Mutumikie Yehova Mbele ya Siku Zenye Musiba
‘Mukumbuke . . . Muumba wako Mukubwa.’—MHU. 12:1.
1, 2. (a) Ni shauri gani ambalo Mungu aliongoza Mufalme Sulemani atolee vijana? (b) Sababu gani shauri hilo linahusu pia Wakristo walio na miaka 50 na zaidi?
MUFALME SULEMANI aliongozwa na roho ya Mungu ili kutolea vijana shauri hili: ‘Mukumbuke . . . Muumba wako Mukubwa katika siku za ujana wako, kabla siku zenye musiba hazijakuja.’ Siku hizo ‘zenye musiba’ ni siku gani? Mufalme Sulemani alitumia maneno ya mufano ili kuzungumuzia matatizo yanayotokea katika miaka ya uzee—mikono yenye kutetemeka, miguu yenye kuyumbayumba, meno kuisha, matatizo ya macho, magumu ya kusikia, nywele zenye imvi, na mugongo wenye kukunjama. Hatupaswe kungojea wakati huo ili kuanza kumutumikia Yehova.—Soma Mhubiri 12:1-5.
2 Wakristo wengi walio na miaka 50 na zaidi wangali na nguvu kimwili. Wanaweza kuwa na nywele zenye imvi, lakini hawajakuwa na afya zaifu kama ile ambayo Mufalme Sulemani alizungumuzia. Je, Wakristo hao wenye umri mukubwa wanaweza kufaidika na shauri hilo lilitolewa kwa vijana: ‘Mukumbuke . . . Muumba wako Mukubwa’? Shauri hilo linamaanisha nini?
3. Kumukumbuka Muumba wetu Mukubwa kunamaanisha nini?
3 Hata ikiwa tumemutumikia Yehova kwa miaka mingi, ni vizuri mara kwa mara kuchukua wakati wa kufikiri juu ya ukubwa wa Muumba wetu. Je, vitu ambavyo Yehova aliumba havikushangaze? Wanadamu hawawezi kuelewa vizuri kabisa vitu ambavyo Yehova aliumba. Yehova ametutolea aina mbalimbali ya vitu ili tuweze kufurahia maisha kwa njia nyingi. Tunapotafakari kuhusu uumbaji, hilo linatusaidia tupendezwe tena zaidi na upendo, hekima, na uwezo wa Yehova. (Zab. 143:5) Lakini kumukumbuka Muumba wetu Mukubwa kunamaanisha pia kufikiri juu ya yale anayotuomba tufanye. Bila shaka, kutafakari juu ya mambo hayo kutatuchochea kuonyesha shukrani yetu kwa Muumba wetu kwa kufanya yote tunayoweza katika kazi yake kwa muda wote wa maisha yetu.—Mhu. 12:13.
NAFASI ZA PEKEE KATIKA MIAKA YA UZEE
4. Ni ulizo gani ambalo Wakristo wenye uzoefu mwingi wanaweza kujiuliza, na sababu gani?
4 Ikiwa umekuwa na uzoefu mwingi katika maisha, unaweza kujiuliza hivi: ‘Kwa kuwa ningali na nguvu kwa kiasi fulani, nitatumia maisha yangu namna gani sasa?’ Kwa kuwa wewe ni Mukristo mwenye uzoefu, una nafasi ambazo wengine hawana. Unaweza kuwafundisha vijana mambo ambayo umejifunza kuhusu Yehova. Unaweza kuwatia wengine nguvu kwa kuwaelezea mambo uliyojionea katika kazi ya Yehova. Mufalme Daudi alisali ili apate nafasi za kufanya hivyo. Aliandika hivi: ‘Ee Mungu, umenifundisha tangu ujana wangu . . . Mupaka wakati wa uzee na wa kuwa na kichwa chenye imvi, Ee Mungu, usiniache, mupaka nikitangazie kizazi habari za mukono wako, habari za nguvu zako, kwa wale wote watakaokuja.’—Zab. 71:17, 18.
5. Namna gani Wakristo wenye umri mukubwa wanaweza kusaidia wengine wafaidike na mambo ambayo wamejifunza?
5 Namna gani unaweza kusaidia wengine wafaidike na hekima ambayo umepata kwa miaka mingi? Je, unaweza kualika watumishi wa Mungu vijana waje kwako ili upitishe wakati muzuri pamoja nao? Je, unaweza kuwaomba wakusindikize katika mahubiri na kuwaelezea furaha ambayo unapata katika kazi ya Yehova? Elihu alisema hivi: “Siku zinapaswa kusema, na wingi wa miaka ndio unaopaswa kujulisha hekima.” (Ayu. 32:7) Mutume Paulo aliwaomba Wakristo wanawake wenye uzoefu watie moyo wengine kwa maneno na matendo. Aliandika hivi: ‘Wanawake wenye umri mukubwa . . . wawe walimu wa yaliyo mema.’—Tito 2:3.
USIZARAU UWEZO WAKO
6. Sababu gani Wakristo wenye umri mukubwa hawapaswe kuzarau uwezo wao?
6 Ikiwa wewe ni Mukristo mwenye uzoefu, kuna mambo mengi unayoweza kufanya ili kuwasaidia wengine. Fikiria mambo unayoelewa sasa ambayo haukujua miaka 30 ao 40 iliyopita. Umejua namna ya kutumia kanuni za Biblia kwa ufundi. Bila shaka una uwezo wa kutumia ukweli wa Biblia ili kugusa mioyo ya wengine. Ikiwa wewe ni muzee wa kutaniko, unajua namna ya kuwasaidia ndugu na dada ambao wamejikwaa. (Gal. 6:1) Pengine umejifunza namna ya kusimamia utendaji mbalimbali wa kutaniko, idara mbalimbali za mikusanyiko, ao ujenzi wa Jumba la Ufalme. Pengine unajua namna ya kuwatia moyo waganga ili watumie ufundi mbalimbali wa kutunza bila kutumia damu. Hata ikiwa umejifunza kweli hivi karibuni tu, umekwisha kujionea mambo mengi katika maisha. Kwa mufano, ikiwa umekwisha kukomalisha watoto, umepata hekima nyingi. Wakristo wenye umri mukubwa wana uwezo mukubwa wa kuwatia moyo watu wa Yehova wanapofundisha, wanapoongoza, na kutia nguvu imani ya ndugu na dada.—Soma Ayubu 12:12.
7. Ni katika njia gani Wakristo wenye umri mukubwa wanaweza kuwazoeza vijana?
7 Unaweza kutumia uwezo wako katika njia gani zingine? Labda unaweza kuwaonyesha vijana namna ya kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia. Ikiwa wewe ni dada, je, unaweza kuonyesha dada vijana wenye kuolewa namna wanavyoweza kutia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza wanapoendelea kuwatunza watoto wao wachanga? Ikiwa wewe ni ndugu, je, unaweza kufundisha vijana namna ya kutoa hotuba kwa uchangamufu na namna ya kuwa na ufundi katika mahubiri? Je, unaweza kuwaonyesha namna unavyowatembelea ndugu na dada wenye kuzeeka ili kuwatia moyo? Hata ikiwa hauna tena nguvu kimwili kama zamani, ungali na nafasi nzuri za kuwazoeza vijana. Neno la Mungu linasema hivi: ‘Uzuri wa vijana ni nguvu zao, na utukufu wa wazee ni kichwa chao chenye imvi.’—Met. 20:29.
TUMIKIA YEHOVA MAHALI AMBAPO KUNA UHITAJI MUKUBWA
8. Ni mambo gani ambayo mutume Paulo alifanya katika uzee?
8 Mutume Paulo alitumia uwezo wake ili kumutumikia Mungu katika uzee. Alipotoka katika gereza huko Roma katika mwaka wa 61 hivi, alikuwa amefanya mengi na kuvumilia matatizo mengi katika kazi ya umisionere, na pengine angechagua kuishi maisha rahisi akihubiri katika Roma. (2 Kor. 11:23-27) Ndugu katika muji huo mukubwa wangefurahi ikiwa mutume Paulo angeendelea kutumika pamoja nao. Lakini Paulo alitambua kwamba kulikuwa uhitaji mukubwa katika maeneo mengine. Aliendelea na kazi yake umisionere pamoja na Timotheo na Tito, walienda Efeso, kisha Krete, na pengine hata Makedonia. (1 Tim. 1:3; Tito 1:5) Hatujue ikiwa alitembelea Hispania, lakini alikuwa na mupango wa kuenda huko.—Rom. 15:24, 28.
9. Pengine mutume Petro alienda kutumikia mahali ambapo palikuwa uhitaji mukubwa wakati gani? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)
9 Inawezekana mutume Petro alikuwa na miaka zaidi ya 50 alipoenda mahali ambapo kulikuwa uhitaji mukubwa. Kwa nini tunasema hivyo? Ikiwa alikuwa na umri unaokaribia ule wa Yesu ao ikiwa pengine alimushinda Yesu miaka fulani, alipaswa kuwa na miaka 50 hivi alipokutana na mitume wengine huko Yerusalemu katika mwaka wa 49. (Mdo. 15:7) Muda fulani kisha mukutano huo, mutume Petro alienda kuishi Babiloni ili kuhubiri Wayahudi wengi waliokuwa katika eneo hilo. (Gal. 2:9) Alikuwa akiishi huko alipoandika barua yake ya kwanza katika mwaka wa 62. (1 Pet. 5:13) Si rahisi kukaa katika inchi ya kigeni, lakini Petro hakuruhusu umri wake mukubwa umunyanganye furaha yake ya kumutumikia Yehova kwa bidii.
10, 11. Ndugu mumoja na bibi yake walifanya nini walipokuwa na umri mukubwa?
10 Leo, Wakristo wengi walio na miaka 50 na zaidi wanaona kwamba hali zao zimebadilika na kwamba wanaweza kumutumikia Yehova katika njia zingine. Ndugu na dada fulani wameenda kutumikia mahali ambapo kuna uhitaji mukubwa wa wahubiri. Kwa mufano, ndugu Robert anaandika hivi: “Mimi na bibi yangu tulikuwa na miaka zaidi ya 50 tulipotambua kwamba tungali na nafasi za kufanya mambo mengi. Mutoto wetu mumoja tuliyekuwa naye alikuwa haishi tena nasi, hatukuwa tunashugulikia tena wazazi wetu waliokuwa wazee, na tulikuwa tumepewa uriti fulani. Nilitambua kwamba ikiwa tungeuzisha nyumba yetu, tungeweza kulipa deni tuliyokuwa nayo na tungebaki na feza za kutosha ambazo zingetusaidia mupaka wakati ambapo ningelipwa pansio ao feza ambazo mutu anapewa anapoacha kazi kwa sababu ya uzee. Tulisikia kwamba katika inchi ya Bolivia hesabu ya watu wanaokubali kujifunza Biblia ni kubwa lakini mutu anaweza kuishi huko na feza kidogo. Kwa hiyo, tuliamua kuhama. Haikuwa rahisi kuzoea makao yetu mapya. Maisha yalikuwa tofauti na yale tuliyozoea katika Amerika ya Kaskazini. Lakini jitihada zetu zilibarikiwa.”
11 Ndugu Robert anaongeza hivi: “Kwa sasa tunapitisha wakati mwingi katika utendaji mbalimbali wa kutaniko. Watu fulani ambao tulijifunza nao Biblia walibatizwa. Familia moja ambayo tulijifunza nayo Biblia ilikuwa na maisha ya hali ya chini katika kijiji kimoja mbali na mahali tulipoishi. Lakini kila juma, washiriki wa familia hiyo walifanya safari ndefu ili kuja kwenye mikutano. Wazia furaha yetu wakati familia hiyo ilifanya maendeleo na wakati kijana wao wa kwanza alianza kazi ya upainia!”
KUNA UHITAJI KATIKA MAENEO YA LUGA ZA KIGENI
12, 13. Eleza namna ndugu mumoja alivyoanza kutumikia Yehova katika njia nyingine kisha kuacha kazi kwa sababu ya uzee.
12 Makutaniko na vikundi vya luga za kigeni vinaweza kufaidika kabisa na mifano ya ndugu na dada wenye umri mukubwa. Pia, wanaweza kufurahia kutumika katika maeneo ya luga za kigeni. Kwa mufano, Ndugu Brian anaandika hivi: “Nilipoacha kazi kwa sababu ya uzee nikiwa na miaka 65, mimi na bibi yangu tuliona kwamba maisha inakuwa yenye kuchokesha. Watoto wetu walikuwa hawaishi tena pamoja nasi, na ilikuwa vigumu kupata watu wa kujifunza nao Biblia. Kisha nilikutana na kijana mumoja Muchina aliyekuwa akifanya utafiti kwenye masomo ya juu ya mahali hapo. Alikubali kuja kwenye mikutano yetu, na nilianza kujifunza Biblia pamoja naye. Kisha majuma machache, alianza kuja na mwanafunzi mwenzake Muchina kwenye mikutano. Majuma mawili baadaye, alileta wengine watatu.
13 “Baadaye Muchina wa tano alipoomba funzo la Biblia, nilifikiri hivi: ‘Sitaacha kazi ya Yehova kwa sababu tu nina miaka 65.’ Kwa hiyo nilimuuliza bibi yangu, niliyemushinda miaka miwili, ikiwa angependa kujifunza Kichina. Tulijifunza Kichina kwa kutumia kaseti za kusikiliza. Kumepita miaka 10 tangu tujifunze luga hiyo. Kuhubiri katika eneo la luga ya kigeni kulitufanya tujisikie kuwa vijana tena. Kufikia sasa, tumejifunza Biblia na Wachina 112! Wengi kati yao wamekuwa wakihuzuria mikutano. Mumoja wao anafanya utumishi wa painia pamoja nasi.”
Pengine haujazeeka sana hivi kwamba usipanue utumishi wako (Ona fungu la 12, 13)
FURAHIA KILE AMBACHO UNAWEZA KUFANYA
14. Wakristo wenye umri mukubwa wanaweza kuwa hakika na jambo gani, na namna gani mufano wa mutume Paulo unawatia moyo?
14 Ijapokuwa Wakristo wengi walio na miaka zaidi ya 50 wanafurahia nafasi mupya za kufanya mambo mengi katika kazi ya Yehova, si wote wanaoweza kufanya hivyo. Wengine kati yao wana afya mbaya, wengine wanashugulikia watoto ao wazazi wao wenye kuzeeka. Unaweza kuwa hakika kwamba Yehova anapendezwa na yale unayoweza kufanya katika kazi yake. Kwa hiyo, kuliko kuhuzunika kwa sababu ya kile ambacho hauwezi kufanya, furahia kile ambacho unaweza kufanya. Fikiria mufano wa mutume Paulo. Kwa miaka mingi aliyopitisha katika gereza, hakuwa na uwezo wa kuendelea na safari zake za umisionere. Lakini kila mara wakati watu walimutembelea, alizungumuza nao kuhusu Maandiko na kutia imani yao nguvu.—Mdo. 28:16, 30, 31.
15. Sababu gani Wakristo wenye kuzeeka wanasaminiwa sana?
15 Yehova anapendezwa pia na yale ambayo watumishi wake wenye umri mukubwa wanaweza kufanya katika kazi yake. Hata ikiwa mufalme Sulemani alionyesha kwamba kipindi hicho chenye kujaa matatizo ya afya si kipindi kizuri, Yehova anasamini sana yale ambayo watumishi wake wenye kuzeeka wanaweza kutimiza ili kumutukuza. (Lu. 21:2-4) Ndugu na dada wanasamini mufano wa uaminifu wa Wakristo hao ambao wamemutumikia Yehova kwa miaka mingi.
16. Inaonekana Ana hangeweza kupata mapendeleo gani, lakini angeweza kufanya nini ili kumuabudu Mungu?
16 Biblia inaeleza kwamba mwanamuke mumoja mwenye kuzeeka anayeitwa Ana aliendelea kumutukuza Yehova kwa uaminifu katika miaka yake ya uzee. Alikuwa mujane wa miaka 84 wakati Yesu alizaliwa. Inaonekana kwamba, hakuendelea kuishi ili afikie kuwa mufuasi wa Yesu, ili atiwe mafuta kwa roho takatifu, ao ili ashiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme. Hata hivyo, Ana alifurahia kile ambacho angeweza kufanya. ‘Alikuwa hakose kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mutakatifu usiku na muchana.’ (Lu. 2:36, 37) Kwa kuwa kuhani alitoa uvumba katika hekalu kila asubuhi na mangaribi, Ana alikuwa kati ya watu wengi waliokusanyika katika uwanja wa hekalu wakitoa sala za kimya-kimya kwa nusu saa hivi. Alipoona mutoto Yesu, alianza ‘kusema juu ya mutoto huyo kwa wale wote waliokuwa wakiungojea ukombozi wa Yerusalemu.’—Lu. 2:38.
17. Namna gani tunaweza kusaidia ndugu na dada wenye kuzeeka ili washiriki katika ibada ya kweli?
17 Leo, tunapaswa kuwa tayari ili kusaidia Wakristo wenzetu wenye kuzeeka ao walio vilema. Wengi kati yao wangependa kuwa kwenye mikutano na mikusanyiko, lakini wakati fulani wanashindwa kufanya hivyo. Mahali fulani, makutaniko yanafanya mipango ili ndugu na dada hao wasikilize mikutano kwa njia ya telefone. Lakini, haiwezekane kufanya hivyo mahali pengine. Hata hivyo, Wakristo ambao hawana nguvu ya kuja kwenye mikutano wanaweza pia kutegemeza ibada ya kweli. Kwa mufano, wanaweza kusali ili Yehova abariki kutaniko la Kikristo.—Soma Zaburi 92:13, 14.
18, 19. (a) Namna gani ndugu na dada wenye kuzeeka wanaweza kuwatia wengine moyo? (b) Ni nani anayeweza kutumia shauri hili: ‘Mukumbuke . . . Muumba wako Mukubwa’?
18 Ndugu na dada wenye kuzeeka hawawezi kutambua namna gani mufano wao unawatia wengine moyo. Kwa mufano, Ana alikuwa mwaminifu miaka yote hiyo kwenye hekalu, lakini pengine hakujua kwamba mufano wake ungeendelea kuwatia wengine moyo miaka mingi baadaye. Upendo wa Ana kwa Yehova uliandikwa katika Maandiko. Bila shaka, waabudu wenzako hawatasahau upendo wako kwa Mungu. Kwa hiyo si jambo la kushangaza wakati Neno la Mungu linasema hivi: ‘Kichwa chenye imvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.’—Met. 16:31.
19 Sisi wote tunashindwa kufanya yote ambayo tunataka kufanya katika kazi ya Yehova. Lakini acheni wale wote kati yetu ambao wangali na nguvu kwa kiasi fulani na uwezo washikamane na maneno haya: ‘Mukumbuke . . . Muumba wako Mukubwa . . . kabla siku zenye musiba hazijakuja.’—Mhu. 12:1.