Ni Jambo Gani Unalotanguliza?
1 Matengenezo mengi ya kidini yanatia mkazo juu ya kufanya kazi za kutoa misaada, kama vile kuandaa majengo kwa ajili ya elimu ya kimwili au mahitaji ya kiganga. Hata hivyo, ingawa Mashahidi wa Yehova hawasahau “kule kutenda mema na kule kushiriki vitu pamoja na wengine,” wanatanguliza kusaidia watu kiroho.—Ebr. 13:16.
2 Mfano wa Karne ya Kwanza: Yesu alifanya kazi nyingi nzuri wakati wa huduma yake duniani, lakini kazi yake kubwa ilikuwa ile ya kutoa ushahidi juu ya ile kweli. (Luka 4:43; Yn. 18:37; Mdo. 10:38) Aliamuru wafuasi wake ‘waende wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwafundisha.’ (Mt. 28:19, 20) Na alionyesha kwamba wale wanaozoea imani katika yeye wangefanya kwa kiwango kikubwa zaidi kazi aliyokuwa ameianzisha. (Yn. 14:12) Yesu alitanguliza kazi ya kuhubiri kwa kuwa inasaidia watu wajifunze njia ya wokovu.—Yn. 17:3.
3 Mtume Paulo aliona kazi yake ya kuhubiri kuwa “sharti,” takwa ambalo hangeweza kupuuza. (1 Kor. 9:16, 17) Alikuwa tayari kujinyima jambo lolote lile, kuvumilia jaribu lolote, au kupata shida yoyote ili kutimiza huduma yake. (Mdo. 20:22-24) Mtume Petro na washiriki wenzake walionyesha mtazamo huohuo. Hata walipotupwa gerezani na kupigwa, ‘waliendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’—Mdo. 5:40-42.
4 Namna gani sisi? Je, tunatanguliza kazi ya kutangaza habari njema ya Ufalme na kufanya wanafunzi? Kama Yesu, je, tunahangaikia kikweli wale walio wenye ‘kuchunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji’? (Mt. 9:36) Matukio ya sasa ya ulimwengu na unabii wa Biblia unaonyesha waziwazi kwamba mwisho wa mfumo huu mbovu utatukia karibuni! Kukazia akilini umaana wa kazi ya kuhubiri kutatuchochea tuendelee kuhubiri kwa bidii.
5 Kadiria Hali Zako: Kwa kuwa hali za watu hubadilika mara kwa mara, ni vizuri kuona pindi kwa pindi ikiwa tunaweza kufanya marekebisho ili kushiriki kikamili zaidi katika kazi ya kuhubiri. Dada mmoja alikuwa amepainia alipokuwa katika miaka ya 50, 60, na 70 lakini akaona kuwa jambo la lazima kusimamisha upainia wa kawaida kwa sababu ya afya mbaya. Lakini, baadaye, afya yake ikakuwa bora. Karibuni alikadiria upya hali yake, na akaamua kwamba angeweza kupainia tena. Alikuwa mwenye furaha kama nini kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia akiwa na umri wa miaka 90! Namna gani wewe? Je, unakaribia kupewa pensheni kazini au kumaliza shule? Hali yako itakapobadilika, je, utakuwa na uwezo wa kupainia?
6 Yesu alipoona kwamba Martha “alivutwa fikira kwa kushughulikia kazi nyingi,” alimshauri kwa upole kwamba angepata baraka kubwa zaidi ikiwa angefanya mambo kuwa mepesi. (Luka 10:40-42) Je, unaweza kufanya maisha yako kuwa mepesi? Je, ni jambo la lazima kweli kwa mume na mke kufanya kazi ya kimwili? Ikiwa marekebisho yanafanywa, je, familia inaweza kuishi kwa kutegemea mshahara wa mtu mmoja? Wengi wamefaidika kiroho kwa kufanya marekebisho ili kushiriki zaidi katika huduma.
7 Sisi sote na tufuate mfano waliotuachia Yesu na mitume! Tunaweza kuwa hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kweli za kushiriki kikamili katika ile kazi ya maana ya kuhubiri habari njema ya Ufalme.—Luka 9:57-62.