Alhamisi, Septemba 11
Thibitisheni upendo wenu kwao.—2 Kor. 8:24.
Tunawaonyesha upendo ndugu na dada zetu kwa kuwakaribisha wawe rafiki zetu. (2 Kor. 6:11-13) Wengi wetu tunashirikiana na makutaniko yenye ndugu na dada kutoka katika malezi mbalimbali na wenye nyutu mbalimbali. Tunaweza kuimarisha upendo wetu kuelekea watu wote kwa kukazia fikira sifa zao nzuri. Tunapojifunza kuwaona wengine kama Yehova anavyowaona, tunathibitisha kwamba tunawapenda. Tutahitaji kuonyeshana upendo wakati wa dhiki kuu. Dhiki kuu itakapoanza tutapata wapi ulinzi? Fikiria jambo ambalo Yehova aliwaagiza watu wake wafanye Babiloni la kale liliposhambuliwa: “Nendeni, watu wangu, ingieni katika vyumba vyenu vya ndani, na mfunge milango nyuma yenu. Jificheni kwa muda mfupi mpaka ghadhabu itakapopita.” (Isa. 26:20) Inaonekana kwamba maneno hayo yanatuhusu pia sisi ambao tutakabiliana na dhiki kuu. w23.07 29:14-16
Ijumaa, Septemba 12
Tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.—1 Kor. 7:31.
Ujulikane kuwa mtu mwenye usawaziko. Jiulize hivi: ‘Je, watu wananiona kuwa mwenye usawaziko, mwenye kukubali sababu, na kuwavumilia wengine? Au je, wanaona kwamba ninashikilia maoni yangu, ni mkali, au mwenye kichwa kigumu? Je, ninawasikiliza wengine na kukubaliana na maoni yao inapofaa?’ Kadiri tunavyozidi kuwa wenye usawaziko, ndivyo tunavyoonyesha kwamba tunamwiga Yehova na Yesu. Usawaziko unahusisha kunyumbulika hali zetu zinapobadilika. Mabadiliko hayo yanaweza kutusababishia matatizo tusiyotarajia. Huenda ukapatwa na ugonjwa ghafla. Au mabadiliko ya ghafla ya hali ya kiuchumi au ya kisiasa yanapotokea mahali tunapoishi yanaweza kuvuruga kabisa maisha yetu. (Mhu. 9:11) Huenda hata tukakabili hali ngumu tunapopata badiliko la mgawo wa kitheokrasi. Tunaweza kufanikiwa kunyumbulika hali zinapobadilika ikiwa tutachukua hatua nne zifuatazo: (1) kubali kwamba mambo yamebadilika, (2) fikiria kuhusu wakati ujao, (3) kazia fikira mambo yanayojenga, na (4) uwasaidie wengine. w23.07 32:7-8
Jumamosi, Septemba 13
Wewe ni mtu mwenye thamani sana.—Dan. 9:23.
Nabii Danieli alikuwa kijana Wababiloni walipomfanya kuwa mfungwa na kumpeleka nchi ya mbali huko Babiloni. Lakini ni wazi kwamba Danieli aliwafurahisha wale waliomchukua mateka. Waliona kile “kinachoonekana kwa macho”—kwamba Danieli ‘hakuwa na kasoro yoyote, alikuwa mzuri kwa umbo’ na alitoka kwenye familia mashuhuri. (1 Sam. 16:7) Kutokana na sababu hizo, Wababiloni walimzoeza ili atumikie kwenye makao ya mfalme. (Dan. 1:3, 4, 6) Yehova alimpenda Danieli kwa sababu ya sifa alizoamua kusitawisha. Kwa kweli, huenda Danieli alikuwa mwishoni mwa miaka yake ya utineja au mwanzoni mwa miaka yake ya 20, Yehova alipomtaja kwa njia nzuri pamoja na Noa na Ayubu, wanaume ambao walikuwa wamemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. (Mwa. 5:32; 6:9, 10; Ayu. 42:16, 17; Eze. 14:14.) Na Yehova aliendelea kumpenda Danieli katika maisha yake yote marefu yenye mambo ya kustaajabisha.—Dan. 10:11, 19. w23.08 33:1-2