Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Lugha ya Alama ya Tanzania
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25.09 36
  • ‘Waite Wazee’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Waite Wazee’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • NI WAKATI GANI TUNAPASWA ‘KUWAITA WAZEE’?
  • KWA NINI TUNAPASWA KUWAITA WAZEE?
  • WAZEE WANATUSAIDIAJE?
  • WAJIBU WETU WA KIBINAFSI
  • Jinsi ya Kuwaonyesha Watenda Dhambi Upendo na Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Jinsi Ambavyo Kutaniko Limepangwa
    Furahia Maisha Milele!​—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • Akina Ndugu—Je, Mnajitahidi Kustahili Kutumikia Mkiwa Wazee wa Kutaniko?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Wazee Wanawezaje Kuwasaidia Wale Wanaoondolewa Kutanikoni?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25.09 36

MAKALA YA 36

WIMBO 103 Wachungaji—Zawadi Katika Wanadamu

‘Waite Wazee’

“Na awaite wazee wa kutaniko.”—YAK. 5:14.

JAMBO KUU

Kupata msaada wa kiroho kutoka kwa wazee wa kutaniko unapouhitaji.

1. Yehova ameonyeshaje kwamba kondoo wake ni wenye thamani?

KONDOO wa Yehova ni wenye thamani kwake. Aliwanunua kwa damu ya Yesu na kuwapa wazee wa kutaniko jukumu la kutunza kondoo Wake. (Mdo. 20:28) Mungu anataka kondoo wake watendewe kwa wororo. Chini ya uongozi wa Kristo, wazee wanawaburudisha na kuwalinda kondoo dhidi ya hatari za kiroho.—Isa. 32:​1, 2.

2. Yehova anawakazia fikira kwa njia ya pekee akina nani? (Ezekieli 34:​15, 16)

2 Yehova anawajali sana kondoo wake wote, lakini anawakazia fikira kwa njia ya pekee wale wanaoteseka. Kupitia wazee, anawasaidia wale wanaoteseka katika maana ya kiroho. (Soma Ezekieli 34:​15, 16.) Hata hivyo, anataka tutafute msaada tunapouhitaji. Katika pindi hizo, mbali na kutoa sala za kutoka moyoni tukimwomba Mungu atutegemeze, tunawaomba pia msaada “wachungaji na walimu” katika kutaniko.—Efe. 4:​11, 12.

3. Sisi sote tunaweza kunufaikaje kwa kuchunguza jukumu walilo nalo wazee?

3 Katika makala hii, tutachunguza mpango wa Mungu wa kutusaidia kupata msaada wa kiroho kupitia wazee. Tutajibu maswali yafuatayo: Ni wakati gani tunapaswa kuwaomba msaada wazee? Kwa nini tunapaswa kufanya hivyo? Na wazee wanatusaidiaje? Hata ikiwa kwa sasa hatuna tatizo, majibu ya maswali hayo yataongeza uthamini wetu kuelekea mpango huo wa Mungu na huenda siku moja yakaokoa uhai wetu.

NI WAKATI GANI TUNAPASWA ‘KUWAITA WAZEE’?

4. Kwa nini tunaweza kusema kwamba andiko la Yakobo 5:​14-16, 19, 20 linarejelea ugonjwa wa kiroho? (Tazama pia picha.)

4 Mwanafunzi Yakobo anaanza kuzungumzia mpango wa Mungu wa kupata msaada wa kiroho kwa kuuliza hivi: “Je, kuna yeyote aliye mgonjwa kati yenu? Na awaite wazee wa kutaniko.” (Soma Yakobo 5:​14-16, 19, 20.) Muktadha unaonyesha kwamba Yakobo anazungumzia ugonjwa wa kiroho. Kwa mfano, mtu ambaye ni mgonjwa anaambiwa amwite, si daktari, bali wazee. Na tunajua anazungumzia ugonjwa wa kiroho kwa sababu uponyaji unaweza kuhusisha kusamehewa dhambi. Kwa njia fulani, hatua zinazohitajika ili kutibu ugonjwa wa kiroho ni sawa na zile zinazohitajika ili kutibu magonjwa ya kimwili. Tunapokuwa na ugonjwa wa kimwili, sisi huenda kwa daktari, tunamweleza dalili zetu, na kufuata mwongozo wake. Vivyo hivyo, tunapokuwa na ugonjwa wa kiroho, tunapaswa kwenda kwa mzee wa kutaniko, tumweleze kuhusu hali yetu, na tutende kulingana na shauri la Kimaandiko analotupatia.

Mkusanyo wa picha: 1. Mwanamume akimweleza daktari kuhusu tatizo lake kwenye bega. 2. Ndugu anamweleza mzee kuhusu hali yake huku wakiwa wameketi nje kwenye benchi.

Tunapokuwa wagonjwa kimwili, tunaenda kwa daktari; tunapokuwa wagonjwa kiroho, tunapaswa kwenda kwa wazee (Tazama fungu la 4)


5. Tunawezaje kujua ikiwa tuko katika hatari ya kuwa wagonjwa wa kiroho?

5 Mpango unaotajwa katika Yakobo sura ya 5 unatutia moyo twende kwa wazee tunapohisi kwamba afya yetu ya kiroho imeanza kudhoofika kwa njia yoyote. Hata hivyo, ni jambo lenye hekima kutafuta msaada kabla ya kuharibu kabisa uhusiano wetu mzuri na Mungu! Ni lazima tujichunguze kwa unyoofu. Maandiko yanatuonya kwamba tunaweza kujidanganya kuhusu hali yetu ya kiroho. (Yak. 1:22) Baadhi ya Wakristo wa mapema huko Sardi walifanya kosa hilo, na Yesu aliwaonya kuhusu hali yao ya kiroho. (Ufu. 3:​1, 2) Njia moja itakayotusaidia kuchunguza afya yetu ya kiroho ni kwa kulinganisha shauku yetu ya sasa kuelekea ibada yetu, na shauku tuliyokuwa nayo zamani. (Ufu. 2:​4, 5) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, shangwe yangu ya kusoma na kutafakari Biblia imepungua? Je, ninatayarisha na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida? Je, bidii yangu kwa ajili ya huduma imepungua? Je, raha au mali zinachukua muda wangu mwingi au ninatumia muda mwingi kuzifikiria?’ Ikiwa jibu la swali lolote kati ya hayo ni ndiyo, hilo linaweza kuonyesha udhaifu ambao ikiwa hautashughulikiwa huenda hali ikawa mbaya zaidi. Ikiwa tutashindwa kurekebisha udhaifu huo sisi wenyewe au ikiwa tayari umesababisha tuvunje viwango vya Mungu, tunapaswa kuomba msaada wa wazee wa kutaniko.

6. Wale waliotenda dhambi nzito wanapaswa kufanya nini?

6 Bila shaka, wale waliotenda dhambi nzito ambayo inaweza kufanya mtu aondolewe kutanikoni, wanapaswa kwenda kwa mzee. (1 Kor. 5:​11-13) Mtu yeyote ambaye ametenda dhambi nzito anahitaji msaada ili arekebishe uhusiano wake na Yehova. Ili kupata msamaha wa Yehova kupitia fidia, ni lazima tufanye “matendo yanayoonyesha toba.” (Mdo. 26:20) Matendo hayo yanatia ndani kwenda kwa wazee ikiwa tumetenda dhambi nzito.

7. Ni nani mwingine anayehitaji kuomba msaada wa wazee?

7 Wazee hawawasaidii tu wale waliofanya dhambi nzito, bali pia wanawasaidia wale ambao ni dhaifu kiroho. (Mdo. 20:35) Kwa mfano, huenda ukahisi kwamba unashindwa katika pambano lako dhidi ya tamaa mbaya. Huenda pambano lako likawa gumu zaidi ikiwa kabla ya kujifunza kweli ulikuwa mraibu wa dawa za kulevya, ulitazama ponografia, au ulifanya uasherati. Usihisi kwamba unahitaji kupambana na changamoto hizo peke yako. Unaweza kuzungumza na mzee wa kutaniko atakayesikiliza mahangaiko yako, atakayekupa ushauri hususa, na kukuhakikishia kwamba unaweza kumpendeza Yehova kwa kukataa kutenda kulingana na tamaa mbaya. (Mhu. 4:12) Ikiwa umevunjika moyo kwa sababu ya pambano lako, wazee wanaweza kukukumbusha kwamba hilo linaonyesha kuwa unachukua kwa uzito uhusiano wako na Yehova na unaepuka kujiamini.—1 Kor. 10:12.

8. Je, tunahitaji kuzungumza na wazee kuhusu kila kosa tunalofanya? Eleza.

8 Hatuhitaji kuwaona wazee kuhusu kila hangaiko ambalo huenda tunalo kuhusu afya yetu ya kiroho. Kwa mfano, tuseme kwamba umemwambia ndugu au dada maneno yenye kuumiza, au hata umemkasirikia sana. Badala ya kwenda kwa mzee, unaweza kutumia shauri la Yesu kwa kufanya amani kati yako na ndugu au dada yako. (Mt. 5:​23, 24) Unaweza kufanya utafiti kuhusu sifa ya upole, subira, na kujizuia ili uweze kuonyesha sifa hizo nzuri kikamili zaidi wakati ujao. Bila shaka, ikiwa utashindwa kusuluhisha tatizo lako, unaweza kumwomba mzee akusaidie. Katika barua yake kwa Wafilipi, mtume Paulo alimwomba ndugu ambaye hatajwi kwa jina, awasaidie Euodia na Sintike kusuluhisha tofauti zao, na mzee katika kutaniko lako anaweza kukusaidia kwa njia hiyo.—Flp. 4:​2, 3.

KWA NINI TUNAPASWA KUWAITA WAZEE?

9. Kwa nini hatupaswi kuruhusu aibu ituzuie kuwaita wazee? (Methali 28:13)

9 Tunahitaji imani na ujasiri ili kuomba msaada tunapotenda dhambi nzito au tunapohisi kwamba tunashindwa katika pambano letu dhidi ya udhaifu tulio nao. Hatupaswi kuruhusu aibu ituzuie kuwaita wazee. Kwa nini? Kwa kufuata mpango wa Yehova, tunaonyesha kwamba tunamtumaini yeye na miongozo yake ili itusaidie kuendelea kuwa na imani yenye nguvu. Tunakubali kwamba tunahitaji msaada wake ili tuendelee kufanya yaliyo sawa. (Zab. 94:18) Na ikiwa tumetenda dhambi, tutapata rehema za Mungu tukiungama na kuacha dhambi zetu.—Soma Methali 28:13.

10. Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa tutajaribu kuficha dhambi zetu?

10 Tunapata baraka kwa kuzungumza na mzee tunapohitaji msaada; hata hivyo, tunaweza kufanya hali yetu iwe mbaya zaidi ikiwa tutajaribu kuficha dhambi zetu. Mfalme Daudi alipojaribu kuficha dhambi zake, aliteseka kiroho, kihisia, na hata kimwili. (Zab. 32:​3-5) Kama ugonjwa wa kimwili au jeraha, mara nyingi tatizo la kiroho huwa baya zaidi ikiwa tutashindwa kulishughulikia. Yehova anaelewa hilo, hivyo anatualika “tunyooshe mambo” pamoja naye kupitia mpango alioweka kwa ajili ya kutuponya kiroho.—Isa. 1:​5, 6, 18.

11. Wengine wanaweza kuathiriwaje ikiwa tutaficha dhambi nzito?

11 Tunaweza kuwaathiri wengine ikiwa tutaficha dhambi nzito tulizofanya. Tunaweza kuzuia roho ya Mungu isitende kazi kwa uhuru katika kutaniko zima na hivyo kuhatarisha amani ya ndugu na dada zetu. (Efe. 4:30) Vivyo hivyo, ikiwa tunajua kwamba mtu fulani katika kutaniko ametenda dhambi nzito, tunapaswa kumhimiza azungumze na wazee kuhusu jambo hilo.a Kuficha dhambi nzito ya mtu mwingine kunatufanya sisi pia tuwe na hatia. (Law. 5:1) Upendo wetu kwa Yehova unapaswa kutuchochea kwenda kwa wazee na kusema ukweli. Hivyo, tunasaidia kudumisha kutaniko likiwa safi na kuwasaidia watenda dhambi warudishe uhusiano wao mzuri na Yehova.

WAZEE WANATUSAIDIAJE?

12. Wazee wanawasaidiaje wale walio dhaifu kiroho?

12 Wazee wameagizwa wawasaidie walio dhaifu kiroho. (1 The. 5:14) Ikiwa umetenda dhambi, huenda wakakuuliza maswali kwa utambuzi ili ‘kuteka’ mawazo na hisia zako za ndani. (Met. 20:5) Unaweza kuwasaidia kwa kujieleza waziwazi hata ikiwa kufanya hivyo ni vigumu kwako kwa sababu ya utamaduni, utu wako, au unaaibika kuzungumzia kilichotukia. Usiogope kwamba huenda maneno yako yakaonekana kama “mazungumzo ya ovyoovyo.” (Ayu. 6:3) Badala ya kufikia mkataa haraka, wazee watajitahidi kukusikiliza kwa makini na kupata habari kamili kabla ya kukupatia shauri. (Met. 18:13) Wanatambua kwamba kulichunga kundi kunachukua muda, hivyo hawatarajii kushughulikia matatizo katika kikao kimoja.

13. Wazee wanawezaje kutusaidia kupitia sala zao na mwongozo wa Kimaandiko? (Tazama pia picha.)

13 Unapowaita wazee, watajitahidi wasikuongezee hisia za hatia. Badala yake, watasali kwa niaba yako. Huenda ukashangazwa na jinsi ambavyo sala zao zina “nguvu nyingi.” Msaada wao unatia ndani pia “[kukupaka] mafuta katika jina la Yehova.” (Yak. 5:​14-16) “Mafuta” hayo yanarejelea kweli ya Neno la Mungu. Kupitia ustadi wao wa kutumia Biblia, wazee wanaweza kukubembeleza na kukufariji, na kukusaidia kurudisha uhusiano wako na Yehova. (Isa. 57:18) Mwongozo wa Kimaandiko wanaokupatia unaweza kuimarisha azimio lako la kuendelea kutenda yaliyo sawa. Kupitia wazee unaweza kusikia sauti ya Yehova ikikuambia hivi: ‘Hii ndiyo njia. Tembea ndani yake.’—Isa. 30:21.

Mkusanyo wa picha: 1. Daktari aliyekuwa katika picha ya awali akichunguza bega la yule mwanamume. Eksirei ya bega la mwanamume huyo imewekwa ukutani. 2. Mzee aliyekuwa katika picha ya awali na mzee mwingine wakitumia Biblia kumtia moyo yule ndugu nyumbani kwake. Ndugu anawasikiliza wazee kwa shangwe.

Wazee wanatumia Biblia kuwabembeleza na kuwafariji wale walio wagonjwa kiroho (Tazama fungu la 13-14)


14. Kulingana na Wagalatia 6:​1, wazee wanamsaidiaje mtu yeyote aliyechukua “hatua isiyofaa”? (Tazama pia picha.)

14 Soma Wagalatia 6:1. Mkristo anayechukua “hatua isiyofaa” hatembei kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu. Hatua isiyofaa inaweza kurejelea kufanya maamuzi yasiyo na busara au kutenda dhambi nzito. Wakichochewa na upendo, wazee Wakristo “[wanajaribu] kumrekebisha upya mtu huyo kwa roho ya upole.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kumrekebisha upya” linaweza pia kutumiwa kufafanua kitendo cha kurudisha mahali pake mfupa uliovunjika ili kuzuia ulemavu wa kudumu. Kama tu daktari stadi anavyojitahidi kurudisha mfupa uliovunjika bila kumsababishia mgonjwa maumivu mengi, wazee hujitahidi kutuponya ugonjwa wetu wa kiroho bila kutuongezea maumivu. Pia, wazee wameagizwa “[waendelee] kujiangalia.” Wanapotusaidia kunyoosha mapito yetu, wazee wanatambua kwamba wao pia si wakamilifu na wana mwelekeo wa kuchukua hatua zisizofaa. Hivyo, badala ya kujiona kuwa bora kuliko wengine, kuwa waadilifu kupita kiasi, au kuwa na mtazamo wa kuwahukumu wengine, wanajitahidi kuwa na hisia mwenzi.—1 Pet. 3:8.

15. Tunaweza kufanya nini ikiwa tuna tatizo?

15 Tunaweza kuwatumaini wazee wetu wa kutaniko. Wamezoezwa kutunza siri inapohusu mambo ya kibinafsi ya wengine, kutegemea Neno la Mungu wanapotoa ushauri badala ya maoni yao wenyewe, na kuendelea kutusaidia kubeba mizigo yetu. (Met. 11:13; Gal. 6:2) Wana utu na uzoefu tofauti, lakini tunaweza kujihisi huru kumfikia mzee yeyote na kumweleza matatizo yetu. Bila shaka, hatutaenda kwa mzee mmoja baada ya mwingine tukiomba ushauri, huku tukitazamia kwamba tutampata yule atakayetuambia mambo ambayo tunataka kusikia. Ikiwa tutafanya hivyo, tutakuwa kama wale ambao wanaona ni bora “masikio yao yafurahishwe” badala ya kujifunza “fundisho lenye manufaa” la Neno la Mungu. (2 Tim. 4:3) Tunapoenda kwa mzee kuzungumzia tatizo letu, anaweza kutuuliza ikiwa tumezungumza na wazee wengine na wametupatia ushauri gani. Na sifa ya kiasi inaweza kumchochea mzee huyo aombe ushauri kutoka kwa mzee mwingine.—Met. 13:10.

WAJIBU WETU WA KIBINAFSI

16. Kila mmoja wetu ana wajibu gani wa kibinafsi?

16 Ingawa wazee wanatulinda tukiwa kondoo wa Mungu, hawatuambii mambo ya kufanya. Ni wajibu wetu wa kibinafsi kuishi maisha ya ujitoaji-kimungu. Ni lazima tutoe hesabu mbele za Mungu kwa sababu ya maneno na matendo yetu. Kwa msaada wake, tunaweza kudumisha utimilifu. (Rom. 14:12) Hivyo, badala ya kutuambia mambo ya kufanya, wazee hutuonyesha njia ya kufikiri ya Mungu inayopatikana katika Neno lake. Kwa kufuata shauri lao linalotegemea Biblia, tunaweza kuzoeza “nguvu [zetu] za utambuzi” ili kufanya maamuzi yenye hekima.—Ebr. 5:14.

17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

17 Ni pendeleo lenye thamani sana kuwa kondoo wa Yehova! Yehova alimtuma Yesu, “mchungaji mwema,” alipe fidia kwa ajili yetu ili tuwe na fursa ya kupata uzima wa milele. (Yoh. 10:11) Na kupitia wazee katika kutaniko la Kikristo, Yehova ametimiza ahadi hii: “Nitawapa wachungaji wanaoupendeza moyo wangu, nao watawalisha kwa ujuzi na ufahamu.” (Yer. 3:15) Tunapokuwa dhaifu au wagonjwa kiroho, hatupaswi kusita kuwaita wazee ili watusaidie. Acheni tuendelee kuazimia kunufaika kikamili na uandalizi wa Yehova wa wazee wa kutaniko.

UNGEJIBUJE?

  • Ni wakati gani tunapaswa ‘kuwaita wazee’ watusaidie?

  • Kwa nini tunapaswa kuwaita wazee?

  • Wazee wanatusaidiaje?

WIMBO 31 Tembea Pamoja na Mungu!

a Ikiwa mtenda dhambi atashindwa kufanya hivyo baada ya kipindi cha kutosha cha wakati, ushikamanifu wako kwa Yehova unapaswa kukuchochea kuwaambia wazee mambo unayojua.

    Tanzanian sign language publications (2020-2026)
    Toka
    Ingia
    • Lugha ya Alama ya Tanzania
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki