Huduma ya Kikristo—Kazi Yetu Kubwa
1 Sisi sote tuna aina mbalimbali za kazi tunazopaswa kufanya. Kuandalia washiriki wa nyumba ya mtu ni takwa la kimungu. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, kazi inayohusika katika takwa hilo la kimungu haipaswi kuwa ya maana zaidi kuliko kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi.—Mt. 24:14; 28:19, 20.
2 Yesu alitutolea mfano wa kufuata katika “kutafuta kwanza ufalme.” (Mt. 6:33; 1 Pet. 2:21) Ingawa hakuwa na vitu vingi vya kimwili, alijitoa kikamili katika kufanya mapenzi ya Baba yake. (Luka 4:43; 9:58; Yn. 4:34) Alijitahidi kutoa ushahidi kila wakati nafasi ilipojitokeza. (Luka 23:43; 1 Tim. 6:13) Alihimiza wanafunzi wake pia wapendezwe sana na kazi ya mavuno.—Mt. 9:37, 38.
3 Kumwiga Yesu Leo: Tunaweza kuiga mfano wa Yesu kwa kujitahidi kuishi maisha mepesi ambayo yanategemea huduma ya Kikristo. Ikiwa tuna mambo ya lazima maishani, acheni tutii shauri la Biblia la kutoendelea kujipatia zaidi na zaidi mali ya ulimwengu huu. (Mt. 6:19, 20; 1 Tim. 6:8) Ni jambo bora zaidi kama nini kutafuta kupanua ushiriki wetu katika kazi ya kuhubiri! Tunapopambana na hali ngumu, na tujitahidi kama alivyofanya Yesu; tusiruhusu mahangaiko ya maisha yawe ya maana zaidi kuliko kazi yetu kubwa ya kutangaza habari njema ya Ufalme.—Luka 8:14; 9:59-62.
4 Hata wale walio na madaraka mengi wanatanguliza kazi ya kuhubiri. Ndugu mmoja aliye na familia kubwa, aliye na madaraka kazini, na anayetumikia akiwa mzee katika kutaniko la Kikristo anasema: “Ninaona huduma kama kazi-maisha yangu.” Dada mmoja painia anasema: “Kupainia ni bora zaidi sana kuliko kazi-maisha ya kimwili yenye mafanikio.”
5 Na tufuate mfano wa Yesu, hata hali zetu ziweje. Jinsi gani? Kwa kufanya huduma ya Kikristo iwe kazi yetu kubwa.