Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi ya 2015 Yatatusaidia Kukomalisha Ufundi Wetu wa Kufundisha
1 Mutunga-Zaburi Daudi aliandika hivi: ‘Maneno ya kinywa changu na kutafakari kwa moyo wangu na yawe yenye kupendeza mbele zako, Ee Yehova Mwamba wangu na Mukombozi wangu.’ (Zab. 19:14) Sisi pia tunataka maneno yetu yamupendeze Yehova kwa sababu tunapendezwa na daraka letu la kutangaza ujumbe wa Biblia katika kutaniko na katika mahubiri. Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi ni njia moja ambayo Yehova anatumia ili kutuzoeza kwa ajili ya mahubiri. Masomo hayo yanafanywa kila juma katika makutaniko zaidi ya 111000 katika dunia yote. Yamesaidia ndugu na dada wa desturi mbalimbali duniani kote ili wastahili kabisa kuwa wahubiri wa habari njema wenye uwezo wa kufundisha kwa usadikisho, kwa busara, na bila woga.—Mdo. 19:8; Kol. 4:6.
2 Habari zilizo katika programu ya masomo ya 2015 zitatoka katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya [bi12], kitabu Étude Perspicace des Écritures [it-1 na 2-F], kijitabu Habari za Kujifunza Katika Neno la Mungu [igw] na Munara wa Mulinzi [w]. Pia, mabadiliko yamefanywa kuhusu wakati ambao mambo makuu ya usomaji wa Biblia na mugawo Na. 1 vitachukua. Mabadiliko hayo na maagizo kuhusu namna migawo inapaswa kutolewa kwenye masomo, yanaonyeshwa kwenye mafungu yanayofuata.
3 Mambo Makuu ya Usomaji wa Biblia: Ndugu ambao wamepewa sehemu hii, watatumia dakika mbili ili kuzungumuzia habari moja yenye kujenga na yenye kufaa kutoka katika usomaji wa Biblia wa kila juma. Kujitayarisha muzuri kutawasaidia wazungumuzie wazo ambalo linafaa kwa ajili ya kutaniko bila kuvuka wakati. Kama kawaida, wasikilizaji wataachiwa dakika sita ili wao pia watoe maelezo yasiyopita segonde 30 kuhusu mambo ambayo wamefurahia katika usomaji wa Biblia wa juma hilo. Inaomba kujitayarisha vizuri na kujikaza sana ili kutoa maelezo mazuri kwa segonde 30, lakini kufanya hivyo kunatuzoeza. Hilo linafanya wengine pia wapate nafasi ya kutoa maelezo kuhusu mambo ambayo wamejifunza katika usomaji wao.
4 Mugawo Na. 1: Wakati uliowekwa kwa ajili ya usomaji wa Biblia umepunguzwa; usomaji huo haupaswe kupita dakika tatu na utachukua maandiko machache ya Biblia. Wale ambao watapewa sehemu hii watafanya mazoezi mengi kwa kusoma kwa sauti na kuwa waangalifu kutamka vizuri maneno na kusoma kwa njia inayotiririka ili usomaji wao uwe wenye kueleweka muzuri. Watumishi wote wa Yehova wanapaswa kujikaza kusoma vizuri, kwa sababu usomaji unachukua sehemu ya maana katika ibada yetu. Tunafurahi sana kwa sababu watoto wetu wengi wanasoma vizuri! Tunawapongeza Wazazi kwa sababu wanajikaza kuwasaidia watoto wao kwa upendo ili wakuwe wasomaji wazuri.
5 Mugawo Na. 2: Sehemu hii itachukua dakika tano na itatolewa na dada. Mwanafunzi anapaswa kutumia kichwa cha habari ambacho alipewa. Ikiwa mugawo unategemea kijitabu Habari za Kujifunza Katika Neno la Mungu, mwanafunzi ataupatanisha na sehemu fulani yenye kufaa ya kazi ya kuhubiri katika eneo lenu. Ikiwa mugawo unategemea mutu fulani anayezungumuziwa katika Biblia, kama vile inaonyeshwa katika kitabu Étude Perspicace des Écritures, mwanafunzi anapaswa kuzungumuzia kichwa ambacho amepewa, kuchagua maandiko yenye kufaa ambayo atatumia, na kuonyesha mambo ambayo tunajifunza kutoka kwa mutu huyo. Maandiko mengine yenye kupatana na kichwa cha habari yanaweza pia kutumiwa. Ni mwangalizi wa masomo ndiye atachagua musikilizaji.
6 Mugawo Na. 3: Sehemu hii itachukua dakika tano na itatolewa na ndugu ao dada. Ikiwa dada ndiye amepewa sehemu hii, ataitoa kama mugawo Na. 2. Ikiwa ndugu ndiye amepewa sehemu inayotegemea kitabu Perspicace, anapaswa kuitoa kama hotuba na kuelekeza maneno yake kwa wasikilizaji. Mwanafunzi anapaswa kuzungumuzia kichwa cha mugawo wake, kutumia maandiko yenye kufaa, na kuonyesha mambo ambayo tunaweza kujifunza kutoka kwa mutu huyo anayezungumuziwa katika Biblia.
7 Namna Mupya ya Kutoa Mugawo Na. 3 Ikiwa Utatolewa na Ndugu: Ikiwa ndugu ndiye amepewa mugawo unaotegemea kijitabu Habari za Kujifunza Katika Neno la Mungu, atautoa kama onyesho la watu wenye kufanya ibada ya familia ao wenye kuhubiri. Mara mingi, mwangalizi wa masomo ndiye atachagua musikilizaji na kikao. Musikilizaji atakuwa mutu wa familia ya mwanafunzi ao ndugu mwengine katika kutaniko. Maandiko mengine yenye kukazia kanuni za Biblia na yenye kupatana na kichwa cha habari yanaweza kutumiwa. Mara kwa mara, sehemu hii itapewa muzee wa kutaniko, na muzee huyo ndiye atachagua musikilizaji na kikao. Bila shaka, kutaniko litatiwa moyo sana kuona namna wazee wanaonyesha ufundi wa kufundisha pamoja na mutu wa familia yao ao ndugu mwengine.
Ukubali na utumikishe mashauri yenye unapewa ili ufanye maendeleo
8 Mashauri: Mwangalizi wa masomo atatumia dakika mbili kisha kila mugawo wa wanafunzi ili kupongeza mwanafunzi na kutoa mashauri yenye kujenga na ambayo yanategemea kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Mwangalizi wa masomo hatataja sifa ya usemi ambayo mwanafunzi anatumikia mbele ya mwanafunzi huyo kutoa mugawo wake. Kisha kila mugawo, mwangalizi atasema maneno yenye kufaa ili kumupongeza mwanafunzi, atataja sifa ya usemi ambayo mwanafunzi anatumikia, na kuonyesha sababu gani mwanafunzi alitumikia vizuri sifa hiyo ya usemi, ao kuonyesha kwa njia yenye kutia moyo sababu gani ingekuwa vizuri mwanafunzi akazie sifa hiyo uangalifu zaidi.
9 Fomu ya mashauri kwa ajili ya mwanafunzi inapatikana kwenye ukurasa wa 79 mupaka 81 wa kitabu Shule ya Huduma. Kisha mikutano, mwangalizi wa masomo ataandika mambo fulani katika kitabu cha mwanafunzi ili kuonyesha kwamba ametimiza ao hakutimiza sifa ya usemi ambayo alipewa na atamuuliza kipekee ikiwa alifanya mazoezi yanayohusiana na sifa hiyo. Mwangalizi wa masomo anaweza kumupongeza mwanafunzi ao kumutolea mashauri mengine kisha mikutano ao wakati mwingine. Kila mwanafunzi anapaswa kuona mashauri ambayo anapewa kipekee kuwa nafasi nzuri ya kumusaidia afanye maendeleo ya kiroho.—1 Tim. 4:15.
10 Ikiwa mwanafunzi anavuka wakati uliowekwa, mwangalizi wa masomo ao musaidizi wake atakuwa mwangalifu kufanya alama fulani, kama vile kupiga ao kugonga kitu fulani ili kumujulisha mwanafunzi kwamba wakati wake umeisha. Atafanya hivyo kwa njia ambayo haitakengeusha wasikilizaji. Mwanafunzi anapaswa kutambua alama hiyo kwa kumaliza sentesi yake na kutoka kwenye jukwaa.—Soma kitabu Shule ya Huduma, uku. 282, fu. 4.
11 Wote ambao wanatimiza mambo yanayoombwa ili kuwa wanafunzi kwenye Masomo ya Huduma ya Kiteokrasi wanatiwa moyo kujiandikisha. (Soma kitabu Shule ya Huduma, uku. 282, fu. 6.) Mazoezi ambayo watumishi wa Yehova wanapata kwenye masomo hayo yamewawezesha kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme kwa uhakika, kwa heshima, na kwa upendo. Bila shaka, Yehova anafurahi sana kuona anasifiwa na watu ambao wanapata mazoezi mengi mazuri kwenye masomo ya kiteokrasi!—Zab. 148:12, 13; Isa. 50:4.