Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Lugha ya Alama ya Tanzania
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25.10 41
  • Upendo wa Mungu Unadumu Milele

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Upendo wa Mungu Unadumu Milele
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UONE UPENDO WA YEHOVA KUWA FUNDISHO LA MSINGI LA BIBLIA
  • TAFAKARI KUHUSU JINSI AMBAVYO YEHOVA ‘ANAKUPENDA WEWE’
  • TAMBUA MAMBO YANAYOSABABISHA SHAKA
  • CHAGUA KUENDELEA KUWA MSHIKAMANIFU
  • Yehova Anakuonyesha Upendo Mwororo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Kubali Upendo wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Upendo Mshikamanifu wa Yehova Unamaanisha Nini Kwako?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Jinsi ya Kushinda Shaka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25.10 41

MAKALA YA 41

WIMBO 108 Upendo Mshikamanifu wa Mungu

Upendo wa Mungu Unadumu Milele

“ Mshukuruni Yehova, kwa maana ni mwema; upendo wake mshikamanifu unadumu milele.”—ZAB. 136:1.

JAMBO KUU

Kufafanua jinsi ambavyo kuwa na mtazamo ulio katika Maandiko kuhusu upendo wa Yehova kunavyoweza kutusaidia kushinda hisia za kuvunjika moyo tunapokabili jaribu.

1-2. Wakristo wengi wanakabili changamoto gani?

WAZIA mashua iliyo katikati ya dhoruba kali. Mawimbi makubwa yanaipandisha na kuishusha mashua hiyo baharini. Mashua itaelekea popote ambapo mawimbi yataipeleka, isipokuwa mtu ashushe nanga. Nanga itaisaidia mashua hiyo kutulia na kuizuia isipeperushwe na dhoruba kali.

2 Unapokabili jaribu kali, huenda ukahisi kama mashua hiyo. Kwa njia ya mfano, hisia zako zinaweza kupanda na kushuka. Siku moja una uhakika kwamba Yehova anakupenda na anakutegemeza; siku nyingine unajiuliza ikiwa hata anaona matatizo unayopitia. (Zab. 10:1; 13:1) Huenda rafiki yako akakufariji, na kwa muda fulani ukahisi vizuri. (Met. 17:17; 25:11) Lakini baadaye, shaka ulizo nazo zinarudi tena. Huenda hata ukafikiri kwamba Yehova hakupendi. Kwa njia ya mfano, unawezaje kushusha nanga unapokabili jaribu? Kwa maneno mengine, unawezaje kuwa na uhakika—na kuendelea kuwa na uhakika—kwamba Yehova anakupenda na atakutegemeza?

3. Kama unavyotajwa katika Zaburi 31:7 na 136:​1, ‘upendo mshikamanifu’ unamaanisha nini, na kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova ndiye mfano bora kabisa wa upendo mshikamanifu? (Tazama pia picha.)

3 Njia moja unayoweza kutia nanga wakati wa jaribu ni kwa kukumbuka upendo mshikamanifu wa Yehova. (Soma Zaburi 31:7; 136:1.) Maneno ‘upendo mshikamanifu’ yanaleta wazo la kushikamana, kufungamana kabisa na mtu. Yehova ndiye mfano bora kabisa wa upendo mshikamanifu. Isitoshe, Biblia inamfafanua kuwa mwenye “upendo mwingi mshikamanifu.” (Kut. 34:​6, 7) Biblia inasema hivi pia kumhusu Yehova: “Una upendo mwingi mshikamanifu kwa wote wanaokuitia.” (Zab. 86:5) Fikiria hilo linamaanisha nini: Yehova hatawaacha kamwe watumishi wake waaminifu! Kukumbuka kwamba Yehova ni mshikamanifu kunaweza kukusaidia kutia nanga unapokabili jaribu kali.—Zab. 23:4.

Nanga iliyo ndani ya maji na iliyofungwa kwenye mashua inasaidia kuzuia mashua isipeperushwe wakati wa dhoruba.

Kama tu ambavyo nanga inaizuia mashua isipeperushwe wakati wa dhoruba kali, ndivyo ambavyo uhakika wetu katika upendo wa Yehova utakavyotusaidia kuwa thabiti tunapokabili hali ngumu (Tazama fungu la 3)


UONE UPENDO WA YEHOVA KUWA FUNDISHO LA MSINGI LA BIBLIA

4. Toa mifano ya mafundisho ya msingi ya Biblia, na fafanua kwa nini hatuwezi kupotoshwa kwa urahisi.

4 Njia nyingine unayoweza kutia nanga unapokabili jaribu ni kwa kuuona upendo wa Yehova kuwa fundisho la msingi la Biblia. Maneno “fundisho la msingi la Biblia” yanamaanisha nini kwako? Huenda ukafikiria mafundisho ya kweli uliyojifunza katika Neno la Mungu. Kwa mfano, umejifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova, Yesu ni Mwana mzaliwa pekee wa Mungu, wafu hawajui lolote, na kwamba kutakuwa na dunia paradiso ambamo wanadamu wataishi milele. (Zab. 83:18; Mhu. 9:5; Yoh. 3:16; Ufu. 21:​3, 4) Ulipokubali mafundisho hayo, haikuwa rahisi kwa mtu kukupotosha. Kwa nini? Kwa sababu ulitambua kwamba msingi wa mafundisho hayo ni mambo hakika. Acheni tuchunguze jinsi ambavyo kuuona upendo wa Yehova kuwa fundisho la msingi la Biblia kunavyoweza kukusaidia kuondoa wazo la kwamba Yehova hajali au hatambui mambo unayopitia.

5. Eleza jinsi mafundisho ya uwongo yanavyopinduliwa.

5 Ulipojifunza Biblia kwa mara ya kwanza, ni jambo gani lililokusaidia kukataa mafundisho ya uwongo? Inaelekea ulisaidiwa kulinganisha mambo uliyofundishwa katika dini yako ya awali na mambo ambayo Maandiko yanafundisha. Fikiria mfano mmoja: Tuseme awali uliamini kwamba Yesu ni Mungu Mweza-Yote. Hata hivyo, kadiri ulivyojifunza Biblia, ulijiuliza, ‘Je, fundisho hili ni la kweli?’ Baada ya kuchunguza uthibitisho wa Kimaandiko, uliweza kujibu hapana. Kisha badala ya fundisho la uwongo ulilokuwa ukiamini, ulianza kuamini kweli hii ya Kimaandiko: Yesu ni “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” “Mwana mzaliwa pekee wa Mungu.” (Kol. 1:15; Yoh. 3:18) Bila shaka, mafundisho ya uwongo yanaweza kuwa kama “ngome zenye nguvu” zilizo ngumu kupindua. (2 Kor. 10:​4, 5) Lakini mara tu ulipoweza kufanya hivyo, hukurudia mafundisho uliyoacha nyuma.—Flp. 3:13.

6. Kwa nini unaweza kuwa na uhakika kwamba ‘upendo mshikamanifu wa Yehova unadumu milele’?

6 Unaweza kufanya vivyo hivyo inapohusu yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu upendo wa Yehova. Unapokabili jaribu na kuanza kuwa na shaka kuhusu upendo wa Yehova, jiulize, ‘Je, ninafikiri kwa njia inayofaa?’ Linganisha shaka ulizo nazo kuhusu upendo wa Yehova na maneno ya Zaburi 136:1—andiko la msingi la makala hii. Kwa nini Yehova anasema kwamba upendo wake ni “mshikamanifu”? Kwa nini wazo la kwamba “upendo wake mshikamanifu unadumu milele” linarudiwa mara 26 katika zaburi hiyo? Kama tulivyochunguza, upendo mshikamanifu wa Yehova kuelekea watu wake ni fundisho la msingi la Biblia, kama tu na mafundisho mengine katika Neno la Mungu ambayo yalikuwa rahisi kwako kuyakubali. Wazo la kwamba Yehova anakuona kuwa huna thamani au hakupendi ni uwongo. Kataa wazo hilo, kama tu ambavyo ungekataa kwa uthabiti fundisho lingine lolote la uwongo!

7. Toa mifano ya baadhi ya maandiko yanayotuhakikishia kwamba Yehova anatupenda.

7 Katika Biblia, tunapata uhakikisho mwingine mwingi wa upendo wa Yehova. Kwa mfano, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.” (Mt. 10:31) Yehova mwenyewe aliwaambia hivi watu wake: “Nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, nitakushika kwelikweli kwa mkono wangu wa kuume wa uadilifu.” (Isa. 41:10) Ona jinsi ambavyo maneno hayo yamesemwa kwa uthabiti. Yesu hasemi kwamba ‘Huenda ninyi ni wenye thamani kuliko,’ na Yehova hasemi, ‘Huenda nitakusaidia.’ Badala yake, wanasema hivi: “Ninyi ni wenye thamani kuliko” na “nitakusaidia.” Ikiwa utakuwa na shaka kuhusu upendo wa Yehova unapokabili jaribu, maandiko hayo yanaweza kufanya mengi zaidi ya kukusaidia uhisi vizuri; yanaweza kukusaidia uwe na uhakika zaidi kwamba anakupenda. Maandiko hayo yanataja mambo hakika. Kusali na kutafakari mambo hayo kutakuchochea kusema maneno ya 1 Yohana 4:16: “Tumejua na tumeamini kwamba Mungu anatupenda.”a

8. Unaweza kufanya nini ikiwa nyakati fulani unatilia shaka upendo wa Yehova kwako?

8 Hata hivyo, namna gani ikiwa nyakati fulani bado una shaka ikiwa Yehova anakupenda? Linganisha hisia hizo na mambo unayojua kumhusu. Hisia hazitegemeki na zinabadilika, lakini tunaweza kutegemea mambo hakika; upendo wa Yehova unaotajwa katika Maandiko ni jambo hakika. Kufikiri kwa njia tofauti na hiyo, ni kupuuza kiini cha utu wa Yehova—upendo wake.—1 Yoh. 4:8.

TAFAKARI KUHUSU JINSI AMBAVYO YEHOVA ‘ANAKUPENDA WEWE’

9-10. Ni katika muktadha gani Yesu alisema maneno haya kwenye Yohana 16:​26, 27, “Baba mwenyewe anawapenda ninyi”? (Tazama pia picha.)

9 Tunaweza kujifunza mengi zaidi kuhusu upendo wa Yehova kwa kufikiria maneno haya ya Yesu kwa wafuasi wake: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi.” (Soma Yohana 16:​26, 27.) Yesu hakusema maneno hayo ili kuwafanya tu wanafunzi wake wajihisi vizuri. Kwa kweli, muktadha unaonyesha kwamba hakuwa akizungumza kuhusu hisia zao wakati huo. Badala yake, alikuwa akizungumzia jambo lingine—sala.

10 Yesu alikuwa ametoka tu kuwaambia wanafunzi wake kuwa walipaswa kusali kupitia kwake, lakini si kwa Yesu. (Yoh. 16:​23, 24) Ilikuwa muhimu kwao kujua jambo hilo. Baada ya Yesu kufufuliwa, huenda wanafunzi wake wangechochewa kusali kwake. Kwa kweli, Yesu alikuwa rafiki yao. Wangeweza kufikia mkataa kwamba kwa kuwa aliwapenda angechochewa kusikiliza maombi yao na kuyafikisha kwa Baba yake. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba hawakupaswa kuwa na mawazo hayo. Kwa nini? Kwa sababu aliwaambia hivi: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi.” Kweli hiyo ni sehemu ya fundisho la msingi la Biblia kuhusu sala. Fikiria hilo linamaanisha nini kwako: Kupitia funzo lako la Biblia, umemjua na kumpenda Yesu. (Yoh. 14:21) Lakini kama wanafunzi wa karne ya kwanza, unaweza kusali kwa Mungu ukiwa na uhakika na ukijua kwamba yeye ‘mwenyewe anakupenda wewe.’ Unaonyesha kwamba unayaamini maneno hayo kila mara unaposali kwa Yehova.—1 Yoh. 5:14.

Mkusanyo wa picha: Ndugu anasali kwa uhakika kuhusu mambo matatu muhimu maishani mwake akiwa ameketi kwenye benchi nje. 1. Amemletea chakula mke wake aliye mgonjwa ambaye amelala kitandani. 2. Binti yake mdogo anafurahia funzo lake la Biblia pamoja naye. 3. Anasoma ripoti kadhaa za kifedha.

Unaweza kusali kwa Yehova ukiwa na uhakika na ukijua kwamba yeye ‘mwenyewe anakupenda wewe’ (Tazama fungu la 9-10)b


TAMBUA MAMBO YANAYOSABABISHA SHAKA

11. Kwa nini Shetani atafurahi ikiwa tutakuwa na shaka kwamba Yehova anatupenda?

11 Shaka kuhusu upendo wa Yehova zinatoka wapi? Huenda ukajibu kwamba chanzo cha shaka ni Shetani, na kwa sehemu jambo hilo ni kweli. Ibilisi ‘anatafuta kutumeza’ sisi, na angefurahi ikiwa tungetilia shaka kwamba Yehova anatupenda. (1 Pet. 5:8) Isitoshe, upendo wa Yehova ulimchochea kuandaa fidia—jambo ambalo Shetani angependa tuhisi kwamba hatustahili. (Ebr. 2:9) Lakini ni nani anayenufaika ikiwa tutatilia shaka upendo wa Yehova? Ni Shetani. Na ni kusudi la nani litatimia ikiwa tutavunjika moyo tunapokabili jaribu? La Shetani. Wazia jambo hilo, Shetani anataka tufikiri kwamba Yehova hatupendi, wakati kwa kweli yeye ndiye ambaye alipoteza upendo wa Yehova. Hata hivyo, mojawapo ya “matendo [yake] yenye hila” zaidi ni kujaribu kutufanya tuhisi kwamba sisi ndio ambao hatupendwi na tumekataliwa na Yehova. (Efe. 6:11) Tunapotambua kile ambacho adui yetu anajaribu kufanya, tunaweza kuimarisha azimio letu la ‘kumpinga Ibilisi.’—Yak. 4:7.

12-13. Hali yetu ya dhambi tuliyorithi inawezaje kufanya tutilie shaka upendo wa Yehova?

12 Shaka kuhusu upendo wa Yehova zinaweza kutoka katika chanzo kingine. Chanzo gani? Hali yetu ya dhambi tuliyorithi. (Zab. 51:5; Rom. 5:12) Dhambi imemtenganisha mwanadamu na Muumba wake. Pia, imeharibu moyo, akili, na mwili wake.

13 Dhambi inaathiri hisia zetu na kusababisha tuhisi hatia, tuwe na mahangaiko, tusijiamini, na tuhisi aibu. Tunaweza kuwa na hisia hizo tunapotenda dhambi. Lakini hisia hizo zinaweza pia kuja kwa sababu muda wote tunakumbuka hali yetu ya dhambi—hali ambayo Mungu alipowaumba wanadamu hakukusudia wawe nayo. (Rom. 8:​20, 21) Kama gari lenye gurudumu lisilokuwa na upepo lisivyoweza kufanya kazi kwa kiwango kilichokusudiwa, tukiwa watu wasio wakamilifu hatuwezi kutenda kwa kiwango kilichokusudiwa awali. Hivyo, haishangazi kwamba pindi fulani sisi hupambana na hisia za shaka kuhusu upendo wa Yehova. Hilo likitokea, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova ni ‘Mungu mkuu na mwenye kuogopesha ambaye anawatendea kwa upendo mshikamanifu wale wanaompenda na kushika amri zake.’—Neh. 1:5.

14. Kutafakari kuhusu fidia kunawezaje kutusaidia kuondoa wazo la kwamba Yehova hawezi kutupenda kamwe? (Waroma 5:8) (Tazama pia sanduku “Jilinde Dhidi ya ‘Nguvu za Udanganyifu za Dhambi.’”)

14 Kwa kweli, huenda pindi fulani tukahisi kwamba hatustahili upendo wa Yehova. Na kwa kweli hatustahili upendo huo—na hilo linafanya upendo wake uwe wa pekee sana. Hatuwezi kustahili upendo wa Yehova kwa jitihada zetu wenyewe. Hata hivyo, fidia inafunika dhambi zetu, na Yehova ametoa uandalizi huo kwa sababu anatupenda. (1 Yoh. 4:10) Pia, kumbuka kwamba Yesu alikuja kuwaokoa watenda dhambi, si watu wakamilifu. (Soma Waroma 5:8.) Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kufanya mambo kikamilifu, na Yehova hatarajii ukamilifu kutoka kwetu. Tunapotambua kwamba hali yetu ya dhambi inaweza kusababisha tutilie shaka upendo wa Yehova, tunaweza kuazimia hata zaidi kupambana ili tusiruhusu hali hiyo iathiri njia yetu ya kufikiri.—Rom. 7:​24, 25.

Jilinde Dhidi ya “Nguvu za Udanganyifu za Dhambi”

Biblia inazungumzia “nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Ebr. 3:13) Zaidi ya kutushawishi ili tutende mambo yasiyofaa, hali yetu ya dhambi inaweza kusababisha tuendelee kutilia shaka ikiwa Yehova anatupenda. Kwa kweli, dhambi ina “nguvu za udanganyifu.”

Huenda tukafikiri kwamba hatuwezi kudanganywa. Kwa mfano, huenda tukaamini kwamba hatutadanganywa na tapeli anayejaribu kutulaghai. Hata hivyo, ikiwa hatujui kuhusu uhalifu wa aina hiyo, tunaweza kupoteza pesa nyingi.

Vivyo hivyo, tunahitaji kuwa na utambuzi wakati hali yetu ya dhambi inapojaribu “kututapeli” tuamini kwamba Yehova hatupendi. Hali yetu ya dhambi inaweza kusababisha tukazie fikira udhaifu na makosa yetu. Lakini hizo ni “nguvu za udanganyifu” za dhambi na tunapaswa kuzikataa.

CHAGUA KUENDELEA KUWA MSHIKAMANIFU

15-16. Ikiwa tutaendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova tunaweza kuwa na uhakika kuhusu nini, na kwa nini? (2 Samweli 22:26)

15 Yehova anataka tufanye uamuzi sahihi kwa “kushikamana naye.” (Kum. 30:​19, 20) Tukifanya hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba ataendelea kuwa mshikamanifu kwetu. (Soma 2 Samweli 22:26.) Maadamu tunaendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatusaidia kukabiliana na hali yoyote itakayotokea maishani.

16 Kama tulivyozungumzia, tuna kila sababu ya kuendelea kutia nanga tunapokabili majaribu. Tunajua kwamba Yehova anatupenda na atatutegemeza. Biblia inafundisha hivyo. Ikiwa tutatilia shaka upendo wake, tunaweza kutafakari kuhusu mambo ya kweli tunayojua, badala ya mambo tunayohisi kuwa ni ya kweli. Acheni tuendelee kuwa na uhakika katika kweli hii inayotegemea Biblia kwamba upendo mshikamanifu wa Yehova unadumu milele.

UNGEJIBUJE?

  • Unaweza kunufaikaje kwa kuuona upendo wa Yehova kuwa fundisho la msingi la Biblia?

  • Dhambi tuliyorithi inawezaje kufanya tutilie shaka upendo wa Yehova?

  • Tunawezaje kushinda shaka kuhusu upendo wa Yehova?

WIMBO 159 Mpe Yehova Utukufu

a Mifano mingine inatia ndani Kumbukumbu la Torati 31:​8, Zaburi 94:​14, na Isaya 49:15.

b MAELEZO YA PICHA: Ndugu akisali ili apate msaada wa kumtunza mke wake ambaye ni mgonjwa, ashughulikie mambo yake ya kifedha kwa hekima, na kumfundisha mtoto wake kumpenda Yehova.

    Tanzanian sign language publications (2020-2026)
    Toka
    Ingia
    • Lugha ya Alama ya Tanzania
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki