SURA YA 17
Endelea Kubakia mu Tengenezo ya Yehova
MWANAFUNZI Yakobo aliandika hivi: “Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Ndiyo, hata kama hatukamilike, Yehova haiko juu sana ao mbali sana ili akose kusikiliza sala zetu. (Mdo. 17:27) Namna gani tunaweza kumukaribia? Tunaweza kufanya vile kwa kuwa na urafiki wa pekee pamoya naye, na ile urafiki inatia ndani kusali kwake kutoka mu moyo. (Zb. 39:12) Pia, jambo ingine yenye inaweza kutusaidia kuwa na urafiki wa vile, ni kujifunza kwa ukawaida Neno yake, Biblia. Kufanya vile, inatusaidia kumujua Yehova Mungu, mipango yake, na mapenzi yake juu yetu. (2 Ti. 3:16, 17) Kwa hiyo, tunajifunza kumupenda na kuogopa kufanya mambo yenye kumuchukiza.—Zb. 25:14.
2 Lakini, ni kupitia Mwana wake tu, Yesu, njo tunaweza kumukaribia. (Yoh. 17:3; Ro. 5:10) Ni Yesu tu njo anaweza kutusaidia tujue muzuri mawazo ya Yehova. Yesu alikuwa na urafiki wa sana pamoya na Baba yake, njo maana alikuwa na sababu ya kusema: “Hakuna mutu mwenye anajua Mwana ni nani isipokuwa Baba, wala mwenye anajua Baba ni nani isipokuwa Mwana, na kila mutu mwenye Mwana anapenda kumufunulia Baba.” (Lu. 10:22) Kwa hiyo, wakati tunajifunza vitabu vya Injili na kuona namna Yesu alikuwa anawaza na kujisikia, tunajua mara moya mawazo ya Yehova na namna anajisikiaka. Kujua ile mambo, kunatusaidia tumukaribie zaidi Mungu wetu.
3 Juu tunaongozwa na Mwana wa Mungu, tunafanya urafiki wetu pamoya na Yehova ukuwe muzuri sana, na ile inafanya tuendelee kushikamana na sehemu yenye kuonekana ya tengenezo yake, yenye inatusaidia tujue namna ya kufanya mapenzi yake. Vile andiko ya Matayo 24:45-47 ilitabiri, Bwana, Yesu Kristo amemuweka “mutumwa muaminifu na mwenye busara” ili apatie watu wa nyumbani ‘chakula kwa wakati wenye kufaa.’ Leo, mutumwa muaminifu anatupatia chakula mingi ya kiroho. Yehova anamutumia juu ya kutushauria tusome Neno yake kila siku, tuhuzurie kwa ukawaida mikutano yetu ya Kikristo, na tuhubiri kwa bidii “habari njema ya Ufalme.” (Mt. 24:14; 28:19, 20; Yos. 1:8; Zb. 1:1-3) Kwa hiyo, tuepuke kabisa kuwa na mawazo yenye haifae juu ya mutumwa muaminifu. Tunapaswa kujikaza kushikamana na sehemu yenye kuonekana ya tengenezo ya Yehova na kutii muongozo wayo. Ile, itatusaidia tumukaribie zaidi Yehova, Mungu wetu, na pia itatusaidia tukuwe nguvu kiroho na kutulinda wakati wa majaribu.
JUU YA NINI WATUMISHI WA YEHOVA WANAENDELEA KUTESWA?
4 Pengine umekuwa mu kweli kwa miaka mingi. Kama ni vile, bila shaka unajua muzuri kama inaomba pia kuvumilia magumu yenye inajaribu uaminifu-mushikamanifu wetu. Lakini, hata kama ni tangu sasa njo umemujua Yehova na kujiunga na watumishi wake, na weye pia unajua kama Shetani Ibilisi anapinga kila mutu mwenye kutii mamlaka makubwa ya Yehova. (2 Ti. 3:12) Kwa hiyo, ikuwe uko navumilia mateso mingi ao kidogo, hauna sababu ya kuogopa ao kuvunjika moyo. Yehova alishatoa ahadi kama atakusaidia na atakubariki, atakuokoa na kukupatia uzima wakati wenye kuya.—Ebr. 13:5, 6; Ufu. 2:10.
5 Siye wote tunaweza kupatwa na majaribu mu hizi siku za mwisho zenye zinabakia za mupangilio wa Shetani. Tangu Ufalme wa Mungu uanze kutawala mu 1914, Shetani haruhusiwe tena kuingia mbinguni, mbele ya Yehova. Alitupwa hapa ku dunia kutoka mbinguni, na ni hapa njo yeye na malaika wake wabaya wanapatikana tangu ile siku. Juu Shetani anakasirika sana, anafanya magumu iongezeke sana hapa ku dunia, na anachochea watu watese sana wale wenye wanajitoa kwa Yehova ili kumutumikia. Ile mambo yote, inatuhakikishia kama tunaishi mu siku za mwisho za utawala mubaya wa Shetani.—Ufu. 12:1-12.
6 Shetani anakasirika sana juu ameshushwa na anajua kama siku zake zinabakia kidogo sana. Yeye na mashetani wake, wanafanya nguvu yao yote ili kuzuia kazi ya kuhubiri Ufalme, na wanafanya yote ili kuharibisha umoja wa watumishi wa Yehova. Kwa hiyo, tuko mu uwanja wa mapigano ili kupigana vita ya kiroho; Biblia inaiita kuwa vita ya ‘kupambana, hapana na damu na mwili, lakini tunapambana na serikali, na mamlaka, na watawala wa ulimwengu wa giza hii, na majeshi ya pepo wachafu katika mahali pa kimbingu.’ Kama tunapenda Yehova atusaidie tupate ushindi mu ile vita, tunapaswa kuendelea kupigana na kuchunga muzuri silaha zetu za kiroho. Tunapaswa “kusimama imara na kupinga matendo ya ujanja ya Ibilisi.” (Efe. 6:10-17) Ile inaomba kuwa na uvumilivu.
TUKUWE NA UVUMILIVU
7 Uvumilivu ni “uwezo wa kushindana na mateso ao majaribu.” Mu maana ya kiroho, uvumilivu ni uwezo wa kuendelea kufanya mambo ya muzuri hata kama unapambana na mateso, majaribu, ao jambo ingine yoyote yenye iko na kusudi ya kukupotezea uaminifu wako kwa Mungu. Mukristo anapaswa kukomalisha sifa ya uvumilivu. Inaomba wakati ili kufanya vile. Kadiri tunaendelea kufanya maendeleo ya kiroho, ni vile uwezo wetu wa kuvumilia unaongezeka. Wakati tunavumilia majaribu ya kidogo-kidogo ya imani yetu, ni kusema, majaribu yenye tunapata wakati tu tunaanza kumutumikia Yehova, ile inafanya tukuwe na nguvu zaidi ya kuvumilia majaribu ya mukubwa zaidi yenye lazima itokee. (Lu. 16:10) Hatutachunga majaribu ya mukubwa itokee njo tuazimie kuwa na imani ya nguvu. Tunapaswa kufanya vile mbele ya wakati. Mutume Petro alieleza kama uvumilivu unaweza kutusaidia tukuwe na sifa zingine za Kikristo. Aliandika hivi: “Mujikaze kabisa kuongeza kwenye imani yenu tabia za muzuri, kwenye tabia zenu za muzuri ujuzi, kwenye ujuzi wenu kujizuia, kwenye kujizuia kwenu uvumilivu, kwenye uvumilivu wenu ushikamanifu kwa Mungu, kwenye ushikamanifu wenu kwa Mungu upendo wa kindugu, kwenye upendo wenu wa kindugu upendo.”—2 Pe. 1:5-7; 1 Ti. 6:11.
Kadiri tunaendelea kupambana na majaribu kila siku na kuishinda, ni vile tunaendelea kuwa wavumilivu zaidi
8 Pia, Yakobo anaonyesha mu barua yake kama ni lazima sana kuwa na uvumilivu. Aliandika hivi: “Muone yote kuwa furaha, ndugu zangu, wakati munapata majaribu mbalimbali, mukijua kama sifa yenye imejaribiwa ya imani yenu inatokeza uvumilivu. Lakini muache uvumilivu ukamilishe kazi yake, ili mukuwe kamili na bila kosa katika mambo yote, bila kukosa kitu chochote.” (Yak. 1:2-4) Yakobo anasema kama Wakristo wanapaswa kukubali majaribu na kuiona kuwa furaha juu inawasaidia kuonyesha sifa ya uvumilivu. Ulishakafikiri vile? Kisha, Yakobo alionyesha kama uvumilivu uko na kazi fulani ya kufanya, ni kusema, unatusaidia tukuwe na sifa za muzuri za Kikristo na unafanya tukubaliwe na Mungu. Ndiyo, kadiri tunaendelea kupambana na majaribu kila siku na kuishinda, ni vile tunaendelea kuwa wavumilivu zaidi. Uvumilivu unatusaidia pia kuwa na sifa zingine za muzuri zenye tuko nazo lazima.
9 Yehova anapendezwa na uvumilivu wetu. Ni sifa yenye itamuchochea atupatie zawadi ya uzima wa milele. Yakobo aliandika tena hivi: “Mwenye furaha ni mutu mwenye anaendelea kuvumilia jaribu, kwa sababu akiisha kukubaliwa atapokea taji la uzima, lenye Yehova aliahidi wale wenye wanaendelea kumupenda.” (Yak. 1:12) Ndiyo, tunavumilia juu tuko na tumaini ya kupata uzima. Haiwezekane kubakia mu kweli kama hatuna sifa ya uvumilivu. Kama tunafuata tamaa za ulimwengu, tutarudia mu ulimwengu. Tena, kama tunakosa kuwa wavumilivu, Yehova hataendelea kutupatia roho yake, na tukikosa ile roho hatuwezi kuwa na tunda ya roho mu maisha yetu.
10 Kama tunapenda kuendelea kuwa wavumilivu mu hii wakati ya hatari, tunapaswa kuepuka kuwa na mawazo yenye haifae juu ya mateso yenye tunapata tukiwa Wakristo. Kumbuka, Yakobo aliandika hivi: “Muone yote kuwa furaha.” Haiko mwepesi kuwa na furaha vile, juu majaribu inaweza kufanya mutu ateseke kimwili ao kiakili. Lakini, usisahau kama ni uzima wako wa wakati wenye kuya njo uko mu hatari. Mufano wa mitume unatusaidia tuelewe muzuri namna ya kuwa na furaha wakati tunapata mateso. Ile habari inapatikana mu kitabu ya Matendo, na inasema hivi: “Wakaita mitume, wakawapiga viboko, na kuwaagiza waache kusema katika jina la Yesu, kisha wakawaacha waende. Basi wakatoka mbele ya Sanhedrini, wakiwa na furaha kwa sababu walikuwa wamehesabiwa kuwa wanastahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 5:40, 41) Mitume walielewa kama ile mateso ilihakikisha kama walitii amri ya Yesu, na kama Yehova alikuwa amewakubali. Kisha miaka fulani, wakati roho ya Mungu ilisaidia mutume Petro kuandika barua yake ya kwanza, alizungumuzia faida ya kuteseka vile juu ya haki.—1 Pe. 4:12-16.
11 Mufano ingine ni ya Paulo na Sila. Wakati walikuwa Filipi ili kufanya kazi yao ya umisionere, walikamatwa na kushitakiwa kama walikuwa nasumbua watu mu ile muji na kufundisha desturi zenye haziruhusiwe na sheria. Kwa hiyo, walipigwa sana na kutupwa mu gereza. Biblia inatuambia namna Paulo na Sila walitenda wakati walikuwa mu gereza, hata kama walikuwa wangali na vidonda. Inasema hivi: “Karibu katikati ya usiku, Paulo na Sila walikuwa wanasali na kumusifu Mungu kwa wimbo, na wafungwa walikuwa wanawasikiliza.” (Mdo. 16:16-25) Paulo na Sila hawakuona mateso yao kwa ajili ya Kristo kuwa tu ushuhuda wa uaminifu-mushikaminifu mbele ya Mungu na mbele ya wanadamu, lakini pia waliiona kuwa njia ya kuhubiria wale wenye wangekuwa tayari kusikiliza habari njema. Uzima wa wengine ulikuwa mu hatari. Mu ileile usiku, mulinzi wa gereza na watu wa nyumba yake wakaamini na kuwa wanafunzi. (Mdo. 16:26-34) Paulo na Sila walitumainia Yehova na nguvu zake, na walijua kama iko tayari kuwasaidia mu mateso yao. Hawakuvunjika moyo.
12 Leo pia, Yehova ametupatia mambo yote yenye tuko nayo lazima juu ya kutusaidia mu hii kipindi ya mateso. Anapenda tuivumilie. Kwa hiyo, Yehova ametupatia Neno yake yenye iliongozwa na roho takatifu juu itusaidie kujua kusudi yake. Kujua vile, kunatia nguvu imani yetu. Tuko na nafasi ya kukusanyika na Wakristo wenzetu na kumutolea Yehova utumishi mutakatifu. Pia, sala inatusaidia tusipoteze pendeleo yetu ya kuendelea kuwa na urafiki wa muzuri sana pamoya na Yehova. Anasikiliza maneno yetu ya kumusifu na sala yetu yenye kutoka mu moyo ya kumuomba atusaidie tuendelee kuonekana safi mbele yake. (Flp. 4:13) Na jambo ingine yenye hatupaswe kusahau hata kidogo, ni nguvu yenye tunapataka wakati tunafikiria tumaini ya muzuri yenye kuwa mbele yetu.—Mt. 24:13; Ebr. 6:18; Ufu. 21:1-4.
KUVUMILIA MAJARIBU MBALIMBALI
13 Majaribu mbalimbali yenye tuko napata leo, inafanana na mateso yenye wanafunzi wa kwanza wa Yesu Kristo walipataka. Leo, wapinzani wanaambiwa habari za uongo kuhusu Mashahidi wa Yehova, na ile inafanya wawatukane na kuwatesa sana. Sawa vile tu mu siku za mitume, ile upinzani inachochewa zaidi sana na watu wenye wanapenda sana dini zao, wenye Neno ya Mungu inapinga kabisa matendo na mafundisho yao. (Mdo. 17:5-9, 13) Wakati fulani, watumishi wa Yehova wanapata kitulizo wakati wanaomba wapewe haki zao zenye kukubaliwa na sheria za serikali. (Mdo. 22:25; 25:11) Lakini, wakati fulani viongozi wa serikali pia wanafikia kukataza kazi zetu, na kutafuta hata kusimamisha utumishi wetu wa Kikristo. (Zb. 2:1-3) Mu hali za vile, tunafuata bila woga mufano wa mitume waaminifu. Walisemaka hivi: “Tunapaswa kumutii Mungu kuwa mutawala kuliko wanadamu.”—Mdo. 5:29.
14 Vile roho ya kila mutu kupenda sana inchi yake inaendelea kuongezeka mu dunia yote, ni vile wahubiri wa habari njema wanaendelea kusukumwa huku na kule juu waache kazi yenye Mungu aliwapatia ya kuhubiri habari njema. Watumishi wote wa Mungu wanajua muzuri sana onyo yenye iko mu Ufunuo 14:9-12, yenye inazungumuzia kuabudu “ule munyama wa pori na sanamu yake.” Tunaelewa maana ya hii maneno ya mutume Yohana: “Hapa watakatifu wanahitaji kuwa na uvumilivu, wale wenye wanashika amri za Mungu na kushika imara imani ya Yesu.”
15 Mambo kama vile, vita, mapinduzi ya serikali, ao mateso ya waziwazi na serikali kukataza kazi yetu, inaweza kukuzuia usimuabudu Yehova waziwazi. Inawezekana kutaniko isikuwe nakusanyika tena pamoya, ao ikuwe nguvu kwa kutaniko kupashana habari na biro ya tawi, ao inakatazwa kwa waangalizi kutembelea makutaniko, na pengine inakuwa nguvu kupata vichapo. Kama hali moya kati ya zile inawafikia, unaweza kufanya nini?
16 Kwa kifupi, ufanye yote yenye unaweza mu hali za vile juu uendelee kuwa nguvu kiroho. Usiache kujifunza kipekee. Kwa kawaida, inawezekana ndugu na dada wakusanyike mu vikundi vidogo-vidogo mu nyumba za ndugu. Biblia na vichapo vyenye tulijifunzaka zamani vinaweza kutumiwa ku ile mikutano. Usiogope ao kuhangaika sana. Kama kawaida, Baraza Yenye Kuongoza itatafuta njia ya kupashana habari bila kukawia na ndugu wenye wako na madaraka.
17 Hata kama unajikuta uko weye peke mbali na Wakristo wenzako, ukumbuke kama hauko mbali na Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Unaweza kuendelea kuwa na tumaini yenye iko nguvu. Yehova ataendelea kusikiliza sala zako, na atakutia nguvu kupitia roho yake. Umuombe aendelee kukuongoza. Usisahau kama uko mutumishi wa Yehova na mwanafunzi wa Yesu Kristo. Kwa hiyo, utumie muzuri nafasi zenye kujitokeza ili kuhubiri. Yehova atabariki bidii yako, na bila kukawia, wengine wanaweza kujiunga na weye mu ibada ya kweli.—Mdo. 4:13-31; 5:27-42; Flp. 1:27-30; 4:6, 7; 2 Ti. 4:16-18.
18 Hata wakati wanakuogopesha na kukuambia kama watakuua, sawa vile waliambiaka mitume na watumishi wengine wa Mungu, utumainie “Mungu mwenye anafufua wafu.” (2 Ko. 1:8-10) Kuamini kama watu wenye washakakufa watafufuliwa, inaweza kukusaidia kuvumilia hata upinzani wa nguvu sana. (Lu. 21:19) Yesu Kristo alituachia mufano; alibakia muaminifu hata kama alipata majaribu, na alijua kama ile itapatia wengine nguvu ya kuvumilia. Na weye kama unavumilia, unaweza kutia nguvu ndugu na dada zako.—Yoh. 16:33; Ebr. 12:2, 3; 1 Pe. 2:21.
19 Zaidi ya mateso na upinzani, pengine kuko hali zingine za nguvu zenye uko napambana nazo. Kwa mufano, Wakristo fulani wanavunjika moyo juu watu wa mu eneo yao hawapendezwe na ujumbe wetu. Wengine wanapambana na magonjwa ya kimwili ao mahangaiko ya akili, ao kuvumilia hali zingine zenye zinatokea juu ya uzaifu wa wanadamu. Mutume Paulo pia, alipaswa kuvumilia jaribu fulani yenye ilimusumbua mu kazi yake, na wakati fulani ilifanya hata ikuwe nguvu kufanya muzuri ile kazi. (2 Ko. 12:7) Pia, Epafrodito, Mukristo mumoya wa wakati wa mitume mwenye alikuwa Filipi, ‘alishuka moyo juu [marafiki wake] walisikia kama alikuwa mugonjwa.’ (Flp. 2:25-27) Juu siye na wengine hatukamilike, ile inaweza kufanya tukuwe na matatizo yenye inaweza kuwa nguvu kuvumilia. Inawezekana Wakristo ao watu wa familia wakose kuelewana. Lakini, wale wenye wanafuata mashauri ya Neno ya Yehova wanaweza kuvumilia na kushinda hali za vile.—Eze. 2:3-5; 1 Ko. 9:27; 13:8; Kol. 3:12-14; 1 Pe. 4:8.
ENDELEA KUBAKIA MUAMINIFU
20 Tunapaswa kushikamana sana na Yesu Kristo, juu ni yeye njo Yehova ameweka kuwa Kichwa ya kutaniko. (Kol. 2:18, 19) Ni lazima tutumike karibu sana na pamoya na “mutumwa muaminifu na mwenye busara,” na wale wenye wamewekwa kuwa waangalizi. (Ebr. 13:7, 17) Wakati tunatii kabisa mipango ya kiteokrasi na kuunga mukono wale wenye kuongoza, tutakuwa tayari kufanya mapenzi ya Yehova. Ni jambo ya lazima tutumie sana pendeleo yetu ya kusali kwa Yehova. Ukumbuke kama, ikuwe gereza ao kasho, haiwezi kukuzuia kuzungumuza na Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo ao kuharibisha umoja wenye uko kati yetu na waabudu wenzetu.
21 Kwa hiyo basi, tuendelee kuvumilia na kuazimia kufanya kazi yenye Yesu aliachia wanafunzi wake kisha kufufuliwa; aliwaambia hivi: “Kwa hiyo, muende, na mufanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, na muwabatize katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na muwafundishe kushika mambo yote yenye nimewaamuru ninyi.” (Mt. 28:19, 20) Tuendelee kuvumilia majaribu sawa vile Yesu. Tuendelee kuweka mu akili yetu tumaini ya Ufalme na tumaini ya uzima wa milele. (Ebr. 12:2) Juu tuko wanafunzi wa Kristo wenye kubatizwa, tuko na pendeleo ya kusaidia kutimiza unabii wa Yesu wenye unahusu “umalizio wa mupangilio wa mambo.” Alisema hivi: “Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote yenye kuikaliwa na watu ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na kisha ule mwisho utakuja.” (Mt. 24:3, 14) Kama mu hii kipindi, tunafanya kazi ya kuhubiri kwa moyo wetu wote, tutakuwa na furaha ya kupata uzima wa milele mu dunia mupya ya Yehova yenye haki!