MAKALA YA 37
WIMBO 114 “Iweni na Subira”
Njia Bora ya Kushughulikia Ukosefu wa Haki
“Aliendelea kutumaini haki itendwe, lakini tazama! kulikuwa na ukosefu wa haki.”—ISA. 5:7.
JAMBO KUU
Jinsi mfano wa Yesu unavyotusaidia kushughulikia ukosefu wa haki kwa njia inayompendeza Yehova.
1-2. Watu wengi wanashughulikiaje ukosefu wa haki, na huenda tukajiuliza maswali gani?
TUNAISHI katika ulimwengu usio na haki. Watu wanatendewa kwa njia isiyo ya haki kwa sababu nyingi, kama vile hali yao ya kiuchumi, jinsia, jamii, au rangi yao. Watu wanateseka kwa sababu ya uharibifu wa mazingira uliosababishwa au kuongezeka kwa sababu ya wafanyabiashara matajiri na viongozi wa serikali wenye pupa na ufisadi. Mambo hayo na ukosefu mwingine wa haki unatuathiri sisi sote kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja.
2 Haishangazi kwamba watu wengi wanakasirishwa na ukosefu wa haki wanaouona ulimwenguni leo. Sisi sote tungependa kuishi kwenye ulimwengu ambao tunahisi tukiwa salama na kutendewa kwa haki. Baadhi ya watu wanajiunga katika harakati za kijamii za kuleta mabadiliko. Wanatia sahihi maombi ya kudai mabadiliko, wanashiriki katika maandamano, na kuwaunga mkono viongozi wa kisiasa wanaoahidi kupambana na ukosefu wa haki. Hata hivyo, tukiwa Wakristo, tunafundishwa kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu” na tuungojee Ufalme wa Mungu utakaoondoa ukosefu wote wa haki. (Yoh. 17:16) Hata hivyo, sisi huvunjika moyo—au hata kukasirika—tunapoona mtu akitendewa isivyo haki. Huenda tukajiuliza hivi: ‘Nitashughulikiaje ukosefu huo wa haki? Je, kuna jambo lolote ninaloweza kufanya sasa ili kushughulikia ukosefu wa haki?’ Ili kujibu maswali hayo, acheni tuanze kwa kuchunguza jinsi Yehova na Yesu wanavyohisi kuhusu ukosefu wa haki.
YEHOVA NA YESU WANACHUKIA UKOSEFU WA HAKI
3. Kwa nini inaeleweka kwamba sisi hukasirika tunapoona ukosefu wa haki? (Isaya 5:7)
3 Biblia inatueleza kwa nini inaeleweka kwamba sisi huhangaishwa na ukosefu wa haki. Inafafanua kwamba Yehova alituumba kwa mfano wake na kwamba yeye “anapenda uadilifu na haki.” (Zab. 33:5; Mwa. 1:26) Hatendi kamwe kwa ukosefu wa haki, na hataki yeyote atende kwa njia isiyo ya haki! (Kum. 32:3, 4; Mika 6:8; Zek. 7:9) Kwa mfano, katika siku za nabii Isaya, Yehova alisikia “kilio cha huzuni” kutoka kwa Waisraeli ambao walikuwa wakitendewa isivyo haki na Waisraeli wenzao. (Soma Isaya 5:7.) Yehova alichukua hatua kwa kuwaadhibu wale walioendelea kupuuza Sheria yake na kuwatendea wengine isivyo haki.—Isa. 5:5, 13.
4. Tukio linalotajwa katika Injili linaonyesha nini kuhusu maoni ya Yesu kuelekea ukosefu wa haki? (Tazama pia picha.)
4 Kama Yehova, Yesu pia anapenda haki na anachukia ukosefu wa haki. Pindi moja alipokuwa katika huduma yake duniani, alimwona mwanamume mlemavu aliyepooza mkono. Yesu alichochewa kumsaidia, lakini viongozi wa dini wenye mioyo migumu walikuwa na maoni tofauti sana. Walihangaikia zaidi kutekeleza ufafanuzi wao mkali wa sheria ya Sabato, badala ya kumsaidia mwanamume huyo. Yesu alihisije kuhusu itikio lao? “[Alihuzunika] sana kwa sababu mioyo yao ilikuwa migumu.”—Marko 3:1-6.
Tofauti na viongozi wa dini ya Kiyahudi, Yesu alikuwa na hisia mwenzi kuelekea wale wenye uhitaji (Tazama fungu la 4)
5. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu hasira ambayo huenda tukahisi kuelekea ukosefu wa haki?
5 Kwa kuwa Yehova na Yesu wanakasirishwa na ukosefu wa haki, si jambo baya ikiwa sisi pia tutahisi hivyo. (Efe. 4:26 na habari za utafiti “Be wrathful,” nwtsty) Hata hivyo, ni lazima tukumbuke kwamba hasira yoyote tutakayohisi—hata ikiwa tuna sababu nzuri—haitaondoa ukosefu wa haki. Isitoshe, hasira ya muda mrefu au isiyodhibitiwa inaweza kutudhuru kihisia na kimwili. (Zab. 37:1, 8; Yak. 1:20) Hivyo, tunawezaje kushughulikia ukosefu wa haki? Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu.
JINSI YESU ALIVYOSHUGHULIKIA UKOSEFU WA HAKI
6. Kulikuwa na ukosefu gani wa haki Yesu alipokuwa duniani? (Tazama pia picha.)
6 Yesu alijionea ukosefu mkubwa wa haki alipokuwa duniani. Alijionea jinsi watu wa kawaida walivyokandamizwa na viongozi wa dini. (Mt. 23:2-4) Alijua pia kuhusu jinsi watawala wa Kiroma walivyowatendea watu kwa ukali. Wayahudi wengi walitamani sana kuwekwa huru kutoka kwa utawala wa Roma. Baadhi yao, kama vile Wazeloti, walikuwa tayari kupigania uhuru huo. Hata hivyo, Yesu hakuanzisha wala kuunga mkono harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii. Alipojua kwamba watu walikuwa wamepanga kumfanya awe mfalme, Yesu alijitenga nao.—Yoh. 6:15.
Yesu aliepuka jitihada za watu za kumhusisha kwenye mambo ya kisiasa katika siku zake (Tazama fungu la 6)
7-8. Kwa nini Yesu hakujaribu kuondoa ukosefu wa haki alipokuwa duniani? (Yohana 18:36)
7 Alipokuwa duniani, Yesu hakujihusisha katika mfumo wa kisiasa wa siku hizo ili kuondoa ukosefu wa haki. Kwa nini? Alijua kwamba wanadamu hawana haki wala uwezo wa kujiongoza. (Zab. 146:3; Yer. 10:23) Pia, hawana uwezo wa kuondoa sababu kuu za ukosefu wa haki. Ulimwengu unatawaliwa na Shetani Ibilisi, kiumbe wa roho muuaji anayetumia mamlaka yake kuchochea ukosefu wa haki. (Yoh. 8:44; Efe. 2:2) Na kutokuwa wakamilifu kunafanya iwe vigumu hata kwa wanadamu wenye nia njema kutenda kwa haki nyakati zote.—Mhu. 7:20.
8 Yesu alijua kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio utakaoondoa kabisa sababu kuu za ukosefu wa haki. Kwa sababu hiyo, alitumia wakati na nguvu zake “akihubiri na kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Aliwahakikishia “wale walio na njaa na kiu ya uadilifu” kwamba mwisho wa ufisadi na ukosefu wa haki utakuja. (Mt. 5:6 na habari za utafiti, nwtsty; Luka 18:7, 8) Hata hivyo, hilo halitatimizwa kupitia mabadiliko ya kijamii, bali kupitia utawala wa serikali ya Mungu iliyo mbinguni, ambayo “si sehemu ya ulimwengu huu.”—Soma Yohana 18:36.
MWIGE YESU UNAPOSHUGHULIKA NA UKOSEFU WA HAKI
9. Ni nini kinachokusadikisha kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio utakaoondoa ukosefu wote wa haki?
9 Leo, tunajionea ukosefu mwingi hata zaidi wa haki kuliko ambao Yesu alijionea alipokuwa duniani. Lakini chanzo cha ukosefu wa haki katika “siku za mwisho” bado ni Shetani na watu wasio wakamilifu walio chini ya uvutano wake. (2 Tim. 3:1-5, 13; Ufu. 12:12) Kama Yesu, tunajua kwamba Ufalme wa Mungu ndio utakaoondoa sababu kuu za ukosefu wa haki. Kwa kuwa tunaunga mkono kikamili Ufalme huo, tunakataa kujihusisha katika maandamano na harakati zozote za kukabiliana na ukosefu wa haki. Fikiria mfano wa dada anayeitwa Stacy.a Kabla ya kujifunza kweli, Stacy alijiunga kwa ukawaida katika harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii. Lakini alianza kuwa na shaka kuhusu harakati hizo. Anasema hivi: “Nilipokuwa katika maandamano hayo, ningejiuliza ikiwa nilikuwa nikiunga mkono upande sahihi. Kwa kuwa sasa ninaunga mkono Ufalme wa Mungu, ninajua kwamba niko upande sahihi. Ninajua kwamba Yehova atamtetea vizuri zaidi kila mtu ambaye ameathiriwa na ukandamizaji kuliko mimi ninavyoweza.”—Zab. 72:1, 4.
10. Ni kwa njia gani harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii hazipatani na shauri la Yesu linalopatikana katika Mathayo 5:43-48? (Tazama pia picha.)
10 Harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii katika ulimwengu huu mara nyingi huhusisha roho ya kujitegemea na hasira ambayo inapingana na mambo aliyofundisha Yesu na mfano wake. (Efe. 4:31) Ndugu anayeitwa Jeffrey anasema hivi: “Ninajua kwamba katika muda mfupi, maandamano yanayoonekana kuwa ya amani yanaweza kubadilika na kuwa yenye vurugu na uporaji.” Hata hivyo, Yesu anatufundisha tuwatendee watu wote kwa upendo, hata wale ambao hawakubaliani na maoni yetu au wanatutesa. (Soma Mathayo 5:43-48.) Tukiwa Wakristo, tunajitahidi kadiri tuwezavyo kuepuka mambo yoyote yasiyopatana na kielelezo ambacho Yesu alituwekea.
Tunahitaji kujitahidi ili tuendelee kutounga mkono upande wowote inapohusu masuala ya kisiasa na kijamii ya siku zetu (Tazama fungu la 10)
11. Ni jambo gani linaloweza kujaribu azimio letu la kutounga mkono harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii?
11 Ingawa tunajua kwamba Ufalme wa Mungu utaondoa kabisa ukosefu wa haki, huenda ikawa vigumu kwetu kumwiga Yesu tunapotendewa isivyo haki. Fikiria jambo lililompata Janiya, aliyeonyeshwa ubaguzi. Anakiri hivi: “Nilikasirika sana. Niliumia pia kihisia na nilitaka watu hao waadhibiwe. Kisha, nikafikiria kuhusu kujiunga na harakati za kupinga ubaguzi wa rangi. Nilihisi kwamba kufanya hivyo kulikuwa njia salama ya kuonyesha hasira yangu.” Hata hivyo, baada ya muda, Janiya alitambua kwamba alihitaji kufanya mabadiliko. Anasema hivi: “Nilikuwa nikiwaruhusu watu wengine wabadili njia yangu ya kufikiri na kunichochea kumtumaini mwanadamu badala ya Yehova. Nikaamua kuacha kushirikiana na wanaharakati hao.” Ni lazima tuwe waangalifu ili tusiruhusu hasira yoyote ya uadilifu tuliyo nayo itufanye tulegeze msimamo wetu inapohusu kutounga mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa na ya kijamii ya ulimwengu huu.—Yoh. 15:19.
12. Kwa nini ni jambo la hekima kuchagua kwa makini habari tunazofuatilia?
12 Ni jambo gani linaloweza kutusaidia kudhibiti hisia za hasira tunapotendewa isivyo haki? Watu wengi wameona jambo linalowasaidia ni kuchagua kwa makini mambo wanayosoma, wanayosikiliza, na wanayotazama. Baadhi ya mitandao ya kijamii imejaa habari nyingi zilizotiwa chumvi kuhusu ukosefu wa haki na zinazoendeleza harakati za kuleta mabadiliko ya kijamii. Mara nyingi, vyombo vya habari hutoa ripoti zinazopendelea upande mmoja. Hata ikiwa tutasikia habari za kweli kuhusu ukosefu wa haki, je, kuendelea kuzikazia fikira kutatusaidia? Ikiwa tutatumia muda mwingi sana kufuatilia habari hizo, huenda tukavunjika moyo au kukasirika isivyo lazima. (Met. 24:10) Jambo baya hata zaidi ni kwamba tunaweza hata kuacha kukazia fikira suluhisho la kudumu la ukosefu wote wa haki, yaani, Ufalme wa Mungu.
13. Ratiba nzuri ya kusoma Biblia inatusaidiaje kudumisha mtazamo unaofaa kuhusu ukosefu wa haki?
13 Ratiba nzuri ya kusoma na kutafakari Biblia inaweza kutusaidia kushughulika na ukosefu wa haki. Dada anayeitwa Alia alihuzunika sana kwa sababu ya njia ambayo watu katika jamii yake walitendewa. Ilionekana kana kwamba wale waliotenda kwa njia isiyofaa hawakuwajibishwa. Anasema hivi: “Nilihitaji kuketi chini na kujiuliza hivi, ‘Je, kweli ninaamini kwamba Yehova atarekebisha matatizo haya?’ Katika kipindi hicho nilisoma Ayubu 34:22-29. Mistari hiyo ilinikumbusha kwamba hakuna mtu anayeweza kujificha kutoka kwa Yehova. Ni yeye tu aliye na haki kamilifu, na ni yeye tu atakayerekebisha mambo kikamili.” Hata hivyo, tunapoendelea kusubiri Ufalme wa Mungu ulete haki ya kweli, tunahitaji kushughulikia ukosefu wa haki tunaokabili leo. Tunawezaje kufanya hivyo?
JINSI TUNAVYOWEZA KUSHUGHULIKIA UKOSEFU WA HAKI LEO
14. Tunaweza kufanya nini ili tuepuke kuchangia ukosefu wa haki ulimwenguni? (Wakolosai 3:10, 11)
14 Huenda tusiweze kudhibiti matendo ya watu wengine ya ukosefu wa haki, lakini tunaweza kudhibiti matendo yetu wenyewe. Kama tulivyozungumzia awali, tunamwiga Yesu kwa kuonyesha upendo. Upendo huo unaweza kutuchochea kuwatendea wengine kwa heshima—hata wale wanaosababisha ukosefu wa haki. (Mt. 7:12; Rom. 12:17) Yehova anafurahi tunapomtendea kila mtu kwa fadhili na haki.—Soma Wakolosai 3:10, 11.
15. Kuwaambia wengine kweli ya Biblia kumekuwa na matokeo gani inapohusu ukosefu wa haki leo?
15 Njia muhimu zaidi tunayoweza kushughulikia ukosefu wa haki ni kwa kuwaambia wengine kweli za Biblia. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu “ujuzi kumhusu Yehova” unaweza kumbadili mtu ambaye zamani alikuwa mwenye hasira na mkatili na kumfanya awe mwenye fadhili, na mpenda amani. (Isa. 11:6, 7, 9) Kabla ya kujifunza kweli, mwanamume anayeitwa Jemal alijiunga na kundi la waasi ili kupambana na serikali aliyohisi inawakandamiza. Anasema hivi: “Huwezi kutumia nguvu ili kuwalazimisha watu wabadilike. Sikulazimishwa kubadilika, bali nilibadilishwa na kweli za Biblia nilizokuwa najifunza.” Mambo aliyojifunza Jemal yalimchochea aache kupigana. Kadiri watu wengi zaidi wanavyobadilishwa na kweli za Biblia, ndivyo kutakavyokuwa na watu wachache zaidi watakaosababisha ukosefu wa haki leo.
16. Kwa nini una hamu ya kuwaambia wengine kuhusu tumaini la Ufalme?
16 Kama Yesu, tuna hamu ya kuwaambia watu kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho la kudumu la ukosefu wa haki. Tumaini hilo linaweza kuwatia moyo wale ambao wametendewa isivyo haki. (Yer. 29:11) Stacy, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Kujifunza kweli kumenisaidia kukabiliana na ukosefu wa haki niliojionea na kupitia kibinafsi. Yehova anatumia ujumbe wa Biblia kutoa faraja.” Unahitaji kujitayarisha vizuri ili kushiriki na wengine ujumbe wa Biblia unaofariji kuhusu suluhisho la ukosefu wa haki. Kadiri unavyokuwa na uhakika zaidi kuhusu ukweli wa mawazo ya Kimaandiko tuliyochunguza katika makala hii, ndivyo utakavyokuwa tayari zaidi kuzungumzia kwa busara suluhisho la ukosefu wa haki iwe ni shuleni au kazini.b
17. Yehova anatusaidiaje kukabiliana na ukosefu wa haki leo?
17 Tunajua kwamba tutaendelea kukabiliana na ukosefu wa haki maadamu Shetani anaendelea kuwa “mtawala wa ulimwengu huu.” Lakini hatujakosa msaada wala tumaini tunaposubiri ‘atupwe nje.’ (Yoh. 12:31) Katika Maandiko, Yehova anafunua kwa nini kuna ukosefu mwingi wa haki na jinsi anavyohisi kuelekea taabu zinazoletwa na hali hizo. (Zab. 34:17-19) Kupitia Mwana wake, Yehova anatufundisha jinsi tunavyopaswa kushughulikia ukosefu wa haki leo, na jinsi ambavyo hivi karibuni Ufalme wake utaondoa kabisa ukosefu wa haki. (2 Pet. 3:13) Acheni tuendelee kuhubiri habari njema za Ufalme huo kwa bidii, tukitazamia kwa hamu wakati ambapo dunia itajaa “haki na uadilifu.”—Isa. 9:7.
WIMBO 158 ‘Haitachelewa!’
a Baadhi ya majina yamebadilishwa.
b Tazama pia Nyongoza A:24-27 katika brochure lmd.