Sababu Gani Tunapaswa Kukusanyika Pamoja ili Kuabudu?
“Wakaendelea kujitoa wenyewe . . . na kushirikiana [kuwa pamoja].”—MATENDO 2:42.
NYIMBO: 20, 119
1-3. (a) Namna gani Wakristo wameonyesha kama wanafurahia kukusanyika pamoja? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?
WAKATI Corinna alikuwa na miaka 17, mama yake alikamatwa na akatumwa kwenye kambi ya kazi za kulazimishwa. Kisha, Corinna naye alipelekwa Siberia, mbali sana na kwao. Huko alitumika katika shamba la kuchungia wanyama na alitendewa kama vile mutumwa. Wakati fulani alilazimishwa kutumika inje katika baridi kali bila kuwa na nguo za kumusaidia ajilinde na baridi. Hata hivyo, Corinna na dada mwengine waliamua kama watafanya yao yote ili kutoka katika shamba hilo na kuenda kwenye mikutano ya kutaniko.
2 Corinna alisema hivi: “Tulitoka nafasi yetu ya kazi mangaribi na tulitembea kilometre 25 ili kufika nafasi kwenye treni zinasimama. Treni iliondoka saa mbili asubui, na tulisafiri saa sita mbele ya kushuka katika treni na tulitembea kwa miguu kilometre 10 ili kufika nafasi ya mikutano.” Corinna alifurahi sana kwa kufanya safari hiyo. Alisema hivi: “Kwenye mikutano, tulijifunza Munara wa Mulinzi na tuliimba nyimbo za Ufalme. Tulijengwa sana kiroho na imani yetu ilitiwa nguvu.” Dada hao wawili walirudia katika shamba kisha siku tatu, lakini mukubwa wa shamba hilo hakujua hata kama walikuwa wameenda mahali fulani.
3 Sikuzote, watu wa Yehova wanangojea kwa hamu kukusanyika pamoja na wengine. Kwa mufano, Wakristo wa kwanza walifurahia kukusanyika pamoja ili kuabudu Yehova na kujifunza juu yake. (Matendo 2:42) Kwa kweli, wewe pia unangojea kwa hamu kuwa kwenye mikutano. Lakini, kama vile ndugu na dada zako wote, unaweza kuwa na magumu ya kuwa kwenye mikutano kwa ukawaida. Pengine unalazimika kutumika saa nyingi ao uko na mambo mengi ya kufanya ao sikuzote unajisikia mwenye kuchoka. Ni nini inaweza kutusaidia tufanye nguvu yetu yote ili tukuwe kwenye mikutano?[1] (Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.) Namna gani tunaweza kutia moyo wanafunzi wetu wa Biblia na wengine ili wakuwe kwenye mikutano yetu kwa ukawaida? Habari hii itaeleza sababu gani kuwa kwenye mikutano (1) kunatuletea faida, (2) kunasaidia wengine, na (3) kunafurahisha Yehova.[2]—Soma maelezo kwenye mwisho wa habari hii.
MIKUTANO INATULETEA FAIDA
4. Namna gani kukusanyika pamoja kunatusaidia tujifunze juu ya Yehova?
4 Mikutano inatufundisha. Kila mukutano unatusaidia kujifunza mambo mengi juu ya Yehova. Kwa mufano, hivi karibuni katika makutaniko mengi ndugu na dada wamejifunza kitabu Mkaribieni Yehova kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko.Ulijisikia namna gani wakati tulizungumuzia sifa za Yehova na wakati ulisikia ndugu na dada zako wanatoa maelezo juu yake? Kwa kweli, jambo hilo lilikuchochea umupende Yehova hata zaidi. Kwenye mikutano, tunajifunza pia mambo mengi juu ya Biblia kwa kusikiliza kwa uangalifu hotuba mbalimbali, usomaji wa Biblia, na kufuata maonyesho. (Nehemia 8:8) Na unaweza kufikiria mambo mengi yenye tunavumbua kila juma wakati tunatayarisha usomaji wa Biblia na kisha kusikiliza mambo yenye wengine walijifunza katika usomaji huo.
5. Namna gani mikutano imekusaidia kutumikisha mambo yenye umejifunza katika Biblia na kukomalisha ufundi wako wa kuhubiri?
5 Mikutano inatufundisha namna ya kutumikisha katika maisha yetu mambo yenye tunajifunza katika Biblia. (1Wathesalonike 4:9, 10) Kwa mufano, umekwisha kuhuzuria Funzo fulani la Munara wa Mulinzi lenye lilikuchochea ufanye mengi katika kazi ya Yehova, kufanya sala zako zikuwe muzuri zaidi, ao kusamehe ndugu ao dada fulani? Mikutano yenye tunafanya katikati ya juma inatufundisha namna ya kuhubiri habari njema na namna ya kusaidia wengine waelewe mafundisho ya Biblia.—Mathayo 28:19, 20.
6. Namna gani mikutano yetu inatutia moyo na kutusaidia tuendelee kuwa na nguvu?
6 Mikutano inatutia moyo. Ulimwengu wa Shetani unajikaza kuregeza imani yetu, na unaweza kutuletea mahangaiko, na kutuvunja moyo. Lakini mikutano yetu inatutia moyo na kutupatia nguvu ya kuendelea kutumikia Yehova. (Soma Matendo 15:30-32.) Kwenye mikutano, mara nyingi tunazungumuzia namna unabii mbalimbali wa Biblia umetimia. Jambo hilo linaweza kutusaidia tukuwe hakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi zake juu ya wakati unaokuja. Wakristo wenzetu wanatutia moyo wakati wanatoa hotuba na pia wakati wanatoa maelezo na wakati wanamusifu Yehova kwa kumuimbia kwa moyo wote. (1 Wakorintho 14:26) Na wakati tunazungumuza nao mbele na kisha mikutano, tunajisikia tumetiwa nguvu kwa sababu tunaona kuwa tuko na marafiki wengi wenye kutuhangaikia kabisa.—1 Wakorintho 16:17, 18.
Mikutano yetu inatutia moyo na kutupatia nguvu ya kuendelea kutumikia Yehova
7. Sababu gani ni jambo la maana sana tukuwe kwenye mikutano yetu?
7 Kwenye mikutano, tunapata musaada wa roho takatifu ya Mungu. Yesu anatumia roho hiyo takatifu ili kuongoza makutaniko. Ndiyo sababu anatuambia kwamba tunapaswa ‘kusikia yale ambayo roho inaambia makutaniko.’ (Ufunuo 2:7) Roho takatifu inaweza kutusaidia tuhubiri kwa bidii na tusishindwe na majaribu. Inaweza kutusaidia pia tuchukue maamuzi ya muzuri. Ndiyo sababu tunapaswa kujikaza sana kuwa kwenye mikutano yetu ili kupata musaada wa roho ya Mungu.
KWENYE MIKUTANO TUNASAIDIA WENGINE
8. Wakati ndugu na dada zetu wanatuona kwenye mikutano, wanatusikia tunatoa maelezo na kuimba, hilo linawasaidia namna gani? (Soma pia kisanduku “Kila Mara Anajisikia Muzuri Kisha Mikutano.”)
8 Kwenye mikutano, tunapata nafasi ya kuonyesha ndugu na dada kwamba tunawapenda. Katika kutaniko letu ndugu na dada wengi wanapambana na magumu makali. Mutume Paulo alisema hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana.” (Waebrania 10:24, 25) Tunaweza kuonyesha kwamba tunahangaikia ndugu na dada zetu wakati tunakusanyika pamoja na kutiana moyo. Wakati tunakuwa kwenye mikutano, tunaonyesha ndugu na dada kama tunapenda kuwa pamoja nao na kuzungumuza nao na kama tunahangaikia namna wanajisikia. Tunawatia moyo pia wakati wanasikia maelezo yetu na namna tunaimba kwa moyo wote.—Wakolosai 3:16.
9, 10. (a) Eleza namna gani maneno ya Yesu katika Yohana 10:16 yanatusaidia kuelewa sababu gani ni jambo la maana kukusanyika pamoja na ndugu na dada zetu. (b) Wakati tunafika kwenye mikutano kwa ukawaida, namna gani hilo linaweza kusaidia mutu fulani mwenye amekataliwa na familia yake?
9 Wakati tunakuwa kwenye mikutano, tunasaidia kutaniko likuwe na umoja. (Soma Yohana 10:16.) Yesu alijilinganisha na muchungaji na alilinganisha pia wafuasi wake na kondoo. Fikiria hali hii: Kondoo wawili wako kwenye mulima, wengine wawili wako katika bonde, na kondoo moja iko nafasi ingine. Tunaweza kusema kwamba kondoo hao tano ni kundi? Hapana, kwa sababu kondoo wenye kuwa katika kundi wanabakia pamoja na kufuata muchungaji wao. Vilevile, hatupaswe kubakia mbali na ndugu na dada zetu kwa kuacha kuwa kwenye mikutano yetu. Tunapaswa kukusanyika pamoja ili tukuwe “kundi moja” na kumufuata ‘muchungaji mumoja.’
10 Mikutano yetu inatusaidia tuishi katika umoja kama watu wa familia wenye kupendana. (Zaburi 133:1) Watu fulani katika kutaniko wameachiliwa na watu wa familia yao kama vile, wazazi wao, ndugu na dada zao. Lakini Yesu alisema kama watapata familia yenye itawapenda na kuwahangaikia. (Marko 10:29, 30) Ikiwa unafika kwenye mikutano kwa ukawaida, unaweza kuwa kama baba, mama, ndugu ao dada ya mutu fulani katika kutaniko. Wakati tunafikiria jambo hilo, tutafanya nguvu yetu yote ili tukuwe kwenye mikutano yote.
TUTAFURAHISHA YEHOVA
11. Namna gani kufika kwenye mikutano kunatusaidia tumutolee Yehova mambo yenye anastahili?
11 Kwenye mikutano, tunamutolea Yehova mambo yenye anastahili. Kwa sababu yeye ni Muumbaji wetu, tunapaswa kumushukuru, kumuheshimu, na kumusifu. (Soma Ufunuo 7:12.) Tunaweza kufanya hivyo kwenye mikutano wakati tunasali, tunaimba, na kutoa maelezo juu yake. Hiyo ni nafasi nzuri sana yenye tuko nayo kila juma ya kumuabudu Yehova!
Yehova anaona kama tunapenda kabisa kuwa kwenye mikutano na anafurahia bidii yenye tunafanya ili kuwa kwenye mikutano hiyo.
12. Yehova anajisikia namna gani wakati tunatii amri yake ya kuwa kwenye mikutano?
12 Kwa sababu Yehova ndiye alituumba, tunapaswa kumutii. Ametupatia amri ya kuendelea kukusanyika, zaidi sana kwa sababu mwisho unakaribia. Yehova anafurahi wakati tunatii amri hiyo. (1 Yohana 3:22) Anaona kama tunapenda kabisa kuwa kwenye mikutano na anafurahia bidii yenye tunafanya ili kuwa kwenye mikutano hiyo.—Waebrania 6:10.
13, 14. Namna gani tunamukaribia Yehova na Yesu kwenye mikutano?
13 Wakati tunaenda kwenye mikutano, tunamuonyesha Yehova kwamba tunapenda kumukaribia zaidi yeye na Mwana wake. Kwenye mikutano, tunajifunza Biblia na Yehova anatufundisha mambo yenye tunapaswa kufanya na namna tunapaswa kuishi. (Isaya 30:20, 21) Hata wakati watu fulani wenye hawamutumikie Yehova wanafika kwenye mikutano yetu, wanatambua kwamba Mungu anaendelea kutuongoza. (1 Wakorintho 14:23-25) Yehova anaongoza mikutano yetu kupitia roho yake takatifu, na mambo yenye tunajifunza kwenye mikutano hiyo yanatoka kwake. Kwa hiyo, wakati tuko kwenye mikutano, tunasikiliza mambo yenye Yehova anasema, tunaona namna anatupenda sana, na tunamukaribia zaidi.
14 Yesu, Kichwa cha kutaniko, alisema hivi: ‘Palipo na wawili ao watatu wakiwa wamekusanyika pamoja katika jina langu, hapo mimi nipo katikati yao.’ (Mathayo 18:20) Biblia inasema pia kama Yesu ‘anatembea katikati’ ya makutaniko. (Ufunuo 1:20–2:1) Kwa kweli, Yehova na Yesu wako pamoja na sisi na wanaendelea kututia nguvu kwenye mikutano yetu. Unawaza Yehova anajisikia namna gani wakati anaona unafanya nguvu yako yote ili kumukaribia yeye na Mwana wake?
15. Wakati tunaenda kwenye mikutano, namna gani tunaonyesha kama tunapenda kumutii Mungu?
15 Wakati tunaenda kwenye mikutano, tunaonyesha Yehova kama tunapenda kumutii. Yehova hatulazimishe tufanye vile anasema. (Isaya 43:23) Kwa hiyo, wakati tunachagua kutii amri yake ya kuwa kwenye mikutano, tunamuonyesha kama tunamupenda na kama tunaamini kuwa ana haki ya kutuambia mambo yenye tunapaswa kufanya. (Waroma 6:17) Kwa mufano, tutafanya nini ikiwa mukubwa wa kazi anatuomba kutumika saa nyingi na tunashindwa kuwa kwenye mikutano yetu kwa ukawaida? Ao pengine serikali inaweza kusema kama ikiwa watu wanakusanyika ili kumuabudu Yehova watalipa kiasi fulani cha feza, watafungwa katika gereza, ao watapewa malipizi makali sana. Ao wakati mwingine tunaweza kupenda kufanya kazi fulani kuliko kuenda kwenye mikutano. Katika hali hizo zote, tunapaswa kuamua jambo la kufanya. (Matendo 5:29) Lakini kila wakati tunaamua kumutii Yehova, tunamufurahisha.—Methali 27:11.
UENDELEE KUKUSANYIKA PAMOJA NA NDUGU NA DADA ZAKO
16, 17. (a) Ni nini inaonyesha kama Wakristo wa kwanza waliona mikutano kuwa ya maana sana? (b) Ndugu George Gangas alijisikia namna gani juu ya mikutano ya Kikristo?
16 Kisha kukusanyika pamoja kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33, Wakristo waliendelea kukusanyika pamoja ili kumuabudu Yehova. Biblia inasema kama ‘waliendelea kujitoa wenyewe kwa fundisho la mitume na kushirikiana.’ (Matendo 2:42) Na hata wakati waliteswa na guvernema ya Roma na viongozi wa dini ya Wayahudi, hawakuacha kukusanyika pamoja. Walifanya nguvu yao yote ili waendelee kukusanyika pamoja hata kama ilikuwa vigumu kufanya hivyo.
17 Leo pia, watumishi wa Yehova ni wenye shukrani sana kwa ajili ya mikutano na wanafurahia kuwa kwenye mikutano hiyo. Ndugu George Gangas alikuwa kati ya ndugu wa Baraza Lenye Kuongoza kwa zaidi ya miaka 22. Alisema hivi: “Jambo lenye linaniletea furaha kubwa zaidi katika maisha yangu na kunitia moyo ni kukusanyika pamoja na ndugu na dada. Ikiwezekana, ninapenda kuwa kati ya watu wa kwanza kufika kwenye Jumba la Ufalme, na kati ya watu wa mwisho kuondoka. Ninasikia furaha katika moyo wangu wakati ninazungumuza na watu wa Mungu. Wakati niko pamoja nao ninajisikia kuwa katika familia yangu, ni kusema, katika paradiso ya kiroho.” Aliongeza hivi: “Mawazo yangu ya ndani sana na tamaa yangu ni kuwa kwenye mikutano.”
18. Unajisikia namna gani juu ya mikutano yetu, na umeamua kufanya nini?
18 Wewe pia unajisikia vile juu ya ibada ya Yehova? Ikiwa unajisikia vile, uendelee kufanya nguvu yako yote ili ukuwe pamoja na ndugu na dada zako kwenye mikutano, hata wakati ni vigumu kufanya vile. Umuonyeshe Yehova kwamba unajisikia kabisa kama Mufalme Daudi. Alisema hivi: “Yehova, nimependa makao ya nyumba yako.”—Zaburi 26:8.
^ [1] (fungu la 3) Ndugu na dada fulani hawawezi kuenda kwenye mikutano kwa ukawaida kwa sababu ya hali zenye hawawezi kuzuia. Kwa mufano, wanaweza kuwa wagonjwa sana. Lakini, wanaweza kuwa hakika kwamba Yehova anaelewa hali yao na anapendezwa sana na yote yenye wanajikaza kufanya ili kumuabudu. Wazee wa kutaniko wanaweza kusaidia ndugu na dada hao wafuate mikutano, pengine kupitia telefone ao kwa kurekodi mikutano kwa ajili yao.
^ [2] (fungu la 3) Soma kisanduku “Sababu Gani Tunapaswa Kuwa Kwenye Mikutano?”