Fanya Kazi Pamoja na Yehova Kila Siku
“Sisi ni wafanyakazi pamoja na Mungu.”—1 KO. 3:9.
NYIMBO: 64, 111
1. Ni katika njia gani tunaweza kufanya kazi pamoja na Yehova?
WAKATI Yehova aliumba wanadamu, alipenda wakuwe wafanyakazi pamoja naye. Hata kama leo wanadamu hawako wakamilifu, watu wenye kuwa waaminifu wanaweza kufanya kazi pamoja na Yehova kila siku. Kwa mufano, tuko “wafanyakazi pamoja na Mungu” wakati tunahubiri habari njema ya Ufalme wake na kufanya wanafunzi. (1 Ko. 3:5-9) Ni pendeleo kubwa kabisa kuona kama Muumbaji mweza-yote ametuchagua ili kufanya kazi hiyo ya maana sana! Lakini, kazi ya kuhubiri haiko tu ndiyo njia moja ya kufanya kazi pamoja na Yehova. Katika habari hii, tutajifunza namna tunafanya pia kazi pamoja naye wakati tunasaidia watu wa familia yetu na wengine katika kutaniko, wakati tunaonyesha ukaribishaji-wageni, wakati tunasaidia katika kazi mbalimbali zenye tengenezo linafanya katika dunia yote, na wakati tunapanua utumishi wetu kwa Yehova.—Kol. 3:23.
2. Sababu gani hatupaswe hata kidogo kulinganisha mambo yenye tunafanya katika kazi ya Yehova na mambo yenye wengine wanafanya?
2 Wakati tuko tunajifunza habari hii, ni jambo la maana tukumbuke kama kila mutu iko tofauti na mwingine. Sisi wote hatuna miaka ileile, afya ileile, hali ileile na uwezo uleule. Kwa hiyo, usilinganishe mambo yenye unaweza kufanya katika kazi ya Yehova na mambo yenye wengine wanaweza kufanya. Mutume Paulo aliandika hivi: “Kila mutu achunguze matendo yake mwenyewe, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi juu yake yeye mwenyewe, na hapana kwa kujilinganisha na mutu mwingine.”—Gal. 6:4.
SAIDIA WATU WA FAMILIA YAKO NA WENGINE KATIKA KUTANIKO
3. Sababu gani tunaweza kusema kama kila mutu mwenye anahangaikia familia yake anafanya kazi pamoja na Mungu?
3 Yehova anatuomba tuhangaikie familia zetu. Kwa mufano, unapaswa kutafuta feza ili kutimiza mahitaji ao mambo ya lazima ya familia yako. Mama wengine wanapaswa kubakia nyumbani ili kuhangaikia watoto wao wadogo. Na wakati wazazi wetu hawana tena uwezo wa kujihangaikia, pengine tunapaswa kuwahangaikia. Hayo ni mambo ya lazima. Biblia inasema hivi: “Kama mutu yeyote hatimize mahitaji ya watu wake mwenyewe, na zaidi sana washiriki wa nyumba yake, amekana imani na ni mubaya kuliko mutu mwenye hana imani.” (1 Ti. 5:8) Kama uko na madaraka ya kuhangaikia familia, pengine haufanye mengi katika kazi ya Yehova kama vile ungependa kufanya. Lakini, usivunjike moyo! Yehova anafurahi wakati unatimizia watu wa familia yako mahitaji yao.—1 Ko. 10:31.
4. Namna gani wazazi wanaweza kutia faida za Ufalme pa nafasi ya kwanza, na hilo linaleta matokeo gani?
4 Wazazi Wakristo wanaweza kufanya kazi pamoja na Yehova wakati wanasaidia watoto wao wajiwekee miradi katika kazi ya Yehova. Wazazi wengi wamefanya vile. Hilo linaleta matokeo gani? Kisha wakati fulani, watoto wao wanaume na wanamuke waliamua kumutumikia Yehova wakati wote, hata walienda mbali sana na kwao. Wamoja wako wamisionere, wengine wanafanya kazi ya upainia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri, na wengine wanatumikia kwenye Beteli. Kwa kweli, wakati watoto wako mbali, wazazi hawawezi kupitisha wakati mwingi pamoja nao kama vile wangependa. Lakini, bila kujifikiria wao wenyewe, wanatia watoto wao moyo waendelee kumutumikia Yehova mahali popote kwenye wanapatikana. Sababu gani? Kwa sababu wazazi hao wanafurahi sana kuona kama watoto wao wanamutia Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yao. (3 Yo. 4) Wengi kati ya wazazi hao wanajisikia kama Hana, mwenye alisema kama ‘alimukopesha’ Yehova mutoto wake Samweli. Wanaona kama ni pendeleo kubwa kufanya kazi pamoja na Yehova katika njia hiyo.—1 Sa. 1:28.
5. Namna gani unaweza kusaidia ndugu na dada katika kutaniko lako? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)
5 Kama hauna madaraka mazito ya kuhangaikia familia, je, unaweza kusaidia ndugu na dada wenye kuwa wagonjwa ao wenye kuzeeka ao wenye kuwa na lazima ya mambo mengine? Ao, unaweza kusaidia wale wenye kuhangaikia watu hao? Tafuta katika kutaniko lako wale wenye wanaweza kuwa na lazima ya musaada huo. Kwa mufano, pengine kuko dada mwenye anahangaikia muzazi wake mwenye kuzeeka. Je, unaweza kupitisha wakati pamoja na muzazi wake ili apate wakati wa kuhangaikia mambo mengine? Ao, pengine unaweza kusaidia mutu fulani kwa kumupeleka kwenye mikutano, kwa kumupeleka wakati anaenda kuuza vitu, ao wakati anaenda kutembelea mutu fulani katika hospitali. Wakati unafanya vile, pengine unafanya kazi pamoja na Yehova ili kujibu sala fulani.—Soma 1 Wakorinto 10:24.
ONYESHA UKARIBISHAJI-WAGENI
6. Namna gani tunaweza kuonyesha ukaribishaji-wageni?
6 Wafanyakazi pamoja na Mungu wanajulikana kupitia ukaribishaji-wageni. Katika Biblia, neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “ukaribisha-wageni” linamaanisha “kuonyesha wageni fazili.” (Ebr. 13:2; maelezo ya chini) Katika Neno la Mungu, kuko mifano yenye kutufundisha namna ya kuonyesha fazili kwa njia hiyo. (Mwa. 18:1-5) Tunaweza na tunapaswa kusaidia wengine kila wakati tunapata nafasi ya kufanya vile, hata kama ni “wenye kuwa wa jamaa yetu katika imani” ao hapana.—Gal. 6:10.
7. Utapata baraka gani wakati unaonyesha watumishi wa wakati wote ukaribishaji-wageni?
7 Je, unaweza kufanya kazi pamoja na Yehova kwa kukaribisha watumishi wa wakati wote wenye wako na lazima ya mahali pa kukaa? (Soma 3 Yohana 5, 8.) Wakati tunafanya vile, hilo linawaletea faida, na sisi pia. Biblia inaita jambo hilo “ubadilishanaji wa kitia-moyo.” (Ro. 1:11, 12) Fikiria mufano wa Olaf. Wakati alikuwa kijana, mwangalizi wa muzunguko mwenye alikuwa hajaoa alitembelea kutaniko lao na alikuwa na lazima ya mahali pa kukaa, lakini hakuna mutu katika kutaniko mwenye aliweza kumukaribisha. Olaf aliuliza wazazi wake, wenye hawakukuwa Mashahidi, ikiwa mwangalizi wa muzunguko angeweza kubakia kwao. Walikubali, lakini walimuambia Olaf kama yeye angepaswa kulala kwenye kiti. Olaf alifanya vile, na hakuhuzunika. Alipitisha juma muzuri sana pamoja na mwangalizi wa muzunguko! Kila siku, walikuwa wanaamuka asubui sana na kuzungumuzia habari nyingi zenye kufurahisha wakati walikuwa wanatumia chakula cha asubui. Mwangalizi wa muzunguko alimutia moyo sana na kwa hiyo akaamua kuanza utumishi wa wakati wote. Kwa miaka 40 yenye imepita, Olaf amefanya kazi ya umisionere katika inchi mbalimbali.
8. Sababu gani tunapaswa kuonyesha fazili hata kama wengine hawana shukrani mwanzoni? Toa mufano.
8 Tunaweza kuonyesha wageni upendo katika njia nyingi, hata kama hawaonyeshe shukrani mwanzoni. Kwa mufano, dada mumoja katika inchi ya Hispania alijifunza Biblia na Yesica, mwanamuke mwenye alitoka katika inchi ya Ekuado (Équateur). Siku moja, wakati walikuwa wanajifunza, Yesica alilia sana. Kwa hiyo, dada huyo alimuuliza sababu gani alikuwa analia. Yesica alisema kama alikuwa maskini sana mbele akuje Hispania. Siku moja, hakukuwa na chakula cha kupatia mutoto wake mwanamuke, alikuwa na maji tu. Yesica alisali ili kupata musaada wakati alikuwa anajaribu kulalisha mutoto wake. Kisha tu wakati kidogo, dada wawili Mashahidi wa Yehova walimutembelea Yesica na wakamupatia gazeti. Lakini aliwakosea adabu na kupasua gazeti hilo, na kuwaambia hivi: “Hii ndiyo chakula nitapatia mutoto wangu?” Dada hao walijaribu kumutuliza Yesica, lakini hakuwasikiliza. Kisha wakati fulani, dada hao walikuja kuacha kitunga ya chakula kwenye mulango wake. Sasa, wakati walikuwa wanajifunza, alilia kwa sababu aliona kama hakutambuaka namna Mungu alijibu sala yake. Lakini Yesica aliazimia kumutumikia Yehova. Jambo hilo linaonyesha wazi kama ukarimu wa dada hao ulileta matokeo ya muzuri.—Muh. 11:1, 6.
UJITOLEE ILI KUSAIDIA KATIKA KAZI MBALIMBALI ZA TENGENEZO
9, 10. (a) Waisraeli walikuwa na nafasi gani za kujitolea? (b) Leo, ndugu wanaweza kusaidia katika kazi gani katika kutaniko?
9 Wakati wa zamani, Waisraeli walikuwa na nafasi nyingi za kujitolea. (Kut. 36:2; 1 Ny. 29:5; Ne. 11:2) Leo, wewe pia uko na nafasi nyingi za kutoa wakati wako, vitu vyako vya kimwili, na ufundi wako ili kusaidia ndugu na dada. Wakati unafanya vile, utakuwa na furaha sana na Yehova atakubariki.
10 Neno la Mungu linatia wanaume moyo katika kutaniko wafanye kazi pamoja na Yehova kwa kujikaza kuwa watumishi wa huduma na wazee ili kutumikia wengine. (1 Ti. 3:1, 8, 9; 1 Pe. 5:2, 3) Wale wenye wanafanya vile wanataka kusaidia wengine katika njia mbalimbali na pia katika mambo ya kiroho. (Mdo. 6:1-4) Je, wazee wamekwisha kukuomba utumike katika kazi ya ukaribishaji ao usaidie katika kazi ya vichapo, ya maeneo, ao kazi ingine? Ndugu wenye wanasaidia katika kazi hizo wanasema kama wanazifurahia sana.
Wale wenye wanajitolea kusaidia katika kazi za ujenzi za tengenezo, mara nyingi wanajifanyia marafiki wapya (Picha hizi zinapatana na fungu la 11)
11. Dada mumoja amepata faida gani kwa kusaidia katika kazi za ujenzi?
11 Wale wenye wanajitolea ili kusaidia katika kazi za ujenzi, mara nyingi wanajifanyia marafiki wapya. Dada mumoja mwenye kuitwa Margie ametumika katika kazi za ujenzi wa Majumba ya Ufalme kwa miaka 18. Katika kazi hizo, anazoea kupendezwa na dada vijana na amesaidia kuwazoeza. Anasema kama hiyo ni nafasi ya muzuri sana yenye wale wenye kujitolea wanapata ili kutiana moyo. (Ro. 1:12) Kwa kweli, wakati alipata magumu katika maisha yake, marafiki wenye alikuwa amejifanyia katika kazi hizo walimutia moyo. Umekwisha kujitolea ili kusaidia katika kazi fulani ya ujenzi? Unaweza kusaidia katika kazi fulani, hata kama haujue ufundi fulani wa pekee.
12. Namna gani unaweza kusaidia kisha musiba fulani?
12 Tunaweza pia kufanya kazi pamoja na Yehova kwa kusaidia ndugu na dada zetu kisha musiba fulani wa asili. Kwa mufano, tunaweza kutoa feza. (Yoh. 13:34, 35; Mdo. 11:27-30) Njia ingine ya kufanya vile ni kusaidia katika kazi ya kusafisha ao kutengeneza vitu vyenye vimeharibika wakati wa musiba. Gabriela, dada mumoja katika inchi ya Polandi (Pologne) mwenye nyumba yake iliharibika sana kwa sababu ya mafuriko (maji mengi yenye kuleta uharibifu), alifurahi sana wakati aliona ndugu na dada wa makutaniko jirani wenye walikuja kumusaidia. Wakati anawaza juu ya jambo hilo, anasema kama hahangaikie vitu vya kimwili vyenye alipoteza, lakini anakazia akili faida zenye alipata. Anasema hivi: “Jambo hilo lilinihakikishia kwamba kuwa katika kutaniko la Kikristo ni pendeleo la pekee na kunaleta furaha kabisa.” Watu wengi wenye wanapata musaada kisha musiba kutokea wanasema kama wao pia wanajisikia vile. Na wale wenye wanafanya kazi pamoja na Yehova ili kusaidia ndugu na dada wenye wamepatwa na musiba wanajisikia pia kuwa wenye furaha sana na wenye kutosheka.—Soma Matendo 20:35; 2 Wakorinto 9:6, 7.
13. Namna gani kujitolea katika kazi fulani kunatusaidia kutia nguvu upendo wetu kwa Yehova? Toa mufano.
13 Dada mumoja mwenye kuitwa Stephanie na wahubiri wengine katika eneo lake, walifanya kazi pamoja na Mungu kwa kusaidia Mashahidi wenye walikimbilia katika inchi ya Amerika, kwa sababu ya vita katika inchi yao. Walisaidia wakimbizi hao wapate nyumba na vitu vya kutia katika nyumba zao. Anasema hivi: “Furaha na shukrani yenye walionyesha wakati walijionea upendo wa ndugu na dada zao wa duniani pote vilitugusa moyo. Watu wa familia mbalimbali wanafikiri kama tumewasaidia, lakini kwa kweli, wao ndio walitusaidia zaidi. Sifa zenye tumejionea kama vile upendo, umoja, imani, na kumutegemea Yehova, zimetusaidia kutia nguvu kabisa upendo wetu kwa Yehova, na hilo limefanya tufurahie sana mambo yote yenye tunapata kupitia tengenezo lake.”
PANUA UTUMISHI WAKO KWA YEHOVA
14, 15. (a) Nabii Isaya alikuwa tayari kufanya nini? (b) Namna gani Wakristo wanaweza kuiga mufano wa Isaya?
14 Ungependa kufanya kazi zaidi pamoja na Yehova? Unaweza kuwa tayari kuhamia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri? Kwa kweli, haiko lazima kuhamia mbali sana ili kuonyesha ukarimu. Lakini, kuko ndugu na dada wenye wanaweza kufanya vile. Wako tayari kama vile nabii Isaya. Wakati Yehova aliuliza hivi: “Nitatuma nani, na ni nani ataenda kwa ajili yetu?” Isaya alisema hivi: “Mimi huyu! Unitume mimi!” (Isa. 6:8) Uko tayari na uko na uwezo wa kusaidia tengenezo la Yehova? Unaweza kusaidia katika njia gani fulani?
15 Juu ya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, Yesu alisema hivi: “Mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi wako kidogo. Kwa hiyo, mumuombe Bwana wa mavuno atume wafanyakazi katika mavuno yake.” (Mt. 9:37, 38) Unaweza kufanya kazi ya upainia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri? Ao, unaweza kusaidia mutu fulani afanye vile? Ndugu na dada wengi wanaona kuwa, njia ya muzuri zaidi ya kuonyesha upendo wao kwa Mungu na kwa jirani yao, ni kufanya kazi ya upainia mahali kwenye kuwa lazima kubwa ya wahubiri. Unaweza kufikiria njia zingine za kufanya mengi katika utumishi wako? Kama unafanya vile, utakuwa na furaha sana.
16, 17. Unaweza kupanua utumishi wako kwa Yehova katika njia gani zingine?
16 Uko tayari kutumikia kwenye Beteli ao kusaidia katika kazi za ujenzi, kwa kutumika kwa muda fulani ao siku moja ao zaidi katika juma? Sikuzote, tengenezo la Yehova liko na lazima ya watu wenye kuwa tayari kutumikia kila mahali kwenye wanahitajiwa na kufanya kila kazi yenye wanaombwa kufanya, hata kama wako na uzoefu katika kazi ingine. Yehova anapendezwa na kila mutu mwenye kuwa tayari kujitoa na kutumikia kila mahali kwenye kuwa lazima.—Zb. 110:3.
17 Ungependa kupata mazoezi zaidi ili upanue utumishi wako kwa Yehova? Pengine unaweza kujaza ombi ili kusoma Masomo kwa Ajili ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Masomo hayo yanazoeza ndugu na dada wenye kukomaa kiroho, wenye wako tayari katika utumishi wa wakati wote, ili tengenezo la Yehova liwatumie kufanya mengi zaidi. Wale wenye wanasoma masomo hayo wanapaswa kuwa tayari kutumikia kila mahali kwenye wanatumwa. Unaweza kuwa tayari kumutumikia Yehova zaidi katika njia hiyo?—1 Ko. 9:23.
18. Kufanya kazi pamoja na Yehova kila siku kunaleta baraka gani?
18 Kwa sababu tuko watu wa Yehova, tuko tunaonyesha ukarimu, wema, fazili, na upendo. Tunahangaikia wengine kila siku. Kufanya vile kunatuletea amani na furaha. (Gal. 5:22, 23) Hata kama uko katika hali gani, utakuwa na furaha wakati unaiga sifa ya Yehova ya ukarimu na kuwa kati ya wafanyakazi pamoja naye wenye anapendezwa nao!—Mez. 3:9, 10.