MAKALA YA 39
WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”
“Waliokuwa na Mwelekeo Unaofaa” Wataitikia Vizuri
“Wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.”—MDO. 13:48.
JAMBO KUU
Umuhimu wa kuwaalika watu wajifunze Biblia na kuwakaribisha wahudhurie mikutano yetu.
1. Watu wanatofautianaje inapohusu jinsi wanavyoitikia wanapohubiriwa habari njema? (Matendo 13:47, 48; 16:14, 15)
WATU wengi katika karne ya kwanza walikubali kweli mara tu waliposikia ujumbe wa Ufalme. (Soma Matendo 13:47, 48; 16:14, 15.) Leo pia, baadhi ya watu hufurahi wanaposikia kwa mara ya kwanza habari njema. Hata wale ambao mwanzoni hawakuonyesha wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme, wanaweza baadaye kufungua moyo wao wazi na kuukubali. Tunapaswa kufanya nini tunapokutana na watu ‘walio na mwelekeo unaofaa’ tunapokuwa katika huduma?
2. Ni katika njia gani kazi yetu ya kufanya wanafunzi inafanana na kazi ya mkulima?
2 Fikiria mfano huu. Kazi yetu ya kufanya wanafunzi inaweza kulinganishwa na kazi ya mkulima. Baadhi ya mazao katika shamba lake yamekomaa na yako tayari kuchumwa. Mkulima anahitaji kuchuma mazao hayo bila kukawia, lakini ataendelea kumwagilia maji na kutunza mazao mengine ambayo bado hayajakomaa. Vivyo hivyo, tunapokutana na mtu ambaye yuko tayari kukubali ujumbe wetu, tunataka kumsaidia awe mwanafunzi wa Kristo haraka iwezekanavyo. Wakati huohuo, tunaendelea kusitawisha upendezi wa wengine ambao wanahitaji muda zaidi ili kuona thamani ya mambo wanayosikia. (Yoh. 4:35, 36) Sifa ya utambuzi itatusaidia kuchagua utangulizi mzuri wa kutumia ili kuwasaidia wasikilizaji wetu kwa njia bora. Sasa, acheni tuchunguze mambo tunayoweza kufanya tunapozungumza kwa mara ya kwanza na watu wanaoitikia vizuri ujumbe wetu. Pia, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuwasaidia watu hao wafanye maendeleo.
WATU WANAPOITIKIA VIZURI
3. Tunapaswa kufanya nini tunapokutana na watu wanaopendezwa tunapokuwa katika huduma? (1 Wakorintho 9:26)
3 Tunapokutana na watu wanaopendezwa tunapokuwa katika huduma yetu, tungependa kuwasaidia waanze kutembea katika barabara inayoongoza kwenye uzima bila kukawia. Katika visa hivyo, hatupaswi kusita kuwaalika wajifunze Biblia na kuwakaribisha katika mikutano yetu tunapozungumza nao kwa mara ya kwanza.—Soma 1 Wakorintho 9:26.
4. Simulia jambo lililoonwa la mtu ambaye alikuwa tayari kuanza kujifunza Biblia bila kukawia.
4 Waalike watu wajifunze Biblia. Baadhi ya watu tunaozungumza nao wako tayari kuanza kujifunza Biblia bila kukawia. Kwa mfano, Alhamisi moja, mwanamke kijana nchini Kanada alienda katika kigari cha machapisho na kuchukua broshua ya Furahia Maisha Milele! Dada aliyekuwa katika kigari cha machapisho alimwambia kwamba anaweza kujifunza Biblia bila malipo kwa kutumia broshua hiyo. Mwanamke huyo kijana alipendezwa na alimpatia dada huyo habari zake za mawasiliano. Baadaye siku hiyo, mwanamke huyo kijana alimtumia ujumbe wa simu dada huyo na kumuuliza wanaweza kuanza lini kujifunza Biblia. Dada alipomweleza kwamba anaweza kumtembelea mwishoni mwa juma hilo, mwanamke huyo kijana alimuuliza hivi: “Unaweza kuja kesho? Nina nafasi.” Wakaanza kujifunza siku ya Ijumaa. Mwanamke huyo kijana alihudhuria mkutano wake wa kwanza mwishoni mwa juma hilo na aliendelea kufanya maendeleo haraka.
5. Tunawezaje kuonyesha sifa ya utambuzi tunapomwalika mtu ajifunze Biblia? (Tazama pia picha.)
5 Bila shaka, hatutarajii kwamba watu wote wanaosikiliza ujumbe wetu watakuwa na hamu kubwa ya kujifunza Biblia kama mwanamke huyo kijana. Huenda watu wengine wakahitaji muda zaidi ili kupendezwa na ujumbe wetu. Huenda kwanza tukahitaji kuanzisha mazungumzo tukitumia habari ambazo zinampendeza mtu huyo. Hata hivyo, ikiwa tutadumisha mtazamo unaofaa na kuendelea kupendezwa nao kibinafsi, huenda baada ya muda mfupi tukaweza kuanzisha funzo la Biblia. Tunaweza kusema nini tunapomwalika mtu ajifunze Biblia? Ndugu na dada kadhaa wenye ustadi wa kuanzisha mafunzo ya Biblia waliulizwa swali hilo. Acheni tuone mapendekezo yao.
Tunawezaje kufanya funzo la Biblia liwe lenye kuvutia zaidi kwa watu hawa? (Tazama fungu la 5)a
6. Tunawezaje kutoa wazo la kuendeleza mazungumzo na mtu aliyependezwa?
6 Wahubiri na mapainia walioulizwa kuhusu kuanzisha mafunzo, walieleza kwamba katika nchi fulani ni vema kuepuka kutumia maneno kama vile “funzo,” “mtaala wa Biblia,” au “nitakufundisha” unapofafanua funzo la Biblia. Walitambua kwamba maneno yenye matokeo mazuri ni kama vile, “mazungumzo,” “majadiliano,” na “kuifahamu vizuri Biblia.” Unaweza kutoa wazo la kuendeleza mazungumzo kwa kusema hivi: “Inashangaza jinsi maswali muhimu kuhusu maisha yanavyojibiwa katika Biblia,” au “Biblia si tu kitabu cha dini; inatusaidia kwa njia hususa maishani.” Unaweza kuongezea hivi: “Haitachukua muda mwingi; dakika 10 au 15 zinatosha kujifunza jambo lenye thamani.” Tunaweza kusema hivyo bila kutumia maneno kama vile, “kukubaliana muda wa kukutana” au “kila juma,” maneno ambayo yanaweza kumfanya ahisi kwamba analazimika kuwepo.
7. Baadhi ya watu walitambua kweli ya Biblia kwa mara ya kwanza wakati gani? (1 Wakorintho 14:23-25)
7 Wakaribishe kwenye mkutano. Inaelekea kwamba katika siku za mtume Paulo, baadhi ya watu walitambua kweli ya Biblia walipohudhuria kwa mara ya kwanza mkutano wa Kikristo. (Soma 1 Wakorintho 14:23-25.) Mara nyingi mambo huwa hivyo leo pia. Watu wengi wapya hufanya maendeleo kwa haraka zaidi wanapoanza kuhudhuria mikutano yetu. Unapaswa kuwaalika wakati gani? Kitabu Furahia Maisha Milele! kina mwaliko wa kuhudhuria mkutano katika somo la 10, lakini huhitaji kusubiri hadi utakapofikia somo hilo. Tangu siku ya kwanza mnapozungumza unaweza kumwalika mtu huyo kwenye mkutano wa mwisho juma, huenda kwa kutaja kichwa cha hotuba ya watu wote au jambo fulani litakalozungumziwa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi.
8. Tunaweza kukazia fikira mambo gani kuhusu mikutano yetu tunapomkaribisha mtu? (Isaya 54:13)
8 Unapomkaribisha mtu anayependezwa, mweleze jinsi mikutano yetu ilivyo tofauti na ibada za dini nyingine ambazo huenda amezoea. Mwanafunzi mmoja wa Biblia alipohudhuria kwa mara ya kwanza Funzo la Mnara wa Mlinzi, alimuuliza hivi mwalimu wake: “Je, anayeongoza funzo anajua majina ya kila mtu?” Dada huyo alimweleza kwamba sote tunajitahidi kukumbuka majina ya watu katika kutaniko letu, kama tu ambavyo tunajua majina ya watu wetu wa familia. Mwanafunzi huyo aliona jambo hilo ni tofauti kabisa na mambo aliyojionea kanisani kwao. Pia, kusudi la mikutano yetu ni jambo jipya kwa watu wengi. (Soma Isaya 54:13.) Tunakutana ili kumwabudu Yehova, kujifunza kutoka kwake, na kutiana moyo. (Ebr. 2:12; 10:24, 25) Matokeo ni kwamba mikutano yetu ina utaratibu mzuri, inatufundisha mambo hususa, na ibada yetu si ya kidesturi. (1 Kor. 14:40) Majumba ya Ufalme yana mwangaza wa kutosha ili iwe rahisi kwetu kujifunza. Hatuzungumzii masuala ya kisiasa, kwa kuwa hatuungi mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Pia, hatuzungumzii au kubishana kuhusu maoni ya kibinafsi. Huenda ikafaa kumwonyesha mapema mwanafunzi video Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? Kwa njia hiyo, atajua mambo ya kutarajia.
9-10. Tunapomwalika mtu kuhudhuria mkutano, tunaweza kufanya nini ili kumhakikishia kwamba hatutamshinikiza kuwa Shahidi au kutoa maelezo? (Tazama pia picha.)
9 Baadhi ya watu husita kuhudhuria mkutano kwa sababu wanaogopa kwamba wataombwa “wajiunge na kanisa.” Mhakikishie mtu huyo kwamba tunafurahi kuwa na wageni na hatumshinikizi yeyote kuwa Shahidi au kutoa maelezo katika mikutano yetu. Familia zinakaribishwa, kutia ndani wale wenye watoto wadogo. Katika mikutano yetu, watoto hawafundishwi wakiwa peke yao. Badala yake, wazazi na watoto huketi na kujifunza pamoja. Kwa njia hiyo, wazazi wanajua watoto wao wako na nani na wanafundishwa nini. (Kum. 31:12) Hatukusanyi sadaka au kupitisha bahasha za michango. Badala yake, tunafuata amri hii ya Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mt. 10:8) Unaweza kumweleza mtu huyo kwamba hahitaji kuwa na nguo za gharama ili kuhudhuria mkutano. Mungu huutazama moyo, na si mwonekano wa mtu.—1 Sam. 16:7.
10 Ikiwa mtu atahudhuria mkutano, jitahidi kumfanya ahisi amekaribishwa. Mtambulishe kwa wazee wa kutaniko na wahubiri wengine. Ikiwa atahisi amekaribishwa, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba atarudi tena. Ikiwa hatakuwa na Biblia wakati wa mkutano, tumia Biblia yako pamoja naye na msaidie kufuatana na habari anayozungumzia msemaji au zinazozungumziwa kwenye funzo.
Kadiri mtu anavyohudhuria mikutano bila kukawia, ndivyo atakavyoweza kunufaika zaidi (Tazama fungu la 9-10)
FUNZO LA BIBLIA LINAPOANZISHWA
11. Unaweza kuonyeshaje kwamba unaheshimu wakati na ratiba ya mwenye nyumba?
11 Ni mambo gani tunayopaswa kukumbuka tunapojifunza Biblia na mtu? Heshimu wakati na ratiba ya mwenye nyumba. Kwa mfano, ikiwa mmepanga wakati wa kukutana, fika kwa wakati, hata ikiwa watu katika eneo lenu hawana kawaida ya kufika kwa wakati. Kwa kuongezea, huenda ikafaa ukitumia muda mfupi mnapojifunza kwa mara ya kwanza. Baadhi ya wahubiri wenye uzoefu wanapendekeza kumaliza funzo mapema, hata ikiwa mtu anataka kusikia habari zaidi. Na usizungumze kupita kiasi. Mruhusu mwenye nyumba ajieleze.—Met. 10:19.
12. Tunapaswa kuwa na lengo gani tunapoanza kujifunza Biblia na mtu?
12 Unapoanza kujifunza na mtu, lengo lako linapaswa kuwa kumsaidia amjue Yehova na Yesu na kuwapenda. Unafanya hivyo kwa kukazia kile ambacho Neno la Mungu linasema badala ya kujikazia fikira mwenyewe na ujuzi wako. (Mdo. 10:25, 26) Mara nyingi, mtume Paulo alipofundisha alimkazia fikira Yesu Kristo, yule ambaye Yehova alimtuma ili atusaidie kumjua na kumpenda Yeye. (1 Kor. 2:1, 2) Paulo alitaja wazi pia jinsi ilivyo muhimu kuwasaidia wanafunzi wapya kusitawisha sifa nzuri zinazoweza kulinganishwa na dhahabu, fedha, na mawe ya thamani. (1 Kor. 3:11-15) Sifa hizo zenye thamani zinatia ndani imani, hekima, utambuzi, na kumwogopa Yehova. (Zab. 19:9, 10; Met. 3:13-15; 1 Pet. 1:7) Iga njia ya Paulo ya kufundisha kwa kuwasaidia wanafunzi wako wasitawishe imani yenye nguvu na uhusiano wa karibu na Baba yao wa mbinguni mwenye upendo.—2 Kor. 1:24.
13. Tunawezaje kuonyesha subira na usawaziko tunapowasaidia watu wanaopendezwa? (2 Wakorintho 10:4, 5) (Tazama pia picha.)
13 Iga njia ya Yesu ya kufundisha kwa kuonyesha subira na usawaziko. Epuka kuuliza maswali yenye kuaibisha. Ikiwa kuna jambo ambalo ni gumu kwa mwanafunzi wako kuelewa, unaweza kuendelea na habari nyingine, kisha kulizungumzia jambo hilo wakati mwingine. Badala ya kumlazimisha akubali fundisho ambalo hayuko tayari kukubali, ruhusu wakati upite ili kweli hiyo itie mizizi moyoni mwake. (Yoh. 16:12; Kol. 2:6, 7) Biblia inalinganisha mafundisho ya uwongo na “ngome zenye nguvu” ambazo tunahitaji kuzipindua. Katika lugha ya awali, Biblia hapa inatumia lugha ya picha ya ngome inayopaswa kuvunjwa. (Soma 2 Wakorintho 10:4, 5.) Badala ya kuvunja ngome ya mwanafunzi wako kwa njia ambayo itamwangukia, msaidie ajenge ngome mpya kwa kumfanya Yehova awe Kimbilio lake.—Zab. 91:9.
Ruhusu wakati upite ili kweli itie mizizi katika moyo wa mwanafunzi wako (Tazama fungu la 13)
WAPYA WANAPOHUDHURIA MIKUTANO
14. Tunapaswa kuwatendeaje wapya wanaohudhuria mikutano yetu?
14 Yehova anatarajia tusiwe na ubaguzi tunaposhughulika na wapya, licha ya utamaduni, hali yao ya kiuchumi, au kabila lao. (Yak. 2:1-4, 9) Hivyo, tunawezaje kuwaonyesha upendo wale wanaohudhuria mikutano yetu?
15-16. Tunawezaje kuwasaidia wapya wahisi wamekaribishwa katika mikutano yetu?
15 Baadhi ya watu huhudhuria mikutano yetu kwa sababu tu ya udadisi au wametiwa moyo kufanya hivyo na mtu anayeishi katika eneo lingine. Hivyo, hatupaswi kusita kuzungumza na watu hao wanapokuja katika mikutano yetu. Uwe mwenye urafiki, lakini epuka kuwafanya wasijihisi huru kwa kuwaonyesha shauku kupita kiasi. Waalike waketi pamoja nawe. Tumia pamoja nao Biblia yako na machapisho ya kujifunzia, au wapatie nakala zao. Zaidi ya hayo, fikiria hisia zao. Mwanamume mmoja ambaye alitembelea Jumba la Ufalme alimwambia ndugu aliyemsalimu kwamba alikuwa na wasiwasi kwa sababu ya nguo alizokuwa amevaa. Ndugu huyo alimsaidia ajihisi huru kwa kumfafanulia kwamba Mashahidi wa Yehova ni watu tu wa kawaida. Mwanamume huyo ambaye alifanya maendeleo na kubatizwa, bado anakumbuka jibu la ndugu huyo. Hata hivyo, zingatia jambo hili: Unapozungumza na wageni kabla na baada ya mkutano, onyesha upendezi wa kibinafsi bila kuingilia mambo ya kibinafsi ya mtu.—1 Pet. 4:15.
16 Tunaweza kuwafanya wageni wetu wahisi wamekaribishwa kwa kuwaonyesha heshima kupitia mazungumzo, maelezo, na migawo yetu tunapowarejelea watu ambao si Mashahidi au mambo wanayoamini. Epuka kutumia maneno ambayo yatawakwaza au yatakayowafanya wahisi wametukanwa. (Tito 2:8; 3:2) Kwa mfano, kamwe hatutazungumzia mambo ambayo wanaamini kwa njia ambayo itawavunjia heshima. (2 Kor. 6:3) Kuhusiana na hilo, ndugu wanaotoa hotuba za watu wote wanapaswa hasa kuwa waangalifu. Wanaonyesha pia kwamba wanawakumbuka wahudhuriaji ambao si Mashahidi kwa kufafanua maneno au mawazo ambayo huenda hawaelewi.
17. Lengo letu ni nini tunapowapata watu ‘walio na mwelekeo unaofaa’ tunapokuwa katika huduma?
17 Kila siku, kazi yetu ya kufanya wanafunzi inaendelea kuwa yenye uharaka zaidi, na tunaendelea kuwatafuta watu ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48) Tunapowapata, hatupaswi kusita kuwaalika wajifunze Biblia au kuwakaribisha katika mikutano yetu. Kwa kufanya hivyo, tunaweza kuwasaidia wachukue hatua ya kwanza katika “barabara inayoongoza kwenye uzima.”—Mt. 7:14.
WIMBO 64 Kuyashiriki Mavuno kwa Furaha
a MAELEZO YA PICHA: Ndugu wawili wakimkaribia mwanajeshi aliyestaafu ambaye amepumzika barazani; dada wawili wakimhubiria kwa ufupi mama aliye na shughuli nyingi.