Kuongoza Mafunzo ya Biblia Yenye Maendeleo
Sehemu 11: Kusaidia Wanafunzi Kufanya Ziara za Kurudia
1 Mwanafunzi wa Biblia anapoanza kushiriki katika kazi ya kuhubiri, atakutana na watu wanaoonyesha kupendezwa na habari njema. Tunawezaje kusaidia mhubiri mpya kufanya ziara za kurudia zenye matokeo na kusitawisha kupendezwa kwa watu anaokutana nao?
2 Kujitayarisha kwa ajili ya ziara ya kurudia kunaanza wakati wa ziara ya kwanza. Mtie moyo mwanafunzi apendezwe kwa unyofu na wale anaozungumza nao. (Flp. 2:4) Hatua kwa hatua umzoeze mhubiri mpya kuomba watu anaozungumza nao watoe mawazo yao, asikilize maelezo yao, na kutambua mambo yanayowahangaisha. Mtu fulani anapoonyesha kupendezwa, mwombe mhubiri mpya aandike habari ya maana kuhusu ziara hiyo. Tumia habari hiyo ili kumsaidia afanye mpango kwa ajili ya mazungumzo zaidi.
3 Kujitayarisha kwa Ajili ya Ziara ya Kurudia: Chunguzeni maandishi ya ziara ya kwanza, na umwonyeshe mwanafunzi jinsi ya kuchagua jambo fulani linalohusiana na ujumbe wa Ufalme litakalovutia mwenye nyumba. (1 Ko. 9:19-23) Tayarisheni pamoja utoaji mfupi unaokazia andiko moja la Biblia pamoja na fungu moja katika kichapo cha funzo. Zaidi ya hilo, tayarisheni ulizo moja mnaloweza kutokeza kwenye umalizio wa mazungumzo ili kuweka msingi kwa ajili ya ziara ijayo. Mwonyeshe mhubiri mpya ajue jinsi ya kuongeza ujuzi wa mtu wa Neno la Mungu kwenye kila ziara.
4 Ni jambo lenye kusaidia pia kufundisha mwanafunzi utangulizi ulio rahisi. Baada ya kusalimia mwenye nyumba, anaweza kusema hivi: “Nilifurahia maongezi yetu yaliyotangulia, na nimerudi ili kuzungumza nawe habari nyingine ya Biblia kuhusu [taja habari].” Huenda ukahitaji pia kuonyesha mhubiri mpya jinsi ya kusema ikiwa mnakuta mtu tofauti na yule mliyeagana naye.
5 Kufuatia Kupendezwa Kwa Bidii: Mtie moyo mwanafunzi kuonyesha mfano mzuri kwa kurudilia bila kukawia watu wote wanaoonyesha kupendezwa. Kupata watu nyumbani labda kunaomba uvumilivu kwa kuwarudilia. Mfundishe mwanafunzi jinsi ya kufanya mipango ili kurudilia tena watu, na umsaidie kuelewa uhitaji wa kuwarudilia kama alivyowaahidi. (Mt. 5:37) Mzoeze mhubiri mpya kuwa mwenye fadhili, mwenye kufikiria wengine, na mwenye heshima anapotafuta watu wenye mfano wa kondoo na kusitawisha kupendezwa kwao.—Tito 3:2.