Jinsi ya Kufikia Miradi Yako ya Kumtumikia Mungu
1 Kwa kuwa wewe ni kijana Mkristo, bila shaka miradi yako inachochewa na upendo wako kwa Yehova na maneno ambayo Yesu aliambia Wakristo wote kuhusu ‘kutafuta kwanza Ufalme.’ (Mt. 6:33) Unaweza kujitilia mradi wa kupanua kazi yako ya kuhubiri kwa kuwa painia au kutumikia mahali ambako kazi ya kuhubiri Ufalme inahitaji wahubiri zaidi. Wengine wanaweza kuwa na wazo la kujitolea katika kazi ya ujenzi au kutumikia kwenye Betheli. Hiyo ni miradi yenye kufurahisha kweli na yenye kusifiwa.
2 Jambo linaloweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kumtumikia Mungu ni kuiandika. Mnara wa Mlinzi wa Julai 15, 2004, unasema hivi: ‘Mambo unayowaza moyoni yatakuwa wazi ukichagua maneno ili kuyaeleza. Kwa hiyo, labda utataka kuandika miradi yako na namna mbalimbali ulizopanga ili kuifikia.’ Kwa kuongezea, miradi ya kufikia kisha muda mfupi inaweza kukusaidia kuchunguza maendeleo unayofanya na kuendelea kukaza akilini mradi ambao unajitilia wa kufikia kisha muda mrefu.
3 Miradi ya Kufikia Kisha Muda Mfupi: Ikiwa bado haujabatizwa, fikiria yale unayohitaji kufanya ili kufikia mradi huo. Labda bado unahitaji kuelewa vizuri zaidi mafundisho ya msingi ya Biblia. Ikiwa ni hivyo, jiwekee mradi wa kujifunza kitabu Biblia Inafundisha na kukimaliza chote, ukisoma maandiko yote yanayotajwa humo. (1 Tim. 4:15) Jiwekee pia mradi wa kusoma Biblia nzima kuanzia kitabu cha Mwanzo mpaka Ufunuo, kama vile Wanabetheli na wanafunzi wa Gileadi wanavyoombwa kufanya. Kisha kufikia mradi huo, endelea na programu ya kawaida ya kusoma Biblia kila siku. (Zab. 1:2, 3) Jambo hilo linaweza kukusaidia kukomaa kiroho. Kila wakati unaposoma au kujifunza Biblia, anza na sala na kumaliza na sala ya kutoka moyoni, na kila mara tafuta namna ya kutumia mambo unayojifunza.—Yak. 1:25.
4 Ikiwa wewe umekwisha kubatizwa, ni miradi gani mingine unayoweza kufuatia? Je, unahitaji kuongeza ufundi wako wa kuhubiri? Kwa mfano, je, unaweza kujitilia mradi wa kuwa fundi zaidi katika kutumia Neno la Mungu katika mahubiri? (2 Tim. 2:15) Unawezaje kupanua kazi yako ya kuhubiri? Jiwekee miradi ya kufikia kisha muda mfupi, miradi inayopatana na miaka yako na hali yako, na ambayo itakusaidia ufikie miradi yako ya kisha muda mrefu.
5 Simulizi Lenye Matokeo Mema: Tony, kijana mmoja mwenye umri wa miaka 19 alipotembelea Betheli fulani ya Mashahidi wa Yehova, alipendezwa na utumishi wa Betheli. Lakini, alikuwa na mwenendo mbaya, naye alikuwa hajatoa maisha yake wakfu kwa Yehova. Tony aliamua kupatanisha maisha yake na mapenzi ya Yehova na akajiwekea mradi wa kutimiza yale yanayoombwa ili kubatizwa. Baada ya kufikia mradi huo, kijana huyo alijiwekea mradi wa kuwa painia msaidizi na kisha painia wa kawaida. Yeye alikuwa akiandika kwenye kalenda yake tarehe ambazo alitaka kuanza utumishi huo. Wazia furaha aliyopata alipoitwa kwenye Betheli, baada ya kutumikia kama painia kwa muda fulani!
6 Wewe pia unaweza kufikia miradi yako ya kumtumikia Mungu unapotafuta kwanza faida za Ufalme. Endelea kusali Yehova kwa ajili ya “kazi zako” na ujikaze kabisa kuzitimiza.—Met. 16:3; 21:5.
[Maulizo ya Funzo]
1. Vijana wengi Wakristo wana miradi gani ya kumtumikia Mungu?
2. Ni nini kinachoweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kumtumikia Mungu?
3. Taja miradi fulani ya kufikia kisha muda mfupi ambayo inaweza kusaidia mtu astahili kubatizwa.
4. Mkristo aliye na mradi wa kutumika kwenye Betheli au kuwa painia wa pekee, anaweza kujiwekea miradi gani ya kufikia kisha muda mfupi?
5. Namna gani kujiwekea miradi ya kufikia kisha muda mfupi kulisaidia ndugu mmoja kufikia mradi wake wa kutumikia kwenye Betheli?
6. Ni jambo gani linaloweza kukusaidia kufikia miradi yako ya kumtumikia Mungu?