MAKALA YA 40
WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe
Yehova Ni ‘Shangwe Yetu Inayofurika’
“ Nitakuja . . . kwa Mungu, shangwe yangu inayofurika.”—ZAB. 43:4.
JAMBO KUU
Tutasaidiwa kutambua mambo ambayo yanaweza kufanya tupoteze shangwe yetu na jinsi tunavyoweza kuipata tena.
1-2. (a) Watu wengi wanakabili hali gani leo? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?
WATU ulimwenguni wanahangaikia sana kutafuta furaha. Hata hivyo, licha ya jitihada hizo, hawana shangwe ya kudumu. Watu wengi wanalemewa na hisia za huzuni na wanahisi kwamba hali zao haziwezi kuwa nzuri. Baadhi ya watu wa Yehova hupatwa na hisia hizo pia. Kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho,” tunatarajia kukabili hali au kuwa na hisia ambazo ni “ngumu kushughulika nazo.”—2 Tim. 3:1.
2 Katika makala hii, tutazungumzia mambo ambayo yanaweza kufanya tupoteze shangwe yetu na jinsi tunavyoweza kuipata tena ikiwa tutaipoteza. Lakini kwanza, ni lazima tutambue Chanzo cha furaha na shangwe ya kweli.
CHANZO CHA FURAHA NA SHANGWE YA KWELI
3. Uumbaji unatufundisha nini kumhusu Yehova? (Tazama pia picha.)
3 Sikuzote Yehova amekuwa mwenye furaha. Naye anataka tuwe na furaha na shangwe. Hivyo, haishangazi kwamba tunaiona shangwe yake kupitia uumbaji wake—sayari yetu maridadi, rangi nyingi mbalimbali, wanyama wanaocheza, na chakula kingi kitamu. Kwa kweli, Mungu anatupenda na anataka tufurahie maisha!
Baby elephant: Image © Romi Gamit/Shutterstock; penguin chicks: Vladimir Seliverstov/500px via Getty Images; baby goats: Rita Kochmarjova/stock.adobe.com; two dolphins: georgeclerk/E+ via Getty Images
Wanyama wanapocheza wanaonyesha jinsi Yehova alivyo mwenye shangwe (Tazama fungu la 3)
4. (a) Yehova anawezaje kuendelea kuwa mwenye furaha licha ya kuteseka kwa watu ulimwenguni? (b) Yehova anatupatia zawadi gani? (Zaburi 16:11)
4 Licha ya kwamba Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” anatambua kikamili maumivu na kuteseka kunakoendelea ulimwenguni. (1 Tim. 1:11) Lakini hajaruhusu hali hiyo ipunguze shangwe yake. Anajua kwamba kuteseka ni kwa muda mfupi tu—tayari yeye mwenyewe ameweka siku ya kuondoa hali hiyo. Naye anangoja kwa subira hadi siku ambayo ataondoa huzuni na kuteseka kote milele. Wakati huohuo, Yehova anaelewa hali tunazopitia na anataka kutusaidia. Anatusaidia kwa njia gani? Jambo moja ni kwamba anatupatia zawadi ya shangwe. (Soma Zaburi 16:11.) Ona jinsi alivyompatia zawadi hiyo Yesu, Mwana wake.
5-6. Kwa nini Yesu ni mwenye shangwe?
5 Kati ya viumbe wote wa Yehova, Yesu ndiye mwenye furaha zaidi. Kwa nini? Fikiria sababu mbili. (1) “Yeye ndiye mfano wa Mungu asiyeonekana” na anaonyesha kikamilifu utu wa Baba yake katika kila njia. (Kol. 1:15; tazama habari za utafiti kuhusu 1 Timotheo 6:15, “happy,” nwtsty.) (2) Yesu ametumia muda mwingi sana na Baba yake, ambaye ndiye Chanzo cha furaha.
6 Sikuzote Yesu amepata shangwe ya kufanya kile ambacho Baba yake anamwagiza. (Met. 8:30, 31; Yoh. 8:29) Kwa sababu ya uaminifu wake, ana kibali cha Yehova.—Mt. 3:17.
7. Tunaweza kupataje shangwe ya kweli?
7 Sisi pia tunaweza kupata shangwe ya kweli kwa kumkaribia Yehova, Chanzo cha furaha. Kadiri tunavyotumia muda mwingi zaidi kujifunza kumhusu Yehova na kumwiga, ndivyo tutakavyokuwa wenye furaha zaidi. Pia, tutapata shangwe ya kufanya mapenzi ya Mungu na kujua kwamba tuna kibali chake.a (Zab. 33:12) Lakini namna gani tunapokosa shangwe kwa pindi fulani au hata kwa muda mrefu? Je, hilo linamaanisha kwamba hatuna kibali cha Mungu? La hasha! Sisi si wakamilifu, hivyo pindi fulani tunapata maumivu, huzuni, na kushuka moyo. Yehova anaelewa hali hizo. (Zab. 103:14) Acheni tuchunguze mambo yanayoweza kufanya tupoteze shangwe yetu na jinsi tunavyoweza kuipata tena.
USIRUHUSU JAMBO LOLOTE LIFANYE UPOTEZE SHANGWE YAKO
8. Matatizo maishani yanaweza kutuathirije?
8 Jambo la kwanza: Matatizo maishani. Je, unakabiliana na mateso, majanga ya asili, umaskini, magonjwa, au madhara ya uzee? Tunaweza kupoteza kirahisi shangwe yetu tunapokabili matatizo hayo, hasa inapohusu hali ambayo hatuwezi kuidhibiti. Biblia inasema kwamba “maumivu ya moyo huiponda roho.” (Met. 15:13) Babis, mzee wa kutaniko ambaye alifiwa na ndugu yake na wazazi wake katika kipindi cha miaka minne, anasema hivi: “Nilihisi upweke na sikujua la kufanya. Nyakati nyingine, nilijihisi vibaya sana kwa sababu nilikuwa na mambo mengi ya kufanya hivi kwamba sikutumia muda wa kutosha na wazazi wangu na ndugu yangu kabla ya vifo vyao.” Kwa kweli, matatizo maishani yanaweza kufanya tuhisi tumechoka kimwili na kihisia.
9. Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata tena shangwe yetu? (Yeremia 29:4-7, 10)
9 Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata tena shangwe yetu? Tunaweza kupata tena shangwe yetu kwa kuona mambo kihalisi na kuwa wenye shukrani. Ulimwengu unaendeleza wazo la kwamba ni lazima maisha yetu yawe mazuri sana ili tuwe wenye furaha. Lakini hilo si kweli. Kwa mfano, Yehova aliwaagiza Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni, wakubali hali yao mpya wakiwa utekwani kwenye nchi ya kigeni na kufanya yote wawezayo chini ya hali hizo ngumu. (Soma Yeremia 29:4-7, 10.) Tunajifunza nini? Jitahidi kukubali hali zako, na uwe mwenye shukrani kwa mambo mazuri uliyo nayo maishani. Kumbuka kwamba Yehova atakusaidia. (Zab. 63:7; 146:5) Effie, ambaye alipata aksidenti iliyosababisha mwili wake upooze na ashindwe kutembea, anasema hivi: “Nilipata msaada na utegemezo mkubwa kutoka kwa Yehova, familia yangu, na kutaniko. Hivyo, nilihisi kwamba nisingekuwa mwenye shukrani ikiwa ningekata tamaa. Ninataka kuonyesha shukrani zangu kwa Yehova na ndugu na dada zangu kwa msaada wao mkubwa.”
10. Kwa nini tunaweza kuwa na shangwe hata tunapokabili matatizo?
10 Hata tunapokuwa na matatizo maishani au mambo mabaya sana yanapotupata sisi au familia yetu, bado tunaweza kuwa na shangwe.b (Zab. 126:5) Kwa nini? Kwa sababu shangwe yetu haitegemei hali zetu. Maria, ambaye ni painia, anasema hivi: “Unapokabili matatizo, kuendelea kuwa na shangwe hakumaanishi kwamba unapuuza hisia zako. Badala yake, kunamaanisha kwamba hujasahau ahadi za Yehova. Baba yetu atatusaidia kulinda shangwe yetu.” Kumbuka, hata hali ziwe ngumu kadiri gani sasa, matatizo yetu ni ya muda mfupi tu—kama alama za nyayo katika ufukwe wa bahari. Hivi karibuni, zitaondolewa na maji na kufutwa kabisa.
11. Mfano wa mtume Paulo unakutia moyo kwa njia gani?
11 Namna gani ikiwa tutaanza kufikiri kuwa matatizo yetu ni uthibitisho wa kwamba tumepoteza kibali cha Yehova? Kufikiria kuhusu watumishi wengine waaminifu wa Yehova ambao walikabili hali ngumu sana kunaweza kutusaidia. Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alichaguliwa na Yesu mwenyewe ili kupeleka kweli “kwa mataifa na pia kwa wafalme na wana wa Israeli.” (Mdo. 9:15) Hilo lilikuwa pendeleo kubwa sana! Hata hivyo, Paulo alikuwa na matatizo mengi maishani. (2 Kor. 11:23-27) Je, matatizo mengi ambayo Paulo alikabili yalimaanisha kwamba alikuwa amepoteza kibali cha Yehova? Bila shaka la! Badala yake, uvumilivu wake ulionyesha kwamba alikuwa na baraka za Yehova. (Rom. 5:3-5) Sasa fikiria kuhusu hali yako. Unavumilia kwa uaminifu licha ya majaribu yote unayokabili. Hivyo, wewe pia unaweza kuwa na uhakika kwamba una kibali cha Yehova.
12. Matarajio yasiyotimizwa yanawezaje kutufanya tupoteze shangwe yetu?
12 Jambo la pili: Matarajio yasiyotimizwa. (Met. 13:12) Upendo na uthamini wetu kwa Yehova unatuchochea kujiwekea malengo katika utumishi wake. Hata hivyo, ikiwa malengo tuliyojiwekea hayapatani na hali zetu, tunaweza kuvunjika moyo. (Met. 17:22) Painia anayeitwa Holly, anasema hivi: “Nilitaka kuhudhuria Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, kutumikia katika nchi nyingine, au kufanya kazi katika mradi wa ujenzi wa Ramapo. Lakini hali zangu zilibadilika, na nisingeweza tena kufikia malengo hayo. Nilivunjika moyo. Inakatisha tamaa sana unapotaka kutimiza mambo fulani, lakini huwezi.” Watu wengi wanahisi hivyo.
13. Ikiwa hali zetu hazituruhusu kutimiza mengi zaidi, tunaweza kujiwekea malengo gani tunayoweza kutimiza?
13 Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata tena shangwe yetu? Kumbuka kwamba Yehova hadai mengi kutoka kwetu. Hatarajii tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu; wala hapimi thamani yetu kwa kutegemea mambo tunayoweza kutimiza katika utumishi wake. Yehova anataka tuwe wenye kiasi na waaminifu. (Mika 6:8; 1 Kor. 4:2) Anajali zaidi mawazo, hisia, na sifa zetu kuliko mambo tunayotimiza. Je, ingefaa tujiwekee matarajio makubwa zaidi ya yale ambayo Yehova anatarajia kutoka kwetu?c Bila shaka la! Hivyo, ikiwa hali zako hazikuruhusu kutimiza mengi zaidi katika utumishi wa Yehova, jitahidi kukazia fikira mambo unayoweza kutimiza. Je, unaweza kuwazoeza vijana au kuwatia moyo ndugu na dada waliozeeka? Je, unaweza kuweka lengo la kumtia moyo mtu ana kwa ana, kupitia simu, au hata kupitia ujumbe mfupi wa simu? Yehova atakubariki kwa kukupatia shangwe unapojitahidi kufikia malengo hayo yenye kuridhisha na unayoweza kutimiza! Na kumbuka kwamba hivi karibuni katika ulimwengu mpya, tutakuwa na fursa za kumtumikia Yehova milele kwa njia ambazo leo hatuwezi kuwazia! Holly, aliyetajwa awali, alimalizia kwa kusema hivi: “Ninaketi na kujiambia hivi, ‘Nitaishi milele.’ Kwa msaada wa Yehova, ninaweza kutimiza baadhi ya malengo yangu katika ulimwengu mpya.”
14. Ni jambo gani lingine linaloweza kutufanya tupoteze shangwe?
14 Jambo la tatu: Kutimiza tamaa za kibinafsi. Baadhi ya watu hutumia mitandao ya kijamii kuendeleza wazo la kwamba furaha ya kweli na kuridhika kunatokana na kujifurahisha wenyewe. Watu wanatiwa moyo wafanye mambo wanayopenda, ununuzi, na kusafiri kuwa jambo kuu maishani. Si vibaya kufurahia mambo hayo. Yehova ametuumba kwa njia ambayo tunaweza kufurahia mambo mazuri. Hata hivyo, watu wengi wamegundua kwamba mambo ambayo walifikiri yangewaletea shangwe yamewafanya waipoteze. Eva, ambaye ni painia, anasema hivi, “Maisha yako yanapotegemea kujifurahisha mwenyewe, huwezi kuridhika.” Kutimiza tu tamaa za kibinafsi kunaweza kutuacha tukiwa na huzuni na tumevunjika moyo.
15. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Mfalme Sulemani?
15 Tunaweza kujifunza kutokana na mambo aliyopitia Mfalme Sulemani inapohusu matokeo mabaya ya kutimiza tamaa za kibinafsi. Alijitahidi kupata furaha kwa kutosheleza tamaa zake za kibinafsi kama vile kufurahia chakula kizuri, muziki wenye kuburudisha, na mambo yote mazuri ambayo angeweza kununua katika siku zake. Lakini licha ya yote hayo hakuridhika. Alisema hivi: “Jicho halitosheki kuona wala sikio halishibi kusikia.” (Mhu. 1:8; 2:1-11) Maoni ya ulimwengu kuhusu mambo yanayoleta shangwe ya kweli ni kama pesa bandia. Zinaonekana kuwa zenye thamani; hata hivyo, haziwezi kutimiza chochote.
16. Kufanya mambo kwa ajili ya wengine kunaweza kutusaidiaje kupata tena shangwe yetu? (Tazama pia picha.)
16 Ni nini kinachoweza kutusaidia kupata tena shangwe yetu? Yesu alitufundisha kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Mzee wa kutaniko anayeitwa Alekos, anasema hivi: “Ninakazia fikira zaidi kufanya mambo madogo-madogo kwa ajili ya wengine. Kadiri ninavyozidi kutoa, ndivyo ambavyo sijifikirii mwenyewe, na ninakuwa na shangwe.” Unaweza kuwafanyia nini wengine? Ukiona mtu ana mahangaiko, jitahidi kumtia moyo. Huenda usiweze kuondoa matatizo yake, lakini unaweza kumfariji kwa kumsikiliza kwa hisia mwenzi, kumwonyesha huruma, na kumkumbusha amtupie mzigo wake Yehova. (Zab. 55:22; 68:19) Unaweza pia kumsaidia atambue kwamba Yehova hajamwacha. (Zab. 37:28; Isa. 59:1) Unaweza hata kufanya jambo hususa kwa ajili yake, kama vile kutayarisha mlo au kwenda matembezi pamoja naye. Mwalike ajiunge nawe katika huduma, jambo ambalo litampatia furaha. Mruhusu Yehova akutumie. Kukazia fikira mahitaji ya wengine badala ya mahitaji yetu kutatupatia shangwe ya kweli!—Met. 11:25.
Badala ya kukazia fikira mahitaji yako, kazia fikira mahitaji ya wengine (Tazama fungu la 16)d
17. Kuna uhusiano gani kati ya Yehova na shangwe yetu? (Zaburi 43:4)
17 Tunaweza kuwa na furaha ya kweli ikiwa tutaendelea kumkaribia Baba yetu wa mbinguni. Biblia inatuhakikishia kwamba Yehova ni ‘shangwe yetu inayofurika.’ (Soma Zaburi 43:4.) Kwa hiyo, hata iwe tunakabili nini maishani, tunaweza kuhisi tukiwa salama. Hivyo, acheni tuendelee kumkazia fikira Yehova, Chanzo hakika cha shangwe yetu!—Zab. 144:15.
WIMBO 155 Shangwe Yetu ya Milele
a Tazama sanduku “Jinsi Yehova Anavyotupatia Shangwe.”
b Kwa mfano, tazama kwenye jw.org mahojiano ya Dennis na Irina Christensen katika Ripoti ya 5 ya Baraza Linaloongoza ya 2023.
c Kwa habari zaidi, tazama makala “Uwe na Matarajio Yenye Usawaziko, na Uwe Mwenye Shangwe” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2008.
d MAELEZO YA PICHA: Dada ametoka kununua vitu vingi, lakini anapata shangwe zaidi kwa kumnunulia maua dada mwenye umri mkubwa anayehitaji kitia moyo.