Vijana, Munajikaza ili Kufikia Mapendeleo ya Kiteokrasi?
1. Ni wakati gani kijana aliyebatizwa anaweza kuanza kutumia shauri lililo katika 1 Timotheo 3:1?
1 Ikiwa mwanamume yeyote anajikaza ili kufikia mapendeleo, “yeye anatamani kazi njema.” (1 Tim. 3:1) Maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanawatia ndugu moyo wajikaze kutimiza mambo yanayoombwa ili kufikia mapendeleo katika kutaniko. Je, ni lazima uwe mutu mukubwa ili utimize mambo hayo? Kwa kweli, ni vizuri zaidi kuanza kujikaza kufikia mapendeleo ya kiteokrasi wakati ungali kijana. Hivyo unaweza kupewa mazoezi na kupata nafasi ya kuonyesha kama unastahili kuwekwa kuwa mutumishi wa huduma unapokomaa. (1 Tim. 3:10) Ikiwa wewe ni kijana aliyebatizwa, unaweza kufanya nini ili kufikia mapendeleo ya kiteokrasi?
2. Namna gani mutu anaweza kukomalisha roho ya kujitoa na kuionyesha?
2 Kuwa na Roho ya Kujitoa: Kumbuka kwamba unajikaza kufikia kazi njema, si kutafuta cheo. Kwa hiyo, komalisha nia ya kuwasaidia ndugu na dada. Njia moja ya kufanya hivyo ni kutafakari juu ya mufano muzuri wa Yesu. (Mt. 20:28; Yoh. 4:6, 7; 13:4, 5) Sali kwa Yehova akusaidie kuwahangaikia wengine. (1 Kor. 10:24) Je, unaweza kuwasaidia wale waliozeeka ao wazaifu kimwili katika kutaniko? Je, unajitoa ili kukata majani, ao kufanya kazi ingine yoyote ya kutengeneza ao kusafisha Jumba la Ufalme? Je, unaweza kujitoa ili kupitisha kipindi cha mutu ambaye hakufika wakati wa Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi? Utaona kwamba kujitoa kwa ajili ya wengine kutakuletea furaha.—Mdo. 20:35.
3. Sababu gani ni vizuri zaidi kuwa na hali nzuri ya kiroho, na tunaweza kuikomalisha namna gani?
3 Kuwa na Hali Nzuri ya Kiroho: Ni vizuri zaidi kuwa na hali nzuri ya kiroho kuliko kuwa na uwezo wa pekee ao uwezo uliozaliwa nao. Mutu aliye na hali nzuri ya kiroho anaona mambo kama Yehova na Yesu wanavyoyaona. (1 Kor. 2:15, 16) Anaonyesha ‘tunda la roho.’ (Gal. 5:22, 23) Ni muhubiri mwenye bidii anayetia mambo ya kiroho pa nafasi ya kwanza. (Mt. 6:33) Unaweza kukomalisha sifa za kiroho kwa kufanya funzo la pekee kwa ukawaida. Hilo linatia ndani kusoma Biblia kila siku, kusoma kila gazeti Munara wa Mulinzi na Amuka!, kutayarisha na kuhuzuria mikutano ya kutaniko. (Zab. 1:1, 2; Ebr. 10:24, 25) Wakati Paulo alimutia moyo kijana Timotheo afanye maendeleo ya kiroho, aliandika hivi: ‘Angalia daima kufundisha kwako.’ (1 Tim. 4:15, 16) Kwa hiyo, tayarisha vizuri migawo unayopewa kwenye Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi. Jitayarishe kwa ajili ya mahubiri, na uhubiri kwa ukawaida. Ujiwekee miradi ya kiroho, kama vile kuwa painia, kutumikia kwenye Beteli, ao kusoma Masomo kwa Ajili ya Ndugu Wasio na Bibi, na ujikaze kufikia miradi yako. Kuwa na hali nzuri ya kiroho kutakusaidia ‘kuzikimbia tamaa zinazotukia katika ujana.’—2 Tim. 2:22.
4. Sababu gani ni jambo la maana kuwa mwenye kutegemeka na mwaminifu?
4 Kuwa Mwenye Kutegemeka na Mwaminifu: Wakati wa mitume, ndugu ambao walipewa kazi ya kugawanya chakula kwa Wakristo waliokuwa katika uhitaji walikuwa watu ‘waliosibitishwa,’ ni kusema waliojulikana kuwa wenye kutegemeka na waaminifu; kwa hiyo mitume hawangeogopa wakijiuliza ikiwa kazi hiyo itafanywa vizuri. Hilo liliwasaidia kushugulikia mambo mengine ya lazima. (Mdo 6:1-4) Ndiyo sababu, unapopewa kazi fulani katika kutaniko, uitimize kwa uaminifu. Umuige Noa, ambaye alifuata kwa uangalifu maagizo aliyopewa ili kujenga safina. (Mwa. 6:22) Uaminifu ni wa maana sana machoni pa Yehova, na unapotimiza kwa uaminifu mugawo wako, hilo linaonyesha kwamba umekomaa kiroho.—1 Kor. 4:2; ona kisanduku chenye kichwa “Faida za Kuwazoeza Vijana.”
5. Sababu gani vijana wanapaswa kujikaza ili kufikia mapendeleo ya kiteokrasi?
5 Kama ilivyotabiriwa, leo Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya watu. (Isa. 60:22) Watu zaidi ya 250000 wanabatizwa kila mwaka. Kwa kuwa wapya wengi wanaikubali kweli, ndugu wenye ufundi walio na hali nzuri ya kiroho wanahitajiwa ili kushugulikia madaraka katika kutaniko. Kuliko wakati mwengine wowote, leo kuna kazi nyingi ya kufanya katika utumishi wa Yehova. (1 Kor. 15:58) Vijana, munajikaza ili kufikia mapendeleo ya kiteokrasi? Ikiwa ni hivyo, munatamani kazi njema kabisa!
[Wazo la fungu kwenye ukurasa 2]
Kwa kuwa wapya wengi wanaikubali kweli, ndugu wenye ufundi walio na hali nzuri ya kiroho wanahitajiwa ili kushugulikia madaraka katika kutaniko
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Faida za Kuwazoeza Vijana
Vijana wanaostahili wanafaidika wakati wazee wanawapatia migawo na kuwazoeza. Kisha mikutano, mwangalizi mumoja wa muzunguko alikuwa akikaa kwenye jukwaa akimutia moyo muhubiri fulani. Alimuona kijana fulani akisimama pembeni yao, kwa hiyo akamuuliza ikiwa alitaka kuzungumuza naye. Ndugu huyo kijana alijibu kwamba alipewa mugawo wa kusafisha jukwaa kisha mikutano. Wazazi wake walikuwa tayari kurudi nyumbani, lakini yeye hakutaka kuenda bila kutimiza mugawo wake. Mwangalizi akafurahi, na akaondoka. Alieleza hivi: “Wazee katika kutaniko hilo walikuwa tayari kuwazoeza vijana wanaostahili kwa kuwapatia migawo katika kutaniko. Kwa hiyo, kila mara nilipotembelea kutaniko lao hawakukosa kupendekeza kijana fulani kuwa mutumishi wa huduma.”