Tufikiriane na Kutiana Moyo
“Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.”—EBR. 10:24.
1, 2. Ni nini kilichowasaidia Mashahidi wa Yehova 230 wavumilie matatizo waliyopata muda wa safari ya kifo mwishoni mwa Vita ya Pili ya Ulimwengu?
UTAWALA wa Nazi ulipokuwa karibu kuanguka mwishoni mwa Vita ya Pili ya Ulimwengu, amri ilitolewa ili kuangamiza maelfu ya wafungwa waliobaki katika kambi za mateso. Wafungwa wa kambi ya Sachsenhausen walipaswa kupelekwa kwenye bandari (mahali ambapo mashua zinasimama) ili wapakizwe ndani ya mashua na kutupwa katika bahari. Hiyo ilikuwa sehemu ya mupango ulioitwa baadaye safari ya kifo.
2 Wafungwa 33000 wa kambi ya mateso ya Sachsenhausen walipaswa kutembea kilometre 250 mupaka Lübeck, muji ulio na bandari wa Ujerumani. Kati ya wafungwa hao kulikuwa Mashahidi wa Yehova 230 kutoka inchi sita, ambao walilazimishwa kufanya safari hiyo wakiwa pamoja. Wote walikuwa wameregea kwa sababu ya njaa na magonjwa. Ni jambo gani lililowasaidia ndugu zetu wavumilie matatizo waliyopata muda wa safari hiyo ya kifo? Ndugu mumoja kati yao alisema hivi: “Tulitiana moyo ili kuendelea na safari.” “Nguvu zinazopita zile za kawaida,” ambazo Yehova aliwatolea na upendo walioonyeshana viliwasaidia kushinda jaribu hilo kali.—2 Kor. 4:7.
3. Sababu gani tunahitaji kutiana moyo?
3 Leo, hatufanye safari ya kifo kama hiyo, lakini tunapambana na matatizo mengi. Kisha Ufalme wa Mungu kuanza kutawala mbinguni katika 1914, Shetani alifukuzwa kutoka mbinguni na kutupwa kwenye ujirani wa dunia akiwa na “hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.” (Ufu. 12:7-9, 12) Kwa kuwa Har-magedoni inakaribia, Shetani anatumia majaribu na mikazo mbalimbali ili kutufanya tuwe zaifu kiroho. Zaidi ya hayo, anatumia pia mahangaiko ya maisha ya kila siku. (Ayu. 14:1; Mhu. 2:23) Wakati fulani magumu mengi ambayo tumepata yanaweza kutulemea sana hivi kwamba nguvu yoyote ya kiroho tuliyo nayo haitoshe ili itusaidie tupambane na kuvunjika moyo. Fikiria ndugu mumoja ambaye kwa miaka mingi amekuwa akiwasaidia watu wengi wawe na uhusiano muzuri na Yehova. Katika miaka ya uzee, yeye na bibi yake walikuwa na afya mbaya, na walianza kuvunjika moyo sana. Kama ndugu huyo, sisi wote tunahitaji “nguvu zinazopita zile za kawaida” kutoka kwa Yehova na vilevile vitia-moyo kutoka kwa ndugu wenzetu.
4. Ikiwa tunapenda kuwatia wengine moyo, ni shauri gani la mutume Paulo ambalo tunapaswa kufikiria sana?
4 Ikiwa tunapenda kuwatia wengine moyo, tunapaswa kufikiria sana shauri ambalo mutume Paulo alitolea Wakristo Waebrania. Alisema hivi: ‘Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri munavyoona siku ile kuwa inakaribia.’ (Ebr. 10:24, 25) Namna gani tunaweza kutumia shauri linalopatikana katika maneno hayo ya maana sana?
“TUFIKIRIANE”
5. “Kufikiriana” kunamaanisha nini, na hilo linaomba tufanye jitihada gani?
5 “Kufikiriana” kunamaanisha “kuhangaikia mahitaji ya wengine, kuyafikiria.” Je, tunaweza kabisa kufikiria mahitaji ya wengine ikiwa tu tunawasalimia haraka-haraka kwenye Jumba la Ufalme ao ikiwa tunazungumuza nao tu kuhusu mambo yasiyo ya maana? Hapana kabisa. Ni kweli kwamba tunapaswa kuwa waangalifu ili ‘tukazie mambo yetu wenyewe’ na ‘tusijiingize katika mambo ya watu wengine.’ (1 Thes. 4:11; 1 Tim. 5:13) Hata hivyo, ikiwa tunapenda kutia ndugu zetu moyo, tunahitaji kabisa kuwajua vizuri, ni kusema, kujua namna wanavyoishi, sifa zao, hali yao ya kiroho, uwezo wao, na uzaifu wao. Ni lazima watuone kama rafiki zao na wawe hakika kwamba tunawapenda. Hilo linaomba kupitisha wakati pamoja nao, si wakati tu wanapambana na magumu na kuvunjika moyo lakini pia nyakati zingine.—Rom. 12:13.
6. Ni nini kitakachosaidia muzee ‘afikirie’ wale walio chini ya uangalizi wake?
6 Wazee katika kutaniko wanashauriwa ‘kuchunga kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wao,’ kwa kupenda na kwa hamu. (1 Pet. 5:1-3) Namna gani wanaweza kuchunga kundi kwa njia inayofaa ikiwa hawajue vizuri kondoo zilizo chini ya uangalizi wao? (Soma Methali 27:23.) Ikiwa wazee wanajikaza kupatikana kwa urahisi na ikiwa wanafurahia kuwa pamoja na waamini wenzao, inaonekana kama ndugu na dada hawataogopa kuwafikia ili kuwaomba musaada wanapouhitaji. Hilo litawasaidia pia ndugu na dada waeleze mambo yote waliyo nayo moyoni mwao na mahangaiko yao yote ili wazee waweze ‘kufikiria’ wale walio chini ya uangalizi wao na kuwatolea musaada wanaohitaji.
7. Namna gani tunapaswa kuona ‘mazungumuzo ya ovyoovyo’ ya wale waliovunjika moyo?
7 Mutume Paulo alipoandikia kutaniko la Thesalonike, alisema hivi: ‘Mutegemeze walio zaifu.’ (Soma 1 Wathesalonike 5:14.) ‘Nafsi zenye kuhuzunika’ ni zaifu, katika maana fulani, na wenye kuvunjika moyo ni wazaifu pia. Methali 24:10 inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” ‘Mazungumuzo’ ya mutu mwenye kuvunjika moyo sana yanaweza kugeuka kuwa ‘ya ovyoovyo.’ (Ayu. 6:2, 3) ‘Tunapofikiria’ ndugu na dada hao, ni lazima tukumbuke kwamba pengine mambo wanayosema si yale yaliyo kabisa katika moyo wao. Rachelle, ambaye mama yake alivunjika moyo sana, alijionea jambo hilo. Rachelle anasema hivi: “Mara nyingi mama yangu alisema jambo fulani lenye kuumiza sana. Lakini kila mara, nilijikaza kufikiria namna alivyo kabisa, ni kusema, mwenye upendo, mupole, na mukarimu. Kwa hiyo, nikaelewa kwamba watu wenye kuvunjika moyo sana wanasema mambo mengi bila kufikiri. Jambo baya sana ambalo mutu anaweza kufanya ni kumujibu na kumutendea mutu mwenye kuvunjika moyo kulingana na maneno ao matendo yake.” Andiko la Methali 19:11 linasema hivi: ‘Ufahamu wa mutu hakika unapunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita [ao anaposamehe] kosa.’
8. Ni nani hasa tunayepaswa kuhakikishia upendo wetu, na sababu gani?
8 Namna gani tunaweza ‘kufikiria’ mutu ambaye amevunjika moyo kwa sababu ya haya na kukata tamaa kuhusiana na matokeo mabaya ya zambi aliyofanya zamani, hata ikiwa amekwisha kufanya hatua za kurekebisha mambo? Kuhusu mutenda-zambi mumoja aliyetubu katika Korintho, mutume Paulo alisema hivi: ‘Munapaswa kumusamehe kwa fazili na kumufariji, ili kwa njia fulani mutu huyo asimezwe na huzuni yake ya kupita kiasi. Kwa hiyo nawahimiza ninyi kumusibitishia [kumuhakikishia] upendo wenu.’ (2 Kor. 2:7, 8) Kulingana na kamusi moja, neno ‘kufikiria’ linamaanisha “kuhakikisha, kufanya makubaliano yawe nguvu kupitia sheria.” Hatuwezi tu kufikiri hivi: “Anajua kama ninamupenda na ninamuhangaikia.” Ni lazima mutu ajionee upendo huo kupitia matendo yetu.
‘TUCHOCHEANE KATIKA UPENDO NA MATENDO MAZURI’
9. Namna gani tunaweza ‘kuwachochea [wengine] katika upendo na matendo mazuri’?
9 Mutume Paulo aliandika hivi: “Acheni tufikiriane na kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” Tunapaswa kuwachochea ndugu na dada zetu waonyeshe upendo na kufanya matendo mazuri. Moto unapokuwa karibu kuzimika, tunahitaji kuchochea makaa ili moto uendelee kuwaka. (2 Tim. 1:6) Vivyo hivyo, tunaweza kuchochea ndugu zetu kwa upendo ili waendelee kuonyesha upendo wao kwa Mungu na jirani. Kuwapongeza wengine kwa njia inayofaa ni jambo la maana ili kuwachochea katika matendo mazuri.
Hubiri pamoja na wengine
10, 11. (a) Ni nani kati yetu anayehitaji pongezi? (b) Toa mufano unaoonyesha namna pongezi linaweza kusaidia mutu ambaye ‘amejikwaa.’
10 Sisi wote tuna lazima ya kupongezwa, iwe tumevunjika moyo ao hapana. Muzee mumoja wa kutaniko aliandika hivi: “Hakuna hata siku moja ambayo baba yangu aliniambia kwamba nilifanya jambo fulani vizuri. Kwa hiyo, nilikomaa na maoni ya kwamba sifae kitu. . . . Ijapokuwa nina miaka 50 sasa, ningali ninafurahi sana wakati rafiki zangu wananihakikishia kwamba ninatimiza vizuri daraka langu la uzee. . . . Mambo niliyojionea yamenifundisha kwamba ni jambo la maana sana kutia wengine moyo, na ninapenda kufanya hivyo.” Pongezi linaweza kuchochea kila mutu—mapainia, watu wenye kuzeeka, na wale ambao labda wamevunjika moyo.—Rom. 12:10.
11 Wakati ‘wale walio na sifa za kustahili kiroho wanajaribu kumurekebisha upya mutu aliyejikwaa,’ pongezi na mashauri yenye upendo yanaweza kusaidia mutenda-zambi aanze kufanya tena matendo mazuri. (Gal. 6:1) Dada anayeitwa Miriamu alijionea jambo hilo. Yeye anaandika hivi: “Nilipambana na kipindi kibaya katika maisha yangu wakati rafiki zangu fulani waliacha kutaniko na, wakati huo huo, baba yangu alipata ugonjwa wa damu kuvuya katika ubongo. Nilivunjika moyo sana. Ili kujaribu kusahau magumu yangu, nilifanya urafiki na kijana mumoja wa ulimwengu.” Hilo lilimufanya Dada Miriamu aone kwamba Yehova hangemupenda tena, kwa hiyo alifikiria kuacha kweli. Wakati muzee mumoja alimukumbusha utumishi aliomutolea Yehova kwa uaminifu hapo zamani, hilo lilimuchochea. Aliwatolea wazee nafasi ya kumuonyesha kwamba Yehova angali anamupenda. Kisha upendo wake kwa Yehova ukawa tena nguvu. Mwishowe alivunja urafiki wake na kijana huyo asiye Shahidi na aliendelea kumutumikia Yehova.
Chochea wengine katika upendo na matendo mazuri
12. Kumulinganisha mutu na mwengine isivyofaa, kumuchambua, ao kumufanya afikiri kwamba yeye hafanye jambo lolote kunaweza kuwa na matokeo gani?
12 Kumulinganisha mutu na mwengine isivyofaa, kumuchambua kwa musingi wa kanuni zilizo ngumu sana, ao kumufanya ajione kuwa mwenye hatia kwa sababu hakufanya mengi, kunaweza kumuchochea aongeze utumishi wake, lakini hilo halitadumu. Kwa upande mwengine, kumutolea ndugu ao dada yetu pongezi na kumutia moyo aendelee kuchochea upendo wake kwa Yehova, hilo linaweza kuwa na matokeo mazuri na yenye kudumu.—Soma Wafilipi 2:1-4.
‘TUTIANE MOYO’
13. Kuwatia wengine moyo kunatia ndani nini? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)
13 Tunahitaji ‘kutiana moyo zaidi kwa kadiri tunavyoona siku ile inakaribia.’ Kutia wengine moyo kunatia ndani kuwachochea wasonge mbele katika kazi ya Mungu. Kama vile kuchochea wengine kwenye upendo na matendo mazuri kunavyoweza kufananishwa na kuchochea ao kupuliza moto ambao ulikuwa karibu kuzimika, kuwatia wengine moyo kunaweza kufananishwa na kuongeza kuni kwenye moto ili uendelee kuwaka sana. Kutia wengine moyo kunamaanisha kuwatia nguvu na kuwafariji. Tunapopata nafasi ya kutia moyo mutu kama huyo, tunapaswa kuzungumuza naye kwa shauku na upole. (Met. 12:18) Tena, acheni tuwe ‘wepesi wa kusikia’ wala ‘si wepesi wa kusema.’ (Yak. 1:19) Tukisikiliza vizuri na kujitia pa nafasi ya Mukristo mwenzetu, tunaweza kutambua hali zinazomuvunja moyo na kusema maneno ambayo yatamusaidia apambane na hali hizo.
Pitisha wakati pamoja na marafiki wazuri
14. Namna gani ndugu mumoja mwenye kuvunjika moyo alisaidiwa?
14 Tuzungumuzie namna muzee mumoja mwenye huruma alivyoweza kusaidia ndugu ambaye alikuwa hahubiri tena muda wa miaka mingi. Kadiri muzee alivyoendelea kumusikiliza, alitambua kwamba ndugu huyo alikuwa angali anamupenda Yehova sana. Alijifunza kila habari ya Munara wa Mulinzi na alijikaza kuhuzuria mikutano yote kwa ukawaida. Lakini, matendo ya ndugu fulani katika kutaniko yalimuvunja moyo na kumufanya akasirike. Muzee huyo alimusikiliza na kujitia pa nafasi yake bila kumulaumu, na alimuhangaikia sana kwa upendo, yeye na familia yake. Polepole, ndugu huyo akaanza kutambua kwamba alikuwa ameacha mambo mabaya aliyokutana nayo zamani maishani yamuzuie kumutumikia Mungu wake aliyemupenda. Muzee alimuomba ndugu huyo aende naye katika mahubiri. Kwa musaada wa muzee huyo, ndugu huyo alirudilia tena kazi ya kuhubiri na mwishowe alikuwa tena muzee wa kutaniko.
Sikiliza kwa uvumilivu mutu anayehitaji kitia-moyo (Ona fungu la 14, na 15)
15. Yehova anatuachia mufano gani kuhusu namna ya kuwatia moyo wale waliovunjika moyo?
15 Pengine mutu anayevunjika moyo hatajisikia mara moja vizuri ao kukubali mara moja musaada tunaomutolea. Pengine itatuomba tuendelee kumusaidia. Mutume Paulo alisema hivi: “Muwasaidie wazaifu, muwe na uvumilivu kwa watu wote.” (1 Thes. 5:14, La Sainte Bible en swahili de la R.D. Congo) Kuliko kuvunjika moyo haraka, acheni tuendelee ‘kuwasaidia,’ na kuendelea kuwavumilia. Wakati uliopita, Yehova aliwatendea kwa uvumilivu watumishi wake ambao mara kwa mara walivunjika moyo. Kwa mufano, Mungu alimutendea Eliya kwa wema, na kusikiliza maoni yake. Yehova alimutolea nabii huyo yale aliyohitaji ili kuendelea na kazi yake. (1 Fal. 19:1-18) Kwa kuwa Daudi alitubu kabisa, Yehova alimusamehe. (Zab. 51:7, 17) Mungu alimusaidia tena mwandikaji wa Zaburi ya 73, ambaye alikuwa karibu kuacha kazi ya Mungu. (Zab. 73:13, 16, 17) Yehova anatutendea kwa wema, zaidi sana tunapolemewa na kuvunjika moyo. (Kut. 34:6) Rehema zake “ni nyipya kila asubuhi,” na “hazitakoma.” (Omb. 3:22, 23) Yehova anataka tufuate mufano wake na tutendee wale waliovunjika moyo kwa upole.
TUTIANE MOYO ILI KUBAKI KATIKA BARABARA INAYOONGOZA KWENYE UZIMA
16, 17. Kwa kuwa mwisho wa ulimwengu huu unakaribia, tunapaswa kuazimia kufanya nini, na sababu gani?
16 Kati ya wale wafungwa 33000 waliotoka katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen, maelfu walikufa. Lakini, Mashahidi wa Yehova wote 230 waliokuwa kati ya wafungwa hao walipona. Kwa kuwa walitiana moyo na kutegemezana, safari hiyo ya kifo iligeuka kuwa safari ya uzima.
17 Leo pia, tunapatikana katika “barabara inayoongoza kwenye uzima.” (Mt. 7:14) Karibuni, waabudu wote wa Yehova wataingia kwa umoja katika ulimwengu mupya wa haki. (2 Pet. 3:13) Acheni basi tuazimie kusaidiana katika barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.