Agosti
Ijumaa, Agosti 1
Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.—Zab. 34:19.
Ona mambo mawili muhimu katika Zaburi hiyo: (1) Watu waadilifu hukabili matatizo. (2) Yehova hutukomboa kutoka katika majaribu yetu. Yehova hutukomboa jinsi gani? Njia moja ni kwa kutusaidia kuona mambo kihalisi kwenye mfumo huu wa mambo. Ingawa Yehova anatuahidi kwamba tutapata shangwe tunapomtumikia, hajatuhakikishia kwamba hatutapatwa na matatizo sasa. (Isa. 66:14) Anatuhimiza tukazie fikira wakati ujao—wakati ambapo tutaishi maisha anayotaka tufurahie milele. (2 Kor. 4:16-18) Kwa sasa, anatusaidia kuendelea kumtumikia kila siku. (Omb. 3:22-24) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mifano ya waabudu waaminifu wa Yehova wanaotajwa katika Biblia na wa nyakati zetu? Huenda tukakabili matatizo tusiyotarajia. Lakini tunapomtegemea Yehova, atatutegemeza sikuzote.—Zab. 55:22. w23.04 17:3-4
Jumamosi, Agosti 2
[Jitiishe] kwa mamlaka zilizo kubwa.—Rom. 13:1.
Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Yosefu na Maria, ambao walikuwa tayari kutii mamlaka zilizo kubwa hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Luka 2:1-6) Maria alipokuwa mjamzito kwa kipindi cha miezi tisa hivi, yeye na Yosefu walikabili jaribu la kutii. Augusto, ambaye alitawala Milki ya Roma, aliamuru watu wote waandikishwe. Yosefu na Maria walilazimika kusafiri kwenda Bethlehemu, safari ya kilomita 150 hivi wakipitia katika eneo lenye milima-milima. Safari hiyo haikuwa rahisi, hasa kwa Maria. Huenda wenzi hao walihofia usalama wao na wa mtoto wao ambaye bado hakuwa amezaliwa. Namna gani ikiwa Maria angepatwa na uchungu wa kuzaa wakiwa njiani? Tumboni mwake alikuwa amembeba Masihi wa wakati ujao. Je, wangetumia hali hiyo kuwa kisingizio cha kutotii serikali? Yosefu na Maria hawakuruhusu mahangaiko hayo yaamue ikiwa watatii sheria. Yehova aliwabariki kwa kutii. Maria aliwasili salama Bethlehemu, akajifungua mtoto mwenye afya, na hata akasaidia kutimiza unabii wa Biblia!—Mika 5:2. w23.10 42:9, 11-12
Jumapili, Agosti 3
Tutiane moyo.—Ebr. 10:25.
Namna gani ikiwa una wasiwasi wa kutoa maelezo katika mikutano? Unaweza kunufaika ikiwa utajitayarisha vizuri. (Met. 21:5) Kadiri unavyofahamu vizuri zaidi habari inayozungumziwa, ndivyo itakavyokuwa rahisi kwako kutoa maelezo. Pia, toa maelezo mafupi. (Met. 15:23; 17:27) Jibu fupi litakupunguzia wasiwasi. Unapotoa maelezo mafupi kwa maneno yako mwenyewe, utaonyesha kwamba umejitayarisha vizuri na kwamba unaelewa vizuri habari inayozungumziwa. Namna gani ikiwa utajaribu kutumia baadhi ya mapendekezo hayo, lakini bado uwe na wasiwasi kuhusu kutoa maelezo zaidi ya mara moja au mbili? Uwe na uhakika kwamba Yehova atathamini jitihada zako za kutoka moyoni za kufanya kile unachoweza. (Luka 21:1-4) Kutoa kilicho bora hakumaanishi kufanya jambo linalozidi uwezo wako. (Flp. 4:5) Amua jambo unaloweza kufanya, weka lengo la kulifanya, na usali ili uwe na moyo mtulivu. Mwanzoni, huenda lengo hilo likawa kutoa maelezo mafupi mara moja. w23.04 18:6-8
Jumatatu, Agosti 4
[Vaa] bamba la kifuani . . . na . . . kofia ya chuma.—1 The. 5:8.
Mtume Paulo anatulinganisha na wanajeshi walio chonjo na waliovaa mavazi ya kivita. Mwanajeshi aliye kwenye zamu anatarajiwa kuwa tayari kwa ajili ya vita wakati wowote. Hali yetu iko hivyo pia. Tunaendelea kuwa tayari kwa ajili ya siku ya Yehova kwa kuvaa bamba la kifuani la imani na upendo na kofia ya chuma ya tumaini. Bamba la kifuani lililinda moyo wa mwanajeshi. Imani na upendo hulinda moyo wetu wa mfano. Sifa hizo zitatusaidia kuendelea kumtumikia Mungu na kumfuata Yesu. Imani inatuhakikishia kwamba Yehova atatuthawabisha tukiendelea kumtafuta kwa moyo wetu wote. (Ebr. 11:6) Itatuchochea kuendelea kuwa washikamanifu kwa Kiongozi wetu, Yesu, hata ikiwa tutakabili hali ngumu. Tunaweza kuimarisha imani yetu ili tukabiliane na hali ngumu maishani kwa kujifunza kutokana na mifano ya siku zetu ya watu waliodumisha utimilifu wao licha ya mateso au hali ngumu za kiuchumi. Na tunaweza kuepuka mtego wa kujikusanyia vitu vya kimwili kwa kuwaiga wale ambao walirahisisha maisha yao ili kutanguliza masilahi ya Ufalme. w23.06 26:8-9
Jumanne, Agosti 5
Anayetazama mawingu hatavuna.—Mhu. 11:4.
Sifa ya kujizuia inamaanisha uwezo wa kudhibiti hisia na matendo yetu. Tunahitaji sifa ya kujizuia ili tuchochewe kufikia malengo yetu, hasa ikiwa lengo tunalotaka kufikia ni gumu au tumekosa kichocheo. Kumbuka, sifa ya kujizuia ni sehemu ya tunda la roho, basi mwombe Yehova akupatie roho takatifu ili ikusaidie kusitawisha sifa hiyo muhimu. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Usisubiri mpaka hali ziwe nzuri kabisa. Katika ulimwengu huu, inaelekea kwamba hatutakuwa kamwe na hali zinazofaa kabisa. Ikiwa tutasubiri hali zinazofaa, huenda tusitimize kamwe lengo letu. Huenda tukakosa kichocheo kwa sababu inaonekana kwamba ni vigumu sana kutimiza lengo letu. Ikiwa unakabili hali hiyo, je, unaweza kugawa lengo lako ili liwe malengo madogo-madogo? Ikiwa una lengo la kusitawisha sifa fulani, kwa nini usianze kujitahidi kuionyesha kwa njia ndogo? Ikiwa lengo lako ni kusoma Biblia nzima, je, unaweza kuanza kwa kupanga vipindi vifupi zaidi vya kusoma? w23.05 24:11-13
Jumatano, Agosti 6
Kijia cha waadilifu ni kama nuru nyangavu ya asubuhi, inayong’aa zaidi na zaidi mpaka mchana kamili.—Met. 4:18.
Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Yehova ametumia tengenezo lake kuendelea kuandaa chakula cha kiroho ili kutusaidia sisi sote tuendelee kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” (Isa. 35:8; 48:17; 60:17) Tunaweza kusema kwamba kila mara mtu anapokubali kujifunza Biblia, anapata nafasi ya kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” Baada ya kutembea kwa muda mfupi, baadhi yao huacha kutembea katika barabara hiyo kuu. Wengine wameazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo hadi watakapofika mwisho wa safari yao. Mwisho huo wa safari ni nini? Kwa wale ambao wana tumaini la kwenda mbinguni, “Njia ya Utakatifu” inaongoza kwenye “paradiso ya Mungu” huko mbinguni. (Ufu. 2:7) Kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani, barabara hiyo kuu itaongoza kwenye ukamilifu mwishoni mwa ile miaka 1,000. Ikiwa leo unatembea katika barabara hiyo kuu, usitazame nyuma. Na usiondoke kwenye barabara hiyo hadi utakapomaliza safari yako na kuingia katika ulimwengu mpya! w23.05 22:15-18
Alhamisi, Agosti 7
Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.—1 Yoh. 4:19.
Unapofikiria mambo yote ambayo Yehova amekufanyia utamthamini sana na utataka kujiweka wakfu kwake. (Zab. 116:12-14) Biblia inamwita kwa usahihi Yehova kuwa ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17) Zawadi bora zaidi kuliko zote ni dhabihu ya Yesu, Mwana wake. Hebu fikiria! Fidia imekuwezesha kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Na imekupatia tumaini la kuishi milele. (1 Yoh. 4:9, 10) Kujiweka wakfu kwa Yehova ni njia ya kuonyesha shukrani kwa ajili ya upendo huo mkubwa zaidi ambao amekuonyesha, pamoja na baraka nyingine ambazo Yehova amekupatia.—Kum. 16:17; 2 Kor. 5:15. w24.03 9:8
Ijumaa, Agosti 8
Mtu anayetembea kwa unyoofu wake anamwogopa Yehova.—Met. 14:2.
Kuhusu viwango vya maadili vilivyo katika ulimwengu huu, tunahisi kama Loti mwadilifu. ‘Alitaabishwa sana na mwenendo mpotovu wa waasi sheria,’ kwa sababu alijua kwamba Baba yetu wa mbinguni anachukia mwenendo mbaya. (2 Pet. 2:7, 8) Kumwogopa na kumpenda Mungu kulimchochea Loti akatae mwenendo mpotovu wa watu waliomzunguka. Sisi pia tumezungukwa na watu ambao wanapuuza viwango vya maadili vya Yehova. Ingawa hivyo, tunaweza kuendelea kuwa safi kiadili ikiwa tutaendelea kumpenda Mungu na kusitawisha woga unaofaa kumwelekea. Ili kutusaidia, Yehova anatutia moyo kwa upendo na kutuchochea kupitia kitabu cha Methali. Wakristo wote wanaume na wanawake, vijana na wazee, wanaweza kunufaika sana kwa kuchunguza ushauri wenye hekima ulio katika kitabu hicho. Ikiwa tunamwogopa Yehova, tutakuwa waangalifu na kuepuka kushirikiana na watu wanaotenda mabaya. w23.06 28:1-2, 5
Jumamosi, Agosti 9
Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso siku baada ya siku na aendelee kunifuata.—Luka 9:23.
Huenda umekabili upinzani kutoka kwa watu wa familia, au labda umeacha kufuatilia mambo fulani ya kimwili ili utangulize masilahi ya Ufalme. (Mt. 6:33) Ikiwa ndivyo, uwe na uhakika kwamba Yehova anatambua mambo yote unayofanya kwa ajili yake. (Ebr. 6:10) Inawezekana umejionea ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hakuna mtu aliyeacha nyumba au ndugu au dada au mama au baba au watoto au mashamba kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema ambaye hatapata mara 100 sasa katika kipindi hiki—nyumba, ndugu, dada, mama, watoto, mashamba, pamoja na mateso—na katika mfumo wa mambo unaokuja, uzima wa milele.” (Marko 10:29, 30) Kwa kweli, baraka ambazo umepata ni nyingi zaidi ukilinganisha na jambo lolote ulilojidhabihu.—Zab. 37:4. w24.03 10:5
Jumapili, Agosti 10
Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.—Met. 17:17.
Wakristo huko Yudea walipokabili njaa kali, akina ndugu katika kutaniko la Antiokia “wakaamua kila mmoja kulingana na uwezo wake, watume msaada kwa akina ndugu walioishi Yudea.” (Mdo. 11:27-30) Ingawa akina ndugu waliokabili njaa waliishi eneo la mbali, Wakristo huko Antiokia waliazimia kuwasaidia. (1 Yoh. 3:17, 18) Leo, sisi pia tunaweza kuonyesha huruma tunapopata habari kwamba waabudu wenzetu wamepatwa na msiba. Tunaitikia upesi—labda kwa kuwauliza wazee ikiwa tunaweza kusaidia katika kazi ya kutoa msaada, kwa kutoa mchango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, au kwa kusali kwa ajili ya wale walioathiriwa na msiba. Huenda ndugu na dada zetu wakahitaji pia msaada ili kupata mahitaji yao ya msingi. Mfalme wetu, Kristo Yesu, atakapokuja kutekeleza hukumu, tungependa atupate tukionyesha huruma, kisha atupatie mwaliko wa ‘kuurithi Ufalme.’—Mt. 25:34-40. w23.07 29:9-10, 12
Jumatatu, Agosti 11
Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote.—Flp. 4:5.
Yesu aliiga usawaziko wa Yehova. Alitumwa duniani ili awahubirie “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Lakini alikuwa mwenye usawaziko alipokuwa akitimiza mgawo huo. Pindi moja, mwanamke asiye Mwisraeli alimsihi Yesu amponye binti yake ambaye alikuwa “anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.” Kwa huruma, Yesu alifanya jambo ambalo mwanamke huyo alimwomba na akamponya binti yake. (Mt. 15:21-28) Fikiria mfano mwingine. Mwanzoni mwa huduma yake, Yesu alisema hivi: “Yeyote anayenikana . . . , mimi pia nitamkana.” (Mt. 10:33) Lakini je, alimkana Petro alipomkana mara tatu? Hapana. Yesu alijua kwamba Petro alitubu na alikuwa mwenye imani. Baada ya kufufuliwa, Yesu alimtokea Petro na inaelekea alimhakikishia kwamba amemsamehe na anampenda. (Luka 24:33, 34) Yehova Mungu na Yesu Kristo ni wenye usawaziko. Namna gani sisi? Yehova anatarajia tuwe wenye usawaziko. w23.07 32:6-7
Jumanne, Agosti 12
Kifo hakitakuwapo tena.—Ufu. 21:4.
Ni uhakikisho gani tunaoweza kushiriki na wale ambao wana shaka kwamba ahadi ya Mungu ya Paradiso itatimia? Kwanza, Yehova mwenyewe ndiye anayetoa ahadi hiyo. Kitabu cha Ufunuo kinasema: “Yule aliyeketi kwenye kiti cha ufalme akasema: ‘Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.’” Yeye ana hekima, nguvu, na tamaa ya kutimiza ahadi yake. Pili, utimizo wa ahadi hiyo ni hakika kabisa, hivi kwamba kwa maoni ya Yehova tayari mambo hayo yametukia. Ndiyo sababu anasema: “Maneno haya ni ya uaminifu na ya kweli. . . . Yametimia!” Tatu, Yehova anapoanza kufanya jambo, anahakikisha linakamilika kwa mafanikio, kama inavyothibitishwa na maneno haya: “Mimi ndiye Alfa na Omega.” (Ufu. 21:6) Yehova atathibitisha kwamba Shetani ni mwongo na ameshindwa. Hivyo, mtu anaposema, “Ahadi hii haiwezi kutimia,” unaweza kusoma na kufafanua Ufunuo 21:5, 6. Mwonyeshe jinsi ambavyo Yehova ametoa uhakikisho wa ahadi yake, kwa kuitia saini yake mwenyewe kwa njia ya mfano.—Isa. 65:16. w23.11 46:18-19
Jumatano, Agosti 13
Nitakufanya kuwa taifa kubwa.—Mwa. 12:2.
Yehova alitoa ahadi hiyo kwa Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 75 na bila mtoto. Je, Abrahamu aliona ahadi hiyo ikitimizwa? Hakuona ikitimizwa kikamili. Baada ya kuvuka Mto Efrati na kusubiri kwa miaka 25, Abrahamu aliona mwana wake, Isaka, akizaliwa kimuujiza, na baada ya miaka mingine 60, wajukuu wake, Esau na Yakobo walizaliwa. (Ebr. 6:15) Lakini Abrahamu hakuona kamwe wazao wake wakiwa taifa kubwa na kurithi Nchi ya Ahadi. Hata hivyo, mwanamume huyo mwaminifu alifurahia urafiki wa karibu pamoja na Muumba wake. (Yak. 2:23) Na Abrahamu atakapofufuliwa, atasisimka sana kujua kwamba imani na subira yake ilitokeza baraka kwa mataifa yote! (Mwa. 22:18) Somo ni nini? Huenda sisi binafsi hatutaona ahadi zote za Yehova zikitimizwa moja kwa moja. Hata hivyo, ikiwa tutakuwa wenye subira kama Abrahamu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatuthawabisha sasa na kwa njia kubwa hata zaidi katika ulimwengu mpya alioahidi.—Marko 10:29, 30. w23.08 35:14
Alhamisi, Agosti 14
Wakati alipokuwa akimtafuta Yehova, Mungu wa kweli alimfanikisha.—2 Nya. 26:5.
Alipokuwa kijana Mfalme Uzia alikuwa mnyenyekevu. Alijifunza “kumwogopa Mungu wa kweli.” Aliishi kwa miaka 68, na kwa sehemu kubwa ya maisha yake Yehova alimbariki. (2 Nya. 26:1-4) Uzia aliwashinda maadui wengi na aliimarisha ulinzi wa jiji la Yerusalemu. (2 Nya. 26:6-15) Bila shaka, Uzia alifurahia mambo yote ambayo Mungu alimsaidia kufanya. (Mhu. 3:12, 13) Mfalme Uzia alizoea kuwapa watu maagizo. Je, hilo lilimfanya afikiri kwamba angeweza kufanya chochote alichotaka? Siku moja, Uzia aliingia katika hekalu la Yehova na kwa kimbelembele alijaribu kufukiza uvumba kwenye madhabahu, jambo ambalo wafalme hawakuruhusiwa kufanya. (2 Nya. 26:16-18) Kuhani Mkuu Azaria alijaribu kumrekebisha, lakini Uzia alikasirika sana. Kwa kusikitisha, Uzia aliharibu rekodi yake ya kutumikia kwa uaminifu na Yehova akampiga kwa ukoma. (2 Nya. 26:19-21) Maisha yake yangekuwa tofauti sana ikiwa angeendelea kuwa mnyenyekevu! w23.09 38:9-10
Ijumaa, Agosti 15
Akajitenga kwa kuwaogopa wale waliotahiriwa.—Gal. 2:12.
Hata baada ya kuwa Mkristo aliyetiwa mafuta, bado mtume Petro alipambana na udhaifu wake mbalimbali. Mwaka wa 36 W.K., Petro alikuwepo wakati Kornelio, Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, alipotiwa mafuta kwa roho takatifu, jambo lililothibitisha wazi kwamba “Mungu hana ubaguzi” na kwamba watu wa mataifa wangekuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo. (Mdo. 10:34, 44, 45) Baada ya hapo, Petro alijihisi huru kula chakula pamoja na Watu wa Mataifa, jambo ambalo hangeweza kufanya kamwe hapo awali. Hata hivyo, baadhi ya Wakristo Wayahudi walihisi kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa hawapaswi kula pamoja. Baadhi ya watu waliokuwa na maoni hayo walipokuja huko Antiokia, Petro aliacha kula pamoja na ndugu zake waliokuwa Watu wa Mataifa, inawezekana ni kwa sababu aliogopa kuwakasirisha Wakristo Wayahudi. Mtume Paulo alipoona unafiki huo alimkemea Petro hadharani. (Gal. 2:13, 14) Licha ya kufanya kosa hilo, Petro aliendelea kuwa mwaminifu. w23.09 40:8
Jumamosi, Agosti 16
Atawapa msingi imara.—1 Pet. 5:10.
Jichunguze kwa unyoofu ili kutambua udhaifu wowote ulio nao, lakini usivunjike moyo. “Bwana ni mwenye fadhili,” na atakusaidia kufanya maendeleo. (1 Pet. 2:3) Mtume Petro anatuhakikishia hivi: “Mungu . . . mwenyewe atamaliza mazoezi yenu. Atafanya muwe imara.” Pindi moja, Petro alihisi kwamba hastahili kuwa pamoja na Mwana wa Mungu. (Luka 5:8) Lakini kwa msaada wa upendo kutoka kwa Yehova na Yesu, Petro aliendelea kuwa mwaminifu akiwa mfuasi wa Kristo. Hivyo, Petro alipata kibali cha “kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:11) Hiyo ilikuwa baraka iliyoje! Ikiwa utaendelea kuwa mwaminifu kama Petro alivyofanya na kukubali kuzoezwa na Yehova, wewe pia utapata thawabu ya uzima wa milele. ‘Utafikia lengo la imani yako, wokovu wako.’—1 Pet. 1:9. w23.09 41:16-17
Jumapili, Agosti 17
Mwabuduni Yule aliyeziumba mbingu na dunia.—Ufu. 14:7.
Hema la ibada la kale lilikuwa na ua mmoja—eneo lililo wazi ambalo lilikuwa limezungushiwa wigo au ukingo, mahali ambapo makuhani walitimiza majukumu yao. Madhabahu kubwa ya shaba ya dhabihu za kuteketezwa ilikuwa katika ua pamoja na beseni kubwa la maji la shaba ambalo makuhani walitumia kujitakasa kabla ya kutimiza utumishi wao mtakatifu. (Kut. 30:17-20; 40:6-8) Leo, watiwa-mafuta waliobaki duniani ambao ni ndugu za Kristo wanatumikia kwa uaminifu katika ua wa ndani wa hekalu la kiroho duniani. Kuwepo kwa beseni kubwa la maji ni kikumbusho muhimu kwao, na kwa Wakristo wote cha kuendelea kuwa safi kiadili na kiroho. Basi, wale wanaofanyiza “umati mkubwa,” wanamwabudu Yehova wakiwa wapi? Mtume Yohana aliwaona wakiwa “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme,” sehemu ambayo inalingana na ua wa nje duniani, ambapo “wanamtolea [Mungu] utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufu. 7:9, 13-15) Tunathamini sana pendeleo la kushiriki katika mpango wa ibada safi ya Yehova! w23.10 45:15-16
Jumatatu, Agosti 18
Kwa sababu ya ahadi ya Mungu, . . . alikuwa mwenye nguvu kwa imani yake.—Rom. 4:20.
Njia moja ambayo Yehova anatupatia nguvu ni kupitia wazee wa kutaniko. (Isa. 32:1, 2) Basi unapohisi wasiwasi, waeleze wazee wa kutaniko mambo yanayokuhangaisha. Wanapokupatia msaada, usisite kuukubali. Kupitia kwao, Yehova anaweza kukupa nguvu. Tumaini letu linalotegemea Biblia la kupata uzima wa milele—iwe ni katika dunia Paradiso au katika Ufalme wa mbinguni—linaweza pia kutujaza nguvu. (Rom. 4:3, 18, 19) Tumaini letu linatutia nguvu ili tuendelee kuvumilia majaribu, tuhubiri habari njema, na tutimize migawo mbalimbali kutanikoni. (1 The. 1:3) Tumaini hilohilo lilimtia nguvu mtume Paulo. Alikuwa ‘amekandamizwa,’ ‘kufadhaishwa,’ ‘kuteswa,’ na ‘kuangushwa chini.’ Hata uhai wake ulikuwa hatarini. (2 Kor. 4:8-10) Paulo alipata nguvu za kuvumilia kwa kukazia fikira tumaini lake. (2 Kor. 4:16-18) Paulo alikazia fikira tumaini lake la wakati wake ujao la kuishi milele mbinguni. Paulo alitafakari kuhusu tumaini hilo. Na matokeo ni kwamba alihisi “anafanywa upya siku kwa siku.” w23.10 43:14-17
Jumanne, Agosti 19
Yehova atawapa nguvu watu wake. Yehova atawabariki watu wake kwa amani.—Zab. 29:11.
Unaposali, fikiria ikiwa huu ndio wakati wa Yehova wa kujibu ombi lako. Huenda tukahisi kwamba tunahitaji kupata jibu la sala zetu papo hapo. Lakini ukweli ni kwamba Yehova anajua wakati unaofaa wa kutusaidia. (Ebr. 4:16) Sala yetu isipojibiwa papo hapo, huenda tukahisi kwamba jibu la Yehova ni ‘Hapana.’ Lakini jibu la Yehova linaweza kuwa ‘Bado wakati haujafika.’ Kwa mfano, ndugu kijana aliomba aponywe ugonjwa wake mbaya. Lakini akaendelea kuugua. Ikiwa Yehova angemponya kimuujiza, Shetani angeweza kudai kwamba ndugu huyo anaendelea kumtumikia Yehova kwa sababu tu ameponywa. (Ayu. 1:9-11; 2:4) Isitoshe, tayari Yehova amepanga wakati wa kuponya magonjwa yote. (Isa. 33:24; Ufu. 21:3, 4) Na mpaka wakati huo ufike, hatuwezi kutarajia kuponywa kimuujiza. Hivyo, ndugu huyo anaweza kumwomba Yehova ampatie nguvu na amani ya akili ili avumilie ugonjwa wake na kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu. w23.11 49:13
Jumatano, Agosti 20
Hajatutendea kulingana na dhambi zetu, wala hajatupa adhabu tuliyostahili kulingana na makosa yetu.—Zab. 103:10.
Samsoni alikuwa amefanya kosa zito lakini hakufa moyo. Alitafuta fursa ya kutimiza mgawo aliopewa na Mungu wa kupigana dhidi ya Wafilisti. (Amu. 16:28-30) Samsoni alimsihi hivi Yehova: “Acha niwalipize kisasi Wafilisti.” Mungu wa kweli alijibu ombi la Samsoni na kumrudishia nguvu zake za kipekee. Matokeo ni kwamba Samsoni aliwaua Wafilisti wengi zaidi pindi hiyo kuliko alivyofanya hapo awali. Ingawa Samsoni alipatwa na matokeo mabaya kwa sababu ya kosa lake, aliendelea kujitahidi kufanya mapenzi ya Yehova. Hata ikiwa tutafanya kosa na kuhitaji kukaripiwa au kupoteza pendeleo fulani, hatupaswi kufa moyo. Kumbuka kwamba Yehova yuko tayari kutusamehe. (Zab. 103:8, 9) Licha ya makosa yetu, Yehova anaweza kutupatia nguvu za kufanya mapenzi yake kama alivyomsaidia Samsoni. w23.09 37:15-16
Alhamisi, Agosti 21
Uvumilivu [hutokeza] hali yenye kukubaliwa; nayo hali yenye kukubaliwa, tumaini.—Rom. 5:4.
Uvumilivu wako hukupatia kibali cha Yehova. Hilo halimaanishi kwamba Yehova anafurahi unapokabili majaribu au matatizo. Wewe ndiye anayekukubali. Uvumilivu wako hutokeza hali yenye kukubaliwa. Baraka bora sana! (Zab. 5:12) Kumbuka kwamba Abrahamu alivumilia majaribu na kufurahia kibali cha Mungu. Yehova alimwona Abrahamu kuwa rafiki Yake na akahesabiwa kuwa mwadilifu. (Mwa. 15:6; Rom. 4:13, 22) Inaweza kuwa hivyo kwetu pia. Mungu hatoi kibali chake kwa msingi wa kiasi cha kazi tunachofanya katika utumishi wake au mapendeleo tunayofurahia. Anatupatia kibali chake kwa sababu ya kuvumilia kwa uaminifu. Sisi sote tunaweza kuvumilia, licha ya umri, hali, au uwezo wetu. Je, kwa sasa unavumilia kwa uaminifu jaribu fulani? Ikiwa ndivyo, kumbuka kwamba una kibali cha Mungu. Kutambua kwamba tuna kibali cha Mungu kunaweza kuwa na matokeo makubwa sana kwetu. Kunaweza kuimarisha tumaini letu. w23.12 51:13-14
Ijumaa, Agosti 22
Jithibitishe kuwa mwanamume.—1 Fal. 2:2.
Ni lazima mwanamume Mkristo ajifunze kuwasiliana vizuri. Mwanamume anayewasiliana vizuri anasikiliza na kutambua mawazo na hisia za wengine. (Met. 20:5) Anaweza kutambua mabadiliko ya sauti ya mtu, ishara za uso, na za mwili. Huwezi kujifunza kufanya mambo hayo bila kutumia muda pamoja na watu. Ikiwa una mazoea ya kutumia tu vifaa vya kielektroni ili kuwasiliana, kama vile kutuma barua-pepe na jumbe za simu, uwezo wako wa kuwasiliana ana kwa ana na watu unaweza kupungua. Hivyo, tafuta fursa za kuzungumza na watu wengine ana kwa ana. (2 Yoh. 12) Ni lazima pia mwanamume Mkristo mkomavu awe na uwezo wa kujitegemeza na kuwategemeza watu wa nyumba yake. (1 Tim. 5:8) Ni vizuri kujifunza ustadi utakaokusaidia kupata kazi. (Mdo. 18:2, 3; 20:34; Efe. 4:28) Fanya kazi kwa bidii na uhakikishe unakamilisha kazi unayoanza. Wengine watatambua hilo na watathamini kazi yako. Hivyo, kuna uwezekano mkubwa zaidi wa kupata kazi na kuidumisha. w23.12 53:12-13
Jumamosi, Agosti 23
Siku ya Yehova inakuja kama vile mwizi anavyokuja usiku.—1 The. 5:2.
Biblia inapozungumza kuhusu “siku ya Yehova,” inarejelea wakati ambapo Yehova anawaharibu maadui wake na kuwaokoa watu wake. Zamani, pindi fulani, Yehova alileta hukumu juu ya mataifa. (Isa. 13:1, 6; Eze. 13:5; Sef. 1:8) Katika nyakati zetu, “siku ya Yehova” itaanza wakati ambapo Babiloni Mkubwa atashambuliwa na itakwisha katika vita vya Har–Magedoni. Ili tuokoke “siku” hiyo, tunahitaji kujitayarisha sasa. Yesu alitufundisha kwamba hatupaswi tu kuwa tayari kwa ajili ya “dhiki kuu” bali pia ‘tuendelee kuwa tayari.’ (Mt. 24:21; Luka 12:40) Katika barua yake ya kwanza iliyoongozwa na roho takatifu ambayo aliwaandikia Wathesalonike, mtume Paulo alitumia mifano kadhaa kuwasaidia Wakristo waendelee kuwa tayari kwa ajili ya siku kuu ya Yehova ya hukumu. Paulo alijua kamba siku ya Yehova haingefika wakati huo. (2 The. 2:1-3) Ingawa hivyo, aliwahimiza ndugu zake wajitayarishe kwa ajili ya siku hiyo kana kwamba ingekuja kesho, na sisi pia tunahitaji kufuata shauri hilo. w23.06 26:1-2
Jumapili, Agosti 24
Ndugu zangu wapendwa, iweni imara, thabiti.—1 Kor. 15:58.
Mwishoni mwa miaka ya 1970, jengo lenye ghorofa 60 lilijengwa hatua kwa hatua huko Tokyo, Japani. Watu walijiuliza jengo hilo lingewezaje kuhimili matetemeko ya ardhi yanayotokea mara kwa mara katika jiji hilo. Siri ilikuwa nini? Mainjinia walikuwa wamebuni jengo hilo liwe imara lakini lenye uwezo wa kunyumbulika ili lihimili mitikisiko ya tetemeko la ardhi. Wakristo ni kama ghorofa hilo refu. Jinsi gani? Mkristo anapaswa kudumisha usawaziko kati ya kuwa imara na kunyumbulika. Anapaswa kuwa imara na thabiti na kuazimia kuendelea kutii sheria na viwango vya Yehova. Anakuwa “tayari kutii” na halegezi msimamo wake. Kwa upande mwingine, anahitaji kuwa mwenye “usawaziko,” au mwenye kunyumbulika, ikiwa hali inaruhusu au hata anapohitajika kufanya hivyo. (Yak. 3:17) Mkristo ambaye amejifunza kuwa na maoni hayo yenye usawaziko ataepuka kushikilia sana maoni yake au kuendekeza mambo yasiyofaa. w23.07 31:1-2
Jumatatu, Agosti 25
Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe.—1 Pet. 1:8
Yesu alihitaji kusimama imara dhidi ya vishawishi vya Shetani Ibilisi, kutia ndani mashambulizi ya moja kwa moja ambayo yangeweza kufanya aache kuwa mshikamanifu kwa Mungu. (Mt. 4:1-11) Shetani alikuwa ameazimia kumfanya Yesu atende dhambi ili asiweze kulipia fidia. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alivumilia majaribu mengine pia. Maadui wake walimtesa na walijaribu kumuua. (Luka 4:28, 29; 13:31) Alihitaji kuvumilia udhaifu wa wafuasi wake. (Marko 9:33, 34) Alipokuwa akihukumiwa kifo, aliteswa na kudhihakiwa. Kisha aliuawa kwa njia ya kuaibisha na yenye maumivu makali sana. (Ebr. 12:1-3) Alipokuwa kwenye mti wa mateso alilazimika kuvumilia mateso makali, bila kuwa na ulinzi wa Yehova. (Mt. 27:46) Ni wazi kwamba Yesu alijidhabihu sana ili kutoa uhai wake kuwa fidia. Je, hatuchochewi kumpenda sana Yesu tunapotafakari jinsi alivyojidhabihu sana kwa hiari kwa ajili yetu? w24.01 2:7-9
Jumanne, Agosti 26
Wote walio na haraka kwa hakika watakuwa maskini.—Met. 21:5.
Kuwa wenye subira kunatusaidia tunaposhughulika na wengine. Hutusaidia kuwasikiliza wengine kwa makini wanapozungumza. (Yak. 1:19) Pia, subira huendeleza amani. Hutulinda dhidi ya kutenda haraka-haraka na kusema jambo lisilo la fadhili tunapokuwa na mkazo. Na ikiwa tuna subira, hatutakuwa wepesi wa hasira mtu fulani anapotukasirisha. Badala ya kulipiza kisasi, ‘tutaendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.’ (Kol. 3:12, 13) Pia, subira inaweza kutusaidia kufanya maamuzi mazuri. Badala ya kutenda haraka-haraka au kuongozwa na hisia, tutatumia muda kufanya utafiti na kuchanganua maamuzi mbalimbali tunayoweza kufanya. Kwa mfano, ikiwa tunatafuta kazi, huenda tukashawishiwa kukubali kazi ya kwanza ambayo tunapata. Hata hivyo, ikiwa tuna subira tutatumia muda kuchunguza jinsi kazi hiyo itakavyoathiri familia yetu na hali yetu ya kiroho. Tunapokuwa na subira, tunaweza kuepuka kufanya uamuzi mbaya. w23.08 35:8-9
Jumatano, Agosti 27
Ninaona ndani ya mwili wangu sheria nyingine ikipigana na sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo ndani ya mwili wangu.—Rom. 7:23.
Ukihisi umevunjika moyo kwa sababu ya mwelekeo wako wa kutenda dhambi, kufikiria kuhusu ahadi uliyomwahidi Yehova ulipojiweka wakfu kwake kutaimarisha azimio lako la kupambana dhidi ya kishawishi. Jinsi gani? Unapojiweka wakfu kwa Yehova, unajikana mwenyewe. Hilo linamaanisha kukataa tamaa na malengo ya kibinafsi ambayo hayampendezi Yehova. (Mt. 16:24) Hivyo, unapokabili jaribu huhitaji kutumia muda mwingi kufikiria cha kufanya. Tayari utakuwa umeamua cha kufanya—kuwa mwaminifu kwa Yehova. Utashikamana na azimio lako la kumpendeza Yehova. Kwa njia hiyo, utakuwa kama Ayubu. Hata ingawa alikabili majaribu makali sana, alisema hivi kwa uhakika: “Sitaukana utimilifu wangu!”—Ayu. 27:5. w24.03 10:6-7
Alhamisi, Agosti 28
Yehova yuko karibu na wote wanaomwitia, wote wanaomwitia yeye katika ukweli.—Zab. 145:18.
Yehova, “Mungu wa upendo,” yuko pamoja nasi! (2 Kor. 13:11) Anapendezwa nasi kibinafsi. Tunasadiki kwamba “[tumezungukwa] na upendo Wake mshikamanifu.” (Zab. 32:10) Kadiri tunavyotafakari jinsi ambavyo ameonyesha upendo wake kwetu, ndivyo anavyokuwa halisi zaidi kwetu, na tunahisi yuko karibu zaidi nasi. Tunaweza kumkaribia kwa uhuru na kumweleza jinsi tunavyohitaji sana upendo wake. Tunaweza kumweleza mahangaiko yetu yote, tukiwa na uhakika kwamba anatuelewa na kwamba yuko tayari kutusaidia. (Zab. 145:19) Kama tunavyovutiwa kuota moto katika siku yenye baridi, ndivyo tunavyovutiwa na upendo mwororo wa Yehova. Ingawa upendo wa Yehova ni wenye nguvu, ni mwororo pia. Kwa hiyo, uruhusu upendo mwororo wa Yehova maishani mwako. Kwa sababu Yehova anatupenda, acheni sisi sote tuseme hivi kwa sauti: “Ninampenda Yehova”!—Zab. 116:1. w24.01 4:19-20
Ijumaa, Agosti 29
Nimewajulisha jina lako.—Yoh. 17:26.
Yesu alifanya mengi zaidi ya kuwaambia tu watu kwamba jina la Mungu ni Yehova. Wayahudi ambao Yesu aliwafundisha tayari walilijua jina la Mungu. Lakini Yesu ndiye aliyekuwa mstari wa mbele akiwa yule ‘aliyeeleza kumhusu.’ (Yoh. 1:17, 18) Kwa mfano, Maandiko ya Kiebrania yanafunua kwamba Yehova ni mwenye rehema na huruma. (Kut. 34:5-7) Yesu alifafanua kweli hiyo hata zaidi aliposimulia kuhusu mfano wa mwana mpotevu na baba yake. Tunaposoma kuhusu jinsi baba huyo anavyomwona mwana wake aliyetubu “akiwa mbali,” anavyokimbia ili kukutana naye, anavyomkumbatia, na kumsamehe kutoka moyoni, tunapata picha kamili zaidi ya rehema na huruma ya Yehova. (Luka 15:11-32) Yesu aliwasaidia wengine waelewe vizuri kabisa utu wa Baba yake. w24.02 6:8-9
Jumamosi, Agosti 30
[Tuwafariji] wengine . . . kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.—2 Kor. 1:4.
Yehova anawaburudisha na kuwafariji wale wanaokabili hali ngumu. Tunawezaje kumwiga Yehova kwa kuwaonyesha wengine huruma na kuwafariji? Njia moja tunayoweza kufanya hivyo ni kwa kusitawisha sifa zitakazotusaidia kuonyesha huruma na kuwafariji wengine. Baadhi ya sifa hizo ni zipi? Ni nini kitakachotusaidia tudumishe upendo wetu na ‘kuendelea kufarijiana’ kila siku? (1 The. 4:18) Tunahitaji kusitawisha sifa nyororo kama vile hisia-mwenzi, upendo wa kindugu, na fadhili. (Kol. 3:12; 1 Pet. 3:8) Sifa hizo zitatusaidiaje? Tunapowahurumia ndugu zetu na kuwajali kikweli, tutakuwa na tamaa yenye nguvu ya kuwafariji wanapoteseka. Kama Yesu alivyosema, “kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni. Mtu mwema hutoa mambo mema katika hazina yake njema.” (Mt. 12:34, 35) Kuwafariji ndugu na dada zetu wenye uhitaji ni njia muhimu sana ya kuwaonyesha kwamba tunawapenda. w23.11 47:10-11
Jumapili, Agosti 31
Wale walio na ufahamu wataelewa.—Dan. 12:10.
Tunahitaji kuomba msaada ili tuelewe unabii wa Biblia. Fikiria mfano ufuatao. Wazia kwamba unatembelea eneo fulani ambalo hulifahamu, lakini rafiki yako ambaye mnasafiri pamoja analielewa vizuri eneo hilo. Anajua kabisa mahali mlipo na anajua kila barabara katika eneo hilo. Bila shaka, utafurahi kwamba rafiki yako alikubali kusafiri pamoja nawe! Vivyo hivyo, Yehova anajua mahali tulipo katika mkondo wa wakati na mambo yatakayotokea wakati ujao. Basi, ili kuelewa unabii wa Biblia, tunapaswa kumwomba Yehova msaada kwa unyenyekevu. (Dan. 2:28; 2 Pet. 1:19, 20) Kama mzazi mwenye upendo, Yehova anataka watoto wake wawe na wakati ujao wenye furaha. (Yer. 29:11) Lakini tofauti na wazazi wa kibinadamu, Yehova anaweza kutabiri kuhusu wakati ujao kwa usahihi kabisa. Aliagiza unabii uandikwe katika Neno lake ili tujue matukio muhimu kabla hayajatokea.—Isa. 46:10. w23.08 34:3-4