Namna ya Kugusa Mioyo ya Watu wa Jamaa Wasio Mashahidi
YESU KRISTO alipokuwa akizungumuza na mutu mumoja aliyetaka kuwa mufuasi wake, alimwambia hivi: “Nenda nyumbani kwa watu wa jamaa yako, ukawaambie mambo yote ambayo Yehova amekufanyia na jinsi alivyokuonyesha rehema.” Pengine wakati huo alikuwa huko Gadara, muji ambao ulikuwa kusini mashariki mwa Bahari ya Galilaya. Maneno ya Yesu yanaonyesha kwamba alielewa tabia ya kawaida ya wanadamu, ni kusema, tamaa ya kila mwanadamu ya kuelezea watu wa jamaa yake mambo yanayomupendeza.—Mk. 5:19.
Mara nyingi tunajionea jambo hilo leo, lakini watu wa mahali fulani wanaonyesha tabia hiyo zaidi kuliko wengine. Kwa kweli, mutu anapoanza kumuabudu Mungu wa kweli, Yehova, anatamani kila mara kuelezea watu wa jamaa yake kuhusu mambo mapya anayojifunza. Lakini anapaswa kufanya hivyo namna gani? Namna gani anaweza kugusa mioyo ya watu wa jamaa walio katika dini nyingine, na hata wale wasiokuwa na dini? Biblia inatoa mashauri mazuri.
‘TUMEMUPATA MASIYA’
Katika siku za Yesu, Andrea alikuwa mumoja wa wale ambao walikuwa wa kwanza kumutambua Masiya. Unajua ni nani ambaye alielezea mara moja habari hiyo? “Huyu [Andrea] alimupata ndugu yake mwenyewe, Simoni, na kumuambia: ‘Tumemupata Masiya’ (ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, ‘Kristo’).” Andrea alimupeleka Petro kwa Yesu, kwa kufanya hivyo alimutolea nafasi ya kuwa mumoja wa wanafunzi wa Yesu.—Yoh. 1:35-42.
Miaka sita hivi baadaye wakati Petro alikuwa katika Yopa, alialikwa kuenda kaskazini mwa Kaisaria ili kumutembelea Kornelio, mukubwa wa jeshi. Ni nani ambao Petro alikuta wamekusanyika katika nyumba ya Kornelio? “Kornelio alikuwa akiwatarajia [Petro na wale waliosafiri pamoja naye] naye alikuwa amewaita pamoja jamaa zake na rafiki zake wa karibu sana.” Kwa njia hiyo, Kornelio alitolea watu wa jamaa yake nafasi ya kumusikiliza Petro na kufanya uamuzi kutokana na yale ambayo walisikia.—Mdo. 10:22-33.
Namna ambavyo Andrea na Kornelio walitendea watu wa jamaa zao inatufundisha nini?
Andrea na Kornelio hawakuacha mambo yajiongoze yenyewe. Andrea mwenyewe alimupeleka Petro kwa Yesu, na Kornelio alifanya mipango ili watu wa jamaa yake waje kumusikiliza Petro. Lakini Andrea na Kornelio hawakuwakaza watu wa jamaa zao ao kutumia ujanja fulani ili kuwageuza kuwa wafuasi wa Kristo. Je, hilo linatufundisha somo fulani? Ni vizuri tuwaige. Tunaweza kuelezea watu wa jamaa zetu mawazo fulani ya Biblia na kufanya mipango ili wajifunze kweli za Biblia na Mashahidi wenzetu. Lakini, tunapaswa kuheshimu uhuru wao wa kuchagua na kuepuka kuwasumbua-sumbua. Mufano wa Jürgen na Petra, ambao ni bibi na bwana wa huko Ujerumani, unaonyesha namna tunaweza kusaidia watu wa jamaa zetu.
Petra alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na baadaye alibatizwa. Bwana yake, Jürgen, alikuwa mukubwa katika jeshi. Mwanzoni, Jürgen hakufurahia uamuzi wa bibi yake. Lakini, kisha muda fulani, alitambua kwamba Mashahidi wanafundisha kweli. Yeye pia alijitoa kwa Yehova na kubatizwa, na leo ni muzee katika kutaniko la kwao. Ni shauri gani ambalo anatoa kuhusu namna ya kugusa moyo wa mutu wa jamaa aliye katika dini nyingine?
Jürgen anasema hivi: “Hatupaswe kuwakaza ao kuwahubiria-hubiria kila wakati. Kufanya hivyo kunaweza kupunguza hamu yao ya kujifunza Biblia. Kadiri wakati unavyopita, ni vizuri zaidi kuwaelezea mara kwa mara mambo machache kwa busara. Ni vizuri pia kusaidia watu wa jamaa zetu wafahamiane na ndugu na dada wa miaka yao na walio na mapendezi kama yao. Kufanya hivyo kunaweza kusaidia sana.”
“Hatupaswe kuwakaza ao kuwahubiria-hubiria kila wakati.”—Jürgen
Mutume Petro na watu wa jamaa ya Kornelio walikubali mara moja ujumbe wa Biblia. Lakini watu wengine wa wakati wa mitume walihitaji wakati zaidi ili kuchukua uamuzi kuhusu mafundisho ambayo walikuwa wamesikia.
NDUGU ZA YESU WALIITIKIA NAMNA GANI?
Yesu alipokuwa akihubiri, watu wengi wa jamaa yake walimuamini. Kwa mufano, inaonekana kwamba mitume Yakobo na Yohana walikuwa binamu wa Yesu na kwamba mama yao, Salome, alikuwa shangazi yake. Pengine Salome alikuwa mumoja wa “wanawake wengine wengi, waliokuwa wakiwahudumia [Yesu na mitume] kwa mali zao.”—Lu. 8:1-3.
Lakini, watu wengine wa jamaa ya Yesu hawakumuamini mara moja. Kwa mufano, mwaka mumoja kisha Yesu kubatizwa, watu wengi walikusanyika katika nyumba moja ili kumusikiliza. “Lakini watu wa jamaa yake waliposikia juu ya hilo, wakatoka kwenda kumushika, kwa maana walikuwa wakisema: ‘Amerukwa na akili.’” Kisha muda fulani, ndugu za Yesu walimuuliza kuhusu mipango yake ya kusafiri, lakini hakuwajibu waziwazi. Sababu gani? Kwa sababu ‘kwa kweli, ndugu zake walikuwa hawamuamini.’—Mk. 3:21; Yoh. 7:5.
Namna ambavyo Yesu aliwatendea watu wa jamaa yake inatufundisha nini? Hakukasirika wakati wengine walisema kwamba alikuwa amepoteza akili. Hata kisha kifo na ufufuo wake, Yesu alitolea watu wa jamaa yake kitia-moyo zaidi kwa kumutokea ndugu yake Yakobo. Kisha Yesu kumutokea Yakobo, yeye na ndugu wengine wa Yesu waliamini kabisa kwamba Yesu ndiye Masiya. Kwa hiyo, walikuwa pamoja na mitume na wengine katika chumba cha juu huko Yerusalemu na ni wazi kwamba walipokea roho takatifu. Baadaye, Yakobo na Yuda, ndugu mwingine wa Yesu, waliendelea kufurahia mapendeleo mengine mazuri.—Mdo. 1:12-14; 2:1-4; 1 Kor. 15:7.
WENGINE WANAHITAJI WAKATI WA KUTOSHA
“Unaweza kupata matokeo mazuri ikiwa unaendelea kuvumilia kabisa.”—Roswitha
Kama ilivyokuwa wakati wa mitume, watu fulani wa jamaa wanahitaji wakati wa kutosha ili waikubali kweli. Tuchukue mufano wa dada Roswitha, aliyekuwa Mukatoliki wa sana wakati bwana yake alibatizwa na kuwa mumoja wa Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 1978. Kwa kuwa aliheshimu sana dini yake, mwanzoni alimupinga bwana yake. Lakini kisha miaka mingi, upinzani wake ulipunguka na alianza kutambua kwamba Mashahidi wanafundisha kweli. Katika mwaka wa 2003, alibatizwa. Ni nini ilisaidia? Bwana yake hakumukasirikia wakati alimupinga mwanzoni, lakini alimutolea Roswitha nafasi za kubadili maoni yake. Bwana yake anatoa shauri gani? “Unaweza kupata matokeo mazuri ikiwa unaendelea kuvumilia kabisa.”
Dada Monika alibatizwa katika mwaka wa 1974, na vijana wake wawili walibatizwa na kuwa Mashahidi miaka kumi baadaye. Hakuna siku ambayo Hans, bwana yake, alipinga imani yake, lakini alikuja kubatizwa kisha miaka mingi, katika mwaka wa 2006. Kisha kujionea jambo hilo, ni shauri gani ambalo dada Monika anatoa? Yeye anasema hivi: “Shikamana sana na Yehova, na usiikane imani yako.” Bila shaka, lilikuwa jambo la lazima amuhakikishie kila mara Hans kwamba wanaendelea kumupenda. Na waliendelea kutumaini kwamba siku moja anaweza kukubali kweli.
MAJI YA UKWELI YANABURUDISHA
Siku moja Yesu alilinganisha ukweli na maji yanayotoa uzima wa milele. (Yoh. 4:13, 14) Tunataka watu wa jamaa yetu wakunywe na kuburudishwa na maji ya ukweli yaliyo mazuri na safi. Lakini, hatungependa washindwe kupumua kwa sababu tunawalazimisha wakunywe maji mengi na kwa wakati mumoja. Namna yetu ya kuwaelezea mambo tunayoamini inaweza kuwafanya wajisikie kuwa wenye kuburudishwa ao washindwe kupumua. Biblia inasema kwamba ‘moyo wa mwadilifu unatafakari ili kujibu’ na kwamba ‘moyo wa mutu mwenye hekima unakifanya kinywa chake kionyeshe ufahamu, na kwenye midomo yake anaongeza ushawishi.’ Namna gani tunaweza kutumia mashauri hayo?—Met. 15:28; 16:23.
Pengine bibi anapenda kumuelezea bwana yake mambo anayoamini. Ikiwa ‘anatafakari ili kujibu,’ hilo litamusaidia kuchagua kwa uangalifu maneno yake na hatasema bila kufikiri. Hatajionyesha kuwa mutu muzuri kuliko wengine. Maneno yake yenye hekima yataburudisha na kuendeleza amani. Ni wakati gani unaofaa kabisa ili kuzungumuza na bwana yake? Ni habari gani bwana yake anapenda kuzungumuzia ao kusoma? Je, anapendezwa sana na sayansi, siasa, ao michezo? Namna gani bibi anaweza kumufanya bwana yake apendezwe na Biblia bila kuzarau mawazo na maoni yake? Kufikiria maulizo hayo kutamusaidia bibi aseme na kutenda kwa hekima.
Ili kugusa mioyo ya watu wa jamaa zetu ambao hawajakuwa Mashahidi, haitoshi tu kuwaelezea mambo mengi tunayoamini. Maneno tunayosema yanapaswa kupatana na matendo yetu.
MWENENDO MUZURI
Jürgen ambaye tulizungumuzia hapo juu anasema hivi: “Tumia siku zote kanuni za Biblia katika maisha yako ya kila siku. Hata ikiwa angali na mashaka, hiyo ndiyo njia nzuri zaidi ya kusaidia mutu wa jamaa aone na kutambua kwamba uko katika kweli.” Ndugu Hans, aliyebatizwa miaka 30 hivi kisha bibi yake, anakubaliana na mawazo hayo. Anasema hivi: “Mwenendo muzuri wa Kikristo ni wa maana sana, unamusaidia mutu wa jamaa aone namna kweli imetusaidia sisi wenyewe.” Watu wa jamaa wanapaswa kuona waziwazi kwamba imani yetu inatufanya tuwe tofauti na wengine katika njia fulani nzuri, wala si katika njia zinazowachukiza ao kuwavunja moyo.
“Mwenendo muzuri wa Kikristo ni wa maana sana, unamusaidia mutu wa jamaa aone namna kweli imetusaidia sisi wenyewe.”—Hans
Mutume Petro alitolea wanawake ambao bwana zao si Mashahidi mashauri haya mazuri: ‘Mujitiishe kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa. Na kujipamba kwenu kusiwe kule kusuka nywele kwa inje na kule kujivika mapambo ya zahabu ao kuvaa mavazi ya inje, bali kuwe yule mutu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya samani kubwa machoni pa Mungu.’—1 Pet. 3:1-4.
Petro anaonyesha kwamba bwana anaweza kuvutiwa na mwenendo muzuri wa bibi yake. Kwa kutumia shauri hilo la maandiko dada anayeitwa Christa amekuwa akijaribu kugusa moyo wa bwana yake kupitia mwenendo wake tangu alipobatizwa katika mwaka wa 1972. Hata ikiwa wakati fulani bwana yake alijifunza na Mashahidi, alikuwa hajaamua kufuata kweli. Alikuwa amehuzuria mikutano fulani na alikuwa na uhusiano muzuri pamoja na ndugu na dada wa kutaniko. Ndugu na dada kwa upande wao, waliheshimu uhuru wake wa kuchagua. Lakini, dada Christa alifanya nini ili kugusa moyo wa bwana yake?
Anasema hivi: “Ninaazimia kuendelea kufuata uongozi wa Yehova. Wakati huohuo, ninajikaza kumuvutia bwana yangu ‘bila neno’ kupitia mwenendo wangu muzuri. Ikiwa hakuna jambo linalovunja kanuni za Biblia, ninafanya yote ninayoweza ili kufanya yale anayoniomba. Ninaheshimu uhuru wake wa kuchagua na ninaacha jambo hilo katika mikono ya Yehova.”
Mufano wa dada Christa unaonyesha ulazima wa kuwa mwenye kubadilika kulingana na hali. Ana programe nzuri ya mambo ya kiroho, anahuzuria mikutano kwa ukawaida na kupitisha wakati wa kutosha katika mahubiri. Lakini, yeye ni mwenye busara, anatambua kwamba anapaswa kuonyesha bwana yake upendo, kupitisha wakati pamoja naye na kumuhangaikia. Ni jambo la maana kuwa mwenye kubadilika kulingana na hali na kutenda kwa hekima unaposhugulika na watu wa jamaa wasio Mashahidi. Biblia inaonyesha kwamba “kuna wakati uliowekwa wa kila kitu.” Huo unatia ndani wakati unaopaswa kupitisha pamoja na watu wa familia yako, zaidi sana bibi ao bwana yako asiyekuwa Shahidi. Kupitisha wakati pamoja kunawatolea nafasi ya kuzungumuza. Mambo yaliyoonwa katika familia nyingi yanaonyesha kwamba kuongea na bwana ao bibi yako asiye Shahidi kunamufanya asisikie wivu, asifikiri kwamba iko pekee yake, ao kwamba umemutupilia.—Mhu. 3:1.
USIKATE TUMAINI
Ndugu Holger ambaye baba yake alibatizwa miaka 20 kisha washiriki wengine wa familia, anasema hivi: “Ni jambo la maana tuonyeshe mushiriki wa familia kwamba tunamupenda na kwamba hatukose kusali kwa ajili yake.” Dada Christa anaongezea kwamba ‘ataendelea kutumaini kwamba siku moja bwana yake atajiweka upande wa Yehova na kuikubali kweli.’ Tunapaswa kuendelea kutazamia mema kuhusu watu wa jamaa ambao si Mashahidi.
Tuendelee kuwa na uhusiano muzuri pamoja na watu wa jamaa wasio Mashahidi, tuwatolee nafasi za kuijua kweli, na tuguse mioyo yao kupitia ujumbe wa Biblia. Na katika mambo yote, acheni tufanye hivyo “kwa tabia-pole na heshima kubwa.”—1 Pet. 3:15.