Jumatano, Septemba 10
Hata nikifanya hivyo bila kupenda, bado nimekabidhiwa usimamizi.—1 Kor. 9:17.
Utafanya nini ikiwa unahisi sala zako hazitoki moyoni, au hufurahii utumishi kama ilivyokuwa zamani? Usifikie mkataa kwamba umepoteza roho ya Yehova. Kwa kuwa wewe si mkamilifu, hisia zako zinaweza kubadilika mara kwa mara. Ikiwa bidii yako inaanza kupungua, tafakari mfano wa mtume Paulo. Ingawa alijitahidi kumwiga Yesu, alijua kwamba nyakati nyingine huenda hangekuwa na tamaa kubwa ya kufanya kile alichohitaji kufanya. Paulo aliazimia kutimiza huduma yake licha ya jinsi ambavyo huenda angehisi wakati huo. Vivyo hivyo, usifanye maamuzi kwa kutegemea tu jinsi unavyohisi. Azimia kufanya lililo sawa licha ya jinsi unavyohisi. Ikiwa utaendelea kufanya yaliyo sawa, baada ya muda huenda hisia zako zikabadilika.—1 Kor. 9:16. w24.03 10:12-13
Alhamisi, Septemba 11
Thibitisheni upendo wenu kwao.—2 Kor. 8:24.
Tunawaonyesha upendo ndugu na dada zetu kwa kuwakaribisha wawe rafiki zetu. (2 Kor. 6:11-13) Wengi wetu tunashirikiana na makutaniko yenye ndugu na dada kutoka katika malezi mbalimbali na wenye nyutu mbalimbali. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kuelekea watu wote kwa kukazia fikira sifa zao nzuri. Tunapojifunza kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona, tunathibitisha kwamba tunawapenda. Tutahitaji kuonyeshana upendo wakati wa dhiki kuu. Dhiki kuu itakapoanza tutapata wapi ulinzi? Fikiria jambo ambalo Yehova aliwaagiza watu wake wafanye Babiloni la kale liliposhambuliwa: “Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Inaonekana kwamba maneno hayo yanatuhusu pia sisi ambao tutakabiliana na dhiki kuu. w23.07 29:14-16
Ijumaa, Septemba 12
Tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.—1 Kor. 7:31.
Ujulikane kuwa mtu mwenye usawaziko. Jiulize hivi: ‘Je, watu wananiona kuwa mwenye usawaziko, mwenye kukubali sababu, na kuwavumilia wengine? Au je, wanaona kwamba ninashikilia maoni yangu, ni mkali, au mwenye kichwa kigumu? Je, ninawasikiliza wengine na kukubaliana na maoni yao inapofaa?’ Kadiri tunavyozidi kuwa wenye usawaziko, ndivyo tunavyoonyesha kwamba tunamwiga Yehova na Yesu. Usawaziko unahusisha kunyumbulika hali zetu zinapobadilika. Mabadiliko hayo yanaweza kutusababishia matatizo tusiyotarajia. Huenda ukapatwa na ugonjwa ghafla. Au mabadiliko ya ghafla ya hali ya kiuchumi au ya kisiasa yanapotokea mahali tunapoishi yanaweza kuvuruga kabisa maisha yetu. (Mhu. 9:11) Huenda hata tukakabili hali ngumu tunapopata badiliko la mgawo wa kitheokrasi. Tunaweza kufanikiwa kunyumbulika hali zinapobadilika ikiwa tutachukua hatua nne zifuatazo: (1) kubali kwamba mambo yamebadilika, (2) fikiria kuhusu wakati ujao, (3) kazia fikira mambo yanayojenga, na (4) uwasaidie wengine. w23.07 32:7-8