Jumanne, Septemba 9
Mwanamke mpumbavu ana kelele. Yeye ni mjinga.—Met. 9:13.
Wale wanaosikia sauti ya “mwanamke mpumbavu” wanahitaji kufanya uamuzi huu: Je, watakubali mwaliko wake au wataukataa? Tuna sababu nzuri sana zinazotuchochea tuepuke uasherati. “Mwanamke mpumbavu” anafafanuliwa kuwa anasema hivi: “Maji yaliyoibwa ni matamu.” (Met. 9:17) “Maji yaliyoibwa” ni nini? Biblia inalinganisha uhusiano wa kingono ambao watu waliofunga ndoa hufurahia na maji yenye kuburudisha. (Met. 5:15-18) Mume na mke waliofunga ndoa kisheria wanaweza kufurahia kufanya ngono. Hata hivyo, mambo ni tofauti kuhusu “maji yaliyoibwa.” Maji hayo yanarejelea uasherati. Watu hufanya uasherati kisiri kama mwizi anavyoiba kisiri. ‘Maji hayo yaliyoibwa’ huenda yakaonekana kuwa matamu hasa ikiwa wale wanaohusika wanafikiri kwamba hakuna mtu atakayejua jambo hilo. Kwa kweli wanajidanganya! Yehova anaona mambo yote. Ikiwa tutapoteza kibali cha Yehova, tutapatwa na uchungu mwingi sana na kwa kweli hilo si jambo ‘tamu’ au linalofurahisha.—1 Kor. 6:9, 10. w23.06 28:7-9
Jumatano, Septemba 10
Hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.—1 Kor. 9:17.
Utafanya nini ikiwa unahisi sala zako hazitoki moyoni, au hufurahii utumishi kama ilivyokuwa zamani? Usifikie mkataa kwamba umepoteza roho ya Yehova. Kwa kuwa wewe si mkamilifu, hisia zako zinaweza kubadilika mara kwa mara. Ikiwa bidii yako inaanza kupungua, tafakari mfano wa mtume Paulo. Ingawa alijitahidi kumwiga Yesu, alijua kwamba nyakati nyingine huenda hangekuwa na tamaa kubwa ya kufanya kile alichohitaji kufanya. Paulo aliazimia kutimiza huduma yake licha ya jinsi ambavyo huenda angehisi wakati huo. Vivyo hivyo, usifanye maamuzi kwa kutegemea tu jinsi unavyohisi. Azimia kufanya lililo sawa licha ya jinsi unavyohisi. Ikiwa utaendelea kufanya yaliyo sawa, baada ya muda huenda hisia zako zikabadilika.—1 Kor. 9:16. w24.03 10:12-13
Alhamisi, Septemba 11
Thibitisheni upendo wenu kwao.—2 Kor. 8:24.
Tunawaonyesha upendo ndugu na dada zetu kwa kuwakaribisha wawe rafiki zetu. (2 Kor. 6:11-13) Wengi wetu tunashirikiana na makutaniko yenye ndugu na dada kutoka katika malezi mbalimbali na wenye nyutu mbalimbali. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kuelekea watu wote kwa kukazia fikira sifa zao nzuri. Tunapojifunza kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona, tunathibitisha kwamba tunawapenda. Tutahitaji kuonyeshana upendo wakati wa dhiki kuu. Dhiki kuu itakapoanza tutapata wapi ulinzi? Fikiria jambo ambalo Yehova aliwaagiza watu wake wafanye Babiloni la kale liliposhambuliwa: “Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Inaonekana kwamba maneno hayo yanatuhusu pia sisi ambao tutakabiliana na dhiki kuu. w23.07 29:14-16