“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
1. Tutajifunza kitabu gani kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko kuanzia juma tokea tarehe 14 mwezi wa 3?
1 Kuanzia juma tokea tarehe 14 mwezi wa 3, 2011, tutajifunza kitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko katika Cibemba, Kifaransa, Kiingereza, na Kiswahili. Kitabu hiki kinazungumzia kitabu cha Matendo kwa njia inayomfanya msomaji aone akilini namna matukio mbalimbali yalivyofuatana; matukio yanayoelezwa katika kitabu hicho. Kitabu Kutoa Ushahidi hakifasirie kitabu cha Matendo mstari kwa mstari, lakini kinazungumzia mambo mbalimbali tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi ya kitabu hicho na kutusaidia kuona jinsi tunavyoweza kuyatumia maishani.—Rom. 15:4.
2. Eleza mambo fulani yaliyo katika kitabu Kutoa Ushahidi.
2 Mambo Mbalimbali Yaliyo Katika Kitabu Hicho: Utangulizi wa kitabu hicho ulio kwenye ukurasa wa 2 ni barua yenye kuchangamsha kutoka Baraza Linaloongoza inayoeleza jinsi ndugu walio katika baraza hilo wanataka tufaidike na kitabu hicho. Kuanzia sura ya 2, kuna maelezo mafupi yanayoonyesha mambo yanayozungumziwa katika kila sura na andiko linaloonyesha sehemu ya kitabu cha Matendo ambayo sura hiyo inazungumzia. Sura nyingi zina visanduku vinavyotoa habari za ziada kuhusu watu, mahali, na matukio yanayotajwa katika kitabu cha Matendo. Tunaweza kutumia nafasi za pembeni zilizo wazi ili kuandika mambo ya maana. Kitabu hicho kina picha nzuri zinazoeleza masimulizi fulani ya Biblia, ili kutusaidia kuona akilini matukio ya maana, na kwenye ukurasa wa mwisho kuna fahirisi (index) ya picha inayotoa maelezo kuhusu picha mbalimbali zilizo katika kitabu. Kwenye ukurasa wa ndani wa jalada ya mbele na ya nyuma kuna ramani (cartes) ili kutusaidia kuona akilini mahali ambapo waabudu wenzetu wa karne ya kwanza walipita walipokuwa wakieneza habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Mdo. 1:8.
3. Kujifunza kitabu cha Matendo kutatusaidia tupate majibu kwa maulizo gani ya maana?
3 Majibu kwa Maulizo ya Maana: Kujifunza kitabu cha Matendo kutatusaidia tupate majibu kwa maulizo ya maana yanayohusu kazi ya kuhubiri. Kwa mfano, ni kazi gani na ujumbe gani unaotambulisha wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo? Ni nani anayeongoza kazi hiyo ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote, na anafanya hivyo namna gani? Mateso na upinzani vinatolea wahubiri nafasi ya kufanya nini? Roho takatifu ina daraka gani katika kazi yetu ya kuhubiri?
4. Namna gani tunaweza kufaidika kabisa na funzo la kitabu hiki?
4 Ili tufaidike kabisa, tujifunze habari mbele ya wakati na tujitayarishe kutoa majibu tunapozungumzia habari hiyo katika kutaniko. Tuhuzurie kila funzo, na tufikirie jinsi tunavyoweza kutumia mambo tuliyojifunza katika kazi yetu ya kuhubiri. Funzo la kitabu hiki chenye kupendeza na lituchochee kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu!—Mdo. 28:23.