Kutoka
9 Kwa hiyo Yehova akamuambia Musa: “Ingia kwa Farao na umuambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania anasema hivi: “Ruhusu watu wangu waende ili waweze kunitumikia.+ 2 Lakini kama unakataa kuwaruhusu waende na ukiendelea kuwazuia, 3 angalia! mukono wa Yehova+ utakuja juu ya mifugo yenye kuwa katika eneo la mashamba. Kutakuwa pigo kali juu ya farasi, punda, ngamia, mifugo, na makundi.+ 4 Na hakika Yehova atafanya kukuwe tofauti kati ya mifugo ya Israeli na mifugo ya Misri, na hakuna munyama wa Waisraeli mwenye atakufa.”’”+ 5 Tena, Yehova akaweka wakati wa kufanya vile, na kusema: “Kesho Yehova atafanya jambo hilo katika inchi.”
6 Na Yehova akafanya vile siku yenye ilifuata, na kila aina ya mifugo ya Misri ikaanza kufa,+ lakini hakuna munyama yeyote kati ya mifugo ya Israeli mwenye alikufa. 7 Wakati Farao aliuliza watu, angalia! hakuna munyama hata mumoja kati ya mifugo ya Israeli mwenye alikuwa amekufa. Lakini, moyo wa Farao ukaendelea kuwa mugumu, na hakuruhusu watu waende.+
8 Kisha Yehova akaambia Musa na Haruni: “Mujaze majivu meusi ya tanuru katika mikono yenu mbili, na Musa anapaswa kuyatupa katika hewa mbele ya Farao. 9 Na yatageuka kuwa mavumbi laini juu ya inchi yote ya Misri, na yatageuka kuwa majipu yenye usaha kwenye miili ya watu na wanyama katika inchi yote ya Misri.”
10 Kwa hiyo wakakamata majivu meusi ya tanuru na kusimama mbele ya Farao, na Musa akayatupa katika hewa, na yakageuka kuwa majipu yenye usaha na yenye kupasuka kwenye miili ya watu na wanyama. 11 Makuhani wenye kufanya uchawi hawakuweza kusimama mbele ya Musa kwa sababu ya majipu, kwa maana majipu hayo yalikuwa yametokea juu ya makuhani wenye kufanya uchawi na juu ya Wamisri wote.+ 12 Lakini Yehova akaacha moyo wa Farao ukuwe mugumu, na hakuwasikiliza, kama vile Yehova alikuwa amemuambia Musa.+
13 Kisha Yehova akamuambia Musa: “Amuka asubui sana na usimame mbele ya Farao, na umuambie, ‘Yehova Mungu wa Waebrania anasema hivi: “Ruhusu watu wangu waende ili waweze kunitumikia. 14 Kwa maana wakati huu ninatuma mapigo yangu ili kupiga moyo wako, watumishi wako, na watu wako, kusudi uweze kujua kwamba hakuna mwenye kuwa kama mimi katika dunia yote.+ 15 Kwa maana kufikia sasa ningekuwa nimenyoosha mukono wangu ili kukupiga wewe na watu wako kwa pigo kali, na ungekuwa umeondolewa* juu ya dunia. 16 Lakini nimekuacha uendelee kuishi kwa sababu hii: ili nikuonyeshe nguvu zangu na ili jina langu litangazwe katika dunia yote.+ 17 Je, ungali unajiendesha kwa kiburi kwa kukataa kuruhusu watu wangu waende? 18 Kesho, wakati kama huu, nitaleta mvua kubwa sana ya majiwe yenye hakuna siku imetokea katika inchi ya Misri tangu wakati musingi wake uliwekwa mupaka sasa. 19 Kwa hiyo, ambia watu watoshe mifugo yako yote na vitu vyako vyote vyenye kuwa katika eneo la mashamba na kuvileta mahali salama. Kila mutu na kila munyama mwenye atapatikana katika eneo la mashamba na mwenye hataletwa katika nyumba atakufa wakati mvua ya majiwe itaanguka juu yao.”’”
20 Kila mutu kati ya watumishi wa Farao mwenye aliogopa neno la Yehova akaleta haraka watumishi wake mwenyewe na mifugo yake katika nyumba, 21 lakini kila mutu mwenye hakuweka katika moyo wake neno la Yehova aliacha watumishi wake na mifugo yake katika eneo la mashamba.
22 Sasa Yehova akamuambia Musa: “Nyoosha mukono wako kuelekea mbinguni, ili mvua ya majiwe ianguke juu ya inchi yote ya Misri,+ juu ya watu na wanyama na juu ya mimea yote ya mashamba katika inchi ya Misri.”+ 23 Kwa hiyo Musa akanyoosha fimbo yake kuelekea mbinguni, na Yehova akatuma mingurumo ya radi na mvua ya majiwe, na moto* ukashuka juu ya dunia, na Yehova akaendelea kufanya mvua ya majiwe inyeshe juu ya inchi ya Misri. 24 Kulikuwa mvua ya majiwe, na moto ulikuwa unawaka katikati ya mvua hiyo ya majiwe. Mvua hiyo ya majiwe ilikuwa kubwa sana; hakuna siku mvua ya majiwe kama hiyo ilikuwa imenyesha katika inchi tangu wakati Misri ilikuwa taifa.+ 25 Mvua hiyo ya majiwe ilipiga kila kitu katika eneo lote la mashamba la inchi ya Misri, kuanzia mutu mupaka munyama, na ilipiga mimea yote na kuvunja-vunja miti yote ya mashamba.+ 26 Ni katika inchi ya Gosheni tu, mahali Waisraeli walikuwa, ndio mvua hiyo ya majiwe haikukuwa.+
27 Kwa hiyo Farao akatuma watu ili Musa na Haruni waletwe na akawaambia: “Mara hii nimefanya zambi. Yehova ni mwenye haki, lakini mimi na watu wangu tumekosea. 28 Mumulilie Yehova ili mingurumo ya radi na mvua hii ya majiwe ya Mungu imalizike. Kisha nitakuwa tayari kuwaruhusu muende, na hamutaendelea kukaa hapa.” 29 Kwa hiyo Musa akamuambia: “Wakati tu nitatoka katika muji, nitanyoosha mikono yangu mbele ya Yehova. Mingurumo ya radi itamalizika na mvua ya majiwe haitaendelea tena, ili uweze kujua kwamba dunia ni ya Yehova.+ 30 Lakini kuhusu wewe na watumishi wako, tayari ninajua kwamba hata wakati huo, hamutamuogopa Yehova Mungu.”
31 Sasa mimea ya kitani na mimea ya shayiri ilikuwa imepigwa, kwa sababu mimea ya shayiri ilikuwa na masuke na mimea ya kitani ilikuwa imetoa matumba ya maua. 32 Lakini ngano na ngano ya kusemeti haikupigwa kwa sababu ilikuwa haijakomaa.* 33 Sasa Musa akatoka katika muji mbele ya Farao na akanyoosha mikono yake mbele ya Yehova na mingurumo ya radi na mvua ya majiwe ikaisha na mvua ikaacha kumwangika juu ya dunia.+ 34 Wakati Farao aliona kwamba mvua, mvua ya majiwe, na mingurumo ya radi vimeisha, akatenda zambi tena na akafanya moyo wake ukuwe mugumu,+ yeye pamoja na watumishi wake. 35 Na moyo wa Farao ukaendelea kuwa mugumu, na hakuruhusu Waisraeli waende, kama vile Yehova alikuwa amemuambia Musa.+