Iweni Timamu Katika Akili kwa Kuwa Mwisho Unakaribia
1 Neno la Mungu linafafanua tena na tena siku ya Yehova kuwa inakuja ‘sawasawa na mwizi’—maana yake, kwa ghafula, kwa siri. (1 Thes. 5:2; Mt. 24:43; 2 Pet. 3:10; Ufu. 3:3; 16:15) “Kwa sababu hiyo,” Yesu alisema, “jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mt. 24:44) Kwa kuwa mwisho unakaribia, tunawezaje kuendelea kuwa macho kiroho? Ufunguo unapatikana katika shauri hili lililotolewa kwa uongozi wa roho ya Mungu: “Iweni timamu katika akili.”—1 Pet. 4:7.
2 Utimamu wa akili unaomba kuona mambo jinsi Yehova anavyoyaona. (Efe. 5:17) Unatusaidia kujiona kuwa “wakaaji wa kigeni na wakazi wa muda” katika mfumo mbovu wa mambo wa sasa. (1 Pet. 2:11) Unatuwezesha kutambua mambo yaliyo ya maana kwelikweli, kujiwekea mambo ya kutanguliza, na kufanya maamuzi mazuri.—Flp. 1:10.
3 Jiwekeeni Miradi ya Kiroho: Kujiwekea na kufikia miradi ya kiroho kunatusaidia kuwa timamu katika akili. Je, unayo miradi ya kiroho unayofuatia sasa? Je, unajitahidi kusoma Biblia kila siku, kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo, kusoma kila toleo ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, au labda kuongeza ushiriki wako katika huduma? Ikiwa unajiwekea miradi inayofaa kwako, ikiwa unadumu katika kuifuatia, na ikiwa unaomba Yehova abariki jitihada zako, huenda matokeo yakakushangaza.
4 Mzee mmoja aliuliza mume na mke vijana wenye kuoana kuhusu miradi yao ya kiroho. Ulizo lake liliwafanya watambue kwamba ikiwa wangefanya maisha yao kuwa mepesi na kuondoa deni zilizowalemea, wangeweza kupainia. Wakaamua kufanya hilo kuwa mradi wao. Wakalipa kwa bidii deni na kupata njia za kuondoa utendaji usio wa lazima uliowagharimu wakati na nguvu. Mwaka mmoja tu baadaye, walikuwa wamefikia mradi wao. Matokeo yakawa nini? Mume anasema: “Bila miradi hatungekuwa mahali tulipo sasa. Sisi ni wenye furaha zaidi. Maisha yetu ni bora na yenye utulivu zaidi. Yana maana na kusudi la kweli.”
5 Kwa kuwa tunangojea siku ya Yehova, na tudumishe hali yetu ya kuwa macho kiroho kwa kuishi kwa utimamu wa akili, tukiendelea kukaza fikira juu ya kufanya mapenzi ya Mungu.—Tito 2:11-13.