NYONGEZA
Visehemu Vidogo-vidogo vya Damu na Ufundi wa Waganga
Visehemu vidogo-vidogo vya damu. Visehemu hivyo vinatokana na zile sehemu ine kubwa-kubwa, ni kusema, chembe nyekundu (globules rouges), chembe nyeupe (globules blancs), vigandisha-damu (plaquettes) na plazima (plasma). Kwa mufano, chembe nyekundu zina proteine inayoitwa hémoglobine. Mutu akipungukiwa kabisa na damu ao akipoteza damu nyingi, waganga wanatumia dawa iliyotengenezwa kwa hémoglobine ya mwanadamu ao munyama.
Plazima: sehemu yake kubwa ni maji (90%), ina hormone nyingi, chumvi, vitamine na vitu vingine vidogo-vidogo kama vile sukari. Pia plazima ina vitu vinavyogandisha damu, na vitu vinavyokinga mwili na kupiganisha magonjwa, na pia proteine zinazoitwa albumine. Mutu akipatwa na ugonjwa kwa sababu mwili wake hauna kinga-mwili, muganga anaweza kuomba atobolewe shindano iliyo na kinga-mwili (gammaglobulines), ambayo inatengenezwa na plazima ya watu ambao wana kinga-mwili za nguvu. Katika chembe nyeupe, wanaweza kupata visehemu vingine vidogo-vidogo (interférons na interleukines) ili kupiganisha mikrobe ya magonjwa fulani na aina mbalimbali ya kansere.
Je, Wakristo wanaweza kukubali dawa iliyotengenezwa na visehemu vidogo-vidogo vya damu? Biblia haitoe maagizo ya waziwazi juu ya jambo hilo, kwa hiyo, kila Mukristo anapaswa kuchukua uamuzi wake mbele ya Mungu, akitumia zamiri yake. Wakristo fulani wanaweza kuamua kukataa visehemu vyote vidogo-vidogo vya damu, kwa sababu Sheria ya Mungu kwa Waisraeli iliomba damu ya kiumbe ‘imwangwe kwenye udongo.’ (Kumbukumbu la Torati 12:22-24) Wengine wanaweza kuamua kukubali dawa iliyotengenezwa kutokana na visehemu hivyo vidogo-vidogo, lakini wanakataa kabisa damu yenyewe ao sehemu zake kubwakubwa. Wanaweza kufikia uamuzi huo kwa sababu wanaona kuwa visehemu vidogo-vidogo vinavyotokana na damu haviwakilishe tena uzima wa kiumbe ambaye damu yake ilitumiwa.
Unapofanya uamuzi juu ya visehemu vidogo-vidogo hivyo, ujiulize: Je, ninaelewa kwamba kukataa visehemu vidogo-vidogo vyote kunamaanisha kwamba sitakubali dawa yoyote inayokinga mwili ao inayoweza kusaidia damu kuganda ili isiendelee kuvuja? Ninaweza kumufasiria muganga sababu gani ninakataa kisehemu kimoja ao visehemu vyote vidogo-vidogo vya damu ao sababu gani ninakubali?
Ufundi wa waganga. Ufundi huo unaweza kuwa ule unaoitwa hémodilution na pia ufundi unaoitwa récupération du sang épanché. Kuhusu ufundi huo wa kwanza, damu ya mugonjwa inafyonzwa na mahali pake wanamutia umajimaji, na kisha kumurudishia tena ile damu yake. Kuhusu ule ufundi wa pili, damu inayovuja wakati wa upasuaji ao mahali palipokatwa inachukuliwa, inasafishwa ao kuchujwa na kisha inarudishwa katika mwili wa mugonjwa. Waganga wanatumia ufundi wote huo kwa njia mbalimbali, kwa hiyo, Mukristo anapaswa kwanza kujua ufundi ambao muganga wake atatumia.
Unapofanya uamuzi juu ya ufundi huo wa matunzo, ujiulize: “Ikiwa sehemu fulani ya damu yangu itapitishwa inje ya mwili wangu, labda hata mutiririko wayo utakatizwa kwa muda fulani, je, zamiri yangu itaona damu hiyo kuwa ingali sehemu ya mwili wangu, ambayo haipaswe ‘kumwangwa kwenye udongo’?” (Kumbukumbu la Torati 12:23, 24) Je, zamiri yangu iliyofundishwa na Biblia haitanisumbua ikiwa wakati ninafanyiwa upasuaji, damu yangu inachukuliwa, inachanganywa na dawa fulani, kisha inarudishwa katika mwili wangu? Je, ninaelewa kwamba nikikataa ufundi wote wa waganga kuhusu matumizi ya damu yangu, hilo linamaanisha kuwa sitakubali kupimwa damu, sitakubali damu yangu ipitishwe katika mashini ya kuchuja na kusafisha damu, kisha irudishwe katika mwili wangu, wala sitakubali mashini inayofanya kazi mahali pa moyo na mapafu?’
Mukristo anapaswa yeye mwenyewe kujiamulia namna damu yake itatumiwa wakati wa matunzo. Ni vilevile pia, ikiwa anataka kupimisha damu ao ikiwa muganga ataondoa sehemu fulani ya damu, kuichanganya na dawa fulani na kisha kuirudisha katika mwili, kulingana na ufundi wa kisasa.