Kisanduku Cha Maulizo
◼ Je, ni jambo lenye kufaa kwa Shahidi wa Yehova kutunzwa kwenye hopitali ao nyumba ya kutunzia watu yenye kusimamiwa na dini fulani?
Dini nyingi zinasimamia hopitali ao nyumba za kutunzia watu zinazotoa matunzo ya kiganga ao kutunza watu walio na magonjwa yasiyopona. Kwa kawaida, hopitali hizo hazifanywi tu kwa faida ya Babiloni Mkuu. (Ufu. 18:2, 4) Labda, mwanzoni, zilijengwa kwa kusudi la kutolea dini fulani feza. Leo, hopitali fulani zinaitwa tu kwa jina la dini fulani, lakini zingine zina nusu ya wafanya-kazi walio viongozi wa dini.
Ikiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova anataka kwenda kwenye hopitali ao nyumba ya kutunzia watu, anapaswa kuamua yeye mwenye ikiwa ataenda mahali panaposimamiwa na dini fulani. Zamiri ya mtu mmoja inaweza kumruhusu kwenda mahali hapo, lakini zamiri ya mwingine inaweza kumzuia. (1 Tim. 1:5) Kuna hali fulani zinazoweza kufanya mtu achukue uamuzi fulani, na ni vizuri kufikiria hali hizo.
Kwa mfano, hopitali fulani ao nyumba ya kutunzia watu inayoitwa kwa jina la dini fulani inaweza kuwa ndiyo mahali palipo karibu. Ao ikiwa kuna hopitali nyingine iliyo karibu, labda ile inayosimamiwa na dini fulani ndiyo yenye kutunza vizuri. Hopitali hiyo yenye kuitwa kwa jina la dini fulani inaweza kuwa ndiyo tu inayoweza kutoa matunzo yenye kuhitajiwa, ao daktari ao mganga anayeweza kukutunza anatumikia tu kwenye hopitali hiyo. Pia, nyakati nyingine hopitali zinazosimamiwa na dini zinaweza kuheshimu uamuzi wako wa Kikristo kuhusu matumizi ya damu, lakini hopitali ya mtu fulani ao ya Leta isikubali kuheshimu uamuzi huo. Kwa hiyo, hayo ni mambo fulani ambayo unaweza kufikiria unapoamua mahali pa kutunziwa.
Ikiwa unaamua kwenda kwenye hopitali ao nyumba ya kutunzia watu inayosimamiwa na dini, unaweza kuiona kama vile kulipa mtu fulani aliyekufanyia kazi ya lazima. Unaweza kuona jambo hilo kama vile biashara inayofanywa na dini, na kununua kitu fulani kutokana na biashara hiyo hakufanyi uchangie moja kwa moja kwa kujipendea ili kutegemeza dini ya uongo. Hilo ni kama kuuza tu kitu fulani ao kulipa mtu aliyekufanyia kazi fulani.
Bila shaka, ukiwa Mkristo, katika hali hizo, unapaswa kuhakikisha kwamba haujihusishe katika tendo lolote lenye kuhusiana na ibada ya uongo. Pia, hautatumia majina ya cheo kama vile “Padiri” ao “Ma soeur,” ili kuita watu wanaotumika ao wanaotembelea kwenye hopitali hizo. (Mt. 23:9) Unaweza kuona jambo hilo kuwa ni mpango wa biashara tu unaokusaidia kupata matunzo, wala si jambo lingine lolote.
Unapopanga kwenye hopitali, unaweza kujulisha kwamba wewe ni Shahidi wa Yehova na kwamba unataka kutembelewa na wazee wa kutaniko lenu. Kwa kufanya hivyo utahakikishwa kwamba utategemezwa kwa njia inayofaa wakati wote utakapokuwa katika hopitali.—1 The. 5:14.
Washiriki wa familia walio waamini, wazee na washiriki wengine wa kutaniko lenu wanapaswa kuhakikisha kwamba wanahangaikia mahitaji ya ndugu na dada wazeewazee walio katika nyumba za kutunzia watu, zaidi sana ikiwa nyumba hizo zinasimamiwa na dini fulani. Kujikaza kufanya hivyo kutatia moyo sana wazee-wazee hao na kutawazuia kujihusisha bila kujua katika miazimisho, ao mambo yoyote yanayohusiana na dini ya uongo yenye kufanywa katika hopitali hiyo.
Tukijua mambo hayo, kila mtu atafikiria hali yoyote inayoweza kujitokeza na kwa hiyo kuamua yeye mwenyewe ni hopitali ao nyumba ya matunzo gani ambako ataenda.—Gal. 6:5.