Vijana—Jengeni Msingi Bora kwa Ajili ya Wakati Ujao
1 Ni jambo gani linalochukua nafasi ya kwanza kabisa akilini mwako? Unafikiria nini? Je, mahangaiko yako ya msingi yanategemea mambo ya sasa, au yanahusu wakati ujao na kutegemea yale ambayo Mungu ameahidi? (Mt. 6:24, 31-33; Luka 8:14) Imani yenye nguvu inahitajiwa ili kutenda kulingana na ahadi za Mungu, kama inavyoweza kuonekana kutokana na mifano ya Abrahamu na Musa. (Ebr. 11:8-10, 24-26) Unawezaje kusitawisha imani kama hiyo na kujenga “msingi bora kwa ajili ya wakati ujao”?—1 Tim. 6:19.
2 Tafuta Yehova: Ikiwa una kawaida ya utendaji wa kiroho pamoja na familia yako, hilo ni jambo la kusifiwa. Lakini usidhani kwamba kawaida hiyo itatokeza yenyewe imani yenye nguvu. Ili kupata “maarifa kwa Mungu,” unapaswa wewe binafsi kutafuta Yehova. (Mit. 2:3-5; 1 Nya. 28:9) Kijana Mfalme Yosia alifanya hivyo. Ingawa alikomalia katika mazingira ya kiroho yasiyofaa, “alianza kutafuta Mungu wa Daudi baba yake” alipokuwa na umri wa miaka 15.—2 Nya. 34:3.
3 Unawezaje kutafuta Yehova? Kwa kuchunguza kwa uangalifu mambo unayoamini na ‘kujithibitishia mwenyewe’ kwamba ni kweli kabisa. (Rom. 12:2) Kwa mfano, je, unaweza kueleza yale ambayo Biblia inasema kuhusu damu na kutoa uhakikisho kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mbinguni katika mwaka wa 1914? Kujipatia “ujuzi sahihi wa kweli” ni sehemu ya maana ya kujenga msingi bora kwa ajili ya wakati ujao.—1 Tim. 2:3, 4.
4 Yosia alipata matokeo mazuri kwa kutafuta Mungu. Kabla afikie umri wa miaka 20, alitenda kwa ujasiri ili kuondoa ibada isiyo ya kweli katika inchi. (2 Nya. 34:3-7) Vivyo hivyo, maendeleo yako ya kiroho yatakuwa wazi kupitia matendo yako. (1 Tim. 4:15) Ikiwa wewe ni mhubiri asiyebatizwa, jitahidi kuboresha huduma yako. Usitosheke tu na kutolea watu vichapo. Jiwekee mradi wa kutumia Biblia, kutafakari na watu, na kukomaza kupendezwa ulikopata. (Rom. 12:7) Hilo litakusaidia ukomae kiroho.
5 Mpeni Yehova Yaliyo Bora Zaidi: Unapoonyesha kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova kwa kubatizwa, unakuwa mhudumu wa Mungu aliyewekwa rasmi. (2 Kor. 3:5, 6) Hilo linakutolea nafasi za kutumikia Yehova wakati wote. Nafasi hizo zinatia ndani upainia na pia utumishi wa Betheli, wa mishonari, na wa kimataifa. Njia nyingine za kupanua huduma yako ni kwa kujifunza lugha nyingine au kwa kuhama ili kutumikia mahali ambapo uhitaji ni mkubwa zaidi.
6 Bila shaka, si wote wanaoweza kushiriki mapendeleo hayo ya utumishi, lakini kila mmoja wetu anaweza kumpatia Yehova kilicho bora alicho nacho. (Mt. 22:37) Hata hali zako ziwe nini, fanya utumishi wa Yehova kuwa jambo la maana zaidi maishani mwako. (Zab. 16:5) Kwa kufanya hivyo, utakuwa ukijenga msingi bora kwa ajili ya wakati ujao.
[Study Questions]
1. Kwa nini vijana Wakristo wanahitaji kusitawisha imani yenye nguvu?
2. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Mfalme Yosia?
3. Vijana Wakristo leo wanawezaje kutafuta Yehova?
4. Wahubiri wasiobatizwa wanawezaje kufanya maendeleo yao yawe wazi?
5. Wakristo waliobatizwa wana nafasi gani za kupanua huduma yao?
6. Sote tunawezaje kujenga msingi bora kwa ajili ya wakati ujao?