Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Lugha ya Alama ya Tanzania
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • es25
  • Juni

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Juni
  • Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
  • Vichwa vidogo
  • Jumapili, Juni 1
  • Jumatatu, Juni 2
  • Jumanne, Juni 3
  • Jumatano, Juni 4
  • Alhamisi, Juni 5
  • Ijumaa, Juni 6
  • Jumamosi, Juni 7
  • Jumapili, Juni 8
  • Jumatatu, Juni 9
  • Jumanne, Juni 10
  • Jumatano, Juni 11
  • Alhamisi, Juni 12
  • Ijumaa, Juni 13
  • Jumamosi, Juni 14
  • Jumapili, Juni 15
  • Jumatatu, Juni 16
  • Jumanne, Juni 17
  • Jumatano, Juni 18
  • Alhamisi, Juni 19
  • Ijumaa, Juni 20
  • Jumamosi, Juni 21
  • Jumapili, Juni 22
  • Jumatatu, Juni 23
  • Jumanne, Juni 24
  • Jumatano, Juni 25
  • Alhamisi, Juni 26
  • Ijumaa, Juni 27
  • Jumamosi, Juni 28
  • Jumapili, Juni 29
  • Jumatatu, Juni 30
Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2025
es25

Juni

Jumapili, Juni 1

Ni lazima tuingie katika Ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.—Mdo. 14:22.

Yehova aliwabariki Wakristo wa karne ya kwanza walipobadilikana kulingana na hali. Waliteswa mara nyingi, pindi nyingine huenda wakati ambao hawakutarajia. Fikiria jambo lililompata Barnaba na mtume Paulo walipokuwa wakihubiri katika eneo la Listra. Mwanzoni, walikaribishwa kwa uchangamfu na watu waliowasikiliza. Lakini baadaye, wapinzani “wakaushawishi umati,” na baadhi ya watu haohao wakampiga mawe Paulo na kumwacha wakiwazia kwamba amekufa. (Mdo. 14:19) Lakini Barnaba na Paulo waliendelea kuhubiri sehemu nyingine. Matokeo yalikuwaje? Waliwafanya “watu wengi kuwa wanafunzi,” na maneno na mfano wao uliwaimarisha waabudu wenzao. (Mdo. 14:​21, 22.) Watu wengi walinufaika kwa sababu Barnaba na Paulo hawakuvunjika moyo hata walipokabili mateso yasiyotarajiwa. Ikiwa hatutavunjika moyo katika kazi ambayo Yehova ametupatia, sisi pia tutabarikiwa. w23.04 17:13-14

Jumatatu, Juni 2

Ee Yehova, sikiliza sala yangu;na usikilize sihi zangu za kuomba msaada. Ninakuitia wewe katika siku ninayotaabika, kwa maana utanijibu.—Zab. 86:​6, 7.

Mfalme Daudi alikabili maadui wengi hatari katika maisha yake yote, na mara nyingi alitafuta msaada wa Yehova kupitia sala. Daudi alikuwa na uhakika kwamba Yehova alisikiliza na kujibu sala zake. Wewe pia unaweza kuwa na uhakika huo. Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova anaweza kutupatia hekima na nguvu tunazohitaji ili kuvumilia. Huenda akawatumia ndugu na dada zetu au watu ambao kwa sasa hawamwabudu ili kutusaidia kwa njia fulani. Ingawa huenda Yehova asijibu sala zetu kila mara kwa njia tuliyotarajia, tunajua kwamba atazijibu. Atatuandalia kile hasa tunachohitaji na kwa wakati hususa tunapokihitaji. Basi, endelea kusali ukiwa na imani na uhakika kwamba Yehova atakutunza sasa na kwamba “[atatosheleza] tamaa ya kila kitu kilicho hai” katika ulimwengu mpya unaokuja.—Zab. 145:16. w23.05 21:4, 17-18

Jumanne, Juni 3

Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea?—Zab. 116:12.

Ni vema kukazia fikira baraka unazopata unapotimiza lengo lako.Unaweza kukazia fikira baraka gani? Ikiwa lengo lako linahusu kusoma Biblia au kusali, fikiria jinsi litakavyokusaidia kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova. (Zab. 145:​18, 19) Ikiwa lengo lako ni kusitawisha sifa fulani ya Kikristo, kazia fikira jinsi sifa hiyo itakavyokusaidia kuboresha uhusiano wako pamoja na wengine. (Kol. 3:14) Kwa nini usiandike orodha ya sababu zote zinazokufanya utamani kutimiza lengo lako? Chunguza orodha hiyo tena na tena. Pia, tumia muda pamoja na wale ambao watakuchochea. (Met. 13:20) Hata hivyo, ukweli ni kwamba kuna wakati ambapo sisi sote hukosa kichocheo. Je, hilo linamaanisha kwamba hatuwezi kujitahidi kutimiza lengo letu? Hapana. Bado tunaweza kufanyia kazi lengo letu hata tunapokosa kichocheo. Ingawa huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, tutapata matokeo mazuri. w23.05 24:5-8

Jumatano, Juni 4

Lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.—Gal. 6:7.

Kutambua kwamba tunawajibika kwa sababu ya maamuzi yetu, kunaweza kutuchochea tuungame dhambi zetu, turekebishe makosa yetu, na tuepuke kurudia makosa hayo. Kuchukua hatua kama hizo kunaweza kutusaidia tuendelee kukimbia katika mbio za uzima. Ikiwa umefanya uamuzi mbaya, kubali hali yako ya sasa. Usipoteze muda na nguvu zako ukijaribu kujitetea au kujilaumu au kuwalaumu wengine. Badala yake, kubali makosa yako, na ujitahidi kufanya yote unayoweza ili kuboresha hali yako. Ikiwa unahisi hatia kwa sababu ya kosa ulilofanya, sali kwa Yehova kwa unyenyekevu, kubali kosa lako, na umwombe akusamehe. (Zab. 25:11; 51:​3, 4) Waombe msamaha wale ambao huenda umewakosea, na ikihitajika, utafute msaada kutoka kwa wazee wa kutaniko. (Yak. 5:​14, 15) Jifunze kutokana na makosa yako na ujitahidi kutoyarudia. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuonyesha rehema na kukupatia msaada ambao unahitaji.—Zab. 103:​8-13. w23.08 36:8-9

Alhamisi, Juni 5

Yehoashi akaendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova sikuzote ambazo kuhani Yehoyada alimfundisha.—2 Fal. 12:2.

Mfalme Yehoashi alinufaika sana kwa kushirikiana na Yehoyada. Matokeo ni kwamba mfalme huyo kijana alitamani kumfurahisha Yehova. Lakini baada ya Yehoyada kufa, Yehoashi aliwasikiliza wakuu walioasi imani. (2 Nya. 24:​4, 17, 18) Ingawa Yehova alihuzunika sana, “aliendelea kuwatuma manabii miongoni mwao ili wawarudishe . . . , lakini walikataa kusikiliza.” Hata hawakumsikiliza Zekaria, mwana wa Yehoyada ambaye alikuwa nabii na kuhani wa Yehova na pia binamu ya Yehoashi. Isitoshe, Mfalme Yehoashi alimuua Zekaria. (2 Nya. 22:11; 24:​19-22) Yehoashi hakudumisha woga unaofaa kumwelekea Yehova. Yehova alikuwa amesema hivi: “Wale wanaonidharau watadharauliwa.” (1 Sam. 2:30) Baadaye, jeshi dogo la Wasiria lilishinda “jeshi kubwa sana” la Yehoashi na ‘kumjeruhi vibaya.’ (2 Nya. 24:​24, 25) Yehoashi aliuawa na watumishi wake mwenyewe kwa sababu ya kumuua Zekaria. w23.06 27:16-17

Ijumaa, Juni 6

Wakati fulani mlikuwa giza, lakini sasa ninyi ni nuru.—Efe. 5:8.

Kwa kipindi fulani mtume Paulo alikuwa jijini Efeso akihubiri na kufundisha habari njema. (Mdo. 19:​1, 8-10; 20:​20, 21) Aliwapenda sana ndugu zake na alitaka kuwasaidia waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova. Waefeso ambao Paulo aliwaandikia barua awali walikuwa watumwa wa mafundisho ya dini za uwongo na ushirikina. Waefeso walijulikana kwa kuwa na maadili na mwenendo mpotovu. Ilikuwa kawaida kusikia maneno machafu katika kumbi za michezo za jiji na hata kwenye sherehe za dini. (Efe. 5:3) Wakaaji wengi wa jiji hilo walikuwa “wamepotoka kabisa kimaadili,” msemo ambao kihalisi unamaanisha “hawahisi tena maumivu.” (Efe. 4:​17-19) Kabla ya kujua kwa usahihi mambo yaliyo sawa na yasiyo sawa, dhamiri za Waefeso hazikuwasumbua kabisa. Kwa sababu hizo, Paulo angeweza kusema kwamba ‘walikuwa gizani kiakili na wametenganishwa na uzima ambao ni wa Mungu.’ Hata hivyo, baadhi ya Waefeso hawakuendelea kubaki gizani. w24.03 12:2, 4-6

Jumamosi, Juni 7

Wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena. . . . Hawatachoka.—Isa. 40:31.

Gideoni alihitaji kufanya kazi kwa bidii akiwa mwamuzi. Wamidiani walipokimbia usiku wakati wa vita, Gideoni aliwafuatilia kutoka kwenye Bonde la Yezreeli hadi kwenye Mto Yordani. (Amu. 7:22) Je, Gideoni aliacha kuwafuatilia alipofika kwenye Mto Yordani? Hapana! Ingawa alikuwa amechoka, yeye na wanajeshi wake 300 walivuka mto huo na kuendelea kuwafuatilia. Mwishowe, waliwafikia Wamidiani na kuwashinda. (Amu. 8:​4-12) Gideoni alikuwa na uhakika kwamba Yehova angemwimarisha na kwa kweli alimwimarisha. (Amu. 6:​14, 34) Pindi moja, Gideoni na wanaume wake walipokuwa wakiwafuatilia wafalme wawili wa Midiani kwa miguu, inaelekea wafalme hao walikuwa wakikimbia kwa kutumia ngamia. (Amu. 8:​12, 21) Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu, Waisraeli waliwafikia na kuwashinda. Vivyo hivyo, wazee wanaweza kumtegemea Yehova, ambaye “hachoki kamwe wala haishiwi na nguvu.” Atawapatia nguvu wanazohitaji.—Isa. 40:​28, 29. w23.06 25:14, 16

Jumapili, Juni 8

[Yehova] hatawatupa wala kuwaacha.—Kum. 31:6.

Tunaweza kuwa na moyo thabiti hata tupatwe na majaribu gani. Hivyo, mtumaini Yehova. Fikiria jinsi Baraka alivyofanikiwa kwa sababu ya kutumaini mwongozo wa Yehova. Ingawa hakukuwa na ngao wala mkuki katika nchi yote, Yehova alimwagiza aende vitani dhidi ya wanajeshi wenye silaha, walioongozwa na mkuu wa jeshi Mkanaani aliyeitwa Sisera. (Amu. 5:8) Nabii wa kike Debora alimwambia Baraka ashuke kwenye eneo tambarare ili kukutana na Sisera na magari yake 900. Ingawa ingekuwa vigumu kwa Waisraeli kupigana na magari hayo yenye kasi kwenye eneo tambarare, Baraka alitii. Wanajeshi walipokuwa wakishuka kwenye Mlima Tabori, Yehova alisababisha mvua kubwa inyeshe. Magari ya Sisera yakakwama kwenye matope, na Yehova akampa Baraka ushindi. (Amu. 4:​1-7, 10, 13-16) Vivyo hivyo, Yehova atatupatia ushindi ikiwa tutamtumaini yeye na mwongozo anaotupatia kupitia tengenezo lake. w23.07 31:17-18

Jumatatu, Juni 9

Yule atakayevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.—Mt. 24:13.

Tunahitaji kuwa wenye subira ili tuokolewe. Kama watumishi waaminifu walioishi zamani, tunahitaji kumngojea Mungu kwa subira ili atimize ahadi zake. (Ebr. 6:​11, 12) Biblia inalinganisha hali yetu na hali ya mkulima. (Yak. 5:​7, 8) Mkulima anajitahidi sana kupanda na kutia maji kwenye mimea yake, lakini hajui wakati hususa ambapo mimea hiyo itakua. Basi, mkulima anangojea kwa subira, akitumaini kwamba atavuna mazao. Vivyo hivyo, tunashiriki katika mambo ya kiroho kwa bidii ingawa ‘hatujui Bwana wetu atakuja siku gani.’ (Mt. 24:42) Tunangoja kwa subira, tukiwa na uhakika kwamba kwa wakati unaofaa, Yehova atatimiza mambo yote ambayo ametuahidi. Ikiwa tutakosa subira, huenda tukachoka kungoja na kuanza kumwacha Yehova hatua kwa hatua. Pia, huenda tukaanza kufuatilia mambo ambayo yatatupa furaha ya muda mfupi. Lakini ikiwa tuna subira, tunaweza kuvumilia hadi mwisho na kuokolewa.—Mika 7:7. w23.08 35:7

Jumanne, Juni 10

Vidole vyake vya miguu vilikuwa kwa sehemu vya chuma na kwa sehemu vya udongo wa mfinyanzi.—Dan. 2:42.

Kwa kulinganisha unabii katika Danieli 2:​41-43 na unabii mwingine katika kitabu cha Danieli na Ufunuo, tunaweza kufikia mkataa kwamba nyayo hizo zinafananisha Muungano wa Uingereza na Marekani, serikali kuu ya ulimwengu inayotawala leo. Kuhusu serikali hiyo kuu ya ulimwengu, Danieli alisema kwamba ufalme huo utakuwa na “nguvu kwa sehemu na kuwa dhaifu kwa sehemu.” Kwa nini utakuwa dhaifu kwa sehemu? Kwa sababu watu wa kawaida, wanaofananishwa na udongo laini wa mfinyanzi, wanadhoofisha uwezo wake wa kutenda kama chuma. Kutokana na ufafanuzi wa Danieli kuhusu ndoto ya ile sanamu, tunajifunza kweli fulani muhimu. Kwanza, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani imeonyesha nguvu zake kwa njia fulani. Kwa mfano, muungano wa nchi hizo ulikuwa kati ya mataifa yaliyoshinda Vita vya Kwanza vya Ulimwengu na Vita vya Pili vya Ulimwengu. Hata hivyo, serikali hiyo kuu ya ulimwengu imedhoofishwa na itaendelea kudhoofishwa na mizozo kati ya raia wake. Pili, muungano wa nchi hizo ndio serikali kuu ya mwisho ya ulimwengu itakayotawala kabla Ufalme wa Mungu haujakomesha falme zote za wanadamu. w23.08 34:12-13

Jumatano, Juni 11

Katika taabu yangu nilimwita Yehova, niliendelea kumlilia Mungu wangu anisaidie. Akiwa katika hekalu lake aliisikia sauti yangu.—Zab. 18:6.

Nyakati nyingine, Daudi alitaabishwa kwa sababu ya matatizo na majaribu aliyokabili. (Zab. 18:​4, 5) Hata hivyo, upendo mwororo wa Yehova na utunzaji wake ulimburudisha. Yehova alimwongoza rafiki yake aliyechoka katika “malisho yenye majani mengi” na “kwenye sehemu za kupumzika zenye maji mengi.” Matokeo ni kwamba Daudi alipata nguvu tena na aliweza kuendelea kumtumikia Yehova kwa shangwe. (Zab. 18:​28-32; 23:2) Vivyo hivyo leo, upendo mshikamanifu wa Yehova unafanya iwezekane kuvumilia tunapokabili majaribu au hali ngumu maishani. (Omb. 3:22; Kol. 1:11) Mara nyingi uhai wa Daudi ulikuwa hatarini, na alikabiliana na maadui wengi wenye nguvu. Hata hivyo, upendo wa Yehova ulimfanya ahisi kuwa analindwa na yuko salama. Daudi alihisi kwamba Yehova alikuwa pamoja naye katika kila hali aliyokabili, na hilo lilimfariji. Hivyo, angeweza kuimba hivi: “[Yehova] aliniokoa kutoka katika mambo yote yanayoniogopesha.” (Zab. 34:4) Daudi alikuwa na sababu nzuri za kuogopa, lakini upendo wa Yehova ulikuwa na nguvu zaidi kuliko woga wake. w24.01 4:15-17

Alhamisi, Juni 12

Watenda dhambi wakijaribu kukushawishi, usikubali.—Met. 1:10.

Jifunze kutokana na maamuzi mabaya ya Yehoashi. Baada ya kifo cha Kuhani Mkuu Yehoyada, Yehoashi alichagua marafiki wabaya. (2 Nya. 24:​17, 18) Alichagua kuwasikiliza wakuu wa Yuda ambao hawakumpenda Yehova. Huenda unakubali kwamba Yehoashi alipaswa kuepuka marafiki hao wasiofaa. Badala yake, alisikiliza ushauri wao mbaya. Hata Zekaria, binamu ya Yehoashi alipojaribu kumrekebisha, Yehoashi aliamuru auawe. (2 Nya. 24:​20, 21; Mt. 23:35) Jambo hilo lilikuwa baya sana na la kipumbavu! Yehoashi alianza maisha yake vizuri, lakini kwa kusikitisha akawa mwasi-imani na muuaji. Hatimaye, watumishi wake mwenyewe walimuua. (2 Nya. 24:​22-25) Maisha yake yangekuwa tofauti kabisa ikiwa angeendelea kumsikiliza Yehova na wale waliompenda Yehova! w23.09 38:6

Ijumaa, Juni 13

Acha kuogopa.—Luka 5:10.

Yesu alijua kwamba mtume Petro angeendelea kuwa mwaminifu. Basi, kwa fadhili Yesu alimwambia Petro ‘aache kuogopa.’ Uhakika ambao Yesu alimwonyesha Petro ulibadili maisha yake. Baadaye, Petro na Andrea, ndugu yake, waliacha biashara yao ya kuvua samaki na wakajiunga na Yesu katika huduma yake, uamuzi ambao uliwaletea baraka nyingi. (Marko 1:​16-18) Petro alijionea mambo mengi yenye kusisimua akiwa mfuasi wa Kristo. Alijionea Yesu akiponya wagonjwa, akifukuza roho waovu, na hata kuwafufua wafu. (Mt. 8:​14-17; Marko 5:​37, 41, 42) Pia, Petro alijionea maono ya utukufu ambao Yesu angekuwa nao katika Ufalme wa Mungu, Petro hakusahau kamwe tukio hilo. (Marko 9:​1-8; 2 Pet. 1:​16-18) Petro aliona mambo ambayo hakutarajia kuona. Kwa kweli alifurahi sana kwamba hakuruhusu hisia zisizofaa kujielekea zimzuie kupata baraka hizo! w23.09 40:4-5

Jumamosi, Juni 14

Yesu akamwambia: “Ninakuambia, si mpaka mara saba, bali mpaka mara 77.”—Mt. 18:22.

Katika barua yake ya kwanza, mtume Petro alisema kwamba ‘kupendana sana,’ kutatusaidia kusamehe, si makosa machache, bali “dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) Huenda Petro alikumbuka somo kuhusu kusamehe ambalo Yesu alikuwa amemfundisha miaka mingi mapema. Wakati huo, Petro alifikiri kwamba angeonyesha fadhili nyingi, alipopendekeza kwamba angemsamehe ndugu yake “mpaka mara saba.” Lakini Yesu alimfundisha Petro—na sisi sote—kusamehe “mpaka mara 77,” yaani, bila kikomo. (Mt. 18:21) Ikiwa unahisi ni vigumu kutumia shauri hilo usife moyo! Kwa kuwa watumishi wote wa Yehova si wakamilifu, nyakati nyingine imekuwa vigumu kwao kusamehe. Jambo muhimu sasa ni kuchukua hatua yoyote inayohitajika ili kumsamehe ndugu yako na kufanya amani pamoja naye. w23.09 41:12

Jumapili, Juni 15

Nilimlilia Yehova, naye akanijibu.—Yona 2:2.

Akiwa katika tumbo la samaki, Yona alikuwa na uhakika kwamba Yehova angesikiliza sala yake ya unyenyekevu na kukubali toba yake, na kwamba Yehova angemsaidia. Baadaye, Yona alirudishwa kwenye nchi kavu na alikuwa tayari kukubali na kutimiza mgawo ambao angepewa. (Yona 2:10–3:4) Unapokabili jaribu je, umewahi kuhisi kwamba kwa sababu ya mahangaiko ni vigumu kujieleza waziwazi katika sala? Au unahisi umechoka sana hivi kwamba huwezi kujifunza? Kumbuka kwamba Yehova anaelewa hali yako kikamilifu. Basi, hata unapotoa sala fupi, unaweza kuwa na uhakika kwamba atakupatia kile hasa unachohitaji. (Efe. 3:20) Ikiwa maumivu yako ya kimwili au kihisia yanafanya iwe vigumu kwako kusoma na kujifunza, unaweza kusikiliza rekodi za sauti za Biblia au machapisho yanayotegemea Biblia. Pia, unaweza kusikiliza wimbo wetu mmoja au kutazama video kwenye jw.org. Ukisali kwa Yehova na kutafuta majibu ya sala zako katika maandalizi ya kiroho ambayo ametupatia, utaonyesha kwamba unataka Yehova akupe nguvu. w23.10 43:6, 9

Jumatatu, Juni 16

Roho takatifu hufanya iwe wazi kwamba njia ya kuingia mahali patakatifu bado haikuwa imefunuliwa lile hema la zamani lilipokuwa limesimama.—Ebr. 9:8.

Hema la ibada na mahekalu ambayo baadaye yalijengwa huko Yerusalemu, kimsingi yalikuwa na mpangilio uleule. Ndani kulikuwa na sehemu mbili—“Patakatifu” na “Patakatifu Zaidi”—na sehemu hizo zilitenganishwa na pazia lililotariziwa. (Ebr. 9:​2-5; Kut. 26:​31-33) Ndani ya Patakatifu kulikuwa na kinara cha taa cha dhahabu, madhabahu iliyotumiwa kuchoma uvumba, na meza ya mikate ya wonyesho. “Makuhani waliotiwa mafuta” ndio tu walioruhusiwa kuingia Patakatifu ili kutimiza majukumu yao ya kikuhani. (Hes. 3:​3, 7, 10) Patakatifu Zaidi palikuwa na sanduku la agano la dhahabu ambalo liliwakilisha kuwepo kwa Yehova. (Kut. 25:​21, 22) Kuhani mkuu peke yake ndiye aliyeruhusiwa kuvuka pazia na kuingia Patakatifu Zaidi kila mwaka katika Siku ya Kufunika Dhambi. (Law. 16:​2, 17) Aliingia akiwa na damu ya wanyama ili kufunika dhambi zake mwenyewe na dhambi za taifa zima. Mwishowe Yehova alionyesha wazi maana ya sehemu hizo mbalimbali za hema la ibada.—Ebr. 9:​6, 7. w23.10 45:12

Jumanne, Juni 17

Mpendane.—Yoh. 15:17.

Katika Neno la Mungu tunasoma mara kwa mara kuhusu amri ya ‘kupendana.’ (Yoh. 15:12; Rom. 13:8; 1 The. 4:9; 1 Pet. 1:22; 1 Yoh. 4:11) Hata hivyo, upendo ni hisia iliyo ndani ya moyo, au yule mtu wa ndani, na hakuna mwanadamu anayeweza kusoma moyo wetu. Hivyo, tunaweza kuwaonyeshaje upendo ndugu na dada zetu? Kupitia maneno na matendo yetu. Kuna njia mbalimbali zinazoweza kuonyesha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu. Fikiria mifano ifuatayo: “Kila mtu amwambie mwenzake ukweli.” (Zek. 8:16) “Mdumishe amani kati yenu.” (Marko 9:50) Iweni wa kwanza “katika kuonyeshana heshima.” (Rom. 12:10) “Mkaribishane.” (Rom. 15:7) “Endeleeni . . . kusameheana.” (Kol. 3:13) “Endeleeni kubebeana mizigo mizito.” (Gal. 6:2) “Endeleeni kufarijiana.” (1 The. 4:18) “Endeleeni . . . kujengana.” (1 The. 5:11) “[Salini] kwa ajili ya mtu na mwenzake.”—Yak. 5:16. w23.11 47:7-8

Jumatano, Juni 18

Shangilieni katika tumaini.—Rom. 12:12.

Kila siku, tunafanya maamuzi ambayo yanahitaji imani yenye nguvu. Kwa mfano, tunafanya maamuzi kuhusu watu tunaoshirikiana nao, burudani, elimu, ndoa, watoto, na kazi ya kimwili. Ni vizuri tujiulize hivi: ‘Je, maamuzi yangu yanaonyesha nina uhakika kwamba mfumo huu hautaendelea kuwepo sikuzote, na hivi karibuni Mungu ataleta ulimwengu mpya? Au je, maamuzi yangu yanaongozwa na watu ambao wanaishi kana kwamba kifo ndio mwisho wa mambo yote?’ (Mt. 6:​19, 20; Luka 12:​16-21) Tutafanya maamuzi bora ikiwa tutaimarisha imani yetu kwamba ulimwengu mpya utafika hivi karibuni. Pia, tunakabili majaribu ambayo yanahitaji imani yenye nguvu. Huenda tukapatwa na mateso, ugonjwa mbaya, au mambo mengine yanayoweza kutuvunja moyo. Huenda mwanzoni tukahisi kwamba tutaweza kuvumilia majaribu hayo. Lakini ikiwa yataendelea kwa muda mrefu—kama inavyokuwa mara nyingi inapohusu majaribu—tutahitaji kuwa na imani yenye nguvu ili tuvumilie na tuendelee kumtumikia Yehova kwa shangwe.—1 Pet. 1:​6, 7. w23.04 19:4-5

Alhamisi, Juni 19

Salini bila kuacha.—1 The. 5:17.

Yehova anatarajia tutende kulingana na sala zetu. Kwa mfano, ndugu anaweza kumwomba Yehova amsaidie kupata ruhusa kazini ili aweze kuhudhuria kusanyiko la eneo. Yehova anaweza kujibuje sala hiyo? Huenda akampa ndugu huyo ujasiri anaohitaji ili aweze kuzungumza na mwajiri wake. Lakini ndugu huyo bado anahitaji kutenda kulingana na sala yake kwa kwenda kuomba ruhusa. Huenda akahitaji kwenda kwa mwajiri tena na tena ili kuomba ruhusa. Hata anaweza kuomba kubadilishana zamu na mfanyakazi mwenzake au huenda akachukua likizo ya bila malipo. Yehova anatarajia tusali tena na tena kuhusu mahangaiko yetu. Kulingana na maneno ya Yesu, baadhi ya maombi yetu hayatajibiwa papo hapo. (Luka 11:9) Hivyo usife moyo! Sali tena na tena na kwa bidii. (Luka 18:​1-7) Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yehova kwamba jambo hilo ni muhimu kwetu. Pia, tunaonyesha kwamba tuna imani katika uwezo wake wa kutusaidia. w23.11 49:10-11

Ijumaa, Juni 20

Tumaini halikatishi tamaa.—Rom. 5:5.

Yehova alimwahidi Abrahamu, rafiki yake, kwamba mataifa yote duniani yangebarikiwa kupitia uzao wake. (Mwa. 15:5; 22:18) Kwa sababu Abrahamu alikuwa na imani yenye nguvu katika Mungu, alikuwa na uhakika kwamba ahadi ya Mungu ingetimia. Hata hivyo, Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na mke wake miaka 90, wenzi hao waaminifu bado hawakuwa na mwana. (Mwa. 21:​1-7) Ingawa hivyo, Biblia inasema hivi: “Kwa kutegemea tumaini, [Abrahamu] alikuwa na imani kwamba angekuwa baba ya mataifa mengi kulingana na yale yaliyokuwa yamesemwa.” (Rom. 4:18) Unajua kwamba tumaini la Abrahamu lilitimizwa. Alikuja kuwa baba ya mwana ambaye alimsubiri kwa muda mrefu, Isaka. Kwa nini Abrahamu alikuwa na uhakika kwamba Yehova angetimiza ahadi yake? Kwa sababu alikuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova, Abrahamu alikuwa na ‘uhakika kamili kwamba kile alichoahidi Mungu’ kingetimia. (Rom. 4:21) Yehova alimkubali Abrahamu na kumtangaza kuwa mwadilifu kwa sababu ya imani yake.—Yak. 2:23. w23.12 51:1-2

Jumamosi, Juni 21

Mtu aliye mwaminifu katika lililo dogo ni mwaminifu katika lililo kubwa pia, na mtu asiye mwaminifu katika lililo dogo si mwaminifu katika lililo kubwa pia.—Luka 16:10.

Mwanamume kijana anayetegemeka, anatimiza majukumu yake yote kwa bidii. Fikiria mfano mkamilifu wa Yesu. Hakuwahi kamwe kuwa mzembe au kutotimiza majukumu yake. Badala yake, alitimiza migawo ambayo Yehova alimpa, hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. Aliwapenda watu—hasa wanafunzi wake—na alikuwa tayari kutoa uhai wake kwa ajili yao. (Yoh. 13:1) Mwige Yesu, kwa kutimiza kwa bidii mgawo wowote unaopewa. Ikiwa hujui jinsi ya kutimiza mgawo huo, uwe mnyenyekevu na uwaombe msaada ndugu wakomavu. Usiridhike kamwe na kutimiza mambo machache. (Rom. 12:11) Badala yake, kamilisha mgawo wako, na kuufanya “kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.” (Kol. 3:23) Bila shaka, wewe si mkamilifu, hivyo, uwe mwenye kiasi na ukubali makosa yoyote unayofanya.—Met. 11:2. w23.12 53:8

Jumapili, Juni 22

Amebarikiwa mtu anayemtumaini Yehova.—Yer. 17:7.

Tunafurahi sana tunapobatizwa na kuwa sehemu ya familia ya Yehova. Wale walio na pendeleo hilo wanaweza kukubaliana na mtunga zaburi Daudi aliyesema hivi: ‘Mwenye furaha ni yule ambaye Yehova amemchagua na kumleta karibu ili akae katika nyua zake. (Zab. 65:4) Yehova hamleti mtu yeyote tu kwenye nyua zake. Anachagua wale ambao wamethibitisha kwamba wanataka kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Yak. 4:8) Unapojiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa, unaweza kuwa na uhakika kwamba baada ya kubatizwa, ‘atakumwagia baraka hivi kwamba hutakosa chochote.’ (Mal. 3:10; Yer. 17:8) Ubatizo ndio mwanzo tu wa maisha yako ya kumtumikia Yehova. Utatamani kujitahidi kuishi kulingana na ahadi uliyotoa ulipojiweka wakfu, hata utakapokabili vishawishi au majaribu ya imani. (Mhu. 5:​4, 5) Ukiwa mwanafunzi wa Yesu, utafuata kadiri uwezavyo mfano na maagizo ya Yesu kwa ukaribu zaidi.—Mt. 28:​19, 20; 1 Pet. 2:21. w24.03 10:1-3

Jumatatu, Juni 23

Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.—Mwa. 2:24.

Namna gani ikiwa wewe na mwenzi wako hamfurahii kutumia muda pamoja? Unaweza kufanya nini? Fikiria moto wa kuni. Hauwaki na kuwa mkali papo hapo. Unahitaji kuanza na kuni ndogo kisha uongeze kuni kubwa zaidi hatua kwa hatua. Vivyo hivyo, kwa nini msianze kwa kutumia muda mfupi pamoja kila siku? Hakikisheni kwamba mnafanya jambo ambalo nyote wawili mnafurahia. (Yak. 3:18) Mkianza na mambo madogo, mnaweza kuimarisha tena upendo wenu. Heshima ni sifa muhimu katika ndoa. Ni kama hewa ya oksijeni inayosaidia moto wa kuni kuwa mkali. Bila oksijeni, moto unaweza kuzima kwa urahisi. Vivyo hivyo, bila kuonyeshana heshima, wenzi wa ndoa wanaweza kutambua kwamba upendo wao unapoa upesi. Kwa upande mwingine, mume na mke wanaojitahidi kuonyeshana heshima watadumisha upendo kati yao. Hata hivyo, kumbuka kwamba jambo muhimu si kuwa wewe unafikiri unaonyesha heshima, bali mwenzi wako anapaswa kuhisi anaheshimiwa. w23.05 23:9, 14-15

Jumanne, Juni 24

Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.—Zab. 94:19.

Katika Biblia, watumishi waaminifu wa Mungu wameeleza kuhusu pindi walizotaabika na kuogopa kwa sababu ya maadui au matatizo mengine. (Zab. 18:4; 55:​1, 5) Vivyo hivyo, tunaweza kukabili upinzani shuleni, kazini, kutoka kwa watu wa familia, au serikali. Huenda hata tukaogopa kwamba tutakufa kwa sababu ya matatizo ya afya. Katika pindi hizo, huenda tukahisi kama mtoto mdogo asiye na msaada. Yehova anatusaidiaje katika hali kama hizo? Anatufariji na kutubembeleza. Hivyo, tumia wakati kwa ukawaida pamoja na Yehova—kwa kusali na kusoma Neno lake. (Zab. 77:​1, 12-14) Kisha unapokuwa chini ya mkazo, ni wazi kwamba utafikiria kumwendea kwanza Baba yako wa mbinguni. Mweleze Yehova mambo yanayokuogopesha na kukuhangaisha. Mruhusu azungumze nawe na kukufariji kupitia Maandiko.—Zab. 119:28. w24.01 3:14-16

Jumatano, Juni 25

Mungu ndiye ambaye . . . anawachochea, na kuwapa hamu na nguvu za kutenda.—Flp. 2:13.

Ni muhimu sana kuwa na motisha au kichocheo ili kutimiza malengo ya kiroho. Mtu mwenye kichocheo ana sababu nzuri sana ya kutimiza lengo lake au anatamani kujitahidi kulitimiza. Na kadiri tunavyochochewa zaidi, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kutimiza malengo yetu. Basi, unaweza kufanya nini ili uhisi umechochewa zaidi? Sali ili upate kichocheo zaidi. Kupitia roho yake takatifu, Yehova anaweza kukuchochea kutimiza lengo lako. Nyakati nyingine tunajiwekea lengo kwa sababu tunajua tunapaswa kufanya hivyo, na hilo ni jambo zuri. Lakini huenda kwa kweli tusiwe na tamaa ya kutimiza lengo hilo. Tafakari kuhusu mambo ambayo Yehova amekufanyia. (Zab. 143:5) Mtume Paulo alitafakari kuhusu fadhili zisizostahiliwa ambazo Yehova alimwonyesha, na hilo lilimchochea kufanya kazi ya Yehova kwa bidii. (1 Kor. 15:​9, 10; 1 Tim. 1:​12-14) Vivyo hivyo, kadiri unavyotafakari mambo ambayo Yehova amekufanyia, ndivyo utakavyochochewa zaidi kutimiza lengo lako.—Zab. 116:12. w23.05 24:3-5

Alhamisi, Juni 26

Lisifuni jina la Yehova.—Zab. 113:1.

Tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni tunapolisifu jina lake. (Zab. 119:108) Je, hilo linamaanisha kwamba Mungu Mweza-Yote ni kama wanadamu wanaotamani kusifiwa kwa sababu hawajiamini na wanahitaji kuhakikishiwa wanathaminiwa? Hapana. Tunapomsifu Baba yetu wa mbinguni, tunasaidia kupinga uwongo unaotuhusu kibinafsi. Shetani anadai kwamba hakuna mwanadamu atakayelitetea jina la Mungu kwa ushikamanifu. Anadai kuwa hakuna yeyote kati yetu aliye mtimilifu. Anasema kwamba sisi sote tutaacha kumtumikia Mungu ikiwa tunahisi kuwa tutanufaika kwa kufanya hivyo. (Ayu. 1:​9-11; 2:4) Lakini Ayubu aliyekuwa mwaminifu alithibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Namna gani wewe? Kila mmoja wetu ana pendeleo la kutetea kwa ushikamanifu jina la Baba yetu na kumfurahisha kwa kumtumikia kwa utimilifu. (Met. 27:11) Kwa kweli, ni pendeleo kubwa sana kufanya hivyo. w24.02 6:3-5

Ijumaa, Juni 27

Iweni na imani katika manabii wake, nanyi mtafanikiwa.—2 Nya. 20:20.

Baada ya siku za Musa na Yoshua, Yehova aliwainua waamuzi ili wawaongoze watu wake. Kisha, katika nyakati za wafalme, Yehova aliwaweka rasmi manabii ili wawaongoze watu wake. Wafalme waliokuwa waaminifu walitii ushauri wa manabii. Kwa mfano, kwa unyenyekevu Mfalme Daudi alikubali kurekebishwa na nabii Nathani. (2 Sam. 12:​7, 13; 1 Nya. 17:​3, 4) Mfalme Yehoshafati alimtegemea nabii Yahazieli ili kupata mwongozo na aliwatia moyo watu wa Yuda wawe “na imani katika manabii [wa Mungu].” (2 Nya. 20:​14, 15) Mfalme Hezekia alipokabili taabu, alimwomba msaada nabii Isaya. (Isa. 37:​1-6) Kila mara wafalme walipofuata mwongozo wa Yehova, walibarikiwa na taifa lililindwa. (2 Nya. 20:​29, 30; 32:22) Ilikuwa wazi kwamba Yehova alikuwa akiwatumia manabii ili kuongoza watu wake. w24.02 8:8

Jumamosi, Juni 28

Msishirikiane nao.—Efe. 5:7.

Shetani anataka tushirikiane na watu ambao watafanya iwe vigumu kwetu kushikamana na viwango vya Yehova. Tunahitaji kukumbuka kwamba watu tunaoshirikiana nao, si wale tu tunaokutana nao uso kwa uso. Wanatia ndani wale ambao tunawasiliana nao kwenye mitandao ya kijamii. Tunapaswa kupinga mawazo ya ulimwengu kwamba mwenendo mpotovu kiadili unakubalika. Tunajua kwamba mawazo hayo si sahihi. (Efe. 4:​19, 20) Itafaa tujiulize hivi: ‘Je, ninakuwa mwangalifu na kuepuka kushirikiana isivyo lazima na wafanyakazi wenzangu, wanafunzi wenzangu, au watu wengine ambao hawaheshimu viwango vya uadilifu vya Yehova? Je, ninashikamana na viwango vya Yehova kwa ujasiri hata ikiwa baadhi ya watu wanasema nina ubaguzi kwa sababu ya kufanya hivyo?’ Kama inavyoonyeshwa kwenye 2 Timotheo 2:​20-22, tunahitaji pia kuwa waangalifu tunapochagua watu tunaoshirikiana nao ndani ya kutaniko la Kikristo. Tunahitaji kukumbuka kwamba baadhi ya watu hawawezi kutusaidia tuendelee kuwa waaminifu katika utumishi wetu kwa Yehova. w24.03 12:11-12

Jumapili, Juni 29

Yehova ni mwenye upendo mwororo sana.—Yak. 5:11.

Je, umewahi kuwazia jinsi Yehova alivyo? Ingawa hatuwezi kumwona Yehova, Biblia inamfafanua kwa njia mbalimbali. Yehova anafafanuliwa kuwa “jua na ngao” na “moto unaoteketeza.” (Zab. 84:11; Ebr. 12:29) Uwepo wake unafananishwa na jiwe la yakuti, mchanganyiko wa dhahabu na fedha unaong’aa, na upinde wa mvua maridadi. (Eze. 1:​26-28) Kwa kuwa hatuwezi kumwona Yehova, huenda isiwe rahisi kuamini kwamba anatupenda. Baadhi ya watu wanahisi kwamba Yehova hawezi kuwapenda kamwe kwa sababu ya mambo mabaya waliyopitia maishani. Yehova anaelewa hisia hizo na jinsi zinavyotuathiri. Ili kutusaidia, anafunua katika Neno lake sifa zake zenye kuvutia. Neno moja linalomfafanua vizuri zaidi Yehova ni upendo. Biblia inasema kwamba “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) Kila kitu anachofanya kinachochewa na upendo. Upendo wa Mungu ni mwingi sana na ni wenye nguvu sana hivi kwamba anauonyesha hata kwa watu wasiompenda.—Mt. 5:​44, 45. w24.01 4:1-3

Jumatatu, Juni 30

Alikuwa akiongea nao kutoka katika nguzo ya wingu.—Zab. 99:7.

Yehova alimweka rasmi Musa awaongoze Waisraeli walipokuwa wakiondoka Misri, na aliandaa uthibitisho ulionekana wazi alipowapatia nguzo ya wingu mchana na nguzo ya moto usiku. (Kut. 13:21) Musa alifuata nguzo hiyo ambayo ilimwongoza yeye na Waisraeli hadi kwenye Bahari Nyekundu. Watu waliingiwa na hofu walipofikiri kwamba hawana pa kukimbilia, wakiwa kati ya bahari na jeshi la Wamisri lililokuwa likiwafuatilia. Lakini hawakuwa wameongozwa kimakosa. Kupitia Musa, Yehova alikuwa amewaongoza kimakusudi watu wake wafike mahali hapo. (Kut. 14:2) Kisha, Mungu akawakomboa kwa njia yenye kustaajabisha sana. (Kut. 14:​26-28). Kwa miaka 40 baada ya hapo, Musa aliendelea kuitegemea nguzo ya wingu ili kuwaongoza watu wa Mungu nyikani. (Kut. 33:​7, 9, 10) Yehova alizungumza na Musa kutoka katika nguzo hiyo, naye Musa aliwasilisha maagizo ya Yehova kwa watu. Waisraeli walikuwa na uthibitisho wa kutosha kwamba Yehova alikuwa akimtumia Musa ili kuwaongoza. w24.02 8:4-5

    Tanzanian sign language publications(2020-2025)
    Toka
    Ingia
    • Lugha ya Alama ya Tanzania
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki