Uwe Mhubiri Mwenye Kufanya Maendeleo
1 Baba yetu wa mbinguni anafurahi watumishi wake wanapofanya maendeleo ya kiroho. Maendeleo hayo yanahusisha kuwa mhubiri wa habari njema mwenye kukomaa kiroho na mwenye matokeo. Paulo alimtia moyo mwangalizi Timotheo aendelee kufanya bidii ili maendeleo yake yawe wazi. (1 Tim. 4:13-15) Hata ikiwa kuna wahubiri wenye uzoefu kati yetu, sisi wote tunapaswa kujikaza kufanya kazi yetu ya kuhubiri iwe yenye matokeo zaidi.
2 Jiwekee Miradi: Ili kufanya maendeleo, inaomba kujiwekea miradi. Ni miradi gani ambayo tunaweza kujiwekea? Tunaweza kujaribu kuwa wenye ufundi zaidi katika kutumia upanga wa kiroho, Biblia. (Efe. 6:17) Labda tunahitaji kufanya maendeleo katika sehemu fulani ya kazi yetu ya kuhubiri, kama vile kuhubiri barabarani, kuhubiri kwa njia ya telefone ao kuhubiri katika eneo la biashara. Labda tunaweza kusaidia zaidi watu tunaorudilia ili wafanye maendeleo. Mradi mwingine mzuri zaidi unaweza kuwa kufanya maendeleo zaidi katika kuanzisha na kuongoza mafunzo ya Biblia.
3 Mipango ya Kukusaidia: Mikutano ya kutaniko, zaidi sana Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi, imepangwa ili kutusaidia kufanya maendeleo katika kazi ya kuhubiri. Kadiri tunavyojikaza zaidi kutayarisha na kuhuzuria mikutano hiyo na kutumia mashauri yanayotolewa huko, ndivyo tutakavyofaidika kabisa.—2 Kor. 9:6.
4 Tunahitaji pia kusaidiana kufanya maendeleo. (Met. 27:17) Kufuata kwa uangalifu utoaji wa yule tunayehubiri naye kutatusaidia kufanya maendeleo zaidi. Pia, mwangalizi wetu wa funzo la kitabu anaweza kufanya mpango ili kutolea kila mmoja wetu msaada. Ni baraka kubwa sana kutolewa msaada na painia ao mhubiri mwenye uzoefu ili tuwe wenye matokeo zaidi na kupata furaha katika kazi ya kuhubiri. Je, kuna mhubiri mpya katika kikundi chetu cha funzo la kitabu? Labda tunaweza kufanya mpango ili kuhubiri naye.
5 Utumishi wa Kikristo ndiyo kazi ya maana zaidi inayofanywa leo. Tunapomtolea Yehova ‘zabihu yetu ya sifa,’ tunataka kumtolea kilicho bora zaidi. (Ebr. 13:15) Ikiwa tunajikaza kufanya maendeleo katika kazi ya kuhubiri, tutakuwa wafanyakazi ‘wasio na lolote la kuonea aibu, tukilitumia sawasawa neno la kweli.’—2 Tim. 2:15.