56
Yosia Alipenda Sheria ya Mungu
Yosia aliwekwa kuwa mufalme wa Yuda wakati alikuwa na miaka munane. Ile wakati, watu walikuwa wanafanya uchawi na kuabudu sanamu. Wakati Yosia alikuwa na miaka 16, alianza kujifunza namna ya kumuabudu Yehova mu njia ya muzuri. Wakati alikuwa na miaka 20, alianza kuharibu sanamu na mazabahu mu inchi yote. Kisha, wakati alikuwa na miaka 26, alifanya mipango juu hekalu la Yehova litengenezwe.
Hilkia, kuhani mukubwa, alipata kitabu cha kukunjwa cha Sheria ya Yehova mu hekalu. Pengine njo kitabu cha kukunjwa chenye Musa aliandikaka. Shafani, mwandishi wa mufalme, alipelekea Yosia kile kitabu cha kukunjwa na akaanza kusoma Sheria kwa sauti kubwa. Wakati Yosia alikuwa anasikiliza, alitambua kama watu walikuwa wamemuasi Yehova kwa miaka mingi. Mufalme Yosia akaambia Hilkia: ‘Yehova ametukasirikia sana. Uende umuulize kama tufanye nini.’ Yehova akajibu kupitia Hulda, nabii mwanamuke, akasema hivi: ‘Watu wa Yuda wameniacha. Watapata malipizi lakini hapana wakati wa utawala wa Yosia, kwa sababu yeye amejinyenyekeza.’
Wakati Mufalme Yosia alisikia vile, akaenda ku hekalu na kukusanya watu wa Yuda. Kisha akasoma Sheria ya Yehova kwa sauti kubwa mbele ya taifa lote. Yosia na watu wote wakatoa ahadi kama watamutii Yehova kwa moyo wao wote.
Miaka mingi ilikuwa imepita bila taifa la Yuda kufanya Pasaka. Lakini wakati Yosia alisoma katika Sheria kama Pasaka ilipaswa kufanywa kila mwaka, akaambia hivi taifa lote: ‘Tutamufanyia Yehova Pasaka.’ Kisha Yosia akatayarisha zabihu mingi na akapanga kukuwe waimbaji ku hekalu. Taifa lote likafanya Pasaka, kisha wakafanya Sikukuu ya Keki Zenye Hazina Chachu yenye ilifanya siku saba. Pasaka kama ile ilikuwa haijafanyika tangu wakati wa Samweli. Yosia alipenda sana Sheria ya Mungu. Na wewe, unapendaka kujifunza juu ya Yehova?
“Neno lako ni taa ya muguu wangu, na mwangaza wa njia yangu.”—Zaburi 119:105