Tujengane Kwa Kutoa Maelezo Kwenye Mikutano
1 Kwenye Waebrania 10:24, tunasihiwa “kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora.” Jambo hilo linatia ndani kujengana kwa kutoa maelezo yenye maana kwenye mikutano ya kutaniko. Kwa nini tunapaswa kutoa maelezo? Tunawezaje kufanya hilo? Ni nani watakaofaidika na jambo hilo?
2 Fikiria zile nyakati nyingi ulizofaidika kwa kusikia wengine wakitoa maneno rahisi, yaliyo wazi ambayo yaliongeza uelewevu wako na kukutia nguvu kiroho. Unalo pendeleo la kufanya vivyo hivyo kwa ajili yao. Wakati unaposhiriki mikutano, unaonyesha tamaa yako ya kuwapa wahudhuriaji wote “baadhi ya zawadi ya kiroho” kwa ajili ya kuwatia moyo.—Rom. 1:11, 12.
3 Jinsi ya Kutoa Maelezo Mazuri: Usitoe maelezo marefu yanayozungumzia mawazo yote ya fungu. Maelezo marefu kwa kawaida hayaonyeshi jibu kamili na yanaweza kuvunja moyo wengine wasishiriki. Maelezo ya kwanza ya fungu yanapaswa kuwa jibu fupi, la moja kwa moja la ulizo lililochapwa. Wale wanaotoa maelezo ya ziada wanaweza kufanya matumizi yafaayo ya habari au kuonyesha jinsi maandiko yanavyotumika. Ona Kiongozi cha Shule, kurasa 90-2.
4 Ikiwa wazo la kutoa maelezo linakutia wasiwasi, tayarisha maelezo mafupi kimbele, na uombe kiongozi akutaje kwenye fungu hilo. Baada ya kufanya hivyo kwenye mikutano michache, kushiriki kutakuwa rahisi zaidi. Kumbuka kwamba Musa na Yeremia walionyesha kukosa uhakika katika uwezo wao wa kusema peupe. (Kut. 4:10; Yer. 1:6, kielezi-chini) Lakini Yehova aliwasaidia waseme mahali pake, na atakusaidia pia.
5 Nani Atakayefaidika na Maelezo Yako? Wewe binafsi utafaidika kwa kuwa maelezo yako yanakaza kwa uthabiti zaidi kweli katika fikira yako na moyo wako, yakifanya iwe rahisi zaidi kwako kukumbuka habari hiyo wakati ujao. Wengine vilevile hufaidika kwa kusikia maneno yako yenye kujenga. Sisi tunatiwa moyo wakati akina ndugu wote, wawe wenye ustadi, vijana, watu wenye haya, au wapya, wanapojitahidi kueleza imani yao kwenye mikutano ya kutaniko.
6 Tuna uhakika wa kuona kwamba ‘maneno kwa wakati wa kufaa ni mema sana’ yanapotumiwa ili kujengana kwenye mikutano!—Mez. 15:23.