Chunguzeni neno la Yehova kila siku!
1 Kila siku huweka mbele yako miito mipya ya kushindania imani. Labda mtu wa ulimwengu unayejuana naye anaendelea kukusonga ili kwenda kwenye mkutano kati ya watu wa jinsia tofauti. Mwalimu wako anataka ufuatie kazi-maisha ya kimwili, au mkubwa wako wa kazi anataka utumike kwa saa ndefu zaidi. Afya yako ya kimwili inaweza kuwa yenye kushuka. Ijapokuwa unaweza kupambana na majaribu hayo wakati wowote, wewe si peke yako. Yehova yuko tayari kukupa hekima inayohitajiwa ili kukabiliana na majaribu hayo. Kuchunguza andiko la Biblia na maelezo katika Kuyachunguza Maandiko Kila Siku ni njia moja ambayo katika hiyo unaweza kutwaa Neno la Yehova kikawaida. Je! unafaidika na uandalizi huo?
2 Msaada unapatikana: Isaya 30:20 linamweleza Yehova kuwa ‘Mwalimu Mtukufu’ ambaye watu wa Mungu wanaweza kuendea ili kupata msaada. Yeye anakuandalia kile unachohitaji ili kupambana na miito ya kushindania imani yako. Namna gani? Mstari wenye kufuata unafasiria: “Masikio yako yatasikia neno nyuma yako, likisema: ‘Njia ni hii, mwifuate.’ ” Leo, Yehova hutuma “neno” lake kupitia Maandiko na vichapo vya “mtumwa mwaminifu.” (Mt. 24:45) Kuna utajiri wa hekima katika makala ya zamani ya Mnara wa Mlinzi pekee, makala yenye kugusa karibu kila upande wa maisha ya Kikristo. Kurudilia yale ambayo hutajwa katika Kuyachunguza Maandiko kunakusaidia kujenga akiba ya ujuzi ulio wenye thamani katika kushughulika na majaribu ya kila aina.—Isa. 48:17.
3 Panga wakati kwa ajili ya hilo: Ingawa asubuhi zilikuwa wakati wenye shughuli sana, mama mmoja alijitahidi kuufanya huo uwe wakati wa kusoma na kuzungumzia andiko na maelezo pamoja na mwana wake wakati huyo alipokuwa akila chakula cha asubuhi. Maneno hayo pamoja na sala yalikuwa maneno ya mwisho ambayo mwana huyo alisikia kila asubuhi kabla ya kuondoka kwenda shuleni. Hayo yalimtia nguvu ili kupinga mapendekezo ya kingono, kuchukua msimamo usiokubali mabaya wakati alipokabiliana na utukuzo wa taifa, na kutoa ushahidi wenye uhodari kwa wanafunzi na walimu pia. Ingawa alikuwa Shahidi pekee kwenye shule hiyo, hakujisikia kamwe akiwa peke yake.
4 Mwendee Yehova na Neno lake ili upate mwelekezo na mwongozo. Ikiwa unafanya hivyo, yeye atakuwa halisi kwako, kama vile rafiki mwenye kutumainika. Mwendee yeye kila siku! Pamoja na mamilioni ya wengine ulimwenguni pote ambao huchunguza Neno la Mungu kila siku, macho yako na yawe ‘macho yenye kuona Mwalimu wako Mtukufu.’