Jiwekee Miradi ya Kiroho
1 Litakuwa pendeleo kama nini kumsifu Yehova kwa umilele wote! Ili kutusaidia tufikie mradi huo, tunaweza sasa kujiwekea miradi ya kiroho na kujitahidi kuifikia. Jambo hilo litatuwezesha kutumia nguvu zetu kwa hekima. (1 Kor. 9:26) Ni miradi gani ambayo ingekuwa yenye kufaa kwako?
2 Funzo la Biblia: Je, unajitayarisha kwa ajili ya kila mkutano wa kutaniko? Ikiwa ndiyo, je, unachukua wakati wa kufanya utafiti na kutafakari unapojifunza? Kwa mfano, unapojitayarisha kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la kila juma, je, unapiga kistari tu chini ya majibu au unatafuta maandiko yaliyotajwa na kutafakari sababu zilizochochea maelezo yaliyotolewa? Je, unaweza kujiwekea mradi wa kufanya utafiti juu ya mawazo machache kila juma kutokana na mgawo uliotolewa wa usomaji wa Biblia kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Utafiti kama huo kuhusu mambo ya kiroho unaomba wakati na jitihada, lakini unathawabisha sana.—Mez. 2:4, 5.
3 Mikutano ya Kutaniko: Mradi mwingine ni kuhudhuria kwa ukawaida mikutano yote mitano ya kutaniko. Kufika mapema vya kutosha ili kushirikiana na waamini wenzetu na kushiriki wimbo na sala ya kufungua kunasaidia katika kutia nguvu hali ya kiroho ya kutaniko. Tunaweza pia kujitahidi kutoa maelezo kwenye kila mkutano na kujaribu kuboresha maelezo yetu. Labda unaweza kuonyesha jinsi andiko katika fungu linavyopatana na mazungumzo au kuonyesha jinsi habari inayozungumziwa inavyotumika katika maisha ya kila siku.—Ebr. 10:24, 25.
4 Utumishi wa Shambani: Huduma yetu inakuwa bora zaidi tunapojiwekea miradi. Je, una mradi wako binafsi wa saa ambazo unapanga kupitisha katika utumishi kila mwezi? Wengi wanaona hilo kuwa jambo lenye kusaidia. Au je, unaweza kuboresha sehemu fulani ya huduma yako, kama vile kutumia Biblia katika utendaji wa nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia zenye matokeo zaidi, kujitahidi kuanzisha funzo la Biblia, au kufundisha kwa matokeo zaidi unapoongoza mafunzo za Biblia?
5 Enyi wazazi, je, mnatia watoto wenu moyo ili wajiwekee miradi katika utumishi wa Yehova? Wasaidieni waone kwamba kutumikia kama painia, mishonari, au mshiriki wa familia ya Betheli ni njia bora kabisa ya kuonyesha kina cha uthamini wao kuelekea Yehova.—Mhu. 12:1.
6 Tunapochunguza utendaji wetu mbalimbali, tunapojiwekea miradi ya kiroho, na tunapojitahidi kuifikia, tutapata furaha kubwa zaidi katika utumishi wetu na kuwa chanzo cha kitia-moyo kwa wengine.—Rom. 1:12.