Endelea Kuweka Ufalme pa Nafasi ya Kwanza
1 Kutia Ufalme pa nafasi ya kwanza maishani na kuendelea kufanya hivyo si jambo jepesi wakati tunapopambana na mikazo ya kiuchumi na matatizo mengine. Tunafanyaje ili kuendelea kuweka Ufalme pa nafasi ya kwanza wakati magumu yanapotokea? Namna gani ikiwa tunatolewa kazi inayoomba tukose mikutano au inayozuia utumishi wetu wa shambani? Je, wakati huo Ufalme unapaswa kuchukua nafasi ya pili maishani?
2 Imani Yenye Nguvu Inahitajiwa: Imani yetu inapojaribiwa chini ya hali kama hizo, hatupaswi kusahau ahadi ya Yehova na uhakikisho wa Yesu kuhusu utegemezo wa kimungu ikiwa tunatafuta kwanza Ufalme. (Zab. 37:25; Mt. 6:31-34) Uvutano na mikazo ya kilimwengu vinaweza kutia giza mtazamo wetu na kutuzuia tusiendelee kufanya Ufalme kuwa jambo la maana zaidi. Wengine wameacha matazamio ya kujulikana kazini au ya kupata fedha yawe jambo la maana zaidi maishani. Lakini, kama Paulo, tunahitaji kukadiria kwa usahihi lile lililo la maana kwelikweli maishani.—Flp. 3:7, 8.
3 Je, Marekebisho Yanahitajiwa? Mhubiri mmoja wa kike alisema: “Moyo wangu ulikuwa katika biashara yangu—ilikuwa ndilo jambo kubwa zaidi nililolipenda. Nilifikiri kwamba bado ningekuwa Shahidi huku nikitoa sehemu kubwa ya wakati wangu kwa faida za biashara.” Lakini, kwa namna yenye kusumbua, alihisi kwamba angeweza kufanya zaidi ili kumtumikia Yehova. Baadaye, akaacha biashara iliyokuwa ikizuia maendeleo yake ya kiroho. Alipojitoa kikamili kwa kazi ya Ufalme, aliweza kusema: “Sasa ninahisi kwamba maisha yangu ni yenye mafanikio machoni pa Yehova, na hilo ndilo jambo la maana kwelikweli.”
4 Jambo la kusifiwa ni kwamba wengi wameacha kazi za kimwili na matazamio ya faida kubwa zaidi za kifedha, wamefanya maisha yao kuwa mepesi, nao wameanza utumishi wa wakati wote. Watumishi wa huduma na wazee walio vijana na waseja wanaohudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wamefanya hivyo, nao wanafurahia mapendeleo mazuri ajabu ya utumishi. Wakiiga mfano wa juu sana wa Paulo, wanatosheka kikweli na vitu vya kimwili vya msingi.—1 Kor. 11:1; 1 Tim. 6:6-8; Ebr. 13:5.
5 Ingawa maoni yetu kuhusu maisha yanaweza kudhihakiwa na ulimwengu, sisi tunabarikiwa na Yehova. (1 Kor. 1:26-31) Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba atatutumia kikamili zaidi iwezekanavyo na kwamba atatusaidia tutimize kazi yake? Nafasi tuliyo nayo sasa ya kutangaza Ufalme wa Mungu uliosimamishwa haitarudiliwa kamwe. Kwa hiyo, huu ndio wakati wa kuendelea kuweka Ufalme pa nafasi ya kwanza maishani mwetu.