hakikia kwamba Yehova atatimiza ahadi yake? Juu Abrahamu alikuwa na urafiki wa karibu pamoja na Yehova, alikuwa “amesadikishwa kabisa kwamba kile chenye Yeye [Mungu] aliahidi” kitatimia. (Ro. 4:21) Yehova alimukubali Abrahamu na akamutangaza kuwa mwenye haki kwa sababu ya imani yake.—Yak. 2:23. w23.12 8 fu. 1-2

Siku ya Posho, 21 Mwezi wa 6

Mutu mwenye iko muaminifu katika mambo ya kidogo zaidi ni muaminifu katika mambo ya mukubwa pia, na mutu mwenye haiko mwenye haki katika mambo ya kidogo zaidi haiko mwenye haki katika mambo ya mukubwa pia.​—Lu. 16:10.

Kijana mwenye kutumainika anatimiza muzuri kabisa migao yake yote. Fikiria mufano mukamilifu wa Yesu. Hakuna siku Yesu alizarau migao yake. Lakini, alitimiza migao yenye Yehova alimupatia, hata wakati ilikuwa nguvu kufanya vile. Alipenda watu, zaidi sana wanafunzi wake, na alitoa uzima wake kwa kupenda kwa ajili yao. (Yoh. 13:1) Ili kumuiga Yesu, ujikaze sana kutimiza mugao wowote wenye wanakupatia. Kama haujue muzuri namna ya kutimiza mugao fulani, ukuwe munyenyekevu na uombe musaada kwa ndugu wenye kukomaa kiroho. Usifanye tu mambo kidogo, ujikaze kufanya yote yenye unaweza. (Ro. 12:11) Timiza mugao wako, kama “kwa ajili ya Yehova, na hapana kwa ajili ya wanadamu.” (Kol. 3:23) Juu haukamilike, ukuwe munyenyekevu na ukubali makosa yote yenye umefanya.​—Mez. 11:2. w23.12 26 fu. 8

Siku ya Yenga, 22 Mwezi wa 6

Amebarikiwa mutu mwenye anaweka tegemeo lake katika Yehova.​—Yer. 17:7.

Ni furaha sana kubatizwa na kuingia mu familia ya Yehova. Wale wenye wanafikia ile pendeleo wanakubaliana na hii maneno ya Daudi: “Mwenye furaha ni ule mwenye unachagua na kumuleta karibu ili akae katika viwanja vyako.” (Zb. 65:4) Haiko kila mutu njo Yehova anaalika mu uwanja wake. Anavuta kwake wale wenye wanaonyesha kama wanapenda kuwa na uhusiano wa karibu pamoya naye. (Yak. 4:8) Wakati unajitoa kwa Yehova na kubatizwa, unaweza kuwa hakika kama kisha pale “atakumwangia baraka mupaka kusikuwe kitu chenye kitakosa.” (Mal. 3:10; Yer. 17: 8) Kubatizwa ni mwanzo tu. Utapenda kufanya yako yote ili kuheshimia naziri yako ya kujitoa kwa Yehova, hata kama unapambana na magumu ao majaribu ya imani. (Muh. 5:4, 5) Juu sasa uko mwanafunzi wa Yesu, utajikaza kabisa kufuata mufano wake na amri zake.​—Mt. 28:19, 20; 1 Pe. 2:21. w24.03 8 fu. 1-3

Siku ya Kwanza, 23 Mwezi wa 6

Mwanaume atamuacha baba yake na mama yake na atashikamana na bibi yake.​—Mwa. 2:24.

Sasa, unaweza kufanya nini kama weye na bibi ao bwana yako hamupendake kupitisha wakati pamoya? Munaweza kufanya nini? Fikiria moto. Hauwakake sana ku mwanzo. Inaomba kuongeza kuni ya munene pole kwa pole. Vilevile, munawaza namna gani kama munaanza kwanza kupitisha wakati kidogo pamoya? Mujikaze kufanya jambo yenye nyiye wote munapendaka. (Yak. 3:18) Wakati munaanza na mambo ya kidogo, mutapendana tena zaidi. Heshima ni ya maana sana mu ndoa. Heshima iko sawa vile oksijeni yenye inasaidiaka moto iwake zaidi. Bila oksijeni, moto inaweza kuzimika haraka. Vilevile, bila heshima upendo wa bibi na bwana unaweza kupunguka haraka. Kwa upande mwingine, bibi na bwana wenye wako najikaza kuheshimiana wanafanyaka upendo wao uendelee. Jambo yenye tuko nazungumuzia hapa haiko kuwaza kama uko naheshimia ao hauheshimie bibi ao bwana yako, lakini, ni kujua kama bibi ao bwana yako anajisikiaka kama unamuheshimia ao hapana. w23.05 22 fu. 9; 24 fu. 14-15

Siku ya Pili, 24 Mwezi wa 6

Wakati mahangaiko yalinilemea, Ulinifariji na kunituliza.​—Zb. 94:19.

Mu Biblia watumishi fulani waaminifu wa Mungu wanaeleza namna wakati fulani walisikia mubaya sana na kutetemeka kwa sababu ya maadui wao ao kwa sababu ya mikazo ingine. (Zb. 18:4; 55:1, 5) Vilevile, tunaweza kupambana na upinzani ku masomo, ku kazi, kutoka kwa watu wa familia yetu, ao wakubwa wa serikali. Tunaweza hata kuogopa kama tutakufa kwa sababu ya ugonjwa fulani. Mu wakati ya vile, tunaweza kujisikia sawa mutoto mudogo mwenye hajue afanye nini. Yehova anatusaidia namna gani mu wakati ya vile? Anatufariji na kututuliza. Kwa hiyo, uzoee kupitisha wakati pamoja na Yehova kwa kusali na kusoma Neno yake. (Zb. 77:1, 12-14) Kisha wakati utakuwa na mahangaiko, jambo ya kwanza yenye utafikiria ni kutafuta musaada wake. Umuambie Yehova mambo yenye inakuogopesha na mahangaiko yako. Acha azungumuze na weye na akufariji kupitia Maandiko.​—Zb. 119:28. w24.01 24-25 fu. 14-16

Siku ya Tatu, 25 Mwezi wa 6

Mungu ndiye . . . anawachochea ninyi, na kuwapatia hamu na pia nguvu za kutenda.​—Flp. 2:13.

Kama tuko na hamu, tunaweza kufikia miradi yetu ya kiroho. Mutu mwenye iko na hamu ao mwenye anapendaka sana muradi wake anajikazaka na anapendaka sana kuufikia. Na kama tuko na hamu, tunaweza kufikia miradi yetu. Sasa, unaweza kufanya nini ili ukuwe na hamu zaidi? Umuombe Yehova akupatie hamu zaidi. Kupitia roho yake takatifu, Yehova anaweza kukusaidia ili ufikie muradi wako. Wakati fulani, tunajiwekeaka muradi juu tunajua kama tunapaswa kufanya vile; na ni muzuri kufanya vile. Lakini, pengine tunaweza kukosa kabisa hamu ya kuufikia. Ufikiri sana juu ya mambo yenye Yehova alishakakufanyia. (Zb. 143:5) Mutume Paulo alifikiri sana juu ya fazili zenye hazistahiliwe zenye Yehova alimuonyesha, na ile ilimuchochea amutumikie sana. (1 Ko. 15:​9, 10; 1 Ti. 1:12-14) Vilevile, kadiri unafikiri sana juu ya mambo yote yenye Yehova alishakakufanyia, ni vile utakuwa na hamu zaidi ya kufikia muradi wako.​—Zb. 116:12. w23.05 27 fu. 3-5

Siku ya Ine, 26 Mwezi wa 6

Musifu jina la Yehova.​—Zb. 113:1.

Tunamufurahisha Baba yetu wa mbinguni wakati tunasifu jina yake. (Zb. 119:108) Ni kusema kama Mungu Mweza-Yote, iko sawa vile wanadamu wenye hawakamilike, wenye wanapenda kusifiwa ili watiwe moyo ao ili waweze kujitumainia? Hapana. Wakati tunasifu Baba yetu wa mbinguni tunasaidia kuonyesha kama jambo yenye Shetani anasema juu ya kila mumoja wetu ni ya uongo. Shetani anasema kama hakuna mwanadamu mwenye atatetea kwa ushikamanifu jina ya Mungu. Anasema pia kama hakuna hata mumoja wetu mwenye kuwa mushikamanifu. Tena anasema kama siye wote tutamukatala Mungu ikiwa tunaona kuwa kufanya vile kutatuletea faida. (Yob. 1:9-11; 2:4) Lakini Yobu mutumishi muaminifu wa Yehova alionyesha kama Shetani ni muongo. Halafu weye? Kila mumoja wetu iko na pendeleo ya kutetea jina ya Baba yetu kwa ushikamanifu na kumufurahisha kwa kumutumikia kwa ushikamanifu. (Mez. 27:11) Ile ni pendeleo kubwa sana. w24.02 8-9 fu. 3-5

Siku ya Tano, 27 Mwezi wa 6

Mukuwe na imani katika manabii wake, na mutakuwa na matokeo ya muzuri.​—2 Ny. 20:20.

Kisha siku za Musa na YoshuaYehova aliweka waamuzi ili waongoze watu wake. Kisha, Yehova aliweka manabii ili waongoze watu wake wakati wa wafalme. Wafalme waaminifu walisikiliza mashauri ya manabii. Kwa mufano, Mufalme Daudi alikubali kwa unyenyekevu wakati nabii Natani alimurekebisha. (2 Sa. 12:7, 13; 1 Ny. 17:3, 4) Mufalme Yehoshafati alifuata muongozo wa nabii Yahazieli na alitia moyo watu wa Yuda “wakuwe na imani katika manabii [wa Mungu].” (2 Ny. 20:14, 15) Wakati Mufalme Hezekia alikuwa mu hali ya nguvu, alitafuta muongozo wa nabii Isaya. (Isa. 37:1-6) Kila wakati wenye wafalme walitafuta muongozo wa Yehova, walibarikiwa na Yehova alilinda taifa. (2 Ny. 20:29, 30; 32:22) Watu wote walipaswa kuona waziwazi kama Yehova alikuwa natumia manabii ili kuongoza watu wake. w24.02 21 fu. 8

Siku ya Posho, 28 Mwezi wa 6

Musishirikiane nao.​—Efe. 5:7.

Shetani anapenda tupitishe wakati pamoya na watu wenye watafanya ikuwe nguvu kwetu kuheshimia kanuni za Yehova. Tunapaswa kukumbuka kama marafiki wetu haiko tu watu wenye tunakutana nao uso kwa uso, lakini pia wale wenye tunazungumuza nao ku site za kupashana habari. Tunapaswa kupiganisha mawazo ya ulimwengu yenye kuonyesha kama haiko mubaya kuwa na mwenendo muchafu. Tunajua ile haiko kweli. (Efe. 4:19, 20) Ni muzuri tujiulize hivi: ‘Wakati haiko lazima nipitishe wakati pamoya na wafanyakazi wenzangu, wanafunzi wenzangu, ao watu wengine wenye hawaheshimie kanuni za Yehova, ninajikaza kuepuka kufanya vile? Ninafuata kwa uhodari kanuni za Yehova hata kama wengine wanaweza kusema kama niko na musimamo mukali?’ Sawa vile 2 Timoteo 2:20-22 inaonyesha, tunapaswa pia kuwa waangalifu wakati tuko tunachagua marafiki mu kutaniko. Tunakumbuka kama watu fulani wenye kuwa mu kutaniko hawatatusaidia kuendelea kuwa waaminifu mu utumishi wetu kwa Yehova. w24.03 22-23 fu. 11-12

Siku ya Yenga, 29 Mwezi wa 6

Yehova ni mwenye upendo mwingi sana.​—Yak. 5:11.

Ulishakapima kuwazia vile Yehova anakuwaka? Hata kama hatuwezi kumuona Yehova, Biblia inatumia maneno mbalimbali ili kufasiria namna anakuwaka. Yehova anaitwa “jua na ngao” na “moto wenye kuteketeza.” (Zb. 84:11; Ebr. 12:29) Mu maono, muandikaji fulani wa Biblia aliona Yehova anafanana na jiwe ya yakuti, metali yenye kungaa, na mwangaza wa upinde wa mvua. (Eze. 1:26-28) Juu hatuwezi kumuona Yehova, inaweza kuwa nguvu kwetu kuamini kama anatupenda. Watu fulani wanawaza kama Yehova hawezi kuwapenda kwa sababu ya mambo fulani yenye iliwafikia mu maisha. Yehova anaelewa namna tunajisikia na juu ya nini ile inaweza kufanya ikuwe nguvu kwetu kumukaribia. Ili kutusaidia, kupitia Neno yake Biblia anatuonyesha yeye ni mutu wa namna gani. Yehova ni upendo. Biblia inasema kama “Mungu ni upendo.” (1 Yo. 4:8) Upendo unachochea mambo yote yenye anafanya. Upendo wake ni mwingi sana na ni wenye nguvu sana mupaka anauonyesha hata wale wenye hawamupendi.​—Mt. 5:44, 45. w24.01 26 fu. 1-3

Siku ya Kwanza, 30 Mwezi wa 6

Alikuwa anasema nao kutoka katika nguzo ya wingu.​—Zb. 99:7.

Yehova alimuweka Musa ili aongoze Waisraeli mu safari yao ya kutoka Misri, na aliweka nguzo ya wingu muchana na nguzo ya moto usiku ili kuonyesha kama alikuwa nawaongoza. (Kut. 13:21) Musa alifuata ile nguzo yenye ilimuongoza yeye na Waisraeli mupaka ku Bahari Nyekundu. Watu waliogopa sana wakati waliwaza kama hawana kwa kukimbilia juu walikuwa kati ya bahari na jeshi ya Wamisri yenye ilikuwa nawafuata. Lakini Musa hakukosea. Ni Yehova mwenyewe njo aliongoza watu wake pale, kupitia Musa. (Kut. 14:2) Kisha Mungu aliwaokoa mu njia ya ajabu sana. (Kut. 14:26-28) Kwa miaka 40 kisha pale, Musa aliendelea kutegemea nguzo ya wingu ili kuongoza watu wa Mungu mu jangwa. (Kut. 33:7, 9, 10) Yehova alizungumuza na Musa kupitia ile wingu, na kisha Musa aliambia watu maagizo ya Yehova. Waisraeli walikuwa na ushuhuda wenye kuwa wazi, wenye ulionyesha kama Yehova alikuwa anatumia Musa ili kuwaongoza. w24.02 21 fu. 4-5

    Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili (Congo)
    • Tumia Wengine
    • Préférences
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Kanuni za Matumizi
    • Kanuni za Kutunza Siri
    • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
    • JW.ORG
    • Ingia
    Tumia Wengine