HABARI YA KUJIFUNZA YA 51
WIMBO 132 Sasa Tunakuwa Mwili Mumoja
Siku Yenu ya Ndoa Imuletee Yehova Utukufu
“Mambo yote yatendeke kwa adabu na kwa utaratibu.”—1 KO. 14:40.
WAZO KUBWA
Namna Bakristo benye biko napanga kuoana banaweza kumuletea Yehova utukufu siku ya ndoa yabo.
1-2. Yehova anapenda nini juu ya siku yenu ya ndoa?
MUKO napanga kufunga ndoa? Kama ni vile pongezi! Inawezekana muko nafanya mambo mbalimbali juu ya kutayarisha siku yenu ya ndoa. Yehova anapenda mufurahie siku yenu ya ndoaa na mufurahie maisha yenu pamoya mu siku zenye ziko nakuya.—Mez. 5:18; Wim. 3:11.
2 Ni jambo ya maana ndoa yenu imuletee Yehova utukufu. Juu ya nini tunasema vile na namna gani munaweza kufanya vile? Hii habari inahusu zaidi sana benye biko napanga kufunga ndoa, lakini kanuni zenye ziko humu zitatusaidia siye bote tumuletee Yehova utukufu ikiwa banatualika ku ndoa ao ikiwa banatulomba tusaidie ku matayarisho fulani.
JUU YA NINI NDOA YENU INAPASWA KULETEA YEHOVA UTUKUFU?
3. Wakati Bakristo benye kuchumbiana biko natayarisha ndoa banapaswa kufikiria nini, na juu ya nini?
3 Bakristo benye kuchumbiana benye biko natayarisha ndoa banapaswa kufikiria kanuni za Biblia. Juu ya nini? Ni juu Yehova njo mwenye alianzisha ndoa. Ndoa ya kwanza yenye alianzisha ni ya Adamu na Eva. (Mwa. 1:28; 2:24) Njo maana benye biko natayarisha ndoa banapaswa kufikiria mawazo ya Yehova.
4. Juu ya nini Bakristo benye kuchumbiana banapaswa kumuletea Yehova utukufu siku ya ndoa yabo?
4 Sababu ingine yenye inapaswa kubachochea mufikirie mawazo ya Yehova siku ya ndoa yenu ni hii: Yehova ni Baba yenu wa mbinguni na ni Rafiki yenu wa sana. (Ebr. 12:9) Juu munapenda kuendelea kuwa na uhusiano muzuri pamoya naye, hamutapenda siku ya ndoa yenu ao siku ingine kutokee kitu yoyote yenye inaweza kuhuzunisha Rafiki yenu wa mbinguni. (Zb. 25:14) Wakati munafikiria mambo yote yenye Yehova alishabafanyia na yenye atabafanyia, bila shaka mutafanya yenu yote juu siku yenu ya ndoa imuletee utukufu.—Zb. 116:12.
MUNAWEZA KUFANYA NINI JUU YA KUMULETEA YEHOVA UTUKUFU?
5. Namna gani Biblia inaweza kusaidia benye biko natayarisha ndoa?
5 Mu Biblia hamuna liste ya sheria zenye Bakristo banapaswa kufuata siku ya ndoa yabo. Kwa hiyo benye bataoana banaweza kufanya ndoa yabo kulingana na hali yabo, desturi ya kwabo, ao kulingana na byenye banapendaka. Bakristo ba kweli banapaswa pia kuheshimia sheria za serikali kuhusu ndoa. (Mt. 22:21) Hata Bakristo baamue kufanya nini siku ya ndoa yabo, kama banafuata kanuni za Biblia batamuletea Yehova utukufu na batamufurahisha. Sasa, munapaswa kufikiria kanuni gani mbalimbali?
6. Juu ya nini ni jambo ya maana benye bataoana bafuate sheria za serikali juu ya ndoa?
6 Mufuate sheria za serikali. (Ro. 13:1, 2) Mu inchi za mingi, benye bataoana banapaswa kufuata sheria fulani za serikali mbele ya kufunga ndoa. Benye bataoana banapaswa kujikaza kujua zile sheria. Kama munapenda kujua habari zaidi juu ya mambo yenye serikali inaomba, munaweza kuomba bazee babasaidie.b
7. Hali inapaswa kuwa namna gani siku yenu ya ndoa?
7 Mufanye hali ikuwe yenye kuheshimika. (1 Ko. 10:31, 32) Juu hali ikuwe muzuri siku yenu ya ndoa mujikaze kuonyesha tunda ya roho ya Mungu, hapana roho ya ulimwengu. (Gal. 5:19-26) Biblia inaonyesha kama bwana njo kichwa. Njo maana yeye njo anapaswa kuhakikisha kama siku ya ndoa itakuwa yenye furaha na itapita mu njia yenye kuheshimika. Nini njo itafanya siku ya ndoa ikuwe vile? Hotuba ya ndoa yenye kutegemea Biblia yenye inatolewa kwa upendo, kwa uchangamufu, na kwa heshima, inasaidia batu baone ndoa kuwa zawadi kutoka kwa Yehova. Bote benye balikuya kusikiliza ile hotuba bataona buzito ya ndoa. Bakristo ba mingi benye biko napanga kuoana banapendaka hotuba yabo ya ndoa ikuwe ku Jumba ya Ufalme kama inawezekana. Kama munapenda hotuba yenu itolewe ku Jumba ya Ufalme, munapaswa kuandikia baraza ya bazee mbele ya wakati.
8. Munaweza kufanya nini juu fete yenu ya ndoa imuletee Yehova utukufu? (Waroma 13:13)
8 Soma Waroma 13:13. Kama munaamua kufanya fete ya ndoa, munaweza kufanya nini juu ya kuepuka roho ya ulimwengu? Neno ya kigiriki yenye kutafsiriwa “karamu za kupitisha mipaka” inazungumuzia fete zenye batu banakunywa pombe kupita kiasi na zenye batu banatia miziki mupaka busiku sana. Kama unaamua kupatia batu pombe ku fete yako, uhakikishe kama hakuna mwenye atakunywa sana.c Kama utatia miziki, uitie mu sauti ya chini juu benye ulialika baweze kuzungumuza. Uchunguze muzuri ile miziki na maneno ya ile miziki juu kusikuwe wa kukwazika.
9. Benye bataoana banapaswa kukumbuka nini kama kuko benye batasema maneno fulani juu yabo ao kama kutakuwa mambo ingine ya kujifurahisha mu fete yabo?
9 Mu maeneo fulani barafiki na batu ya familia banasimamaka na kusema mambo fulani juu ya benye biko naoana. Pia, ku mafete fulani banaonyeshaka mapicha na mavideo ya benye biko naoana ao banafanyaka mambo ingine ya kujifurahisha. Ile mambo yote inaweza kuongeza butamu ya fete. Lakini uhakikishe kama mambo yote yenye itafanywa itakuwa ya kujenga. (Flp. 4:8) Ujiulize hivi: ‘Italetea bengine heshima? Itaheshimisha mupango wa ndoa?’ Na ya maana sana, ujiulize: ‘Itamuletea Yehova utukufu?’ Hata kama haiko mubaya kufanya mizaha, inaomba kuepuka mizaha ya mubaya, kwa mufano yenye inaweza kufanya batu bawaze juu ya ngono. (Efe. 5:3) Uhakikishe kama batu ya familia na benye batasema maneno fulani banaelewa mambo yenye banaweza kusema na yenye habapaswe kusema.
10. Juu ya nini benye bataoana banapaswa kuwa na kiasi wakati biko natayarisha ndoa yabo? (1 Yohana 2:15-17)
10 Mukuwe na kiasi. (Soma 1 Yohana 2:15-17.) Yehova anafurahi wakati batumishi yake banatafuta kumuletea yeye utukufu kuliko kujionyesha. Kwa hiyo Bakristo benye biko na kiasi banapaswa kuepuka kutumia makuta ya mingi sana na ‘kujionyesha mali yabo.’ Mutapata faida gani kama munafanya ndoa ya kiasi? Pengine ndoa yenu itakuwa sawa vile ya ndugu moya wa Norvege mwenye kuitwa Mike. Anasema hivi: “Hatukuingia mu madeni na tuliendelea na kazi ya upainia. Ndoa yetu ilikuwa ya kiasi lakini ya kupendeza na yenye tutaendelea kukumbuka.” Dada moya wa India mwenye kuitwa Tabitha anasema hivi: “Tuliepuka mahangaiko ya mingi juu ndoa yetu ilikuwa ya kiasi. Tulikuwa na mambo kidogo ya kutayarisha na hakukuwa mambo ya mingi ya kukosa kukubaliana.”
Hata tuishi wapi, ndoa ya Kikristo inaweza kuwa yenye kiasi, yenye kupendeza, na yenye tutaendelea kukumbuka kwa furaha (Ona fungu ya 10-11)
11. Namna gani benye bataoana banaweza kuonyesha kiasi wakati biko natafuta bya kuvala na kujipamba? (Ona pia picha.)
11 Ulishaamua byenye utavala? Bila shaka unapenda upendeze sana ile siku. Hata zamani benye bataoana balikuwa nahangaikia vile bataonekana. (Isa. 61:10) Ni kweli kama byenye utavala ku ndoa yako binaweza kuwa tofauti na byenye unavalaka zingine siku. Hata vile binapaswa kuwa na kiasi. (1 Ti. 2:9) Usiache manguo yako ao bitu bingine bya kimwili njo bikuwe mambo yenye batu bataendelea kukumbuka juu ya ndoa yako.—1 Pe. 3:3, 4.
12. Juu ya nini benye bataoana banapaswa kuepuka desturi za ndoa zenye haziko za Kikristo zenye batu ya mu eneo yabo banafanyaka?
12 Epuka desturi zenye hazipatane na Maandiko. (Ufu. 18:4) Mu hii dunia ya leo mambo ya mingi yenye inafanyikaka ku mandoa inatoka mu dini za bongo ao mu mambo ya uchawi. Yehova anatuambia waziwazi tuepuke kabisa mambo ya vile yenye haiko safi. (2 Ko. 6:14-17) Kama kuko desturi ao mambo fulani yenye muko nayo mashaka yenye batu ya mu eneo yenu banafanyaka ku ndoa, mutafute kwenye ilianziaka na mutafute kanuni za Biblia zenye zinahusu ile mambo mbele ya kuamua ikiwa mutaifanya ku ndoa yenu.
13. Namna gani benye bataoana banaweza kuiga mawazo ya Yehova kuhusu kupokea zawadi?
13 Kwenye unaishi, batu benye balialikwa ku ndoa banaletaka zawadi? Tukumbuke kama zawadi yenye mutu ataleta inategemea makuta yenye iko nayo. Ni kweli kama Bakristo banatiwa moyo kutoa, na ile inabaleteaka furaha. (Mez. 11:25; Mdo. 20:35) Lakini, tutaepuka kufanya benye tulialika bajisikie sawa vile banalazimishwa kutoa, ao bajisikie sawa vile hatutafurahia zawadi ya bei chini. Tunamuiga Yehova wakati tunajikaza kuwa na mawazo sawa yake kuhusu zawadi kwa kuacha bengine batoe kulingana na uwezo wabo na kwa moyo wote.—2 Ko. 9:7.
NAMNA YA KUEPUKA NA KUPIGANISHA MAGUMU
14. Bakristo benye biko natayarisha ndoa banaweza kupambana na magumu gani?
14 Munaweza kupambana na magumu wakati muko najikaza kutayarisha ndoa yenye itamuletea Yehova utukufu. Kwa mufano, munaweza kuona kama haiko mwepesi kufanya ndoa ya kiasi. Charlie, wa mu Visiwa vya Solomon, anasema hivi: “Ilikuwa nguvu kuamua nani tutaalika ku ndoa yetu. Tuko na barafiki ba mingi, na mu desturi yetu kila mutu anangoyaka bamualike!” Tabitha, mwenye tulishazungumuzia anasema hivi: “Kwenye ninaishi, batu banafanyaka mafete ya batu mingi. Ilikamata wakati juu bazazi yetu baitike uamuzi wetu wa kualika batu karibu 100 tu.” Dada fulani wa India mwenye jina yake Sarah, anasema hivi: “Batu fulani banakaziaka sana makuta na vile bengine batabaona. Bandugu yangu balifanya ndoa ya kabambi sana, kwa hiyo nilijisikia sawa vile na miye ninapaswa kufanya ndoa ya kabambi hata zaidi.” Nini njo inaweza kusaidia benye bataoana bapiganishe ile magumu na magumu ingine?
15. Juu ya nini kusali ni jambo ya maana wakati muko natayarisha ndoa?
15 Musali juu ya matayarisho yenu ya ndoa. Munaweza kuambia Yehova mu sala magumu yoyote yenye muko nayo ao namna muko najisikia. (Flp. 4:6, 7) Munaweza kumuomba abasaidie mukamate maamuzi ya muzuri, mubakie benye kutulia wakati muko na mahangaiko, na muonyeshe uhodari wakati ni lazima kufanya vile. (1 Pe. 5:7) Mutamutumainia Yehova zaidi wakati mutaona vile iko nabasaidia. Tabitha, mwenye tulishazungumuzia anasema hivi: “Miye na muchumba wangu tulikuwa naogopa kama hatutakubaliana mu mambo fulani, na kama familia zetu hazitakubaliana. Njo maana tulikuwa kwanza nasali mbele ya kuzungumuza juu ya matayarisho yetu ya ndoa. Tulijionea vile Yehova alitusaidia na tulikuwa na amani kati yetu na kati ya familia zetu.”
16-17. Namna gani kuzungumuza waziwazi na kwa heshima kunaweza kubasaidia wakati muko natayarisha ndoa?
16 Muzungumuze waziwazi na kwa heshima. (Mez. 15:22) Nyie benye mutaoana, munapaswa kukamata maamuzi ya mingi juu ya ndoa yenu. Mutaamua tarehe ya ndoa yenu, kiasi ya makuta yenye mutatumikisha, batu benye mutaalika, na mambo ingine ya mingi. Mbele ya kukamata uamuzi, muzungumuzie mambo yenye munapenda kufanya, na kanuni za Biblia zenye zinahusu ile mambo. Pia munaweza kulomba mashauri kwa Bakristo benye kukomala kiroho. Wakati uko nasema mambo yenye weye unapendelea, ufanye vile kwa upole, ukuwe na usawaziko, na ukuwe tayari kujipatanisha na hali. Kama batu ya familia yenu, sawa vile bazazi, banabapendekeza jambo fulani yenye munaona inawezekana kufanya, munaweza kuitika. Ile ni siku ya pekee kwabo pia. Na kama haiwezekane mufanye byenye balipendekeza, kwa upole mubafasirie juu ya nini. (Kol. 4:6) Mueleweshe batu ya familia yenu kama munapenda siku yenu ya ndoa ikuwe yenye kufurahisha na yenye itamuletea Yehova utukufu.
17 Kama bazazi yenu habiko Mashahidi, inaweza kuwa nguvu sana kubafasiria maamuzi yenu, lakini mutaweza. Ndugu mwenye kuitwa Santhosh wa India, anasema hivi: “Batu ya familia yetu balipenda tufanye desturi fulani za Kihindu. Ilitukamata wakati ya mingi juu miye na muchumba wangu tubafasirie maamuzi yetu. Tulifanya mabadiliko fulani kwenye iliwezekana, bila kujiingiza mu mambo yenye haingemufurahisha Yehova. Kwa mufano, tuliamua kubadilisha chakula na kutia chakula yenye ilibafurahisha, pia tuliamua kama hakutakuwa bya kuimba ao bya kucheza juu hababizoee.”
18. Munaweza kufanya nini juu ya kuhakikisha kama mambo itapitikana muzuri siku ya ndoa yenu? (1 Wakorinto 14:40) (Ona pia picha.)
18 Mupange mambo muzuri. Kama munapanga mambo muzuri hamutakuwa na mahangaiko ya mingi siku ya ndoa. (Soma 1 Wakorinto 14:40.) Ndugu Wayne wa mu Taiwan anasema hivi: “Siku kidogo mbele ya ndoa yetu, tulifanya mukutano ya mufupi pamoya na batu benye balijitolea kutusaidia siku ya ndoa. Tulizungumuzia mipango yetu na tukafanya mazoezi juu ya mambo fulani yenye tutafanya siku ya ndoa yetu, juu ya kuhakikisha kama mambo yote itapitikana muzuri.” Pia, mujikaze kuheshimia wakati juu ya kuonyesha kama munaheshimia benye mulialika.
Siku ya ndoa inaweza kupitikana muzuri kama mulipanga mambo muzuri mbele ya wakati (Ona fungu ya 18)
19. Munaweza kufanya nini juu ya kuhakikisha kama fete ya ndoa yenu itakuwa ya kuheshimika?
19 Munaweza kuepuka magumu ya mingi kama munaifikiria mbele ya wakati. (Mez. 22:3) Kwa mufano, kama munaishi mu eneo yenye batu banakuyaka ku fete hata kama habakualikwa, mufikirie mbele ya wakati namna munaweza kuzuia ile jambo. Muhakikishe kama batu ya familia benye habiko Mashahidi banaelewa vile mambo itapitikana, na mubafasirie mawazo yenu juu ya desturi fulani za ndoa. Unaweza kubaonyesha habari “Ndoa ya Mashahidi wa Yehova Inakuwaka Namna Gani?” yenye kuwa ku jw.org. Juu ya kuhakikisha kama mambo itapitikana muzuri ku fete, muchagule ndugu mwenye kukomala kiroho juu akuwe “musimamizi wa karamu.” (Yoh. 2:8) Kama munamuambia waziwazi vile munapenda ndoa yenu ikuwe, atabasaidia kuhakikisha kama ndoa yenu itakuwa yenye kuheshimika na itapitikana vile mulipanga.
20. Benye bataoana banapaswa kukumbuka nini juu ya ndoa yabo?
20 Munaweza kuvurugika wakati munafikiria mambo yote yenye inaomba mupange juu ya siku ya ndoa yenu. Lakini, mukumbuke kama ile ni mambo ya siku moya tu. Ni siku ya kwanza yenye munaanza kumutumikia Yehova pamoya. Kwa hiyo mufanye yenu yote juu siku yenu ya ndoa ikuwe na kiasi na yenye kuheshimika. Mumutumainie Yehova. Kwa musaada wake, mutaweza kutayarisha ndoa ya muzuri yenye wakati mutakuwa naikumbuka, hamutahuzunika lakini mutakuwa na furaha.—Zb. 37:3, 4.
WIMBO 107 Tuonyeshe Upendo Kama Mungu
a MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Mu desturi za mingi, benye kuoana banafanyaka naziri mbele ya Mungu siku ya ndoa yabo. Kisha pale, banafanyaka fete. Hata mu desturi zenye habafanyake fete ya ndoa, benye bataoana banapaswa kufuata kanuni za Biblia juu ya siku ya ndoa.
b Ili kupata habari zaidi juu ya mawazo ya Bakristo kuhusu sheria za serikali juu ya ndoa, ona habari “Arusi Zenye Kuheshimika Machoni pa Mungu na Wanadamu” mu Munara wa Mulinzi wa tarehe 15, Mwezi wa 10, 2006.
c Ona ku jw.org video Nipatie Watu Pombe?