Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 10: Kuzoeza Wanafunzi Katika Huduma ya Nyumba kwa Nyumba
1 Wakati ambapo wazee wanaamua kwamba mwanafunzi wa Biblia anastahili kuwa mhubiri asiyebatizwa, anaweza kuanza kushiriki pamoja na kutaniko katika kazi ya kuhubiri waziwazi. (Ona kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Mapenzi ya Yehova, uku. 79-81.) Tunawezaje kusaidia mwanafunzi apambane na tatizo la kuhubiri nyumba kwa nyumba?
2 Kutayarisha Pamoja: Kujitayarisha vizuri ndilo jambo la maana. Onyesha mwanafunzi mahali anapoweza kupata utoaji uliopendekezwa katika Huduma Yetu ya Ufalme na katika kitabu Kutoa Sababu, na umsaidie kuchagua utangulizi ulio rahisi na wenye kufaa eneo lenu. Kuanzia mwanzo, mtie moyo kukazia Biblia katika huduma yake.—2 Tim. 4:2.
3 Vipindi vya mazoezi ni vya lazima kwa mhubiri mpya. Mwanafunzi anavyojizoeza utoaji, umwonyeshe jinsi ya kushughulikia kwa busara hali mbalimbali ambazo ni za kawaida katika eneo. (Kol. 4:6) Umhakikishie kwamba wahudumu Wakristo hawahitaji kujua jibu kwa kila ulizo ambalo mwenye nyumba anaweza kutokeza. Mara nyingi ni vizuri zaidi kujibu kwamba utafanya utafiti na kurudia kuzungumzia jambo hilo baadaye.—Met. 15:28.
4 Kuhubiri Pamoja: Mara ya kwanza mwanafunzi anaposhiriki katika huduma ya nyumba kwa nyumba, umwache atazame jinsi unavyotoa utangulizi ambao ninyi wawili mlitayarisha pamoja. Kisha umwombe ashiriki. Katika visa fulani, inaweza kuwa jambo nzuri zaidi kumwomba mhubiri mpya ashiriki tu sehemu fulani ya utoaji, kama vile kusoma na kutoa maelezo kuhusu andiko fulani. Ufikirie utu na uwezo wa mwanafunzi. (Flp. 4:5) Umpongeze sana kadiri unavyoendelea kumzoeza katika sehemu mbalimbali za kazi ya kuhubiri.
5 Ni jambo la maana kusaidia mhubiri mpya ajiwekee programu ya kawaida ya kushiriki katika huduma, afanye hivyo kila juma ikiwezekana. (Flp. 3:16) Fanyeni mipango kamili ili kufanya kazi pamoja katika utumishi, na umtie moyo kutumika pamoja na wahubiri wengine wenye bidii pia. Mfano wao na ushirika wao vitamsaidia kukuza ufundi na kupata furaha katika kuhubiri nyumba kwa nyumba.