Watchtower—MAKTABA KU ENTERNETE
Watchtower
MAKTABA KU ENTERNETE
Kiswahili (Congo)
  • BIBLIA
  • VICHAPO
  • MIKUTANO
  • Wakati Mutu Mwenye Unapenda Anakufa
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 3
    • Habari Kubwa

      Wakati Mutu Mwenye Unapenda Anakufa

      “Mungu anajua muzuri, mupendwa. . . . U . . . si . . . lie.”

      Mwanamuke mumoja mwenye kuitwa Bebe ndiye aliambiwa maneno hayo kwa sauti ya chini kwenye sikio. Alikuwa kwenye maziko ya baba yake, mwenye alikufa katika aksidenti ya motokari.

      Bebe na baba yake walikuwa wanapendana sana. Bebe aliambiwa maneno hayo na rafiki fulani wa familia yao mwenye nia ya muzuri, lakini maneno hayo yalimuumiza kuliko kumufariji ao kumutuliza moyo. Aliendelea kujiambia hivi: “Kifo chake halikukuwa jambo la muzuri.” Miaka mingi kisha hapo, wakati Bebe alieleza habari hiyo katika kitabu fulani, ni wazi kama alikuwa angali na huzuni nyingi.

      Kama vile Bebe alijionea, inaomba wakati ili kupiganisha huzuni, zaidi sana ikiwa mutu mwenye alifiwa alipendana sana na marehemu. Katika Biblia, kifo kinaitwa kwa kufaa “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Kifo kinatokea na kuvuruga maisha yetu na hakuna kitu chenye kinaweza kukizuia, mara nyingi kinafika wakati hatuko tayari kabisa, na kinatunyanganya watu wenye tulipenda sana. Hakuna mutu mwenye anaweza kuepuka matokeo ya kifo. Kwa hiyo, haishangaze kuona tunajisikia kuwa hatujue la kufanya ili kupambana na kifo na matokeo yake.

      Pengine umekwisha kujiuliza hivi: ‘Inaomba muda gani ili huzuni imalizike? Namna gani mutu anaweza kupiganisha huzuni? Namna gani ninaweza kufariji watu wenye wamefiwa? Kuko tumaini fulani kwa ajili ya watu wenye tunapenda wenye wamekufa?’

  • Ni Mubaya Kuhuzunika?
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 3
    • HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

      Ni Mubaya Kuhuzunika?

      Umekwisha kugonjwa kwa muda mufupi? Pengine ulipona haraka na kusahau kabisa jambo hilo. Lakini, huzuni haiko vile. Musomi Alan Wolfelt anaandika hivi: “Hakuna jambo ngumu kama vile ‘kumaliza huzuni.’” Lakini anaongeza hivi: “Kisha muda na kupitia musaada wa wengine, huzuni yako itapunguka.” (Healing a Spouse’s Grieving Heart)

      Kwa mufano, fikiria namna Abrahamu alitenda wakati bibi yake alikufa. Maandishi ya kwanza ya Biblia yanasema kama “Abrahamu akaanza kumuombolezea Sara na kumulilia.” Neno “akaanza” linaonyesha kama iliomba wakati fulani ili kupiganisha huzuni ya kufiwa na mupendwa wake.a Fikiria pia mufano wa Yakobo mwenye alidanganywa na akaamini kama Yosefu, mutoto wake, alikuwa ameuawa na munyama wa pori. Alihuzunika kwa “siku nyingi,” na watu wa familia yake hawakuweza kumufariji. Miaka mingi kisha hapo, kifo cha Yosefu kiliendelea kumuhangaisha katika akili.—Mwanzo 23:2; 37:34, 35; 42:36; 45:28.

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Abrahamu alihuzunika kwa sababu ya kifo cha Sara mupendwa wake

      Leo, ni vile pia juu ya watu wengi wenye kulia mutu mwenye walikuwa wanapenda sana. Fikiria mifano mbili yenye kufuata.

      • “Bwana yangu, Robert, alikufa tarehe 09/07/2008. Asubui yenye alifanya aksidenti ambayo ilimuua, ilikuwa kama asubui ya siku zingine. Kisha kula chakula cha asubui, kama kawaida mbele aende kwenye kazi, tulipatiana busu (baiser), tulikumbatiana, na kuambiana ‘ninakupenda.’ Miaka sita kisha hapo ningali na huzuni katika moyo. Siwazie kama huzuni yangu ya kufiwa na Rob itaishaka siku fulani.”—Gail, mwenye miaka 60.

      • “Hata kama bibi yangu mupendwa alikufa kumepita miaka 18, ningali ninamukumbuka na kuhuzunika juu yake. Wakati wowote ninaona kitu fulani chenye kuvutia katika uumbaji, ninamukumbuka, na ninajiuliza namna angefurahia kuona kitu chenye niko naona.”—Etienne, mwenye miaka 84.

      Kwa kweli, ni jambo la kawaida kusikia huzuni kwa muda murefu kama watu hao. Kila mutu ana namna yake ya kuhuzunika, na ni kukosa hekima kama tunahukumu namna mutu mwengine anatenda wakati anapatwa na jambo la kuhuzunisha. Na wakati uleule, inaweza kuwa muzuri tuepuke kujihukumu ikiwa namna tulitenda inaonekana kuwa yenye kupita mipaka. Namna gani tunaweza kupiganisha huzuni?

      a Isaka, mutoto wa Abrahamu alikuwa pia na huzuni yenye kuendelea. Kama vile habari “Tuige Imani Yao” katika gazeti hili inaonyesha, Isaka alikuwa angali na huzuni miaka tatu kisha kifo cha Sara, mama yake.—Mwanzo 24:67.

  • Namna ya Kupiganisha Huzuni Yako
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 3
    • HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

      Namna ya Kupiganisha Huzuni Yako

      Kuko mashauri mengi sana juu ya namna ya kupiganisha huzuni. Lakini, yote hayawezi kusaidia. Kwa mufano, pengine watu fulani watakushauria usilie ao usionyeshe kwa njia yoyote namna unajisikia. Wengine wanaweza kukuchochea ulie na kuonyesha kabisa namna unajisikia. Biblia inaonyesha mawazo yenye usawaziko ao yenye kuwa katikati; uchunguzi wa leo unaitika mawazo hayo.

      Katika desturi fulani, watu wanaona kuwa mwanaume hapaswe kulia. Lakini, kuko sababu kabisa ya kusikia haya ya kulia, hata mbele ya watu? Wanganga wa magonjwa ya akili wanatambua kama kulia ni sehemu ya kawaida ya kuonyesha huzuni. Na kisha wakati fulani, kuonyesha huzuni kunaweza kukusaidia uendelee na maisha hata kama unajisikia mubaya sana. Lakini kuzuia huzuni kunaweza kuwa na matokeo ya mubaya kuliko kuwa na matokeo ya muzuri. Biblia haiunge mukono wazo la kwamba ni mubaya kulia ao kwamba mwanaume hapaswe kulia. Kwa mufano, fikiria Yesu. Hata kama alikuwa na uwezo wa kufufua wafu, alilia mbele ya watu wakati Lazaro, rafiki yake mupendwa alikufa!—Yohana 11:33-35.

      Mara nyingi kusikia hasira ni sehemu ya huzuni, zaidi sana kama ni kifo cha kushitukia. Kuko sababu nyingi zenye zinaweza kufanya mutu mwenye alifiwa asikie hasira, kwa mufano wakati mutu mwenye kuheshimika anamuambia bila kufikiri mambo fulani yenye hayana musingi. Mwanaume mumoja wa Afrika Kusini mwenye kuitwa Mike anasema hivi: “Nilikuwa tu na miaka 14 wakati baba yangu alikufa. Kwenye maziko, muhubiri mumoja wa kanisa la Anglikani alisema kama Mungu ana lazima ya watu wazuri na anawachukua mbele ya wakati.a Jambo hilo liliniletea hasira kwa sababu tulikuwa na lazima sana ya baba yetu. Sasa, kisha miaka 63, jambo hilo linaendelea kuniumiza moyoni.”

      Na tuseme nini wakati mutu fulani anajisikia kuwa ni kosa lake? Zaidi sana kama ni kifo cha kushitukia, mutu mwenye alifiwa anaweza kuwaza tena na tena, ‘Kifo hakingetokea kama tu nilifanya hiki ao kile.’ Ao pengine mulikosana na marehemu wakati ulikutana naye mara ya mwisho. Tena, hilo linaweza kufanya ujisikie sana kuwa ni kosa lako.

      Ikiwa unasumbuliwa na hasira na hali ya kujisikia kuwa ni kosa lako, ni jambo la maana uonyeshe wengine namna unajisikia. Zungumuza na rafiki mwenye atakusikiliza na kukuhakikishia kama ni jambo la kawaida kwa watu wenye walifiwa kujisikia vile. Biblia inatukumbusha hivi: “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.”—Methali 17:17.

      Rafiki muzuri zaidi mwenye mutu ambaye alifiwa anaweza kuwa naye ni Muumbaji wetu, Yehova Mungu. Umufungulie moyo wako katika sala kwa sababu ‘yeye anakujali [anakuhangaikia].’ (1 Petro 5:7) Tena, anaahidi kama watu wote wenye wanafanya vile watafarijiwa kupitia “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Wafilipi 4:6, 7) Umuache pia Mungu akusaidie kupona kupitia Neno lake lenye kufariji, ni kusema, Biblia. Uandike liste ya maandiko yenye kufariji. (Soma kisanduku kwenye ukurasa huu.) Unaweza hata kuweka katika akili maandiko fulani kati ya hayo. Kuwaza sana juu ya maandiko hayo kunaweza kukusaidia zaidi sana usiku wakati uko peke yako na haupate usingizi.—Isaya 57:15.

      Hivi karibuni, mwanaume wa miaka 40 mwenye tunaweza kuita Jack, alifiwa na bibi yake kwa sababu ya ugonjwa wa kansere. Jack anasema kama wakati fulani anajisikia sana kuwa peke yake. Lakini sala imemusaidia. Anafasiria hivi: “Wakati ninasali kwa Yehova, sijisikie tena kuwa peke yangu. Mara nyingi, ninaamuka usiku na ninashindwa kuenda kulala tena. Kisha kusoma na kuwaza sana juu ya mawazo yenye kufariji ya Maandiko na kufungua moyo wangu katika sala, ninajisikia mwenye kutulia na amani yenye kupita zote inashuka juu yangu, na kufanya akili yangu na moyo wangu vipumuzike na kuniwezesha kulala.”

      Kijana mumoja mwanamuke mwenye kuitwa Vanessa alifiwa na mama yake kwa sababu ya ugonjwa. Yeye pia alijionea nguvu ya sala. Anasema hivi: “Katika wakati mugumu zaidi, nilikuwa tu naita jina la Mungu na kuanza kulia. Yehova alisikiliza sala zangu na sikuzote alinipatia nguvu yenye nilikuwa nayo lazima.”

      Watu fulani ambao wanashauria watu wenye walifiwa, wanawaambia kama ili kupiganisha huzuni, wajikaze kusaidia wengine ao kutumia wakati wao katika kazi zenye kuletea wengine faida. Kufanya vile kunaleta furaha na kunaweza kupunguza huzuni ya mutu. (Matendo 20:35) Wakristo wengi wenye walifiwa wametambua kama kujikaza kusaidia wengine kumewafariji sana.—2 Wakorintho 1:3, 4.

      a Hilo haliko fundisho la Biblia. Biblia inaonyesha mambo tatu yenye kuleta kifo.—Mhubiri 9:11; Yohana 8:44; Waroma 5:12.

      Maandiko Ya Biblia Yenye Kufariji

      • Mungu hafurahi wakati anaona unateseka.—Zaburi 55:22; 1 Petro 5:7.

      • Mungu anasikiliza kwa uvumilivu sala za watumishi wake.—Zaburi 86:5; 1 Wathesalonike 5:17.

      • Mungu anatamani kufufua watu wenye wamekufa.—Ayubu 14:13-15.

      • Mungu anaahidi kufufua watu wenye wamekufa.—Isaya 26:19; Yohana 5:28, 29.

  • Namna ya Kufariji Watu Wenye Walifiwa
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 3
    • HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

      Namna ya Kufariji Watu Wenye Walifiwa

      Umekwisha kujisikia kuwa haujue namna ya kusaidia mutu fulani mwenye kuhuzunika kwa sababu ya kifo cha mutu mwenye anapenda? Wakati fulani tunaweza kuona kuwa hatujue tuseme nini ao tufanye nini, kwa hiyo tunabakia bila kusema ao kufanya jambo lolote. Lakini kuko mambo yenye kufaa, na yenye kusaidia ambayo tunaweza kufanya.

      Mara nyingi, jambo la lazima ni kuwa hapo na kusema tu maneno mepesi kama vile, “pole sana.” Katika desturi nyingi, kukumbatia mutu mwenye alifiwa ao kumusalimia na mukono kwa upole ni njia ya muzuri ya kuonyesha kama unamuhangaikia. Kama mutu mwenye alifiwa anataka kuzungumuza, umusikilize kwa huruma. Na jambo la muzuri zaidi, ufanye kazi fulani kwa ajili ya watu wa familia wenye walifiwa, pengine kazi yenye hawakuweza kufanya, kama vile kupika chakula, kuhangaikia watoto, ao kusaidia katika mipango ya maziko kama ni lazima kufanya vile. Matendo hayo yanaweza kuwa na matokeo ya muzuri kuliko maneno yenye kupangwa muzuri sana.

      Kisha wakati fulani, unaweza kuzungumuza juu ya mutu mwenye alikufa, pengine kwa kukazia sifa zake fulani za muzuri ao mambo fulani ya kufurahisha yenye mulifanya pamoja. Mazungumuzo kama hayo yanaweza hata kufanya mutu mwenye alifiwa acheke kidogo. Kwa mufano, Pam alifiwa na bwana yake, Ian, kumepita miaka sita. Anasema hivi: “Wakati fulani watu wananiambia mambo ya muzuri yenye Ian alifanya yenye nilikuwa sijue, na hilo linafanya moyo wangu ufurahi.”

      Kulingana na ripoti moja ya wachunguzi, watu wenye walifiwa wanapata musaada wa kwanza tu, lakini mambo yenye wako nayo lazima yanasahauliwa haraka wakati marafiki wanarudilia mambo yenye kuhusu maisha yao wenyewe. Kwa hiyo, kisha rafiki yako kufiwa, ujikaze kuzungumuza naye mara kwa mara.a Watu wengi wenye walifiwa wanafurahia sana nafasi hiyo ili kumaliza huzuni yao ya muda murefu.

      Fikiria mufano wa Kaori, kijana mumoja mwanamuke wa Japani. Alivunjika moyo sana kwa sababu ya kifo cha mama yake na kifo cha dada yake mukubwa mwaka moja na miezi tatu kisha kifo cha mama yake. Jambo la kufurahisha ni hili: marafiki waaminifu waliendelea kumutolea musaada. Mumoja kati yao mwenye kuitwa Ritsuko ni mukubwa sana kumupita. Alifanya naye urafiki wa sana. Kaori anasema hivi: “Kusema kweli, sikufurahia jambo hilo. Sikupenda mutu yeyote akamate nafasi ya mama yangu, na sikuwazia kama mutu fulani angeweza kufanya vile. Lakini, nilifikia kumukaribia sana Mama Ritsuko kwa sababu ya namna alinitendea. Kila juma, tulienda katika kazi ya kuhubiri pamoja na tulienda kwenye mikutano ya Kikristo pamoja. Mara nyingi, aliniita ili tukunywe chai pamoja, aliniletea chakula, na kuniandikia barua. Mawazo ya muzuri ya Mama Ritsuko yalinisaidia sana.”

      Kumepita miaka 12 tangu mama yake na Kaori alikufa, na leo yeye na bwana yake ni wahubiri wa wakati wote. Kaori anasema hivi: “Mama Ritsuko anaendelea kunihangaikia. Wakati ninarudia nyumbani, ninamutembelea kila mara na kufurahia urafiki wenye kujenga.”

      Poli, Shahidi wa Yehova katika inchi ya Saiprasi, na yeye pia alipata faida kwa sababu wengine waliendelea kumusaidia. Poli alikuwa na bwana muzuri mwenye kuitwa Sozos. Sozos aliweka mufano muzuri wa muchungaji Mukristo; alizoea kualika mayatima na wajane kwenye nyumba yake ili kula na kupitisha wakati pamoja. (Yakobo 1:27) Jambo la huzuni ni hili: wakati Sozos alikuwa na miaka 53 alikufa kwa sababu sehemu moja kwenye ubongo wake ilikuwa yenye kuvimba. Poli anasema hivi: “Nilipoteza bwana yangu muaminifu mwenye nilifanya naye miaka 33 katika ndoa.”

      [Picha katika ukurasa wa 7]

      Tafuta namna za kusaidia watu wenye walifiwa

      Kisha maziko, Poli alihamia Kanada pamoja na Daniel, mutoto wake mudogo mwanaume wa miaka 15. Huko, walianza kujiunga na kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Poli anakumbuka hivi: “Marafiki katika kutaniko letu mupya hawakujua kitu juu ya maisha yetu ya zamani na juu ya hali zetu ngumu. Hata hivyo, walitukaribia na kutuambia maneno yenye kufariji na kutusaidia. Musaada huo ulikuwa wa maana, zaidi sana wakati huo wenye mutoto wangu mwanaume alikuwa na lazima ya baba yake! Wale wenye kuongoza katika kutaniko walimuhangaikia Daniel sana. Zaidi sana mumoja wao hakumusahau Daniel wakati alipenda kupitisha wakati pamoja na marafiki ao wakati alienda kucheza nao kabumbu.” Leo, mama na mutoto, wote wawili wanaendelea muzuri.

      Kwa kweli, kuko namna nyingi za kusaidia na kufariji watu wenye walifiwa. Biblia inatufariji pia kupitia tumaini la muzuri sana la wakati unaokuja.

      a Watu fulani wametia hata alama kwenye tarehe ya kifo cha mutu fulani kwenye kalenda yao ili wakumbuke tarehe hiyo na kufariji mutu mwenye alifiwa wakati anakuwa na lazima zaidi ya kufarijiwa, tarehe hiyo ao wakati inakaribia.

  • Watu Wenye Wamekufa Wataishi Tena!
    Munara wa Mulinzi (Gazeti la Watu Wote)—2016 | No. 3
    • HABARI KUBWA | WAKATI MUTU MWENYE UNAPENDA ANAKUFA

      Watu Wenye Wamekufa Wataishi Tena!

      Unaweza kukumbuka Gail, mwenye tulizungumuzia katika habari ya pili. Alikuwa na mashaka kama angeweza kushinda huzuni yenye alikuwa nayo juu ya kifo cha bwana yake, Rob. Lakini, anangojea kwa hamu kumuona tena katika dunia mupya yenye Mungu anaahidi. Anasema hivi: “Andiko lenye ninapenda sana ni Ufunuo 21:3, 4.” Linasema hivi: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”

      Gail anasema hivi: “Ahadi hiyo inasema mambo yote. Kwa kweli, ninasikilia huruma watu wenye walifiwa na mutu mwenye wanapenda lakini hawajue kama kuko tumaini la kumuona tena.” Gail anatenda kupatana na mambo anaamini kwa kufanya kazi ya kujitolea. Yeye ni muhubiri wa wakati wote; anazungumuzia majirani wake ahadi ya Mungu ya wakati unaokuja ambapo “kifo hakitakuwapo tena.”

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Ayubu alikuwa hakika kama angeishi tena

      Pengine unaweza kusema, ‘Hiyo ni ndoto tu!’ Lakini fikiria mufano wa mwanaume mwenye kuitwa Ayubu. Alikuwa mugonjwa sana. (Ayubu 2:7) Hata kama Ayubu aliona kuwa ni muzuri kufa, alikuwa angali na imani kama Mungu ana nguvu ya kumufufua ili aishi tena kwenye dunia. Alisema kwa uhakika hivi: “Laiti [ingekuwa muzuri kama] ungenificha katika Kaburi . . . Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:13, 15) Ayubu alikuwa hakika kama Mungu angemukumbuka na kama angetamani kumurudishia uzima.

      Hivi karibuni, Mungu atarudishia Ayubu na watu wengine wengi uzima, wakati dunia hii itageuzwa kuwa paradiso. (Luka 23:42, 43) Katika andiko la Matendo 24:15, Biblia inahakikisha hivi: ‘Kutakuwa ufufuo.’ Yesu anatuhakikishia hivi: ‘Musistaajabie [musishangae] jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake na kutoka.’ (Yohana 5:28, 29) Ayubu ataona wakati ahadi hiyo itatimizwa. Atakuwa na tumaini la kuwa tena na “nguvu za ujana wake” na nyama ya mwili wake itabakia sikuzote “laini [teketeke] kuliko wakati wa ujana.” (Ayubu 33:24, 25) Itakuwa vile pia kwa watu wote wenye wanaonyesha shukrani kwa ajili ya mupango wa Mungu wenye huruma wa kufufua watu ili waishi tena duniani.

      Kama umekwisha kuhuzunika sana kwa sababu ya kifo cha mutu mwenye unapenda, pengine mambo yenye tumezungumuzia hayatamaliza kabisa-kabisa huzuni yako. Lakini, ukiwaza sana juu ya ahadi za Mungu zenye kuwa katika Biblia, unaweza kupata tumaini la kweli na nguvu ya kuendelea na maisha.—1 Wathesalonike 4:13.

      Unapenda kujua mengi juu ya namna ya kupiganisha huzuni? Ao uko na maulizo juu ya jambo hilo, kama vile “Sababu gani Mungu anaacha mambo mabaya na mateso yaendelee?” Tafazali, fungua adresi yetu ya Internete, jw.org, ili uone majibu ya Biblia yenye kufariji na yenye kusaidia.

Vichapo vya Swahili (Congo) (1996-2026)
Toka
Ingia
  • Kiswahili (Congo)
  • Tumia Wengine
  • Préférences
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Kanuni za Matumizi
  • Kanuni za Kutunza Siri
  • Paramètres Kuhusu Kutunza Siri
  • JW.ORG
  • Ingia
Tumia Wengine