KULINGANA NA MATHAYO
1 Kitabu cha historia ya* Yesu Kristo,* mwana wa Daudi,+ mwana wa Abrahamu:+
2 Abrahamu akawa baba ya Isaka;+
Isaka akawa baba ya Yakobo;+
Yakobo akawa baba ya Yuda+ na ndugu zake;
3 Yuda akawa baba ya Perezi na Zera+ kupitia Tamari;
Perezi akawa baba ya Hezroni;+
Hezroni akawa baba ya Ramu;+
4 Ramu akawa baba ya Aminadabu;
Aminadabu akawa baba ya Nashoni;+
Nashoni akawa baba ya Salmoni;
5 Salmoni akawa baba ya Boazi kupitia Rahabu;+
Boazi akawa baba ya Obedi kupitia Ruthu;+
Obedi akawa baba ya Yese;+
6 Yese akawa baba ya Mfalme Daudi.+
Daudi akawa baba ya Sulemani+ kupitia mke wa Uria;
7 Sulemani akawa baba ya Rehoboamu;+
Rehoboamu akawa baba ya Abiya;
Abiya akawa baba ya Asa;+
8 Asa akawa baba ya Yehoshafati;+
Yehoshafati akawa baba ya Yehoramu;+
Yehoramu akawa baba ya Uzia;
9 Uzia akawa baba ya Yothamu;+
Yothamu akawa baba ya Ahazi;+
Ahazi akawa baba ya Hezekia;+
10 Hezekia akawa baba ya Manase;+
Manase akawa baba ya Amoni;+
Amoni akawa baba ya Yosia;+
11 Yosia+ akawa baba ya Yekonia+ na ndugu zake, wakati wa kupelekwa uhamishoni Babiloni.+
12 Baada ya kupelekwa uhamishoni Babiloni, Yekonia akawa baba ya Shealtieli;
Shealtieli akawa baba ya Zerubabeli;+
13 Zerubabeli akawa baba ya Abiudi;
Abiudi akawa baba ya Eliakimu;
Eliakimu akawa baba ya Azori;
14 Azori akawa baba ya Sadoki;
Sadoki akawa baba ya Akimu;
Akimu akawa baba ya Eliudi;
15 Eliudi akawa baba ya Eleazari;
Eleazari akawa baba ya Mathani;
Mathani akawa baba ya Yakobo;
16 Yakobo akawa baba ya Yosefu mume wa Maria, aliyemzaa Yesu,+ aitwaye Kristo.+
17 Kuanzia Abrahamu mpaka Daudi kulikuwa na vizazi 14; kuanzia Daudi mpaka wakati wa kupelekwa uhamishoni Babiloni, vizazi 14; kuanzia wakati wa kupelekwa uhamishoni Babiloni mpaka Kristo, vizazi 14.
18 Basi kuzaliwa kwa Yesu Kristo kulikuwa hivi: Maria mama ya Yesu alichumbiwa na Yosefu, lakini kabla hawajafunga ndoa akapata mimba kupitia roho takatifu.*+ 19 Hata hivyo, kwa sababu Yosefu mume wake alikuwa mwadilifu na hakutaka kumwaibisha hadharani, alikusudia kumtaliki kisiri.+ 20 Lakini baada ya kufikiria mambo hayo, tazama! malaika wa Yehova* alimtokea katika ndoto na kumwambia: “Yosefu, mwana wa Daudi, usiogope kumpeleka Maria mke wako nyumbani, kwa sababu amepata mimba kupitia roho takatifu.+ 21 Atamzaa mwana, nawe utamwita jina Yesu,*+ kwa maana atawaokoa watu wake kutoka katika dhambi zao.”+ 22 Kwa kweli, yote hayo yalitukia ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa na Yehova* kupitia nabii wake: 23 “Tazama! Bikira atapata mimba naye atazaa mwana, nao watamwita jina Imanueli,”+ ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, “Mungu Yuko Pamoja Nasi.”+
24 Ndipo Yosefu akaamka kutoka usingizini na kufanya kama alivyoambiwa na malaika wa Yehova,* akampeleka mke wake nyumbani. 25 Lakini hakufanya ngono naye mpaka alipozaa mwana,+ kisha Yosefu akamwita jina Yesu.+
2 Baada ya Yesu kuzaliwa huko Bethlehemu+ ya Yudea katika siku za Mfalme Herode,*+ tazama! wanajimu* kutoka Mashariki walikuja Yerusalemu, 2 wakisema: “Yuko wapi yule aliyezaliwa awe mfalme wa Wayahudi?+ Kwa maana tuliiona nyota yake tulipokuwa Mashariki, nasi tumekuja kumsujudia.”* 3 Mfalme Herode aliposikia jambo hilo, yeye na watu wote huko Yerusalemu wakafadhaika. 4 Akawakusanya wakuu wote wa makuhani na waandishi wa watu na kuwauliza mahali ambapo Kristo* alipaswa kuzaliwa. 5 Wakamwambia: “Katika Bethlehemu+ ya Yudea; kwa maana nabii aliandika hivi: 6 ‘Na wewe, ewe Bethlehemu ya nchi ya Yuda, wewe si mji mdogo zaidi miongoni mwa magavana wa Yuda, kwa maana kutoka kwako atakuja kiongozi, atakayewachunga watu wangu Israeli.’”+
7 Ndipo Herode akawaita wale wanajimu kwa siri na kuhakikisha kwa uangalifu kutoka kwao wakati ambapo ile nyota ilionekana. 8 Akawatuma Bethlehemu na kuwaambia: “Nendeni mkamtafute kwa uangalifu huyo mtoto, na baada ya kumpata mniletee habari, ili mimi pia niende kumsujudia.” 9 Baada ya kumsikiliza mfalme, wakaondoka, na tazama! nyota waliyokuwa wameona walipokuwa Mashariki+ ikawaongoza mpaka iliposimama juu ya mahali alipokuwa yule mtoto. 10 Walipoiona ile nyota wakashangilia sana. 11 Walipoingia ndani ya nyumba wakamwona yule mtoto pamoja na Maria mama yake, wakapiga magoti na kumsujudia* mtoto. Pia, wakafungua hazina zao na kumpa yule mtoto zawadi—dhahabu, ubani, na manemane. 12 Hata hivyo, kwa sababu Mungu aliwaonya kupitia ndoto+ wasirudi kwa Herode, wakarudi nchini kwao kupitia njia nyingine.
13 Baada ya kuondoka, tazama! malaika wa Yehova* akamtokea Yosefu katika ndoto+ na kumwambia: “Simama, mchukue huyo mtoto na mama yake mkimbilie Misri, mkae huko mpaka nitakapokwambia, kwa maana Herode yuko karibu kumtafuta huyo mtoto ili amuue.” 14 Basi Yosefu akaamka usiku, akamchukua Maria pamoja na yule mtoto wakaenda Misri. 15 Wakakaa huko mpaka Herode alipokufa. Basi yakatimia maneno haya yaliyosemwa na Yehova* kupitia nabii wake: “Nikamwita mwanangu atoke Misri.”+
16 Herode alipoona ameshindwa akili na wale wanajimu, akakasirika sana, akaamuru wavulana wote huko Bethlehemu na wilaya zake zote wauawe, kuanzia umri wa miaka miwili kwenda chini, kulingana na wakati aliokuwa amehakikisha kwa uangalifu kutoka kwa wale wanajimu.+ 17 Ndipo yakatimia maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Yeremia: 18 “Sauti ilisikika kule Rama, kilio na kuomboleza kwingi. Raheli+ akiwalilia watoto wake, naye hakutaka kufarijiwa, kwa sababu hawako tena.”+
19 Herode alipokufa, tazama! malaika wa Yehova* akamtokea Yosefu katika ndoto+ huko Misri 20 akamwambia: “Simama, umchukue mtoto na mama yake, nanyi mrudi katika nchi ya Israeli, kwa sababu wale waliotaka kumuua* mtoto wamekufa.” 21 Basi akaamka akamchukua mtoto na mama yake, wakarudi katika nchi ya Israeli. 22 Lakini aliposikia kwamba Arkelao alikuwa akitawala Yudea baada ya Herode baba yake, akaogopa kwenda huko. Zaidi ya hayo, alionywa na Mungu kupitia ndoto,+ basi akaenda katika eneo la Galilaya.+ 23 Akaenda kuishi katika jiji liitwalo Nazareti,+ ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia manabii: “Ataitwa Mnazareti.”*+
3 Siku hizo Yohana+ Mbatizaji alikuja kuhubiri+ katika nyika ya Yudea, 2 akisema: “Tubuni, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia.”+ 3 Kwa kweli, huyu ndiye anayezungumziwa kupitia nabii Isaya+ kwa maneno haya: “Kuna mtu anayepaza sauti nyikani: ‘Tayarisheni njia ya Yehova!* Nyoosheni barabara zake.’”+ 4 Yohana alivaa mavazi yaliyofumwa kwa manyoya ya ngamia na alijifunga mshipi wa ngozi kiunoni.+ Chakula chake kilikuwa nzige na asali ya mwituni.+ 5 Basi watu kutoka Yerusalemu na Yudea yote na maeneo yote yaliyokuwa karibu na Yordani walikuwa wakimwendea,+ 6 naye akawabatiza* katika Mto Yordani,+ nao wakaungama dhambi zao waziwazi.
7 Alipoona Mafarisayo na Masadukayo+ wengi wakija kwenye ubatizo, akawaambia: “Enyi uzao wa nyoka,*+ ni nani amewaonya ili mkimbie ghadhabu inayokuja?+ 8 Basi zaeni matunda yanayoonyesha toba. 9 Msithubutu kujiambia, ‘Abrahamu ndiye baba yetu.’+ Kwa maana ninawaambia, Mungu anaweza kumwinulia Abrahamu watoto kutoka kwenye mawe haya. 10 Tayari shoka limewekwa kwenye mzizi wa miti. Basi, kila mti usiozaa matunda mazuri utakatwa na kutupwa motoni.+ 11 Mimi ninawabatiza kwa maji kwa sababu mmetubu,+ lakini yule anayekuja baada yangu ana nguvu kuliko mimi, nami sistahili kuvivua viatu vyake.+ Yeye atawabatiza ninyi kwa roho takatifu+ na kwa moto.+ 12 Sepetu yake ya kupepetea imo mkononi mwake, naye atausafisha kabisa uwanja wake wa kupuria, na kukusanya ngano yake katika ghala, lakini atayateketeza makapi kwa moto+ usioweza kuzimwa.”
13 Ndipo Yesu akatoka Galilaya na kwenda Yordani ili abatizwe na Yohana.+ 14 Lakini Yohana akajaribu kumzuia, akisema: “Mimi ndiye ninayehitaji kubatizwa na wewe, nawe unakuja kwangu?” 15 Yesu akamjibu: “Acha iwe hivyo wakati huu, kwa maana kwa njia hiyo inafaa tufanye yote yaliyo ya uadilifu.” Ndipo Yohana akaacha kumzuia. 16 Baada ya kubatizwa, mara moja Yesu akainuka kutoka katika maji; na tazama! mbingu zikafunguliwa,+ naye akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake.+ 17 Tazama! Pia, sauti ikasikika kutoka mbinguni+ ikisema: “Huyu ni Mwanangu,+ mpendwa, ambaye nimemkubali.”+
4 Ndipo Yesu akaongozwa na roho kuingia nyikani ili akajaribiwe+ na Ibilisi.+ 2 Baada ya kufunga kwa siku 40, mchana na usiku, akahisi njaa. 3 Naye Mjaribu+ akaja na kumwambia: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, yaambie mawe haya yawe mikate.” 4 Lakini akajibu: “Imeandikwa: ‘Mwanadamu hataishi kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’”*+
5 Ndipo Ibilisi akampeleka kwenye lile jiji takatifu,+ akamsimamisha juu ya mnara* wa hekalu+ 6 na kumwambia: “Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, jitupe chini, kwa maana imeandikwa: ‘Atawaagiza malaika zake kukuhusu wewe,’ nao ‘Watakubeba mikononi mwao, ili mguu wako usigonge jiwe.’”+ 7 Yesu akamwambia: “Tena imeandikwa: ‘Usimjaribu Yehova* Mungu wako.’”+
8 Tena Ibilisi akampeleka Yesu kwenye mlima mrefu sana, akamwonyesha falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.+ 9 Naye akamwambia: “Nitakupa vitu hivi vyote ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” 10 Ndipo Yesu akamwambia: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa: ‘Yehova* Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu,+ na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’”+ 11 Ndipo Ibilisi akamwacha,+ na tazama! malaika wakaja na kuanza kumhudumia.+
12 Yesu aliposikia kwamba Yohana alikuwa amekamatwa,+ akaenda Galilaya.+ 13 Isitoshe, baada ya kuondoka Nazareti, akaenda kukaa Kapernaumu+ kando ya bahari katika wilaya za Zabuloni na Naftali, 14 ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Isaya, aliyesema: 15 “Ewe nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali, kando ya barabara ya bahari, ng’ambo ya Yordani, katika Galilaya ya mataifa! 16 Watu wanaokaa katika giza waliona nuru kuu, na wale wanaokaa katika eneo la kivuli cha kifo, nuru+ iliwaangazia.”+ 17 Tangu wakati huo, Yesu alianza kuhubiri na kusema: “Tubuni, kwa maana Ufalme wa mbinguni umekaribia.”+
18 Alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya aliwaona ndugu wawili, Simoni, anayeitwa Petro,+ na Andrea ndugu yake, wakishusha wavu baharini, kwa maana walikuwa wavuvi.+ 19 Akawaambia: “Nifuateni, nami nitawafanya muwe wavuvi wa watu.”+ 20 Mara moja wakaziacha nyavu zao na kumfuata.+ 21 Alipoenda mbele kidogo akawaona ndugu wengine wawili, Yakobo na Yohana wana wa Zebedayo.+ Walikuwa kwenye mashua pamoja na baba yao Zebedayo wakitengeneza nyavu zao, naye akawaita.+ 22 Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.
23 Kisha akaenda katika Galilaya yote,+ akifundisha katika masinagogi+ yao na kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuwaponya watu kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.+ 24 Na habari kumhusu zikaenea katika Siria yote, nao wakamletea wote waliokuwa na magonjwa mbalimbali na walioteseka,+ wenye roho waovu+ na wenye kifafa+ na watu waliopooza, naye akawaponya. 25 Kwa hiyo, umati mkubwa ukamfuata kutoka Galilaya, Dekapoli,* Yerusalemu, Yudea, na ng’ambo ya Yordani.
5 Alipouona umati, akapanda mlimani; na baada ya kuketi wanafunzi wake wakamjia. 2 Kisha akafungua kinywa chake akaanza kuwafundisha, akisema:
3 “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho,*+ kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao.
4 “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.+
5 “Wenye furaha ni wale walio wapole,+ kwa kuwa watairithi dunia.+
6 “Wenye furaha ni wale walio na njaa na kiu+ ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.*+
7 “Wenye furaha ni wale wenye rehema,+ kwa kuwa wataonyeshwa rehema.
8 “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni,+ kwa kuwa watamwona Mungu.
9 “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani,+ kwa kuwa wataitwa wana wa Mungu.
10 “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu,+ kwa kuwa Ufalme wa mbinguni ni wao.
11 “Wenye furaha ni ninyi, watu wanapowashutumu+ na kuwatesa+ na kuwasingizia kila aina ya uovu kwa sababu yangu.+ 12 Furahini na kushangilia sana,+ kwa kuwa thawabu+ yenu ni kubwa mbinguni, kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwapo kabla yenu.+
13 “Ninyi ndio chumvi ya dunia, lakini chumvi+ ikipoteza nguvu yake, ladha yake itarudishwaje? Haifai tena, inapaswa kutupwa nje+ na kukanyagwa-kanyagwa na watu.
14 “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu.+ Jiji lililo mlimani haliwezi kufichwa. 15 Watu hawawashi taa na kuiweka chini ya kikapu* bali huiweka kwenye kinara cha taa ili iwaangazie wote walio ndani ya nyumba.+ 16 Vivyo hivyo, acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu,+ ili waone matendo yenu mema+ na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.+
17 “Msifikiri nilikuja kuharibu Sheria au Manabii. Sikuja kuharibu, bali kutimiza.+ 18 Kwa kweli ninawaambia ni rahisi zaidi kwa mbingu na dunia kupitilia mbali, kuliko herufi moja iliyo ndogo zaidi au sehemu yoyote ya herufi kuondolewa katika Sheria mpaka mambo yote yatimie.+ 19 Kwa hiyo, yeyote anayevunja mojawapo ya amri hizi ndogo na kufundisha wengine kufanya hivyo, ataitwa mdogo kuhusiana na Ufalme wa mbinguni. Lakini yeyote anayeshika na kufundisha amri hizi ataitwa mkubwa kuhusiana na Ufalme wa mbinguni. 20 Kwa maana ninawaambia ikiwa uadilifu wenu hauzidi ule wa waandishi na Mafarisayo,+ hamtaingia kamwe katika Ufalme wa mbinguni.+
21 “Mlisikia kwamba zamani watu waliambiwa: ‘Usiue,+ lakini yeyote anayeua atawajibika mahakamani.’+ 22 Hata hivyo, ninawaambia kila mtu anayeendelea kumkasirikia+ ndugu yake atawajibika mahakamani; na yeyote anayemtukana ndugu yake kwa neno la dharau atawajibika katika Mahakama Kuu; na yeyote anayesema, ‘Wewe mpumbavu usiyefaa kitu!’ atastahili moto wa Gehena.*+
23 “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu+ na hapo unakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, 24 iache zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, uende zako. Kwanza fanya amani na ndugu yako, kisha urudi na kutoa zawadi yako.+
25 “Suluhisha mambo upesi na mtu anayekushtaki, ukiwa naye njiani kwenda mahakamani, ili asikupeleke kwa hakimu, naye hakimu kwa mtumishi wa mahakama, nawe utupwe gerezani.+ 26 Hakika ninakuambia hutatoka humo mpaka utakapolipa sarafu yako ndogo ya mwisho.*
27 “Mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Usifanye uzinzi.’+ 28 Lakini ninawaambia kila mtu anayeendelea kumtazama mwanamke+ na kumtamani tayari amefanya uzinzi naye moyoni+ mwake. 29 Basi, ikiwa jicho lako la kulia linafanya ujikwae, ling’oe na kulitupilia mbali.+ Kwa maana ni afadhali upoteze kiungo kimoja kuliko mwili wako wote utupwe katika Gehena.*+ 30 Pia, ikiwa mkono wako wa kulia unakufanya ujikwae, ukate na kuutupilia mbali.+ Kwa maana ni afadhali upoteze kiungo kimoja kuliko mwili wako wote utupwe katika Gehena.*+
31 “Zaidi ya hayo, ilisemwa: ‘Yeyote anayemtaliki mke wake, anapaswa kumpa cheti cha talaka.’+ 32 Hata hivyo, ninawaambia kila mtu anayemtaliki mke wake kwa sababu nyingine isipokuwa uasherati,* anamweka katika kishawishi cha kufanya uzinzi, na yeyote anayemwoa mwanamke aliyetalikiwa anafanya uzinzi.+
33 “Tena mlisikia kwamba zamani watu waliambiwa: ‘Usikose kutimiza kiapo chako,+ unapaswa kutimiza nadhiri zako kwa Yehova.’*+ 34 Hata hivyo, ninawaambia: Msiape kamwe+ kwa mbingu kwa sababu ni kiti cha ufalme cha Mungu; 35 wala kwa dunia kwa sababu ni mahali pake pa kuwekea miguu;+ wala kwa Yerusalemu kwa sababu ni jiji la Mfalme mkuu.+ 36 Usiape kwa kichwa chako kwa sababu huwezi kugeuza unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. 37 Acheni ‘Ndiyo’ yenu imaanishe ndiyo, na ‘Siyo’ yenu, siyo,+ kwa maana linalozidi hayo linatoka kwa yule mwovu.+
38 “Mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Jicho kwa jicho na jino kwa jino.’+ 39 Hata hivyo, ninawaambia: Msimzuie mtu mwovu, bali yeyote anayekupiga kofi kwenye shavu la kulia, mgeuzie pia shavu la kushoto.+ 40 Na ikiwa mtu anataka kukupeleka mahakamani ili alichukue vazi lako la ndani, mwachie pia vazi lako la nje;+ 41 na mtu mwenye mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilomita moja,* nenda naye kilomita mbili. 42 Mpe yule anayekuomba, wala usimpe kisogo yule anayetaka umkopeshe.*+
43 “Mlisikia kwamba ilisemwa: ‘Lazima umpende jirani yako+ na kumchukia adui yako.’ 44 Hata hivyo, ninawaambia: Endeleeni kuwapenda adui zenu+ na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi,+ 45 ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni,+ kwa kuwa yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, na hunyesha mvua juu ya waadilifu na wasio waadilifu.+ 46 Kwa maana mkiwapenda wale wanaowapenda, mnapata thawabu gani?+ Je, wakusanya kodi hawafanyi vivyo hivyo? 47 Na mkiwasalimu ndugu zenu tu, mnafanya jambo gani lisilo la kawaida? Je, watu wa mataifa hawafanyi vivyo hivyo? 48 Basi lazima muwe wakamilifu* kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.+
6 “Iweni waangalifu msionyeshe uadilifu wenu mbele ya watu ili wawaone;+ la sivyo hamtapata thawabu kutoka kwa Baba yenu aliye mbinguni. 2 Basi unapotoa zawadi za rehema,* usipige tarumbeta mbele yako kama wanavyofanya wanafiki katika masinagogi na barabarani, ili wasifiwe na watu. Kwa kweli ninawaambia, wanapata thawabu yao kikamili. 3 Lakini wewe, unapotoa zawadi za rehema, usiache mkono wako wa kushoto ujue kile ambacho mkono wako wa kulia unafanya, 4 ili utoe zawadi za rehema kwa siri. Naye Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.+
5 “Pia, mnaposali msifanye kama wanafiki,+ kwa maana wanapenda kusali wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye kona za barabara kuu ili watu wawaone.+ Kwa kweli ninawaambia, wanapata thawabu yao kikamili. 6 Lakini unaposali, ingia ndani ya chumba chako faraghani, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri.+ Naye Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa. 7 Mnaposali msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao hufikiri watasikiwa kwa kutumia maneno mengi. 8 Kwa hiyo, msiwe kama wao, kwa sababu Baba yenu anajua kile mnachohitaji+ hata kabla hamjamwomba.
“‘Baba yetu uliye mbinguni, jina lako+ na litakaswe.*+ 10 Ufalme wako+ na uje. Mapenzi yako+ na yatendeke duniani+ kama ilivyo mbinguni. 11 Utupatie leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii;+ 12 na utusamehe madeni yetu, kama vile tunavyowasamehe wadeni wetu.+ 13 Na usituingize katika majaribu,+ bali utukomboe* kutoka kwa yule mwovu.’+
14 “Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia;+ 15 lakini msipowasamehe watu makosa yao, naye Baba yenu hatawasamehe makosa yenu.+
16 “Mnapofunga,+ msiwe na nyuso zenye huzuni kama wanafiki, kwa maana wao hukunja nyuso zao* ili watu waone kwamba wanafunga.+ Kwa kweli ninawaambia, wanapata thawabu yao kikamili. 17 Lakini wewe unapofunga, paka kichwa chako mafuta na unawe uso, 18 ili usionekane kwamba unafunga kwa wanadamu bali kwa Baba yako aliye mahali pa siri. Naye Baba yako anayeona akiwa mahali pa siri atakulipa.
19 “Acheni kujiwekea hazina duniani,+ ambako nondo* na kutu hula na ambako wezi huvunja na kuiba. 20 Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni,+ ambako hazitaliwa na nondo* wala kutu,+ na ambako wezi hawatavunja na kuiba. 21 Kwa maana mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.
22 “Taa ya mwili ni jicho.+ Basi, ikiwa jicho lako linakazia jambo hususa,* mwili wako wote utakuwa mwangavu.* 23 Lakini ikiwa jicho lako lina wivu,*+ mwili wako wote utakuwa na giza. Ikiwa nuru iliyo ndani yako kwa kweli ni giza, basi giza hilo ni kubwa sana!
24 “Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana atamchukia mmoja na kumpenda mwingine,+ au atashikamana na mmoja na kumdharau mwingine. Hamwezi kutumikia Mungu na Utajiri.+
25 “Kwa hiyo ninawaambia: Acheni kuhangaikia+ uhai wenu* kuhusu kile mtakachokula au kunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa.+ Je, uhai* si zaidi ya chakula na mwili zaidi ya mavazi?+ 26 Waangalieni kwa makini ndege wa angani;+ hawapandi mbegu, hawavuni, wala kukusanya ghalani, na bado Baba yenu wa mbinguni huwalisha. Je, ninyi si wenye thamani kuliko wao? 27 Ni nani kati yenu ambaye kwa kuhangaika anaweza kurefusha uhai wake kwa mkono mmoja?*+ 28 Pia, kwa nini mnahangaika kuhusu mavazi? Jifunzeni kutoka kwa mayungiyungi* ya shambani, jinsi yanavyokua; hayafanyi kazi, wala hayasokoti; 29 lakini ninawaambia hata Sulemani+ katika utukufu wake wote hakupambwa kama maua hayo. 30 Basi, ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo hapa leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, hatawavika vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo? 31 Kwa hiyo msihangaike+ kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’+ 32 Kwa maana mataifa yanatafuta vitu hivi vyote kwa bidii. Baba yenu wa mbinguni anajua kwamba mnahitaji vitu hivi vyote.
33 “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake,* nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.+ 34 Basi, msihangaike kamwe kuhusu kesho,+ kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Kila siku ina matatizo yake ya kutosha.
7 “Acheni kuhukumu+ ili msihukumiwe; 2 kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa,+ na kwa kipimo mnachowapimia watu, ndicho watakachowapimia.+ 3 Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako lakini huoni boriti lililo katika jicho lako mwenyewe?+ 4 Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako,’ na huku tazama! una boriti katika jicho lako? 5 Mnafiki! Kwanza toa boriti katika jicho lako, kisha utaona vizuri jinsi ya kuutoa unyasi katika jicho la ndugu yako.
6 “Msiwape mbwa kitu kitakatifu, wala msiwatupie nguruwe lulu zenu,+ wasije wakazikanyaga-kanyaga chini ya miguu yao, kisha wageuke na kuwararua ninyi.
7 “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa;+ endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa;+ 8 kwa maana kila mtu anayeomba hupokea,+ na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi, atafunguliwa. 9 Kwa kweli, ni nani miongoni mwenu ambaye mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? 10 Au akimwomba samaki, je, atampa nyoka? 11 Kwa hiyo, ingawa ninyi ni waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema+ wale wanaomwomba?+
12 “Basi, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima ninyi pia mwatendee vivyo hivyo.+ Kwa kweli, hiyo ndiyo maana ya Sheria na Manabii.+
13 “Ingieni kupitia lango jembamba,+ kwa sababu lango ni pana, na barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa, na ni wengi wanaoipitia; 14 lakini lango ni jembamba na barabara inayoongoza kwenye uzima ina nafasi ndogo, na ni wachache wanaoipata.+
15 “Jihadharini na manabii wa uwongo+ ambao huja kwenu katika mavazi ya kondoo,+ lakini ndani wao ni mbwamwitu wakali.+ 16 Kwa matunda yao mtawatambua. Je, watu huchuma zabibu kwenye miiba au tini kwenye michongoma?+ 17 Vivyo hivyo, kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda mabaya.+ 18 Mti mzuri hauwezi kuzaa matunda mabaya, wala mti uliooza hauwezi kuzaa matunda mazuri.+ 19 Kila mti usiozaa matunda mazuri hukatwa na kutupwa ndani ya moto.+ 20 Kwa kweli, mtawatambua watu hao kwa matunda yao.+
21 “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika Ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.+ 22 Wengi wataniambia siku hiyo: ‘Bwana, Bwana,+ je, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’+ 23 Ndipo nitakapowaambia: ‘Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi mnaotenda uasi sheria!’+
24 “Kwa hiyo, kila mtu anayesikia haya maneno yangu na kuyatenda ni kama mtu mwenye busara aliyejenga nyumba yake kwenye mwamba.+ 25 Kisha mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, upepo ukavuma na kuipiga nyumba hiyo, lakini haikuporomoka, kwa maana msingi wake ulikuwa umejengwa kwenye mwamba. 26 Zaidi ya hayo, kila mtu anayesikia haya maneno yangu lakini hayatendi ni kama mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba juu ya mchanga.+ 27 Kisha mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, upepo ukavuma na kuipiga nyumba hiyo,+ nayo ikaporomoka na kuharibika kabisa.”
28 Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha,+ 29 kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka,+ na si kama waandishi wao.
8 Yesu aliposhuka kutoka mlimani, umati mkubwa ukamfuata. 2 Na tazama! mtu fulani mwenye ukoma akaja na kumsujudia* akimwambia: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.”+ 3 Basi akaunyoosha mkono wake, akamgusa na kusema: “Ninataka! Takasika.”+ Mara moja ukoma wake ukatakasika.+ 4 Kisha Yesu akamwambia: “Usimwambie mtu yeyote,+ bali nenda, ukajionyeshe kwa kuhani,+ na utoe zawadi ambayo Musa aliagiza,+ ili kuwa ushahidi kwao.”
5 Alipoingia Kapernaumu, ofisa mmoja wa jeshi alimjia, akamsihi+ 6 na kusema: “Bwana, mtumishi wangu amelala nyumbani na ana ugonjwa wa kupooza, naye anateseka sana.” 7 Akamwambia: “Nikifika huko, nitamponya.” 8 Ofisa huyo akamjibu: “Bwana, sistahili uingie ndani ya nyumba yangu, lakini sema tu neno na mtumishi wangu atapona. 9 Kwa maana mimi pia niko chini ya mamlaka, na nina wanajeshi walio chini yangu, nami humwambia mmoja, ‘Nenda!’ naye huenda, na mwingine, ‘Njoo!’ naye huja, na mtumwa wangu, ‘Fanya hili!’ naye hulifanya.” 10 Yesu aliposikia hayo, akashangaa na kuwaambia wale waliomfuata: “Ninawaambia ukweli, sijaona mtu yeyote katika Israeli mwenye imani kubwa kama hii.+ 11 Lakini ninawaambia kwamba wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi na kuketi mezani pamoja na Abrahamu, Isaka, na Yakobo katika Ufalme wa mbinguni;+ 12 lakini wana wa Ufalme watatupwa nje gizani. Huko ndiko watalia na kusaga meno yao.”+ 13 Kisha Yesu akamwambia yule ofisa wa jeshi: “Nenda. Na iwe kama ulivyoamini.”+ Na yule mtumishi akapona saa ileile.+
14 Yesu alipoingia nyumbani kwa Petro, alimwona mama mkwe wa Petro+ akiwa amelala akiugua homa.+ 15 Basi Yesu akamgusa mkono,+ naye akapona homa, akasimama na kuanza kumhudumia. 16 Lakini ilipofika jioni, watu walimletea watu wengi wenye roho waovu; akawafukuza hao roho kwa kusema neno moja, naye akawaponya wote waliokuwa wakiteseka, 17 ili yatimie maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Isaya: “Yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu na kuyabeba maradhi yetu.”+
18 Yesu alipoona umati umemzunguka, akaagiza wavuke kwenda ng’ambo ya bahari.+ 19 Mwandishi fulani akaja na kumwambia: “Mwalimu, nitakufuata popote utakapoenda.”+ 20 Lakini Yesu akamwambia: “Mbweha wana mapango na ndege wa angani wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali pa kulaza kichwa chake.”+ 21 Kisha mwanafunzi mwingine akamwambia: “Bwana, niruhusu kwanza niende nikamzike baba yangu.”+ 22 Yesu akamwambia: “Endelea kunifuata, waache wafu wawazike wafu wao.”+
23 Alipopanda kwenye mashua, wanafunzi wake wakamfuata.+ 24 Na tazama! dhoruba kubwa ikatokea baharini, hata mawimbi yakaanza kuifunika mashua; lakini Yesu alikuwa amelala usingizi.+ 25 Wakaja na kumwamsha wakisema: “Bwana, tuokoe, tuko karibu kuangamia!” 26 Lakini akawauliza: “Kwa nini mnaogopa sana, ninyi wenye imani ndogo?”+ Kisha akasimama na kuukemea upepo na bahari, kukawa shwari kabisa.+ 27 Basi wanafunzi wakashangaa na kusema: “Huyu ni mtu wa aina gani? Hata upepo na bahari vinamtii.”
28 Alipofika upande ule mwingine na kuingia katika eneo la Wagadarene, alikutana na wanaume wawili waliokuwa na roho waovu wakitoka makaburini.*+ Walikuwa wakali sana, hivi kwamba hakuna mtu aliyekuwa na ujasiri wa kupita katika barabara hiyo. 29 Na tazama! wakapiga mayowe wakisema: “Kwa nini unatusumbua, Mwana wa Mungu?+ Je, umekuja kututesa+ kabla ya wakati uliowekwa?”+ 30 Lakini kule mbali nao kulikuwa na kundi la nguruwe wengi wakila.+ 31 Kwa hiyo wale roho waovu wakaanza kumsihi: “Ukitufukuza, turuhusu tuingie katika lile kundi la nguruwe.”+ 32 Basi akawaambia: “Nendeni!” Ndipo wakatoka na kuingia ndani ya wale nguruwe, na tazama! kundi zima likatimua mbio, likaruka poromoko* likazama baharini na kufa maji. 33 Lakini wachungaji wakakimbia, na walipoingia jijini, wakasimulia mambo yote, kutia ndani habari kuhusu wale watu waliokuwa na roho waovu. 34 Na tazama! watu wote katika jiji hilo wakaenda kukutana na Yesu, na walipomwona, wakamsihi aondoke katika eneo lao.+
9 Basi akapanda mashua, akavuka bahari na kwenda katika jiji lake.+ 2 Na tazama! wakamletea mtu aliyepooza, akiwa amelala kwenye kitanda.* Alipoona imani yao, Yesu akamwambia yule mtu aliyepooza: “Jipe moyo mwanangu! Umesamehewa dhambi zako.”+ 3 Sasa baadhi ya waandishi wakaambiana: “Mtu huyu anakufuru.” 4 Yesu, akijua fikira zao, akasema: “Kwa nini mnawaza mambo maovu katika mioyo yenu?+ 5 Kwa mfano, ni jambo gani rahisi zaidi kusema, ‘Umesamehewa dhambi zako,’ au kusema, ‘Simama utembee’?+ 6 Hata hivyo, ili mjue kwamba Mwana wa binadamu ana mamlaka ya kusamehe dhambi duniani—” kisha akamwambia yule mtu aliyepooza: “Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani.”+ 7 Ndipo akasimama, akaenda nyumbani. 8 Umati ulipoona hivyo ukaogopa, nao wakamtukuza Mungu aliyewapa wanadamu mamlaka ya namna hiyo.
9 Yesu alipokuwa akiondoka mahali hapo akamwona mtu aliyeitwa Mathayo akiwa ameketi kwenye ofisi ya kodi, akamwambia: “Njoo uwe mfuasi wangu.” Mara moja akasimama na kumfuata.+ 10 Baadaye alipokuwa akila* katika nyumba, tazama! wakusanya kodi wengi na watenda dhambi wakaja na kuanza kula* pamoja na Yesu na wanafunzi wake.+ 11 Lakini Mafarisayo walipoona hivyo wakawauliza wanafunzi wake: “Kwa nini mwalimu wenu anakula pamoja na wakusanya kodi na watenda dhambi?”+ 12 Yesu alipowasikia, akasema: “Watu wenye afya hawahitaji daktari, lakini wagonjwa wanamhitaji.+ 13 Nendeni, basi, mkajifunze maana ya maneno haya: ‘Ninataka rehema, si dhabihu.’+ Kwa maana sikuja kuwaita waadilifu, bali watenda dhambi.”
14 Kisha wanafunzi wa Yohana wakaja na kumuuliza: “Kwa nini sisi na Mafarisayo hufunga lakini wanafunzi wako hawafungi?”+ 15 Ndipo Yesu akawaambia: “Rafiki za bwana harusi hawahitaji kuomboleza bwana harusi+ anapokuwa pamoja nao, sivyo? Lakini siku zitakuja ambapo bwana harusi ataondolewa kwao,+ ndipo watakapofunga. 16 Hakuna mtu anayeshona kiraka cha kitambaa kipya juu ya vazi la nje la zamani; kwa maana hicho kitambaa kipya kitatoka kwenye hilo vazi nalo litararuka vibaya zaidi.+ 17 Wala watu hawaweki divai mpya katika viriba vya divai vilivyochakaa. Wakifanya hivyo, viriba hivyo vitapasuka na divai itamwagika navyo viriba vitaharibika. Lakini watu huweka divai mpya katika viriba vipya vya divai, na vitu vyote viwili huhifadhiwa.”
18 Alipokuwa akiwaambia mambo hayo, tazama! mtawala fulani aliyekuwa amekaribia, akaja na kumsujudia* akisema: “Kufikia sasa binti yangu atakuwa amekufa; lakini njoo uweke mkono wako juu yake naye atakuwa hai.”+
19 Ndipo Yesu akasimama, akamfuata pamoja na wanafunzi wake. 20 Na tazama! mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu+ kwa miaka 12 akaja kutoka nyuma na kugusa upindo wa vazi lake la nje,+ 21 kwa maana alikuwa akijiambia: “Nikigusa tu vazi lake la nje, nitapona.” 22 Yesu akageuka, na alipomwona, akamwambia: “Binti, usiogope! Imani yako imekuponya.”+ Na kutoka saa hiyo, yule mwanamke akapona.+
23 Basi alipoingia katika nyumba ya yule mtawala na kuwaona watu waliokuwa wakipiga filimbi na umati uliokuwa na vurugu,+ 24 Yesu akasema: “Ondokeni hapa, kwa maana msichana huyu mdogo hajafa bali amelala usingizi.”+ Ndipo wakaanza kumcheka kwa dharau. 25 Mara tu umati ulipoondolewa, Yesu akaingia na kumshika mkono,+ kisha yule msichana mdogo akainuka.+ 26 Bila shaka, habari hiyo ilienea katika eneo hilo lote.
27 Yesu alipokuwa akitoka huko, wanaume wawili vipofu+ wakamfuata, wakipaza sauti: “Tuhurumie,* Mwana wa Daudi.” 28 Alipoingia ndani ya nyumba, wale wanaume vipofu wakamjia, Yesu akawauliza: “Je, mna imani kwamba ninaweza kufanya hivyo?”+ Wakamjibu: “Ndiyo Bwana.” 29 Kisha akayagusa macho yao,+ akasema: “Na itendeke kwenu kulingana na imani yenu.” 30 Na macho yao yakaanza kuona. Zaidi ya hayo, Yesu akawaonya vikali: “Msimwambie yeyote jambo hili.”+ 31 Lakini walipotoka nje, wakaeneza habari kumhusu katika eneo hilo lote.
32 Walipokuwa wakiondoka, tazama! watu wakamletea bubu aliyekuwa na roho mwovu;+ 33 baada ya yule roho mwovu kufukuzwa, yule bubu akaongea.+ Basi, umati ukashangaa na kusema: “Jambo kama hili halijawahi kuonekana katika Israeli.”+ 34 Lakini Mafarisayo walikuwa wakisema: “Anawafukuza roho waovu kwa nguvu za mtawala wa roho waovu.”+
35 Yesu akaondoka ili kutembelea majiji na vijiji vyote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya Ufalme na kuponya kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.+ 36 Alipoona umati akausikitikia,+ kwa sababu walikuwa wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.+ 37 Ndipo akawaambia wanafunzi wake: “Ndiyo, mavuno ni mengi, lakini wafanyakazi ni wachache.+ 38 Kwa hiyo, mwombeni Bwana wa mavuno awatume wafanyakazi katika mavuno yake.”+
10 Basi akawaita wanafunzi wake 12 na kuwapa mamlaka ya kuwafukuza roho waovu+ na kuponya kila aina ya ugonjwa na kila aina ya udhaifu.
2 Haya ndiyo majina ya wale mitume 12:+ Simoni, aitwaye Petro,+ na Andrea+ ndugu yake; Yakobo na Yohana+ wana wa Zebedayo; 3 Filipo na Bartholomayo;+ Tomasi+ na Mathayo+ mkusanya kodi; Yakobo mwana wa Alfayo; Thadayo; 4 Simoni Mkananayo;* na Yuda Iskariote, ambaye baadaye alimsaliti.+
5 Yesu akawatuma hao 12 na kuwaagiza:+ “Msiende katika barabara ya mataifa, wala msiingie katika jiji lolote la Wasamaria;+ 6 badala yake, nendeni kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.+ 7 Mnapoenda, hubirini mkisema: ‘Ufalme wa mbinguni umekaribia.’+ 8 Ponyeni wagonjwa,+ fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, fukuzeni roho waovu. Mlipokea bure, toeni bure. 9 Msichukue dhahabu, fedha, wala shaba kwenye mishipi yenu ya pesa,+ 10 wala mfuko wa chakula kwa ajili ya safari, wala mavazi mawili,* wala viatu, wala fimbo,+ kwa maana mfanyakazi anastahili chakula chake.+
11 “Mtakapoingia katika jiji au kijiji chochote, tafuteni humo mtu anayestahili, na mkae humo mpaka mtakapoondoka.+ 12 Mnapoingia katika nyumba, wasalimuni watu wa nyumba hiyo. 13 Ikiwa nyumba hiyo inastahili, amani mnayoitakia na iwe juu yake;+ lakini kama haistahili, amani yenu na iwarudie ninyi. 14 Popote pale ambapo mtu hawakaribishi au kusikiliza maneno yenu, mnapotoka katika nyumba hiyo au jiji hilo, kung’uteni mavumbi yaliyo kwenye miguu yenu.+ 15 Kwa kweli ninawaambia, katika Siku ya Hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa Sodoma na Gomora+ kuliko kwa jiji hilo.
16 “Tazama! Ninawatuma kama kondoo katikati ya mbwamwitu; kwa hiyo iweni waangalifu* kama nyoka na wasio na hatia kama njiwa.+ 17 Jihadharini na watu, kwa maana watawapeleka mahakamani+ na kuwapiga mijeledi+ katika masinagogi+ yao. 18 Nanyi mtapelekwa mbele ya magavana na wafalme+ kwa ajili yangu, ili kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.+ 19 Hata hivyo, mtakapopelekwa, msihangaike kuhusu jambo mtakalosema au jinsi mtakavyolisema, kwa sababu mtapewa jambo la kusema katika saa hiyo;+ 20 kwa maana si ninyi tu mnaosema, bali ni roho ya Baba yenu inayosema kupitia ninyi.+ 21 Zaidi ya hayo, mtu atamtoa ndugu yake auawe, na baba atamtoa mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe.+ 22 Nanyi mtachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu,+ lakini yule atakayevumilia* mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.+ 23 Mnapoteswa katika jiji moja, kimbilieni jiji lingine;+ kwa kweli ninawaambia, hamtamaliza kamwe kuzunguka majiji ya Israeli kabla ya Mwana wa binadamu kufika.
24 “Mwanafunzi hamzidi mwalimu wake, wala mtumwa hamzidi bwana wake.+ 25 Inatosha mwanafunzi kuwa kama mwalimu wake, na mtumwa kuwa kama bwana wake.+ Ikiwa watu wamemwita bwana wa nyumba Beelzebuli,*+ namna gani watu wa nyumbani mwake? 26 Basi msiwaogope, kwa maana hakuna jambo lolote lililofunikwa ambalo halitafunuliwa, na hakuna siri yoyote ambayo haitafichuliwa.+ 27 Jambo ninalowaambia gizani, lisemeni nuruni, na jambo mnalosikia likinong’onwa, lihubirini juu ya paa za nyumba.+ 28 Na msiwaogope wale wanaoua mwili lakini hawawezi kuua nafsi;*+ badala yake, mwogopeni yule anayeweza kuangamiza nafsi na mwili katika Gehena.*+ 29 Shore wawili huuzwa kwa sarafu ya thamani ndogo,* sivyo? Lakini hakuna hata mmoja wao atakayeanguka chini bila Baba yenu kujua.+ 30 Lakini hata nywele zote za vichwa vyenu zimehesabiwa. 31 Kwa hiyo msiogope; ninyi ni wenye thamani kuliko shore wengi.+
32 “Basi kila mtu anayenikiri mbele ya watu,+ mimi pia nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni.+ 33 Lakini yeyote anayenikana mbele ya watu, mimi pia nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.+ 34 Msifikiri nilikuja kuleta amani duniani, sikuja kuleta amani, bali upanga.+ 35 Kwa maana nilikuja kuleta mgawanyiko, mtu dhidi ya baba yake, binti dhidi ya mama yake, na binti mkwe dhidi ya mama mkwe wake.+ 36 Kwa kweli, adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake. 37 Yeyote anayempenda baba au mama kuliko anavyonipenda hanistahili; na yeyote anayempenda mwana au binti kuliko anavyonipenda hanistahili.+ 38 Na yeyote asiyechukua mti wake wa mateso* na kunifuata hanistahili.+ 39 Yeyote anayeipata nafsi yake* ataipoteza, na yeyote anayeipoteza nafsi yake* kwa ajili yangu ataipata.+
40 “Yeyote anayewapokea ninyi ananipokea mimi pia, na yeyote anayenipokea mimi anampokea pia Yule aliyenituma.+ 41 Yeyote anayempokea nabii kwa sababu ni nabii atapata thawabu ya nabii,+ na yeyote anayempokea mtu mwadilifu kwa sababu ni mwadilifu atapata thawabu ya mtu mwadilifu. 42 Na yeyote anayempa mmoja wa hawa wadogo kikombe tu cha maji baridi ya kunywa kwa sababu ni mwanafunzi wangu, kwa kweli ninawaambia, hatapoteza kamwe thawabu yake.”+
11 Yesu alipomaliza kuwapa wanafunzi wake 12 maagizo, akaondoka huko na kwenda kufundisha na kuhubiri katika majiji yao.+
2 Lakini Yohana akiwa jela+ alisikia mambo ambayo Kristo alikuwa akifanya, akawatuma wanafunzi wake+ 3 wamuulize: “Je, wewe ndiye Yule Anayekuja, au tumtarajie mwingine?”+ 4 Yesu akawajibu: “Nendeni mkamwambie Yohana mambo mnayosikia na kuona:+ 5 Vipofu wanaona,+ viwete wanatembea, wenye ukoma+ wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema.+ 6 Mwenye furaha ni mtu ambaye hapati ndani yangu sababu ya kukwaza.”+
7 Hao walipoondoka, Yesu akaanza kuuambia umati kumhusu Yohana: “Mlienda nyikani kuona nini?+ Tete likitikiswa na upepo?+ 8 Basi, mlienda kuona nini? Mtu aliyevaa mavazi laini?* Kwa maana wale wanaovaa mavazi laini wamo katika nyumba za wafalme. 9 Basi kwa kweli, kwa nini mlienda? Kumwona nabii? Ndiyo, ninawaambia, mtu aliye zaidi ya nabii.+ 10 Huyu ndiye ambaye imeandikwa hivi kumhusu: ‘Tazama! Ninamtuma mjumbe wangu mbele yako,* ili akutayarishie njia mbele yako!’+ 11 Kwa kweli ninawaambia, kati ya wale waliozaliwa na wanawake hajatokea mtu mkuu kuliko Yohana Mbatizaji, lakini mtu mdogo zaidi katika Ufalme wa mbinguni ni mkuu kuliko yeye.+ 12 Tangu siku za Yohana Mbatizaji mpaka sasa, Ufalme wa mbinguni ndio mradi ambao watu wanajitahidi kuufikia, na wale wanaojitahidi sana wanaupata.+ 13 Kwa maana, maneno yote ya Manabii na Sheria yalitabiri hadi wakati wa Yohana;+ 14 na mkitaka kukubali, yeye ndiye ‘Eliya anayepaswa kuja.’+ 15 Aliye na masikio na asikilize.
16 “Nitakifananisha kizazi hiki na nani?+ Ni kama watoto walioketi sokoni wakiwapazia wenzao sauti, 17 wakisema: ‘Tuliwapigia filimbi, lakini hamkucheza dansi; tuliomboleza, lakini hamkujipiga-piga kwa huzuni.’ 18 Vivyo hivyo, Yohana hakuja akila wala kunywa, lakini watu wanasema, ‘Ana roho mwovu.’ 19 Mwana wa binadamu alikuja akila na kunywa,+ lakini watu wanasema, ‘Tazama! Yeye ni mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai, rafiki ya wakusanya kodi na watenda dhambi.’+ Hata hivyo, hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu* kupitia kazi zake.”*+
20 Kisha Yesu akaanza kuyakemea majiji ambako alifanya matendo mengi yenye nguvu, kwa sababu hawakutubu: 21 “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! kwa sababu kama matendo yenye nguvu yaliyofanywa kwenu yangefanywa huko Tiro na Sidoni, watu wa majiji hayo wangekuwa wametubu zamani katika nguo za magunia na katika majivu.+ 22 Lakini ninawaambia, katika Siku ya Hukumu, itakuwa afadhali zaidi kwa Tiro na Sidoni kuliko kwenu.+ 23 Nawe Kapernaumu,+ je, utainuliwa mpaka mbinguni? Utashuka mpaka Kaburini;*+ kwa sababu kama matendo yenye nguvu yaliyofanywa ndani yako yangefanywa huko Sodoma, jiji hilo lingekuwepo mpaka leo hii. 24 Lakini ninawaambia, katika Siku ya Hukumu itakuwa afadhali zaidi kwa nchi ya Sodoma kuliko kwenu.”+
25 Ndipo Yesu akasema: “Ninakusifu hadharani, Baba, Bwana wa mbingu na dunia, kwa sababu umewaficha mambo haya wenye hekima na wenye elimu nawe umeyafunua kwa watoto wadogo.+ 26 Ndiyo, Ee Baba, kwa sababu umekubali iwe hivyo. 27 Baba yangu amenikabidhi vitu vyote,+ na hakuna mtu anayemjua Mwana kikamili isipokuwa Baba;+ wala hakuna anayemjua Baba kikamili isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.+ 28 Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha. 29 Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni,+ nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu.* 30 Kwa maana nira yangu ni laini,* na mzigo wangu ni mwepesi.”
12 Wakati huo, Yesu alipitia katikati ya mashamba ya nafaka siku ya Sabato. Wanafunzi wake wakahisi njaa wakaanza kukata masuke ya nafaka na kula.+ 2 Mafarisayo walipoona hilo, wakamwambia: “Tazama! Wanafunzi wako wanafanya jambo lisilo halali siku ya Sabato.”+ 3 Yesu akawaambia: “Je, hamjasoma alilofanya Daudi wakati yeye na wanaume waliokuwa pamoja naye walipohisi njaa?+ 4 Jinsi alivyoingia katika nyumba ya Mungu, nao wakala mikate ya toleo,*+ kitu ambacho hakikuwa halali kwake au kwa wale waliokuwa pamoja naye kula, ila makuhani tu?+ 5 Au, je, hamjasoma katika Sheria kwamba siku ya Sabato makuhani huvunja Sabato na wanabaki bila hatia?+ 6 Lakini ninawaambia, hapa pana mtu mkuu kuliko hekalu.+ 7 Hata hivyo, kama mngeelewa maana ya maneno haya, ‘Ninataka rehema+ si dhabihu,’+ hamngewalaumu watu wasio na hatia. 8 Kwa maana Mwana wa binadamu ndiye Bwana wa Sabato.”+
9 Baada ya kutoka hapo, akaingia ndani ya sinagogi lao, 10 na tazama! kulikuwa na mtu aliyepooza mkono!+ Basi, ili wapate sababu ya kumshtaki wakamuuliza, “Je, ni halali kumponya mtu siku ya Sabato?”+ 11 Akawaambia: “Ukiwa na kondoo mmoja, naye kondoo huyo atumbukie shimoni siku ya Sabato, je, kuna yeyote kati yenu ambaye hatamshika na kumtoa humo?+ 12 Kwa kweli, mwanadamu ni mwenye thamani sana kuliko kondoo! Basi ni halali kutenda mema siku ya Sabato.” 13 Kisha akamwambia mtu huyo: “Nyoosha mkono wako.” Akaunyoosha, nao ukawa mzima kama ule mkono mwingine. 14 Lakini Mafarisayo wakaenda nje na kupanga njama ili wamuue. 15 Yesu alipojua jambo hilo, akaondoka hapo. Watu wengi wakamfuata,+ naye akawaponya wote, 16 lakini akawaagiza kwa kusisitiza wasimtangaze,+ 17 ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Isaya:
18 “Tazama! Mtumishi wangu+ niliyemchagua, mpendwa wangu, ambaye nimemkubali!*+ Nitaweka roho yangu juu yake,+ naye atayatangazia mataifa haki. 19 Hatagombana+ wala kupiga kelele, wala yeyote hatasikia sauti yake kwenye barabara kuu. 20 Hataponda tete lililovunjika, wala hatazima utambi unaofifia,+ hadi atakapofanikiwa kuleta haki. 21 Kwa kweli, mataifa yatalitumainia jina lake.”+
22 Kisha wakamletea mwanamume kipofu aliyekuwa bubu kwa sababu alikuwa na roho mwovu, Yesu akamponya, na yule bubu akaanza kuongea na kuona. 23 Basi, umati wote ukashangaa na kusema: “Je, inawezekana kwamba huyu ndiye Mwana wa Daudi?” 24 Mafarisayo waliposikia jambo hilo wakasema: “Mtu huyu anawafukuza roho waovu kwa nguvu za Beelzebuli,* mtawala wa roho waovu.”+ 25 Akijua fikira zao, akawaambia: “Kila ufalme uliogawanyika dhidi yake wenyewe utaangamia, na kila jiji au nyumba iliyogawanyika dhidi yake yenyewe haitasimama. 26 Vivyo hivyo, ikiwa Shetani anamfukuza Shetani, amegawanyika dhidi yake mwenyewe; basi, ufalme wake utawezaje kusimama? 27 Zaidi ya hayo, ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia Beelzebuli, wana wenu wanawafukuza kupitia nani? Hiyo ndiyo sababu watakuwa waamuzi wenu. 28 Lakini ikiwa ninawafukuza roho waovu kupitia roho ya Mungu, kwa kweli Ufalme wa Mungu umewafikia ninyi ghafla.+ 29 Au yeyote anawezaje kuivamia nyumba ya mtu mwenye nguvu na kuchukua mali zake isipokuwa kwanza amfunge mtu huyo? Hapo ndipo anaweza kuipora nyumba yake. 30 Yeyote asiye upande wangu ananipinga, na yeyote asiyekusanya pamoja nami anatawanya.+
31 “Kwa hiyo mimi ninawaambia, watu watasamehewa kila aina ya dhambi na makufuru, lakini yeyote anayekufuru roho takatifu hatasamehewa.+ 32 Kwa mfano, yeyote anayesema neno baya dhidi ya Mwana wa binadamu, atasamehewa;+ lakini yeyote anayesema vibaya dhidi ya roho takatifu, hatasamehewa, hapana, si katika mfumo huu wa mambo* wala ule utakaokuja.+
33 “Ufanyeni mti kuwa mzuri na matunda yake yawe mazuri, au muufanye mti uoze na matunda yake yaoze, kwa maana mti hujulikana kwa matunda yake.+ 34 Uzao wa nyoka,*+ mnawezaje kusema mambo mema, wakati ninyi ni waovu? Kwa maana kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.+ 35 Mtu mwema hutoa mambo mema katika hazina yake njema, lakini mtu mwovu hutoa mambo mabaya katika hazina yake mbovu.+ 36 Ninawaambia kwamba katika Siku ya Hukumu watu watatoa hesabu+ kuhusu kila neno lisilofaa wanalosema; 37 kwa maneno yako utatangazwa kuwa mwadilifu, na kwa maneno yako utahukumiwa.”
38 Ndipo baadhi ya waandishi na Mafarisayo wakamjibu kwa kumwambia: “Mwalimu, tunataka kuona ishara kutoka kwako.”+ 39 Akawajibu: “Kizazi kiovu na chenye uzinzi* kinaendelea kutafuta ishara, lakini hakitapewa ishara yoyote isipokuwa ishara ya nabii Yona.+ 40 Kwa maana kama vile Yona alivyokuwa katika tumbo la samaki mkubwa kwa siku tatu mchana na usiku,+ ndivyo Mwana wa binadamu atakavyokuwa katika moyo wa ardhi siku tatu mchana na usiku.+ 41 Watu wa Ninawi watasimama katika hukumu pamoja na kizazi hiki nao watakihukumu, kwa sababu walitubu Yona alipowahubiria.+ Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Yona.+ 42 Malkia wa kusini atasimamishwa katika hukumu pamoja na kizazi hiki naye atakihukumu, kwa sababu alikuja kutoka miisho ya dunia ili asikie hekima ya Sulemani.+ Lakini tazama! hapa pana mtu mkuu kuliko Sulemani.+
43 “Roho mwovu anapomtoka mtu, yeye hupitia maeneo yasiyo na maji akitafuta mahali pa kupumzika, lakini hapati.+ 44 Kisha anasema, ‘Nitarudi kwenye nyumba yangu niliyoihama’; naye anapofika, anakuta haijakaliwa lakini imefagiwa ikawa safi na kupambwa. 45 Naye huenda na kuwaleta roho wengine saba walio waovu kuliko yeye, na baada ya kuingia ndani, wao hukaa humo; na hali ya mwisho ya mtu huyo huwa mbaya zaidi kuliko ya kwanza.+ Hivyo ndivyo itakavyokuwa pia kwa kizazi hiki kiovu.”
46 Alipokuwa bado akizungumza na umati, mama yake na ndugu zake+ walikuwa wamesimama nje, wakitaka kuongea naye.+ 47 Basi mtu fulani akamwambia: “Tazama! Mama yako na ndugu zako wamesimama nje, wanataka kuongea nawe.” 48 Yesu akamjibu mtu huyo: “Mama yangu ni nani, na ndugu zangu ni nani?” 49 Akinyoosha mkono wake kuelekea wanafunzi wake, akasema: “Tazama! Mama yangu na ndugu zangu!+ 50 Kwa maana yeyote anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyo ndiye ndugu yangu, dada yangu, na mama yangu.”+
13 Siku hiyo Yesu akatoka ndani ya nyumba na kuketi kando ya bahari. 2 Na umati mkubwa sana ukakusanyika karibu naye hivi kwamba akapanda ndani ya mashua na kuketi, na umati wote ulikuwa umesimama ufuoni.+ 3 Ndipo akawaambia mambo mengi kwa kutumia mifano,+ akisema: “Tazama! Mpandaji alienda kupanda mbegu.+ 4 Alipokuwa akipanda, mbegu fulani zikaanguka kando ya barabara, ndege wakaja na kuzila.+ 5 Nyingine zikaanguka kwenye miamba, mahali pasipo na udongo mwingi, na mara moja zikachipuka kwa sababu udongo haukuwa na kina.+ 6 Lakini jua lilipochomoza, ziliungua na kunyauka kwa sababu hazikuwa na mizizi. 7 Nyingine zikaanguka kwenye miiba, nayo miiba ikakua na kuzisonga.+ 8 Mbegu nyingine zikaanguka kwenye udongo mzuri nazo zikaanza kuzaa matunda, nyingine mara 100 zaidi, nyingine 60, na nyingine 30.+ 9 Aliye na masikio na asikilize.”+
10 Basi wanafunzi wakaja na kumuuliza: “Kwa nini unazungumza nao kwa kutumia mifano?”+ 11 Akawajibu: “Ninyi mmepewa uwezo wa kuzielewa siri takatifu+ za Ufalme wa mbinguni, lakini wao hawajapewa. 12 Kwa maana yeyote aliye na kitu ataongezewa, naye atazidishiwa; lakini yeyote asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.+ 13 Ndiyo maana ninazungumza nao kwa kutumia mifano, kwa sababu, wanatazama lakini hawaoni, wanasikiliza lakini hawasikii, wala hawaelewi.+ 14 Na unabii wa Isaya unatimia kwao unaosema: ‘Kwa kweli mtasikia lakini hamtaelewa, nanyi kwa kweli mtatazama lakini hamtaona.+ 15 Kwa maana mioyo ya watu hawa imekuwa migumu, nao wamesikia kwa masikio yao bila kuitikia, nao wamefunga macho yao, ili wasione kamwe kwa macho yao na kusikia kwa masikio yao na kuelewa kwa mioyo yao, kisha wageuke nami niwaponye.’+
16 “Hata hivyo, macho yenu ni yenye furaha kwa sababu yanaona na masikio yenu kwa sababu yanasikia.+ 17 Kwa kweli ninawaambia, manabii wengi na watu waadilifu walitamani kuona mambo mnayoona lakini hawakuyaona,+ na kusikia mambo mnayosikia lakini hawakuyasikia.
18 “Basi, sikilizeni maana ya mfano wa yule mtu aliyepanda mbegu.+ 19 Mtu yeyote anaposikia neno la Ufalme lakini halielewi, yule mwovu+ huja na kunyakua kilichopandwa moyoni mwake; hiyo ndiyo mbegu iliyopandwa kando ya barabara.+ 20 Na mbegu iliyopandwa kwenye miamba, ni yule anayelisikia neno na kulipokea mara moja kwa shangwe.+ 21 Lakini hana mizizi ndani yake bali anaendelea kwa wakati fulani, hata hivyo dhiki au mateso yakitokea kwa sababu ya lile neno mara moja anakwazika. 22 Na mbegu iliyopandwa kwenye miiba, ni yule anayelisikia neno, lakini mahangaiko ya mfumo huu wa mambo*+ na nguvu za udanganyifu za utajiri hulisonga neno, nalo halizai matunda.+ 23 Na mbegu iliyopandwa kwenye udongo mzuri ni wale wanaosikia neno na kulielewa, ambao kwa kweli huzaa matunda, mmoja huzaa mara 100 zaidi, mwingine 60, na mwingine 30.”+
24 Akawatolea mfano mwingine, akisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama mtu aliyepanda mbegu nzuri katika shamba lake. 25 Watu walipokuwa wamelala usingizi, adui yake akaja na kupanda magugu kati ya ngano kisha akaondoka. 26 Ngano ilipoota na kuzaa matunda, magugu pia yalionekana. 27 Kwa hiyo watumwa wa bwana wa nyumba wakaja na kumwambia, ‘Bwana, je, hukupanda mbegu nzuri katika shamba lako? Basi magugu yametoka wapi?’ 28 Akawaambia, ‘Adui, mtu fulani, ndiye aliyefanya hivyo.’+ Watumwa wakamuuliza, ‘Basi, je, unataka twende tukayang’oe?’ 29 Akasema, ‘Hapana, ili mnapong’oa magugu, msije mkang’oa ngano pia. 30 Acheni vikue pamoja mpaka wakati wa mavuno, na katika majira ya mavuno nitawaambia wavunaji: Kusanyeni magugu kwanza na kuyafunga matita-matita ili yateketezwe motoni; kisha mkusanye ngano ghalani mwangu.’”+
31 Akawatolea mfano mwingine akisema: “Ufalme wa mbinguni ni kama mbegu ya haradali ambayo mtu aliichukua na kuipanda katika shamba lake.+ 32 Kwa kweli, mbegu hiyo ni ndogo kuliko mbegu zote, lakini inapokua huwa kubwa kuliko mimea yote ya mboga na huwa mti, hivi kwamba ndege wa angani huja na kupata makao katika matawi yake.”
33 Akawaambia mfano mwingine: “Ufalme wa mbinguni ni kama chachu* ambayo mwanamke aliichukua na kuchanganya na vipimo vikubwa vitatu vya unga, mpaka unga wote ukachacha.”*+
34 Yesu alizungumza mambo hayo yote na umati kwa kutumia mifano. Kwa kweli, hakuwa akizungumza nao bila mfano,+ 35 ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii: “Nitafungua kinywa changu kwa mifano; nitatangaza mambo yaliyofichwa tangu kuwekwa msingi.”*+
36 Baada ya kuuaga umati, akaingia ndani ya nyumba. Wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Tufafanulie ule mfano wa magugu katika shamba.” 37 Akawajibu: “Mpandaji aliyepanda mbegu nzuri ni Mwana wa binadamu; 38 lile shamba ni ulimwengu.+ Nazo mbegu nzuri ni wana wa Ufalme, lakini magugu ni wana wa yule mwovu,+ 39 na adui aliyepanda magugu ni Ibilisi. Mavuno ni umalizio wa mfumo wa mambo,* na wavunaji ni malaika. 40 Kwa hiyo, kama vile magugu hukusanywa na kuteketezwa kwa moto, ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo.*+ 41 Mwana wa binadamu atawatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika Ufalme wake vitu vyote vinavyosababisha kukwazika na watu wenye mazoea ya kuasi sheria, 42 nao watawatupa ndani ya tanuru la moto.+ Humo ndimo watalia na kusaga meno yao. 43 Wakati huo waadilifu watang’aa kwa uangavu kama jua+ katika Ufalme wa Baba yao. Aliye na masikio na asikilize.
44 “Ufalme wa mbinguni ni kama hazina iliyofichwa katika shamba, ambayo mtu fulani aliipata na kuificha; na kwa sababu ya shangwe aliyo nayo, anaenda na kuuza kila kitu alicho nacho na kununua shamba hilo.+
45 “Tena Ufalme wa mbinguni ni kama mfanyabiashara anayesafiri akitafuta lulu nzuri. 46 Alipopata lulu moja yenye thamani kubwa, alienda na mara moja akauza vitu vyote alivyokuwa navyo na kuinunua.+
47 “Tena Ufalme wa mbinguni ni kama wavu wa kukokotwa ulioshushwa baharini, ukavua samaki wa kila aina. 48 Ulipojaa waliuvuta hadi ufuoni, nao wakaketi na kuwaweka samaki wazuri+ ndani ya vyombo, lakini wakawatupa wale wasiofaa.+ 49 Hivyo ndivyo itakavyokuwa katika umalizio wa mfumo wa mambo.* Malaika wataenda kuwatenganisha waovu kutoka kwa waadilifu. 50 Nao watawatupa waovu ndani ya tanuru la moto. Humo ndimo watalia na kusaga meno yao.
51 “Je, mmeelewa mambo hayo yote?” Wakamjibu: “Ndiyo.” 52 Ndipo akawaambia: “Ikiwa ni hivyo, kila mwalimu wa watu wote, anapofundishwa kuhusu Ufalme wa mbinguni ni kama bwana wa nyumba, ambaye hutoa katika hazina yake vitu vipya na pia vya zamani.”
53 Yesu alipomaliza kutoa mifano hiyo akaondoka hapo. 54 Baada ya kuingia katika eneo lake la nyumbani,+ akaanza kuwafundisha katika sinagogi lao, hivi kwamba wakashangaa na kuuliza: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii na matendo haya yenye nguvu?+ 55 Je, huyu si mwana wa yule seremala?+ Je, mama yake haitwi Maria, na ndugu zake Yakobo, Yosefu, Simoni, na Yuda?+ 56 Na dada zake, je, wote hawako pamoja nasi? Basi, alipata wapi mambo haya yote?”+ 57 Kwa hiyo, wakaanza kukwazika kwa sababu yake.+ Lakini Yesu akawaambia: “Nabii anaheshimiwa kila mahali isipokuwa katika eneo lake la nyumbani na katika nyumba yake mwenyewe.”+ 58 Naye hakufanya matendo mengi yenye nguvu huko kwa sababu hawakuwa na imani.
14 Wakati huo Herode, mtawala wa wilaya,* akasikia habari kumhusu Yesu.+ 2 Akawaambia watumishi wake: “Huyu ni Yohana Mbatizaji. Alifufuliwa kutoka kwa wafu na ndiyo sababu anafanya matendo yenye nguvu.”+ 3 Herode* alikuwa amemkamata Yohana akamfunga na kumtia gerezani kwa sababu ya Herodia, mke wa Filipo ndugu yake.+ 4 Kwa maana Yohana alikuwa akimwambia: “Si halali kwako kuwa na mwanamke huyo.”+ 5 Hata hivyo, ingawa Herode alitaka kumuua, aliuogopa umati, kwa sababu walimwona kuwa nabii.+ 6 Lakini wakati wa sherehe ya sikukuu ya kuzaliwa kwa Herode,+ binti ya Herodia alicheza dansi na kumfurahisha sana Herode+ 7 hivi kwamba akaahidi kwa kiapo kumpa chochote ambacho angeomba. 8 Ndipo yule binti, akichochewa na mama yake, akasema: “Nipe kwenye sinia kichwa cha Yohana Mbatizaji.”+ 9 Mfalme akahuzunika, lakini kwa sababu ya viapo alivyotoa mbele ya wageni* wake, akaamuru apewe kichwa hicho. 10 Basi akawatuma watu gerezani, nao wakamkata Yohana kichwa. 11 Kichwa chake kikaletwa kwenye sinia akapewa yule msichana, naye akampelekea mama yake. 12 Baadaye wanafunzi wake wakaja wakaondoa maiti hiyo na kuizika, kisha wakaenda kumjulisha Yesu. 13 Yesu aliposikia hilo, akaondoka hapo kwa mashua, akaenda mahali pasipo na watu ili awe peke yake. Lakini umati ulipopata habari, ukamfuata kwa miguu kutoka katika majiji.+
14 Alipofika ufuoni, akaona umati mkubwa, akawasikitikia+ na kuwaponya wagonjwa wao.+ 15 Lakini ilipofika jioni, wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mahali hapa hapana watu na muda umesonga sana; uambie umati uondoke, waende vijijini wakajinunulie chakula.”+ 16 Hata hivyo, Yesu akawaambia: “Si lazima waondoke; ninyi wapeni chakula.” 17 Wakamwambia: “Hatuna kitu hapa isipokuwa mikate mitano na samaki wawili tu.” 18 Akasema: “Nileteeni hapa.” 19 Akauagiza umati uketi kwenye nyasi. Kisha akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama mbinguni, akatoa baraka+ na baada ya kuimega mikate, akawapa wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia umati. 20 Basi wote wakala wakashiba, nao wakakusanya vipande vilivyobaki, wakajaza vikapu 12.+ 21 Sasa wale waliokula walikuwa wanaume karibu 5,000, na pia wanawake na watoto wadogo.+ 22 Kisha, bila kukawia, akawaagiza wanafunzi wake wapande mashua na kumtangulia kwenda ng’ambo ya bahari, huku yeye akiuaga umati.+
23 Baada ya kuuaga umati, akapanda mlimani akiwa peke yake ili kusali.+ Ilipofika jioni, alikuwa peke yake huko. 24 Kufikia sasa mashua ilikuwa mamia ya mita* kutoka kwenye nchi kavu, ikitaabishwa na mawimbi kwa sababu upepo ulikuwa ukivuma kinyume chao. 25 Lakini katika kesha la nne la usiku* akawajia, akitembea juu ya bahari. 26 Wanafunzi walipomwona akitembea juu ya bahari, wakahangaika na kusema: “Ni mzuka!” Wakapaza sauti kwa hofu. 27 Lakini mara moja Yesu akawaambia: “Jipeni moyo! Ni mimi; msiogope.”+ 28 Petro akamjibu: “Bwana, ikiwa ni wewe, niamuru nije kwako nikitembea juu ya maji.” 29 Akamwambia: “Njoo!” Ndipo Petro akatoka kwenye mashua, akatembea juu ya maji kumwelekea Yesu. 30 Lakini alipoitazama ile dhoruba ya upepo akaogopa. Alipoanza kuzama, akapaza sauti: “Bwana, niokoe!” 31 Mara moja Yesu akaunyoosha mkono wake, akamshika na kumwambia: “Wewe mwenye imani ndogo, kwa nini umekuwa na shaka?”+ 32 Walipopanda kwenye mashua, ile dhoruba ikatulia. 33 Ndipo wale waliokuwa ndani ya mashua wakamsujudia* wakisema: “Kwa kweli wewe ni Mwana wa Mungu.” 34 Basi wakavuka na kufika kwenye nchi kavu huko Genesareti.+
35 Watu wa huko walipomtambua, wakaeneza habari katika maeneo yote yaliyokuwa karibu, basi watu wakamletea wagonjwa wote. 36 Nao wakamsihi awaruhusu waguse tu upindo wa vazi lake la nje,+ na wote waliougusa wakaponywa kabisa.
15 Ndipo Mafarisayo na waandishi kutoka Yerusalemu wakamjia Yesu+ wakisema: 2 “Kwa nini wanafunzi wako huvunja mapokeo ya mababu zetu? Kwa mfano, hawanawi* mikono kabla ya kula.”+
3 Akawajibu: “Kwa nini ninyi pia huvunja amri ya Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu?+ 4 Kwa mfano, Mungu alisema, ‘Mheshimu baba yako na mama yako,’+ na, ‘Yeyote anayemtukana* baba yake au mama yake anapaswa kuuawa.’+ 5 Lakini ninyi mnasema, ‘Yeyote anayemwambia baba yake au mama yake: “Chochote nilicho nacho ambacho kingekusaidia ni zawadi iliyowekwa wakfu kwa Mungu,”+ 6 anakosa kabisa kumheshimu baba yake.’ Kwa hiyo, mmelibatilisha neno la Mungu kwa sababu ya mapokeo yenu.+ 7 Ninyi wanafiki, kwa kufaa Isaya alitabiri kuwahusu aliposema:+ 8 ‘Watu hawa huniheshimu kwa midomo yao, lakini mioyo yao iko mbali nami. 9 Wao huniabudu bure, kwa maana wanafundisha amri za wanadamu kuwa mafundisho.’”+ 10 Ndipo akauita umati ukaribie na kuwaambia: “Sikilizeni na kuelewa maneno haya:+ 11 Mtu hachafuliwi na kile kinachoingia kinywani mwake, bali huchafuliwa na kile kinachotoka kinywani mwake.”+
12 Ndipo wanafunzi wakaja na kumwambia: “Unajua kwamba Mafarisayo walikwazika waliposikia mambo uliyosema?”+ 13 Akawajibu: “Kila mmea ambao Baba yangu wa mbinguni hakuupanda utang’olewa. 14 Waacheni. Wao ni viongozi vipofu. Basi, kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili watatumbukia ndani ya shimo.”+ 15 Petro akamwambia: “Tufafanulie mfano huo.” 16 Ndipo akasema: “Je, ninyi pia bado hamwelewi?+ 17 Je, hamjui kwamba chochote kinachoingia kinywani hupita tumboni kisha hutoka na kuingia chooni? 18 Hata hivyo, mambo yanayotoka kinywani hutoka moyoni, nayo ndiyo yanayomchafua mtu.+ 19 Kwa mfano, moyoni hutoka mawazo mabaya,+ mauaji, uzinzi, uasherati,* wizi, ushahidi wa uwongo, na makufuru. 20 Hayo ndiyo mambo yanayomchafua mtu; lakini kula bila kunawa* mikono hakumchafui mtu.”
21 Yesu akatoka hapo na kwenda katika eneo la Tiro na Sidoni.+ 22 Na tazama! mwanamke fulani Mfoinike kutoka eneo hilo akamjia, akapaza sauti: “Nihurumie,* Bwana, Mwana wa Daudi. Binti yangu anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.”+ 23 Lakini Yesu hakumjibu mwanamke huyo. Kwa hiyo wanafunzi wake wakaja na kumwambia: “Mwambie aende, kwa sababu anaendelea kutufuata akipaza sauti.” 24 Yesu akajibu: “Sikutumwa kwa yeyote isipokuwa kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.”+ 25 Lakini mwanamke huyo akaja na kumsujudia* akisema: “Bwana, nisaidie!” 26 Yesu akamjibu: “Haifai kuuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.” 27 Mwanamke huyo akasema: “Ndiyo Bwana, lakini hata hao mbwa wadogo hula makombo yanayoanguka kutoka kwenye meza ya mabwana wao.”+ 28 Ndipo Yesu akamwambia: “Ewe mwanamke, imani yako ni kubwa; na itendeke kama unavyotaka.” Na kuanzia saa hiyo binti yake akapona.
29 Yesu akaondoka hapo na kwenda karibu na Bahari ya Galilaya,+ kisha akapanda mlimani, akaketi huko. 30 Ndipo umati mkubwa ukamjia, na kuwaleta watu waliokuwa viwete, vilema, vipofu, mabubu, na wengine wengi, nao wakawaweka miguuni pake, naye akawaponya.+ 31 Basi umati ukashangaa ulipoona mabubu wakiongea, vilema wakiponywa, viwete wakitembea, na vipofu wakiona, nao wakamsifu Mungu wa Israeli.+
32 Lakini Yesu akawaita wanafunzi wake na kuwaambia: “Ninausikitikia umati,+ kwa sababu tayari wamekaa pamoja nami siku tatu nao hawajala chochote. Sitaki kuwaacha waende wakiwa na njaa,* wasije wakazimia njiani.”+ 33 Hata hivyo, wanafunzi wakamwambia: “Tutapata wapi mikate ya kutosha kuushibisha umati huu mkubwa mahali hapa pasipo na watu?”+ 34 Ndipo Yesu akawauliza: “Mna mikate mingapi?” Wakajibu: “Saba, na samaki wachache wadogo.” 35 Kwa hiyo, baada ya kuuagiza umati uketi chini, 36 akachukua ile mikate saba na wale samaki, na baada ya kutoa shukrani, akamega na kuanza kuwagawia wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia umati.+ 37 Na wote wakala wakashiba, kisha wakakusanya vipande vilivyobaki, wakajaza vikapu saba vikubwa.+ 38 Sasa wale waliokula walikuwa wanaume 4,000, na pia wanawake na watoto wadogo. 39 Mwishowe, baada ya kuuaga umati, akaingia kwenye mashua na kwenda katika eneo la Magadani.+
16 Mafarisayo na Masadukayo wakamjia Yesu, na ili kumjaribu wakamwomba awaonyeshe ishara kutoka mbinguni.+ 2 Akawajibu: “Inapofika jioni ninyi husema, ‘Hali ya hewa itakuwa nzuri kwa maana anga ni jekundu,’ 3 na asubuhi mnasema: ‘Leo kutakuwa na baridi kali na mvua, kwa maana anga ni jekundu na lina mawingu mazito.’ Mnajua jinsi ya kufafanua hali ya anga, lakini hamwezi kufafanua ishara za nyakati. 4 Kizazi kiovu na chenye uzinzi* kinaendelea kutafuta ishara, lakini hakitapewa ishara yoyote+ isipokuwa ishara ya Yona.”+ Ndipo akawaacha, akaenda zake.
5 Sasa wanafunzi wakavuka kwenda ng’ambo ya bahari lakini wakasahau kuchukua mikate.+ 6 Yesu akawaambia: “Muwe macho na mjihadhari na chachu ya Mafarisayo na Masadukayo.”+ 7 Basi wakaanza kujadiliana, wakisema: “Hatukubeba mikate yoyote.” 8 Akijua hilo, Yesu akawauliza: “Ninyi wenye imani ndogo, kwa nini mnajadiliana kati yenu kuhusu kutokuwa na mikate? 9 Je, bado hamwelewi, au je, hamkumbuki ile mikate mitano kuhusiana na wale watu 5,000, na ni vikapu vingapi mlivyokusanya?+ 10 Au ile mikate saba kuhusiana na wale watu 4,000 na ni vikapu vingapi vikubwa mlivyokusanya?+ 11 Kwa nini hamwelewi kwamba sikuongea nanyi kuhusu mikate? Bali jihadharini na chachu* ya Mafarisayo na Masadukayo.”+ 12 Ndipo wakaelewa kwamba hakuwa akizungumza kuhusu chachu ya mikate, bali kujihadhari na mafundisho ya Mafarisayo na Masadukayo.
13 Alipofika katika eneo la Kaisaria Filipi, Yesu akawauliza wanafunzi wake: “Watu wanasema Mwana wa binadamu ni nani?”+ 14 Wakajibu: “Baadhi yao husema Yohana Mbatizaji,+ wengine Eliya,+ na bado wengine Yeremia au mmoja wa manabii.” 15 Akawauliza: “Hata hivyo, ninyi mnasema mimi ni nani?” 16 Simoni Petro akajibu: “Wewe ndiye Kristo,+ Mwana wa Mungu aliye hai.”+ 17 Yesu akamwambia: “Mwenye furaha ni wewe, Simoni mwana wa Yona, kwa sababu mwili na damu havikukufunulia* hilo, bali Baba yangu aliye mbinguni ndiye aliyekufunulia.+ 18 Pia, ninakuambia: Wewe ni Petro,+ na juu ya mwamba+ huu nitajenga kutaniko langu, na malango ya Kaburi* hayatalishinda. 19 Nitakupa funguo za Ufalme wa mbinguni, na lolote utakalofunga duniani tayari litakuwa limefungwa mbinguni, na lolote utakalofungua duniani tayari litakuwa limefunguliwa mbinguni.” 20 Ndipo akawaagiza wanafunzi kwa kusisitiza wasimwambie yeyote kwamba yeye ndiye Kristo.+
21 Tangu wakati huo, Yesu akaanza kuwafafanulia wanafunzi wake kwamba ni lazima aende Yerusalemu na kuteswa sana na wazee, wakuu wa makuhani, na waandishi, kisha atauawa, na siku ya tatu afufuliwe.+ 22 Ndipo Petro akampeleka kando na kuanza kumkemea, akisema: “Bwana jihurumie;* hutapatwa kamwe na mambo hayo.”+ 23 Lakini Yesu akamgeuzia mgongo, akamwambia Petro: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.”+
24 Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso* na aendelee kunifuata.+ 25 Kwa maana yeyote anayetaka kuuokoa uhai wake* ataupoteza, lakini yeyote anayeupoteza uhai wake* kwa ajili yangu ataupata.+ 26 Kwa kweli mtu atapata faida gani akiupata ulimwengu wote lakini apoteze uhai wake?*+ Au mtu atatoa nini ili abadilishane na uhai wake?*+ 27 Kwa maana Mwana wa binadamu atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika zake, kisha atamlipa kila mtu kulingana na mwenendo wake.+ 28 Kwa kweli ninawaambia kwamba kuna baadhi ya wale waliosimama hapa ambao hawataonja kifo kamwe kabla ya kumwona Mwana wa binadamu akija katika Ufalme wake.”+
17 Siku sita baadaye, Yesu alienda pamoja na Petro, Yakobo na Yohana ndugu yake kwenye mlima mrefu wakiwa peke yao.+ 2 Sura yake ikageuka mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, na mavazi yake ya nje yakang’aa* kama nuru.+ 3 Tazama! wakaona Musa na Eliya wakizungumza na Yesu. 4 Ndipo Petro akamwambia Yesu: “Bwana, ni vizuri sisi tuwe hapa. Ukitaka, nitasimamisha mahema matatu hapa, moja lako, moja la Musa, na moja la Eliya.” 5 Alipokuwa bado akizungumza, tazama! wingu jangavu likawafunika, na tazama! sauti kutoka katika lile wingu ikasema: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.+ Msikilizeni.”+ 6 Wanafunzi waliposikia hilo wakaanguka kifudifudi, wakaogopa sana. 7 Ndipo Yesu akawakaribia, akawagusa na kuwaambia: “Simameni. Msiogope.” 8 Walipotazama juu, hawakumwona mtu yeyote ila Yesu tu. 9 Walipokuwa wakishuka kutoka mlimani, Yesu akawaamuru: “Msimwambie mtu yeyote maono hayo mpaka Mwana wa binadamu atakapofufuliwa kutoka kwa wafu.”+
10 Hata hivyo, wanafunzi wakamuuliza: “Kwa nini basi waandishi husema kwamba lazima Eliya aje kwanza?”+ 11 Akawajibu: “Kwa kweli Eliya anakuja naye atarudisha mambo yote.+ 12 Hata hivyo, ninawaambia kwamba tayari Eliya amekuja lakini hawakumtambua bali walimtendea kama walivyotaka.+ Vivyo hivyo, Mwana wa binadamu atateseka mikononi mwao.”+ 13 Ndipo wanafunzi wakatambua kwamba alikuwa akiwaeleza kumhusu Yohana Mbatizaji.
14 Walipofika karibu na umati,+ mtu fulani akamkaribia Yesu, akapiga magoti, na kusema: 15 “Bwana, mhurumie* mwanangu, kwa sababu ana kifafa na ni mgonjwa sana. Yeye huanguka ndani ya moto na ndani ya maji mara nyingi.+ 16 Nilimleta kwa wanafunzi wako, lakini walishindwa kumponya.” 17 Yesu akajibu: “Enyi kizazi kisicho na imani na kilichopotoka,+ nitaendelea kuwa pamoja nanyi mpaka lini? Nitawavumilia mpaka lini? Mleteni hapa.” 18 Kisha Yesu akamkemea yule roho mwovu, naye akamtoka, na yule mvulana akapona kuanzia saa hiyo.+ 19 Ndipo wanafunzi wakamjia Yesu faraghani na kumuuliza: “Kwa nini tulishindwa kumfukuza?” 20 Akawaambia: “Ni kwa sababu ya imani yenu ndogo. Kwa kweli ninawaambia, mkiwa na imani inayolingana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.”+ 21* ——
22 Walipokuwa wamekusanyika huko Galilaya, Yesu akawaambia: “Mwana wa binadamu atasalitiwa mikononi mwa watu,+ 23 nao watamuua, na siku ya tatu atafufuliwa.”+ Kwa hiyo wakahuzunika sana.
24 Baada ya kufika Kapernaumu watu wanaokusanya kodi ya drakma* mbili wakaja na kumuuliza Petro: “Je, mwalimu wenu hulipa kodi ya drakma mbili?”+ 25 Akajibu: “Ndiyo.” Hata hivyo, mara tu alipoingia ndani ya nyumba Yesu akamuuliza: “Unaonaje Simoni? Wafalme wa dunia hupokea ushuru au kodi* kutoka kwa nani? Kutoka kwa wana wao au kutoka kwa wageni?” 26 Alipojibu: “Kutoka kwa wageni,” Yesu akamwambia: “Basi, kwa kweli wana hawalipi kodi. 27 Lakini ili tusiwakwaze,+ nenda baharini utupe ndoano na uchukue samaki wa kwanza atakayetokea, na utakapofungua kinywa chake, utapata sarafu ya fedha.* Ichukue nawe uwape kwa ajili yangu na kwa ajili yako.”
18 Katika saa hiyo wanafunzi wakamkaribia Yesu na kumuuliza: “Kwa kweli ni nani aliye mkuu zaidi katika Ufalme wa mbinguni?”+ 2 Basi akamwita mtoto mdogo, akamsimamisha katikati yao 3 na kusema: “Kwa kweli ninawaambia, msipogeuka* na kuwa kama watoto wadogo,+ hamtaingia kamwe katika Ufalme wa mbinguni.+ 4 Kwa hiyo, yeyote atakayejinyenyekeza kama mtoto huyu mdogo ndiye mkuu zaidi katika Ufalme wa mbinguni;+ 5 na yeyote anayempokea mtoto mdogo kama huyu kwa msingi wa jina langu ananipokea mimi pia. 6 Lakini yeyote anayemkwaza mmoja wa hawa wadogo wanaoniamini, ingekuwa afadhali afungiwe shingoni jiwe la kusagia ambalo huzungushwa na punda, kisha azamishwe baharini.+
7 “Ole kwa ulimwengu kwa sababu ya vikwazo! Bila shaka, lazima vikwazo vije, lakini ole wake mtu ambaye kikwazo kitakuja kupitia kwake! 8 Basi, ikiwa mkono wako au mguu wako unakufanya ukwazike, ukate na kuutupa mbali nawe.+ Ni afadhali uingie katika uzima ukiwa kilema au kiwete kuliko kutupwa ndani ya moto wa milele ukiwa na mikono miwili au miguu miwili.+ 9 Pia, ikiwa jicho lako linakufanya ukwazike, ling’oe na kulitupa mbali nawe. Afadhali uingie katika uzima ukiwa na jicho moja kuliko kutupwa katika Gehena* ya moto ukiwa na macho mawili.+ 10 Angalieni msimdharau mmoja wa hawa wadogo, kwa maana ninawaambia kwamba malaika zao mbinguni sikuzote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni.+ 11* ——
12 “Mnaonaje? Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee,+ je, hatawaacha wale 99 mlimani na kwenda kumtafuta yule aliyepotea?+ 13 Naye akimpata, hakika ninawaambia, yeye humshangilia huyo kuliko wale 99 ambao hawakupotea. 14 Vivyo hivyo, Baba yangu* aliye mbinguni hapendi hata mmoja wa hawa wadogo aangamie.+
15 “Zaidi ya hayo, ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake* kati yako na yeye peke yenu.+ Akikusikiliza, umempata ndugu yako.+ 16 Lakini asipokusikiliza, nenda pamoja na mtu mmoja au wawili, ili kwa ushahidi wa* mashahidi wawili au watatu kila jambo lithibitishwe.+ 17 Asipowasikiliza hao, liambie kutaniko. Asipolisikiliza kutaniko pia, na awe kwako kama mtu wa mataifa+ na kama mkusanya kodi.+
18 “Kwa kweli ninawaambia, mambo yoyote mtakayofunga duniani tayari yatakuwa yamefungwa mbinguni, na mambo yoyote mtakayofungua duniani tayari yatakuwa yamefunguliwa mbinguni. 19 Tena kwa kweli ninawaambia, wawili kati yenu duniani wakikubaliana kuomba jambo lolote muhimu, litatendeka kwa ajili yao kwa sababu ya Baba yangu aliye mbinguni.+ 20 Kwa maana mahali wanapokusanyika wawili au watatu katika jina langu,+ nipo hapo kati yao.”
21 Ndipo Petro akaja na kumuuliza: “Bwana, ndugu yangu atanitendea dhambi mara ngapi nami nimsamehe? Mpaka mara saba?” 22 Yesu akamwambia: “Ninakuambia, si mpaka mara saba, bali mpaka mara 77.+
23 “Ndiyo sababu Ufalme wa mbinguni ni kama mfalme aliyetaka kufanya hesabu pamoja na watumwa wake. 24 Alipoanza kufanya hesabu, akaletewa mtu aliyekuwa na deni lake la talanta 10,000.* 25 Lakini kwa sababu hakuwa na uwezo wa kulipa, bwana wake akaamuru wamuuze mtumwa huyo, mke wake, watoto wake, na mali zake zote ili kulipa deni.+ 26 Ndipo mtumwa huyo akaanguka chini na kumsujudia,* akisema, ‘Naomba univumilie, nitakulipa kila kitu.’ 27 Bwana wake akamsikitikia mtumwa huyo, akamwachilia na kulifuta deni lake.+ 28 Lakini mtumwa huyo alipotoka akamkuta mmoja wa watumwa wenzake aliyekuwa na deni lake la dinari* 100, akamshika na kumkaba koo, akisema, ‘Nilipe ninachokudai.’ 29 Basi mtumwa mwenzake akaanguka chini na kuanza kumsihi, ‘Naomba univumilie, nami nitakulipa.’ 30 Hata hivyo, akakataa, akaenda na kuagiza atupwe gerezani mpaka alipe deni lake. 31 Watumwa wenzake walipoona jambo hilo, wakahuzunika sana, wakaenda kumweleza bwana wao mambo yote yaliyokuwa yametendeka. 32 Ndipo bwana wake akamwita na kumwambia: ‘Mtumwa mwovu, nilifuta deni lako lote uliponisihi. 33 Je, hukupaswa pia kumwonyesha rehema mtumwa mwenzako kama nilivyokuonyesha rehema?’+ 34 Ndipo bwana wake akiwa amekasirika sana, akamkabidhi kwa walinzi wa jela mpaka alipe deni lake lote. 35 Baba yangu wa mbinguni atawatendea ninyi vivyo hivyo+ ikiwa kila mmoja wenu hatamsamehe ndugu yake kutoka moyoni.”+
19 Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, akaondoka Galilaya na kwenda kwenye mipaka ya* Yudea ng’ambo ya Yordani.+ 2 Pia, umati mkubwa ukamfuata, naye akawaponya huko.
3 Mafarisayo wakaja wakikusudia kumjaribu Yesu, wakamuuliza: “Je, ni halali mwanamume kumtaliki mke wake kwa sababu yoyote ile?”+ 4 Akawajibu: “Je, hamkusoma kwamba yule aliyewaumba tangu mwanzo aliwaumba mwanamume na mwanamke+ 5 na kusema: ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’?+ 6 Basi wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”+ 7 Wakamuuliza: “Basi, kwa nini Musa aliagiza kutoa cheti cha kumfukuza na kumtaliki?”+ 8 Akawajibu: “Musa aliwaruhusu kuwataliki wake zenu kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu,+ lakini haikuwa hivyo tangu mwanzo.+ 9 Ninawaambia kwamba mtu yeyote anayemtaliki mke wake isipokuwa kwa sababu ya uasherati,* na kumwoa mwingine, anafanya uzinzi.”+
10 Wanafunzi wakamwambia: “Ikiwa hali iko hivyo kati ya mtu na mke wake, ni afadhali mtu asioe.” 11 Yesu akawaambia: “Si watu wote wanaolipa nafasi jambo hilo, ila tu wale walio na zawadi.+ 12 Kwa maana kuna wale waliozaliwa wakiwa matowashi, wengine wamefanywa matowashi na watu, na wengine wamejifanya wenyewe kuwa matowashi kwa ajili ya Ufalme wa mbinguni. Yule anayeweza kulipa nafasi jambo hilo na afanye hivyo.”+
13 Ndipo watu wakamletea watoto wadogo ili aweke mikono yake juu yao na kusali, lakini wanafunzi wakawakemea.+ 14 Hata hivyo, Yesu akawaambia: “Waacheni watoto wadogo waje kwangu, na msijaribu kuwazuia, kwa maana Ufalme wa mbinguni ni wa wale walio kama wao.”+ 15 Naye akaweka mikono yake juu yao kisha akaondoka hapo.
16 Sasa tazama! mtu fulani akamjia na kumuuliza: “Mwalimu, ninapaswa kufanya mambo gani mema ili nipate uzima wa milele?”+ 17 Yesu akamwambia: “Kwa nini unaniuliza kuhusu mambo mema? Kuna Mmoja tu aliye mwema.+ Hata hivyo, ikiwa unataka kuingia katika uzima, zishike amri sikuzote.”+ 18 Akamuuliza: “Amri gani?” Yesu akajibu: “Usiue,+ usifanye uzinzi,+ usiibe,+ usitoe ushahidi wa uwongo,+ 19 mheshimu baba yako na mama yako,+ na lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”+ 20 Yule mwanamume kijana akamwambia: “Nimeyashika yote hayo; nifanye nini zaidi?” 21 Yesu akamwambia: “Ikiwa unataka kuwa mkamilifu,* nenda ukauze mali zako na uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni;+ kisha uje uwe mfuasi wangu.”+ 22 Yule mwanamume kijana aliposikia hivyo, akaenda zake akiwa na huzuni, kwa maana alikuwa na mali nyingi.+ 23 Ndipo Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Kwa kweli ninawaambia, itakuwa vigumu kwa tajiri kuingia katika Ufalme wa mbinguni.+ 24 Tena ninawaambia, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.”+
25 Wanafunzi waliposikia hilo, wakashangaa sana na kumuuliza: “Ni nani kwa kweli anayeweza kuokolewa?”+ 26 Yesu akawatazama kwa makini na kusema: “Kwa wanadamu jambo hilo haliwezekani, lakini kwa Mungu mambo yote yanawezekana.”+
27 Ndipo Petro akamwambia: “Tazama! Tumeacha kila kitu na kukufuata; basi tutapata nini?”+ 28 Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia, katika uumbaji mpya, Mwana wa binadamu atakapoketi katika kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi katika viti vya ufalme 12, mkiyahukumu makabila 12 ya Israeli.+ 29 Na kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara 100 zaidi, naye ataurithi uzima wa milele.+
30 “Lakini wengi walio wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.+
20 “Kwa maana Ufalme wa mbinguni ni kama bwana mwenye nyumba aliyetoka asubuhi na mapema kwenda kuajiri wafanyakazi kwa ajili ya shamba lake la mizabibu.+ 2 Baada ya kukubaliana na wafanyakazi hao awalipe dinari* moja kwa siku, akawatuma katika shamba lake la mizabibu. 3 Akatoka pia karibu saa tatu,* akaona wengine wamesimama sokoni bila kazi; 4 akawaambia, ‘Ninyi pia, nendeni katika shamba la mizabibu, nami nitawalipa haki yenu.’ 5 Basi wakaenda. Tena akatoka karibu saa sita* na saa tisa* na kufanya vivyo hivyo. 6 Mwishowe, akatoka karibu saa kumi na moja,* akakuta wengine wakiwa wamesimama tu, naye akawauliza, ‘Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi?’ 7 Wakamjibu, ‘Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri.’ Akawaambia, ‘Ninyi pia nendeni katika shamba la mizabibu.’
8 “Ilipofika jioni, mwenye shamba la mizabibu akamwambia msimamizi wake, ‘Waite wafanyakazi uwalipe mshahara wao,+ ukianza na wa mwisho na kumalizia na wa kwanza.’ 9 Wale watu wa saa 11 walipokuja, wakapokea kila mmoja dinari* moja. 10 Basi, wale wa kwanza walipokuja, walidhani wangepokea zaidi; lakini wao pia wakalipwa dinari* moja. 11 Walipoipokea wakaanza kumlalamikia bwana mwenye nyumba 12 na kusema, ‘Watu hawa wa mwisho walifanya kazi kwa saa moja tu; na bado umewalipa sawa na sisi tuliofanya kazi ngumu mchana kutwa kwenye jua kali!’ 13 Lakini akamjibu mmoja wao, akasema, ‘Mwenzangu, sijakukosea. Tulikubaliana dinari* moja, sivyo?+ 14 Chukua mshahara wako uende. Ninataka kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe. 15 Je, sina haki ya kufanya kile ninachotaka na vitu vyangu? Au jicho lako lina wivu* kwa sababu mimi ni mwema?’*+ 16 Vivyo hivyo, wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho.”+
17 Alipokuwa akipanda kwenda Yerusalemu, Yesu akawaita faraghani wale wanafunzi 12 na kuwaambia wakiwa barabarani:+ 18 “Tazama! Tunapanda kwenda Yerusalemu, na Mwana wa binadamu atatiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani na waandishi. Nao watamhukumia kifo+ 19 na kumtia mikononi mwa watu wa mataifa ili wamdhihaki, wampige mijeledi, na kumuua kwenye mti;+ na siku ya tatu atafufuliwa.”+
20 Ndipo mama ya wana wa Zebedayo+ akamjia akiwa na wanawe, akamsujudia* na kumwomba jambo fulani.+ 21 Yesu akamuuliza: “Unataka nini?” Akamjibu: “Toa agizo kwamba hawa wanangu wawili waketi mmoja upande wako wa kuume na mwingine upande wako wa kushoto, katika Ufalme wako.”+ 22 Yesu akajibu: “Hamjui kile mnachoomba. Je, mnaweza kunywa kikombe ambacho niko karibu kukinywa?”+ Wakamwambia: “Tunaweza.” 23 Akawaambia: “Kwa kweli mtakunywa kikombe changu,+ lakini kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto si haki yangu kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.”+
24 Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawakasirikia hao ndugu wawili.+ 25 Lakini Yesu akawaita, akawaambia: “Mnajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na wakuu hutumia mamlaka juu yao.+ 26 Haipaswi kuwa hivyo kati yenu;+ bali yeyote anayetaka kuwa mkubwa kati yenu lazima awe mhudumu wenu,+ 27 na yeyote anayetaka kuwa wa kwanza kati yenu lazima awe mtumwa wenu.+ 28 Kama vile Mwana wa binadamu alivyokuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu+ na kutoa uhai wake* uwe fidia badala ya wengi.”+
29 Walipokuwa wakitoka Yeriko umati mkubwa ukamfuata. 30 Na tazama! wanaume wawili vipofu waliokuwa wameketi kando ya barabara waliposikia kwamba Yesu anapitia hapo, wakapaza sauti: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”*+ 31 Hata hivyo, umati ukawakemea na kuwaambia wanyamaze; lakini wakapaza sauti hata zaidi, wakisema: “Bwana, Mwana wa Daudi, tuhurumie!”* 32 Basi Yesu akasimama, akawaita na kuwauliza: “Mnataka niwafanyie nini?” 33 Wakamjibu: “Bwana, tunaomba macho yetu yafunguliwe.” 34 Yesu akawasikitikia, akayagusa macho yao,+ na mara moja wakaanza kuona, nao wakamfuata.
21 Walipokaribia Yerusalemu na kufika Bethfage kwenye Mlima wa Mizeituni, Yesu akawatuma wanafunzi wawili,+ 2 akawaambia: “Nendeni katika kijiji mtakachokiona, na mara moja mtamwona punda amefungwa, na mwanapunda akiwa pamoja naye. Wafungueni na kuniletea. 3 Mtu yeyote akiwauliza, semeni, ‘Bwana anawahitaji.’ Na mara moja atawaruhusu mwachukue.”
4 Kwa kweli hilo lilitukia ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii: 5 “Mwambieni binti ya Sayuni, ‘Tazama! Mfalme wako anakuja kwako,+ naye ni mpole+ na amepanda juu ya punda, naam, juu ya mwanapunda, uzao wa mnyama wa kubeba mizigo.’”+
6 Kwa hiyo wale wanafunzi wakaenda na kufanya kama Yesu alivyowaagiza.+ 7 Wakamleta huyo punda na mwanapunda wake, kisha wakatandika juu yao mavazi yao ya nje, naye akayakalia.+ 8 Wengi katika umati wakatandaza mavazi yao ya nje barabarani,+ na wengine wakakata matawi ya miti na kuyatandaza barabarani. 9 Isitoshe umati uliomtangulia na wale waliomfuata waliendelea kupaza sauti: “Tunaomba umwokoe, Mwana wa Daudi!+ Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!*+ Tunaomba umwokoe, katika vilele vilivyo juu!”+
10 Alipoingia Yerusalemu, jiji lote likawa na msukosuko, na kuulizana: “Ni nani huyu?” 11 Umati ukaendelea kusema: “Huyu ndiye nabii Yesu,+ kutoka Nazareti ya Galilaya!”
12 Yesu akaingia hekaluni na kuwafukuza wote waliokuwa wakiuza na kununua hekaluni, akazipindua meza za wale waliokuwa wakibadili pesa na viti vya wale waliokuwa wakiuza njiwa.+ 13 Akawaambia: “Imeandikwa, ‘Nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala,’+ lakini ninyi mnaifanya kuwa pango la wanyang’anyi.”+ 14 Pia, vipofu na vilema wakamwendea hekaluni, naye akawaponya.
15 Wakuu wa makuhani na waandishi walipoona mambo ya kustaajabisha aliyofanya na pia wavulana waliokuwa wakipaza sauti hekaluni wakisema: “Tunaomba umwokoe, Mwana wa Daudi!”+ wakakasirika+ 16 na kumwambia: “Je, unasikia wanachosema?” Yesu akajibu: “Ndiyo. Je, hamkusoma jambo hili, ‘Kutoka katika vinywa vya watoto wadogo na wanaonyonya, umetoa sifa’?”+ 17 Kisha akawaacha, akatoka nje ya jiji na kwenda Bethania, akalala huko.+
18 Alipokuwa akirudi jijini asubuhi na mapema, akahisi njaa.+ 19 Akaona mtini kando ya barabara, akaukaribia lakini hakupata chochote ila majani tu,+ akauambia: “Usizae matunda tena kamwe.”+ Mara moja ule mtini ukanyauka. 20 Wanafunzi walipoona hilo, wakashangaa na kusema: “Kwa nini mtini huu umenyauka mara moja?”+ 21 Yesu akawajibu: “Kwa kweli ninawaambia, mkiwa na imani nanyi msiwe na shaka, hamtafanya tu nilichoufanyia mtini huo, bali hata mkiuambia mlima huu, ‘Ng’oka, ukatupwe baharini,’ jambo hilo litatendeka.+ 22 Na mambo yote mnayoomba katika sala, mkiwa na imani, mtapokea.”+
23 Baada ya kuingia hekaluni, wakuu wa makuhani na wazee wa watu wakaja alipokuwa akifundisha, wakamuuliza: “Unafanya mambo haya kwa mamlaka gani? Na ni nani aliyekupa mamlaka hayo?”+ 24 Yesu akawajibu: “Nami nitawauliza swali. Mkinijibu basi nitawaambia ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani: 25 Ubatizo wa Yohana, ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni au kwa wanadamu?”* Lakini wakaanza kujadiliana kati yao wakisema: “Tukisema, ‘Ulitoka mbinguni,’ atatuuliza, ‘Kwa nini hamkumwamini?’+ 26 Lakini tukisema, ‘Ulitoka kwa wanadamu,’ tunaogopa umati, kwa maana wote wanamwona Yohana kuwa nabii.” 27 Basi wakamjibu: “Hatujui.” Naye Yesu akawaambia: “Nami siwaambii ninafanya mambo haya kwa mamlaka gani.
28 “Mnaonaje? Mtu fulani alikuwa na watoto wawili. Akamwendea wa kwanza, akamwambia, ‘Mwanangu, leo nenda ukafanye kazi katika shamba la mizabibu.’ 29 Akamjibu, ‘Sitaenda,’ lakini baadaye akajuta na akaenda. 30 Akamwendea wa pili na kumwambia jambo hilohilo. Naye akamjibu, ‘Nitaenda Baba,’ lakini hakwenda. 31 Kati ya hao wawili ni yupi aliyefanya mapenzi ya baba yake?” Wakasema: “Yule wa kwanza.” Yesu akasema: “Kwa kweli ninawaambia wakusanya kodi na makahaba wanawatangulia ninyi kuingia katika Ufalme wa Mungu. 32 Kwa maana Yohana alikuja kwenu katika njia ya uadilifu, lakini hamkumwamini. Hata hivyo, wakusanya kodi na makahaba walimwamini,+ nanyi, ijapokuwa mliona hilo, hamkujuta na kumwamini.
33 “Sikilizeni mfano mwingine: Kulikuwa na mtu aliyemiliki shamba, akapanda shamba la mizabibu+ na kulizungushia ua, akachimba shinikizo la divai* ndani yake, akajenga mnara;+ kisha akalikodisha kwa wakulima, naye akasafiri kwenda ng’ambo.+ 34 Majira ya matunda yalipofika, akawatuma watumwa wake kwa wakulima ili wakachukue matunda yake. 35 Hata hivyo, wakulima hao wakawakamata wale watumwa, mmoja wakampiga, mwingine wakamuua, na mwingine wakampiga mawe.+ 36 Akawatuma tena watumwa wengine, wengi zaidi ya wale wa kwanza, lakini wakawatendea vivyo hivyo.+ 37 Mwishowe akamtuma mwana wake kwao, akisema, ‘Watamheshimu mwanangu.’ 38 Wakulima walipomwona yule mwana wakaambiana, ‘Huyu ndiye mrithi.+ Njooni tumuue ili tuuchukue urithi wake!’ 39 Kwa hiyo wakamkamata, wakamtupa nje ya shamba la mizabibu na kumuua.+ 40 Basi, mwenye shamba la mizabibu atakapokuja, atawatendea nini wakulima hao?” 41 Wakamwambia: “Kwa sababu ni waovu, atawaangamiza kabisa na kulikodisha shamba la mizabibu kwa wakulima wengine, ambao watampa matunda yatakapoiva.”
42 Yesu akawaambia: “Je, hamkusoma kamwe katika Maandiko kwamba ‘Jiwe ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni.*+ Hili limetoka kwa Yehova,* na ni lenye kustaajabisha machoni petu’?+ 43 Ndiyo sababu ninawaambia, Ufalme wa Mungu utaondolewa kwenu na kupewa taifa linalozaa matunda yake. 44 Pia, mtu atakayeanguka kwenye jiwe hilo atavunjika vipandevipande.+ Na litamponda yeyote litakayemwangukia.”+
45 Wakuu wa makuhani na Mafarisayo waliposikia mifano ya Yesu, wakajua kwamba alikuwa akizungumza kuwahusu.+ 46 Ingawa walitaka kumkamata, waliogopa umati, kwa sababu walimwona kuwa nabii.+
22 Yesu akasema tena nao akitumia mifano, akawaambia: 2 “Ufalme wa mbinguni ni kama mfalme aliyemwandalia mwanawe karamu ya ndoa.+ 3 Akawatuma watumwa wake wawaite wale walioalikwa kwenye karamu ya ndoa, lakini hawakutaka kuja.+ 4 Tena akawatuma watumwa wengine, akasema, ‘Waambieni wale walioalikwa: “Tazameni! Nimetayarisha chakula changu cha mchana, ng’ombe dume wangu na wanyama waliononeshwa wamechinjwa, na vitu vyote viko tayari. Njooni kwenye karamu ya ndoa.”’ 5 Lakini wakapuuza na kwenda zao, wengine kwenye mashamba yao, na wengine kwenye biashara zao;+ 6 lakini wengine wakawakamata wale watumwa wakawatendea kwa dharau na kuwaua.
7 “Mfalme akakasirika sana, akatuma majeshi yake yakawaue wauaji hao na kulichoma jiji lao.+ 8 Kisha akawaambia watumwa wake, ‘Karamu ya ndoa iko tayari, lakini walioalikwa hawakustahili.+ 9 Kwa hiyo, nendeni kwenye barabara zinazotoka jijini, na kumwalika kwenye karamu ya ndoa mtu yeyote mtakayemwona.’+ 10 Basi watumwa wakaenda barabarani na kuwaalika wote waliowaona, waovu na wema; na chumba cha sherehe za harusi kikajaa wageni.*
11 “Mfalme alipoingia kuwakagua wageni, akamwona mtu ambaye hakuwa amevaa vazi la ndoa. 12 Basi akamuuliza, ‘Mwenzangu, umeingiaje humu bila vazi la ndoa?’ Akakosa la kusema. 13 Ndipo mfalme akawaambia watumishi wake, ‘Mfungeni mikono na miguu, kisha mmtupe nje gizani. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’
14 “Kwa maana kuna wengi walioalikwa, lakini waliochaguliwa ni wachache.”
15 Ndipo Mafarisayo wakaenda kupanga njama pamoja ili wamtege Yesu kwa maneno yake.+ 16 Basi wakawatuma wanafunzi wao kwake, pamoja na wafuasi wa chama cha Herode.+ Wakamwambia: “Mwalimu, tunajua wewe husema ukweli nawe hufundisha njia ya Mungu katika kweli, na hutafuti kibali cha yeyote, kwa maana huangalii sura ya nje ya mtu. 17 Basi tuambie, unaonaje? Je, ni halali* au si halali kumlipa Kaisari kodi?”* 18 Lakini Yesu akijua uovu wao, akasema: “Kwa nini mnanijaribu, ninyi wanafiki? 19 Nionyesheni sarafu ya kodi.” Wakamletea dinari.* 20 Akawauliza: “Sura hii na maandishi haya ni ya nani?” 21 Wakajibu: “Ni ya Kaisari.” Ndipo akawaambia: “Basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, na Mungu vitu vya Mungu.”+ 22 Waliposikia hilo, wakashangaa, wakamwacha na kwenda zao.
23 Siku hiyo, Masadukayo ambao husema hakuna ufufuo,+ wakaja na kumuuliza:+ 24 “Mwalimu, Musa alisema: ‘Mtu yeyote akifa bila kupata watoto, ndugu yake anapaswa kumwoa mke wake ili kumwinulia ndugu yake uzao.’+ 25 Basi kulikuwa na ndugu saba kati yetu. Wa kwanza akaoa kisha akafa, na kwa sababu hakuwa na watoto, akamwachia ndugu yake mke wake. 26 Ikawa vivyo hivyo kwa yule wa pili na wa tatu, na kwa wote saba. 27 Mwishowe, yule mwanamke akafa. 28 Basi, katika ufufuo, atakuwa mke wa nani kati ya wale saba? Kwa maana aliolewa na wote.”
29 Yesu akawajibu: “Ninyi mmekosea, kwa sababu hamjui Maandiko wala nguvu za Mungu;+ 30 kwa maana katika ufufuo, wanaume hawaoi, wala wanawake hawaolewi, bali wao ni kama malaika mbinguni.+ 31 Kuhusu ufufuo wa wafu, je, hamkusoma mliloambiwa na Mungu, aliposema: 32 ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu na Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo’?+ Yeye si Mungu wa wafu, bali wa walio hai.”+ 33 Umati uliposikia hilo, ukashangazwa na mafundisho yake.+
34 Mafarisayo waliposikia kwamba Yesu amewanyamazisha Masadukayo, wakaja wakiwa kikundi kimoja. 35 Na mmoja wao aliyekuwa na ujuzi wa Sheria, akamuuliza swali ili kumjaribu: 36 “Mwalimu, ni amri gani iliyo kuu zaidi katika Sheria?”+ 37 Akamwambia: “‘Lazima umpende Yehova* Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi* yako yote na kwa akili yako yote.’+ 38 Hii ndiyo amri ya kwanza na iliyo kuu zaidi. 39 Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.’+ 40 Sheria yote na Manabii hutegemea amri hizo mbili.”+
41 Basi Mafarisayo walipokuwa wamekusanyika, Yesu akawauliza:+ 42 “Mna maoni gani kuhusu Kristo? Ni mwana wa nani?” Wakamwambia: “Wa Daudi.”+ 43 Akawauliza: “Basi, kwa nini Daudi akiongozwa na roho+ anamwita Bwana, akisema, 44 ‘Yehova* alimwambia Bwana wangu: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke maadui wako chini ya miguu yako”’?+ 45 Basi ikiwa Daudi anamwita Bwana, anawezaje kuwa mwanawe?”+ 46 Na hakuna mtu aliyeweza kumjibu neno, na tangu siku hiyo hakuna mtu aliyethubutu tena kumuuliza swali.
23 Ndipo Yesu akauambia umati pamoja na wanafunzi wake: 2 “Waandishi na Mafarisayo wamejiketisha kwenye kiti cha Musa. 3 Kwa hiyo, fanyeni mambo yote wanayowaambia, lakini msitende kama wao, kwa maana wao husema lakini hawatendi mambo wanayosema.+ 4 Wao hufunga mizigo mizito na kuiweka kwenye mabega ya watu,+ lakini wao wenyewe hawataki kuisogeza hata kwa kidole chao.+ 5 Kazi zote wanazofanya, wanazifanya ili waonwe na watu,+ kwa maana wanapanua visanduku vyenye maandiko wanavyovaa kama ulinzi,*+ na kurefusha pindo zenye nyuzi za mavazi yao.+ 6 Wao hupenda mahali penye heshima zaidi kwenye milo ya jioni na viti vya mbele* katika masinagogi+ 7 na kusalimiwa sokoni na kuitwa Rabi* na watu. 8 Lakini ninyi, msiitwe Rabi, kwa maana Mwalimu+ wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. 9 Zaidi ya hayo, msimwite mtu yeyote baba yenu duniani, kwa maana Baba yenu+ ni mmoja, Yule aliye mbinguni. 10 Wala msiitwe viongozi, kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo. 11 Lakini aliye mkuu zaidi kati yenu lazima awe mhudumu wenu.+ 12 Yeyote anayejiinua atanyenyekezwa,+ na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.+
13 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa sababu mnawafungia watu Ufalme wa mbinguni; kwa maana ninyi wenyewe hamwingii, na mnawazuia wale wanaotaka kuingia.+ 14* ——
15 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki!+ kwa sababu mnasafiri baharini na kwenye nchi kavu ili kumgeuza imani mtu mmoja, na anapogeuka, mnamfanya astahili Gehena* mara mbili zaidi yenu.
16 “Ole wenu, viongozi vipofu+ mnaosema, ‘Yeyote akiapa kwa hekalu, si kitu; lakini yeyote akiapa kwa dhahabu ya hekalu, yuko chini ya wajibu.’+ 17 Wapumbavu na vipofu! Kwa kweli, ni kipi kilicho kikubwa zaidi, dhahabu au hekalu linaloitakasa dhahabu hiyo? 18 Isitoshe, ‘Yeyote akiapa kwa madhabahu, si kitu; lakini yeyote akiapa kwa zawadi iliyo kwenye madhabahu, yuko chini ya wajibu.’ 19 Ninyi vipofu! Kwa kweli, ni kipi kilicho kikubwa zaidi, zawadi au madhabahu ambayo huitakasa zawadi hiyo? 20 Kwa hiyo yeyote anayeapa kwa madhabahu anaapa kwa madhabahu na kwa kila kitu kilicho juu yake; 21 na yeyote anayeapa kwa hekalu anaapa kwa hekalu na kwa Yule anayekaa ndani yake;+ 22 na yeyote anayeapa kwa mbingu anaapa kwa kiti cha ufalme cha Mungu na kwa Yule anayeketi juu yake.
23 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki! kwa sababu mnatoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na bizari,+ lakini mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki,+ rehema,+ na uaminifu. Mlipaswa kufanya mambo hayo, bila kupuuza yale mengine.+ 24 Viongozi vipofu,+ ambao huchuja mbu+ lakini hummeza ngamia!+
25 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki! kwa sababu mnasafisha upande wa nje wa kikombe na wa sahani,+ lakini ndani vimejaa pupa*+ na kutojizuia.+ 26 Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe na sahani ili upande wa nje uwe safi pia.
27 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki!+ kwa sababu mnafanana na makaburi yaliyopakwa chokaa,+ ambayo kwa nje yanapendeza lakini ndani yamejaa mifupa ya wafu na kila namna ya uchafu. 28 Vivyo hivyo, kwa nje mnaonekana waadilifu kwa watu, lakini ndani mmejaa unafiki na uasi sheria.+
29 “Ole wenu, waandishi na Mafarisayo wanafiki!+ kwa sababu mnajenga makaburi ya manabii na kuyarembesha makaburi* ya waadilifu,+ 30 nanyi mnasema, ‘Kama tungeishi katika siku za mababu zetu, hatungeshirikiana nao kumwaga damu ya manabii.’ 31 Kwa hiyo, mnashuhudia dhidi yenu wenyewe kwamba ninyi ni wana wa wale waliowaua manabii.+ 32 Basi, kijazeni kipimo cha mababu zenu.
33 “Ninyi nyoka, wana wa nyoka,*+ mtaikimbiaje hukumu ya Gehena?*+ 34 Kwa sababu hiyo, ninawatuma kwenu manabii+ na watu wenye hekima na walimu wa watu wote.+ Baadhi yao mtawaua+ na kuwatundika kwenye miti, na baadhi yao mtawapiga mijeledi+ katika masinagogi yenu na kuwatesa+ katika jiji baada ya jiji, 35 ili damu yote ya waadilifu iliyomwagwa duniani ije juu yenu, kuanzia damu ya Abeli+ mwadilifu mpaka damu ya Zekaria mwana wa Barakia, ambaye mlimuua kati ya patakatifu na madhabahu.+ 36 Kwa kweli ninawaambia, mambo yote haya yatakipata kizazi hiki.
37 “Yerusalemu, Yerusalemu, muuaji wa manabii na aliyewapiga mawe wale waliotumwa kwake+—nilijaribu mara ngapi kuwakusanya watoto wako, kama vile kuku anavyokusanya vifaranga wake chini ya mabawa yake! Lakini hamkutaka.+ 38 Tazama! Mmeachiwa nyumba yenu.*+ 39 Kwa maana ninawaambia, tangu sasa hamtaniona tena mpaka mtakaposema, ‘Amebarikiwa yule anayekuja katika jina la Yehova!’”*+
24 Yesu alipokuwa akitoka hekaluni, wanafunzi wake wakamkaribia na kumwonyesha majengo ya hekalu. 2 Akawaambia: “Je, mnaona vitu hivi vyote? Kwa kweli ninawaambia, hakuna jiwe litakaloachwa hapa juu ya jiwe lingine bila kuangushwa chini.”+
3 Alipokuwa ameketi kwenye Mlima wa Mizeituni, wanafunzi wakamkaribia faraghani, wakamuuliza: “Tuambie, mambo haya yatatukia lini, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo*+ kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”*+
4 Yesu akawajibu: “Jihadharini ili mtu yeyote asiwapotoshe,+ 5 kwa maana wengi watakuja kwa msingi wa jina langu, wakisema, ‘Mimi ndiye Kristo,’ nao watawapotosha wengi.+ 6 Mtasikia kuhusu vita na habari za vita. Msishtuke kwa maana lazima mambo hayo yatukie, lakini ule mwisho bado.+
7 “Kwa maana taifa litapigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme,+ kutakuwa na upungufu wa chakula+ na matetemeko ya ardhi sehemu mbalimbali.+ 8 Mambo hayo yote ni mwanzo wa maumivu ya taabu.
9 “Kisha watu watawakabidhi kwenye dhiki+ na kuwaua ninyi,+ nanyi mtachukiwa na mataifa yote kwa sababu ya jina langu.+ 10 Pia, wengi watakwazika, nao watasalitiana na kuchukiana. 11 Manabii wengi wa uwongo watatokea na kuwapotosha wengi;+ 12 na kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi sheria, upendo wa wengi utapoa. 13 Lakini yule atakayevumilia* mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.+ 14 Na hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote,+ na ndipo ule mwisho utakapokuja.
15 “Kwa hiyo, mtakapoona kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa, kama alivyosema nabii Danieli, kikiwa kimesimama mahali patakatifu+ (msomaji na atumie utambuzi), 16 ndipo wale walio Yudea waanze kukimbilia milimani.+ 17 Mtu aliye juu ya paa la nyumba asishuke kuchukua mali ndani ya nyumba yake; 18 na mtu aliye shambani asirudi kuchukua vazi lake la nje. 19 Ole wao wanawake wenye mimba na wale wanaonyonyesha mtoto katika siku hizo! 20 Endeleeni kusali ili mtakapokimbia isiwe wakati wa majira ya baridi kali wala siku ya Sabato; 21 kwa maana wakati huo kutakuwa na dhiki kuu+ ambayo haijawahi kutokea tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, hapana, wala haitatokea tena.+ 22 Kwa kweli, kama siku hizo hazingefupishwa, hakuna mwili wowote ambao ungeokolewa; lakini kwa sababu ya wale waliochaguliwa, siku hizo zitafupishwa.+
23 “Na ikiwa mtu yeyote atawaambia, ‘Tazama! Kristo yuko hapa,’+ au, ‘Yuko pale!’ msiamini.+ 24 Kwa maana Kristo wengi wa uwongo na manabii wa uwongo+ watatokea na kufanya ishara kubwa na maajabu ili kuwapotosha,+ ikiwezekana, hata wale waliochaguliwa. 25 Tazama! Nimewaonya mapema. 26 Basi, watu wakiwaambia, ‘Tazama! Yuko nyikani,’ msiende; ‘Tazama! Yumo katika vyumba vya ndani,’ msiamini.+ 27 Kwa maana kama radi inavyotokea mashariki na kuangaza mpaka magharibi, ndivyo kuwapo* kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.+ 28 Popote palipo na mzoga, hapo ndipo tai watakapokusanyika.+
29 “Mara tu baada ya dhiki ya siku hizo jua litatiwa giza,+ mwezi hautatoa nuru yake, nyota zitaanguka kutoka mbinguni, na nguvu za mbingu zitatikiswa.+ 30 Ndipo ishara ya Mwana wa binadamu itakapoonekana mbinguni, na makabila yote ya dunia yatajipigapiga kwa huzuni,+ nayo yatamwona Mwana wa binadamu+ akija juu ya mawingu ya mbinguni akiwa na nguvu na utukufu mwingi.+ 31 Kisha atawatuma malaika zake pamoja na sauti kubwa ya tarumbeta, nao watawakusanya watu wake waliochaguliwa kutoka kwenye zile pepo nne za dunia, kuanzia mwisho mmoja wa mbingu mpaka mwisho mwingine.+
32 “Basi jifunzeni mfano huu kutokana na mtini: Mara tu matawi yake machanga yanapokuwa laini na kuchipua majani, mnajua kwamba kiangazi kinakaribia.+ 33 Vivyo hivyo, ninyi pia mtakapoona mambo yote hayo, jueni kwamba yuko karibu milangoni.+ 34 Kwa kweli ninawaambia kizazi hiki hakitapitilia mbali kamwe mpaka mambo haya yote yatukie. 35 Mbingu na dunia zitapitilia mbali, lakini maneno yangu hayatapitilia mbali kamwe.+
36 “Kuhusu siku hiyo na saa hiyo, hakuna mtu anayejua,+ hata malaika wa mbinguni wala Mwana, ila Baba tu.+ 37 Kwa maana kama siku za Noa zilivyokuwa,+ ndivyo kuwapo* kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.+ 38 Kwa maana kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya Gharika, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiolewa, mpaka siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina,+ 39 nao hawakujali mpaka Gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote,+ ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa. 40 Kisha wanaume wawili watakuwa shambani; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa. 41 Wanawake wawili watakuwa wakisaga kwenye jiwe la kusagia; mmoja atachukuliwa na mwingine ataachwa.+ 42 Kwa hiyo, endeleeni kukesha kwa sababu hamjui Bwana wenu atakuja siku gani.+
43 “Lakini jueni jambo hili: Ikiwa mwenye nyumba angejua mwizi atakuja katika kesha gani,*+ angekaa macho na hangeruhusu nyumba yake ivunjwe.+ 44 Kwa hiyo ninyi pia iweni tayari,+ kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja saa msiyotazamia.
45 “Kwa kweli ni nani mtumwa mwaminifu na mwenye busara* ambaye bwana wake alimweka rasmi asimamie watumishi wake wa nyumbani na kuwapa chakula chao kwa wakati unaofaa?+ 46 Mwenye furaha ni mtumwa huyo ikiwa bwana wake atakapokuja atamkuta akifanya hivyo!+ 47 Kwa kweli ninawaambia, atamweka rasmi asimamie mali zake zote.
48 “Lakini ikiwa mtumwa huyo mwovu atasema moyoni mwake, ‘Bwana wangu anakawia,’+ 49 naye aanze kuwapiga watumwa wenzake na kula na kunywa pamoja na walevi wa kupindukia, 50 bwana wa mtumwa huyo atakuja siku asiyotazamia na katika saa asiyoijua,+ 51 naye atamwadhibu kwa ukali sana na kumweka pamoja na wanafiki. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.+
25 “Basi Ufalme wa mbinguni ni kama mabikira kumi waliochukua taa zao+ na kwenda kumpokea bwana harusi.+ 2 Watano kati yao walikuwa wapumbavu, na watano walikuwa wenye busara.*+ 3 Wale wapumbavu walibeba taa zao lakini hawakubeba mafuta, 4 lakini wale wenye busara walibeba mafuta kwenye chupa zao pamoja na taa zao. 5 Bwana harusi alipokawia kuja, wote walisinzia na kulala. 6 Katikati ya usiku kukatokea mwito, ‘Huyu hapa Bwana harusi! Nendeni mkamlaki.’ 7 Ndipo mabikira wote wakasimama na kuzitayarisha taa zao.+ 8 Wale wapumbavu wakawaambia wenye busara, ‘Tugawieni mafuta yenu, kwa sababu taa zetu zinakaribia kuzimika.’ 9 Wale wenye busara wakawajibu: ‘Labda hayatatutosha sisi sote. Nendeni kwa wauzaji mkajinunulie.’ 10 Walipokuwa wakienda kununua mafuta, bwana harusi akaja. Mabikira waliokuwa tayari wakaingia pamoja naye kwenye karamu ya ndoa,+ na mlango ukafungwa. 11 Baadaye wale mabikira wengine pia wakaja, wakisema, ‘Bwana, Bwana, tufungulie!’+ 12 Akawajibu, ‘Kwa kweli ninawaambia, siwajui ninyi.’
13 “Kwa hiyo, endeleeni kukesha+ kwa sababu hamjui ile siku wala saa.+
14 “Kwa maana ni kama mtu aliye karibu kusafiri ng’ambo, aliyewaita watumwa wake na kuwakabidhi mali zake.+ 15 Akampa mmoja talanta* tano, mwingine mbili, na mwingine moja, kila mtumwa kulingana na uwezo wake, kisha akaenda ng’ambo. 16 Mara moja yule aliyepokea talanta tano akaenda kufanya biashara nazo, akapata talanta tano zaidi. 17 Vivyo hivyo, yule aliyepokea mbili akapata talanta mbili zaidi. 18 Lakini mtumwa aliyepokea moja tu akaenda akachimba shimo ardhini na kuficha zile pesa* za bwana wake.
19 “Baada ya muda mrefu, bwana wa watumwa hao akarudi na kufanya hesabu nao.+ 20 Basi, yule aliyepokea talanta tano akaja na kuleta talanta tano zaidi, akisema, ‘Bwana, ulinikabidhi talanta tano, ona, nimepata talanta tano zaidi.’+ 21 Bwana wake akamwambia: ‘Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Umekuwa mwaminifu katika mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi.+ Ingia katika shangwe ya bwana wako.’+ 22 Kisha yule aliyepokea talanta mbili akaja na kusema, ‘Bwana, ulinikabidhi talanta mbili, ona, nimepata talanta mbili zaidi.’+ 23 Bwana wake akamwambia: ‘Vema, mtumwa mwema na mwaminifu! Umekuwa mwaminifu katika mambo machache. Nitakuweka juu ya mambo mengi. Ingia katika shangwe ya bwana wako.’
24 “Mwishowe mtumwa aliyepokea talanta moja akaja na kusema: ‘Bwana nilijua wewe ni mtu mgumu, ambaye huvuna mahali ambapo hukupanda na kukusanya mahali ambapo hukupepeta.+ 25 Kwa hiyo, niliogopa nikaenda na kuficha talanta yako ardhini. Chukua mali yako.’ 26 Bwana wake akamjibu: ‘Mtumwa mwovu na mvivu, ulijua kwamba nilivuna mahali ambapo sikupanda na kukusanya mahali ambapo sikupepeta, sivyo? 27 Basi, ungeweka pesa* zangu benki, ili nitakaporudi nizichukue pamoja na faida.
28 “‘Kwa hiyo, ichukueni talanta hiyo kutoka kwake mkampe yule mwenye talanta kumi.+ 29 Kwa maana kila mtu aliye na kitu ataongezewa, naye atakuwa na vitu vingi. Lakini mtu asiye na kitu, hata kile alicho nacho kitachukuliwa.+ 30 Basi mtupeni nje gizani mtumwa huyo asiyefaa kitu. Huko ndiko atalia na kusaga meno yake.’
31 “Mwana wa binadamu+ atakapokuja katika utukufu wake, pamoja na malaika wote,+ ataketi kwenye kiti chake cha ufalme chenye utukufu. 32 Mataifa yote yatakusanyika mbele yake, naye atawatenganisha watu mmoja kutoka kwa mwenzake, kama vile mchungaji anavyotenganisha kondoo na mbuzi. 33 Naye atawaweka kondoo+ kwenye mkono wake wa kuume, lakini mbuzi kwenye mkono wake wa kushoto.+
34 “Ndipo Mfalme atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume: ‘Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini Ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu. 35 Kwa maana nilikuwa na njaa mkanipa chakula; nilikuwa na kiu mkanipa kinywaji. Nilikuwa mgeni mkanikaribisha vizuri;+ 36 nilikuwa uchi,* mkanivika nguo.+ Nilikuwa mgonjwa mkanitunza. Nilikuwa gerezani mkanitembelea.’+ 37 Ndipo waadilifu watamuuliza: ‘Bwana, ni lini tulipokuona ukiwa na njaa tukakulisha, au ukiwa na kiu tukakupa kinywaji?+ 38 Ni lini tulipokuona ukiwa mgeni tukakukaribisha, au ukiwa uchi tukakuvika? 39 Ni lini tulipokuona ukiwa mgonjwa au ukiwa gerezani tukakutembelea?’ 40 Mfalme atawajibu, ‘Kwa kweli ninawaambia, kwa kadiri ambavyo mlimtendea aliye mdogo zaidi kati ya hawa ndugu zangu, mlinitendea mimi.’+
41 “Kisha atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kushoto: ‘Ondokeni kwangu+ ninyi mliolaaniwa, nendeni katika moto wa milele+ aliotayarishiwa Ibilisi na malaika zake.+ 42 Kwa maana nilikuwa na njaa, lakini hamkunipa chakula, nilikuwa na kiu, lakini hamkunipa kinywaji. 43 Nilikuwa mgeni, lakini hamkunikaribisha; nilikuwa uchi, lakini hamkunivika nguo; nilikuwa mgonjwa na nilikuwa gerezani lakini hamkunitunza.’ 44 Nao pia watamuuliza: ‘Bwana, ni lini tulipokuona ukiwa na njaa au ukiwa na kiu au ukiwa mgeni au ukiwa uchi au ukiwa mgonjwa au ukiwa gerezani tukakosa kukuhudumia?’ 45 Ndipo atawajibu: ‘Kwa kweli ninawaambia, kwa kadiri ambavyo hamkumtendea mmoja wa hawa wadogo zaidi, hamkunitendea mimi.’+ 46 Hao watakatiliwa mbali milele,*+ lakini waadilifu watapata uzima wa milele.”+
26 Basi Yesu alipomaliza kusema hayo yote, akawaambia wanafunzi wake: 2 “Mnajua kwamba baada ya siku mbili kutakuwa na Pasaka,+ naye Mwana wa binadamu atatolewa ili auawe kwenye mti.”+
3 Ndipo wakuu wa makuhani na wazee wa watu wakakusanyika katika ua wa kuhani mkuu aliyeitwa Kayafa,+ 4 nao wakapanga njama pamoja+ ili kumkamata Yesu kwa hila* na kumuua. 5 Hata hivyo, walikuwa wakisema: “Si kwenye sherehe, ili watu wasifanye ghasia.”
6 Yesu alipokuwa Bethania katika nyumba ya Simoni mwenye ukoma,+ 7 mwanamke fulani aliyekuwa na chupa ya alabasta yenye mafuta ghali yenye marashi akamkaribia, akaanza kuyamimina juu ya kichwa cha Yesu alipokuwa akila.* 8 Walipoona hilo wanafunzi wakakasirika na kusema: “Hasara hii ni ya nini? 9 Kwa maana mafuta haya yangeuzwa kwa kiasi kikubwa cha pesa na kupewa maskini.” 10 Akijua jambo hilo, Yesu akawaambia: “Kwa nini mnataka kumsumbua mwanamke huyu? Amenitendea jambo jema. 11 Kwa maana maskini mnao sikuzote,+ lakini mimi hamtakuwa nami sikuzote.+ 12 Alipomimina mafuta haya yenye marashi kwenye mwili wangu, alifanya hivyo ili kunitayarisha kwa ajili ya mazishi.+ 13 Kwa kweli ninawaambia, popote ambapo hii habari njema itahubiriwa ulimwenguni, jambo alilofanya mwanamke huyu litatajwa pia ili kumkumbuka.”+
14 Ndipo mmoja wa wale 12, aliyeitwa Yuda Iskariote,+ akaenda kwa wakuu wa makuhani+ 15 na kuwauliza: “Mtanipa nini ili nimsaliti kwenu?”+ Wakakubaliana naye vipande 30 vya fedha.+ 16 Basi tangu wakati huo akaanza kutafuta nafasi nzuri ya kumsaliti.
17 Siku ya kwanza ya Sherehe ya Mikate Isiyo na Chachu+ wanafunzi wakaja kumuuliza Yesu: “Unataka tukutayarishie wapi mlo wa Pasaka?”+ 18 Akawaambia: “Nendeni jijini kwa mwanamume fulani mkamwambie, ‘Mwalimu anasema: “Wakati wangu uliowekwa umekaribia; nitasherehekea Pasaka pamoja na wanafunzi wangu nyumbani kwako.”’” 19 Basi, wanafunzi wakafanya kama Yesu alivyowaagiza, wakaandaa Pasaka.
20 Ilipofika jioni,+ Yesu alikuwa ameketi mezani pamoja na wale wanafunzi 12.+ 21 Walipokuwa wakila, akasema: “Kwa kweli ninawaambia, mmoja wenu atanisaliti.”+ 22 Wakiwa wamehuzunishwa sana na jambo hilo, kila mmoja wao akaanza kumuuliza: “Bwana, je, ni mimi?” 23 Akawajibu: “Anayechovya mkono wake pamoja nami katika bakuli ndiye atakayenisaliti.+ 24 Kwa kweli, Mwana wa binadamu anaenda zake, kama ilivyoandikwa kumhusu, lakini ole+ wake mtu atakayemsaliti Mwana wa binadamu!+ Ingekuwa afadhali kama mtu huyo hangezaliwa.”+ 25 Yuda, aliyekuwa karibu kumsaliti akauliza: “Je, ni mimi, Rabi?” Yesu akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema.”
26 Walipokuwa wakiendelea kula, Yesu akachukua mkate, na baada ya kutoa baraka, akaumega,+ akawapa wanafunzi wake, akasema: “Chukueni mle. Huu unamaanisha mwili wangu.”+ 27 Kisha akachukua kikombe, akashukuru na kuwapa akisema: “Kunyweni ninyi nyote,+ 28 kwa maana hii inamaanisha ‘damu yangu+ ya agano,’+ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi+ ili wasamehewe dhambi.+ 29 Lakini ninawaambia: sitakunywa tena kamwe divai yoyote ya mzabibu mpaka siku nitakapoinywa ikiwa mpya pamoja nanyi katika Ufalme wa Baba yangu.”+ 30 Mwishowe, baada ya kuimba sifa,* wakaenda kwenye Mlima wa Mizeituni.+
31 Ndipo Yesu akawaambia: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku wa leo, kwa maana imeandikwa: ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika.’+ 32 Lakini baada ya kufufuliwa nitawatangulia kuingia Galilaya.”+ 33 Lakini Petro akajibu: “Hata wengine wote wakikwazika kuhusiana nawe, mimi sitakwazika kamwe!”+ 34 Yesu akamwambia: “Kwa kweli ninakuambia, usiku huu, kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”+ 35 Petro akamwambia: “Hata nikilazimika kufa pamoja nawe, sitakukana kamwe.”+ Wale wanafunzi wengine wote wakasema vivyo hivyo.
36 Ndipo Yesu akaja pamoja nao mpaka mahali panapoitwa Gethsemane,+ akawaambia wanafunzi: “Ketini hapa, mimi naenda pale kusali.”+ 37 Akamchukua Petro na wale wana wawili wa Zebedayo, naye akaanza kuhuzunika na kutaabika sana.+ 38 Ndipo akawaambia: “Nimehuzunika* sana, kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.”+ 39 Akasonga mbele kidogo, akaanguka kifudifudi, akasali:+ “Baba yangu, ikiwa inawezekana, niondolee kikombe hiki.+ Lakini, si kama ninavyopenda, bali kama unavyopenda.”+
40 Akarudi na kuwakuta wanafunzi wakiwa wamelala usingizi, akamuuliza Petro: “Je, hamngeweza kukesha pamoja nami hata kwa saa moja?+ 41 Endeleeni kukesha+ na kusali bila kuacha,+ ili msiingie katika majaribu.+ Bila shaka, roho inataka* lakini mwili ni dhaifu.”+ 42 Akaenda tena mara ya pili na kusali: “Baba yangu, ikiwa siwezi kuepuka kunywa kikombe hiki, acha mapenzi yako yatendeke.”+ 43 Akaja tena na kuwakuta wakiwa wamelala usingizi, kwa maana macho yao yalikuwa mazito. 44 Basi akawaacha, akaenda tena kusali mara ya tatu, akisema tena jambo lilelile. 45 Kisha akarudi na kuwaambia wanafunzi: “Mnalala na kupumzika wakati kama huu! Tazama! Saa imekaribia ya Mwana wa binadamu kusalitiwa mikononi mwa watenda dhambi. 46 Simameni twende. Tazama! Msaliti wangu amekaribia.” 47 Alipokuwa bado akizungumza, tazama! Yuda, mmoja wa wale 12, akaja pamoja na umati mkubwa wakiwa na mapanga na marungu, walikuwa wametumwa na wakuu wa makuhani na wazee wa watu.+
48 Basi msaliti wake alikuwa amewapa ishara, akisema: “Yule nitakayembusu, huyo ndiye; mkamateni.” 49 Akaenda moja kwa moja kwa Yesu akasema: “Salamu, Rabi!” kisha akambusu kwa wororo. 50 Lakini Yesu akamuuliza: “Mwenzangu, umekuja kufanya nini?”+ Ndipo wakaja na kumkamata Yesu na kumtia nguvuni. 51 Lakini tazama! mmoja wa wale waliokuwa pamoja na Yesu akanyoosha mkono wake, akauchomoa upanga wake, akampiga mtumwa wa kuhani mkuu na kumkata sikio.+ 52 Ndipo Yesu akamwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake,+ kwa maana wote wanaochukua upanga wataangamia kwa upanga.+ 53 Au unafikiri siwezi kumwomba Baba yangu anipe sasa hivi vikosi zaidi ya 12 vya malaika?+ 54 Hata hivyo, Maandiko yanayosema lazima itendeke hivi yatatimizwaje?” 55 Saa hiyo, Yesu akauambia umati: “Je, mmekuja kunikamata mkiwa na mapanga na marungu kana kwamba mimi ni mwizi? Siku baada ya siku nilikuwa nikiketi hekaluni nikifundisha+ lakini hamkunikamata.+ 56 Lakini yote haya yametokea ili kutimiza mambo yaliyoandikwa* na manabii.”+ Ndipo wanafunzi wote wakamwacha na kukimbia.+
57 Wale waliomkamata Yesu wakampeleka kwa Kayafa+ kuhani mkuu, ambako waandishi na wazee walikuwa wamekusanyika.+ 58 Lakini Petro akaendelea kumfuata kwa mbali, mpaka katika ua wa kuhani mkuu, na baada ya kuingia ndani, akaketi pamoja na watumishi wa nyumbani ili aone itakavyokuwa.+
59 Sasa wakuu wa makuhani na Sanhedrini yote walikuwa wakitafuta ushahidi wa uwongo dhidi ya Yesu ili wamuue.+ 60 Lakini hawakupata, ingawa mashahidi wengi wa uwongo walijitokeza.+ Baadaye, mashahidi wawili wakajitokeza 61 na kusema: “Mtu huyu alisema, ‘Ninaweza kuliangusha chini hekalu la Mungu na kulijenga kwa siku tatu.’”+ 62 Ndipo kuhani mkuu akasimama na kumuuliza: “Kwa nini hujibu? Watu hawa wanashuhudia nini kukuhusu?”+ 63 Lakini Yesu akakaa kimya.+ Basi kuhani mkuu akamwambia: “Ninakuapisha mbele za Mungu aliye hai utuambie kama wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu!”+ 64 Yesu akamjibu: “Wewe mwenyewe umesema. Lakini ninawaambia: Tangu sasa mtamwona Mwana wa binadamu+ akiwa ameketi kwenye mkono wa kuume wa nguvu,+ akija juu ya mawingu ya mbinguni.”+ 65 Ndipo kuhani mkuu akayararua mavazi yake ya nje, akisema: “Amekufuru! Tunahitaji mashahidi wengine wa nini? Tazama! Sasa mmemsikia akikufuru. 66 Mnaonaje?” Wakamjibu: “Anastahili kufa.”+ 67 Kisha wakamtemea mate usoni+ na kumpiga ngumi.+ Wengine wakampiga makofi usoni,+ 68 wakisema: “Tutolee unabii, wewe Kristo. Ni nani aliyekupiga?”
69 Basi Petro alikuwa ameketi nje katika ua, kijakazi akamjia na kumwambia: “Hata wewe ulikuwa pamoja na Yesu Mgalilaya!”+ 70 Lakini akakana mbele yao wote, akisema: “Sijui unachosema.” 71 Alipoenda kwenye chumba kilicho langoni, msichana mwingine akamwona na kuwaambia wale waliokuwa hapo: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu Mnazareti.”+ 72 Akakana tena akiapa: “Simjui mtu huyo!” 73 Baada ya muda mfupi wale waliokuwa wamesimama hapo wakaja na kumwambia Petro: “Hakika wewe pia ni mmoja wao, kwa maana matamshi* yako yanakutambulisha.” 74 Ndipo akaanza kulaani na kuapa: “Simjui mtu huyo!” Na mara moja jogoo akawika. 75 Naye Petro akakumbuka maneno aliyosema Yesu, yaani: “Kabla jogoo hajawika, utanikana mara tatu.”+ Naye akaenda nje akalia kwa uchungu.
27 Ilipofika asubuhi, wakuu wote wa makuhani na wazee wa watu wakashauriana pamoja kumhusu Yesu ili auawe.+ 2 Baada ya kumfunga, wakampeleka na kumkabidhi kwa Pilato, gavana.+
3 Ndipo Yuda, ambaye alimsaliti, alipoona Yesu amehukumiwa, akajuta na kuwarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande 30 vya fedha,+ 4 akisema: “Nilitenda dhambi niliposaliti damu isiyo na hatia.” Wakamwambia: “Hilo linatuhusuje? Shauri yako!”* 5 Basi akavitupa vile vipande vya fedha hekaluni. Kisha akaenda zake akajinyonga.+ 6 Lakini wakuu wa makuhani wakachukua pesa hizo wakasema: “Si halali kuziweka katika hazina takatifu, kwa sababu ni bei ya damu.” 7 Baada ya kushauriana, wakatumia pesa hizo kununua shamba la mfinyanzi liwe mahali pa kuzika wageni. 8 Kwa hiyo, shamba hilo limeitwa Shamba la Damu+ hadi leo hii. 9 Ndipo yakatimia maneno haya yaliyosemwa kupitia nabii Yeremia: “Nao wakavichukua vile vipande 30 vya fedha, bei iliyoamuliwa juu ya mtu huyo, ambaye bei yake iliamuliwa na baadhi ya wana wa Israeli, 10 nao wakavitoa ili kununua shamba la mfinyanzi, kama Yehova* alivyoniamuru.”+
11 Sasa Yesu akasimama mbele ya gavana, naye gavana akamuuliza: “Je, wewe ndiye Mfalme wa Wayahudi?” Yesu akajibu: “Wewe mwenyewe umesema.”+ 12 Lakini alipokuwa akishtakiwa na wakuu wa makuhani na wazee, hakujibu.+ 13 Ndipo Pilato akamwambia: “Je, husikii ni mambo mangapi wanayoshuhudia dhidi yako?” 14 Lakini hakumjibu hata neno moja, hivi kwamba gavana akashangaa sana.
15 Sasa kila sherehe ya pasaka, gavana alikuwa na desturi ya kumfungua mfungwa yeyote ambaye umati ulimtaka.+ 16 Wakati huo walikuwa wamemkamata mhalifu sugu aitwaye Baraba. 17 Basi walipokuwa wamekusanyika, Pilato akawauliza: “Mnataka niwafungulie nani, Baraba au Yesu anayeitwa Kristo?” 18 Kwa maana Pilato alijua kwamba walikuwa wamemkabidhi Yesu kwake kwa sababu ya wivu. 19 Zaidi ya hayo, alipokuwa ameketi kwenye kiti cha hukumu, mke wake akampelekea ujumbe huu: “Mwache mtu huyo mwadilifu, kwa maana niliteseka sana leo katika ndoto kwa sababu yake.” 20 Lakini wakuu wa makuhani na wazee wakaushawishi umati uombe Baraba afunguliwe,+ lakini Yesu auawe.+ 21 Gavana akawauliza: “Mnataka niwafungulie nani kati ya hawa wawili?” Wakasema: “Baraba.” 22 Pilato akawaambia: “Basi, nifanye nini na Yesu anayeitwa Kristo?” Wote wakasema: “Atundikwe mtini!”*+ 23 Akawauliza: “Kwa nini? Amefanya kosa gani?” Wakaendelea kusema kwa sauti kubwa hata zaidi: “Atundikwe mtini!”+
24 Pilato alipoona jitihada zake hazifaulu, na badala yake ghasia zilikuwa zikitokea, akachukua maji akanawa mikono mbele ya umati, akisema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu huyu. Shauri yenu.” 25 Ndipo watu wote wakajibu: “Damu yake na iwe juu yetu na juu ya watoto wetu.”+ 26 Ndipo akawafungulia Baraba, lakini akaagiza Yesu apigwe mijeledi+ na kumtoa ili auawe kwenye mti.+
27 Ndipo wanajeshi wa gavana wakampeleka Yesu katika makao ya gavana, wakakusanya kikosi chote cha wanajeshi kumzunguka.+ 28 Wakamvua kanzu yake na kumvisha joho jekundu,+ 29 kisha wakasokota taji la miiba na kumvisha kichwani na kutia utete kwenye mkono wake wa kuume. Wakampigia magoti, wakamdhihaki wakisema: “Salamu,* ewe Mfalme wa Wayahudi!” 30 Wakamtemea mate+ na kuuchukua ule utete, wakaanza kumpiga kichwani. 31 Mwishowe, baada ya kumdhihaki, wakamvua lile joho wakamvisha mavazi yake ya nje, wakampeleka akatundikwe mtini.+
32 Walipokuwa wakitoka wakakutana na mwanamume kutoka Kirene aitwaye Simoni. Wakamlazimisha aubebe mti wa mateso*+ wa Yesu. 33 Na walipofika mahali panapoitwa Golgotha, yaani, Mahali pa Fuvu la Kichwa,+ 34 wakampa divai iliyochanganywa na nyongo* anywe;+ lakini alipoionja, akakataa kuinywa. 35 Baada ya kumtundika kwenye mti, wakagawana mavazi yake ya nje kwa kupiga kura,+ 36 kisha wakaketi hapo wakimlinda. 37 Pia, wakabandika juu ya kichwa chake mashtaka dhidi yake, yalikuwa yameandikwa: “Huyu ni Yesu Mfalme wa Wayahudi.”+
38 Ndipo wezi wawili wakatundikwa kwenye mti kando yake, mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.+ 39 Na wale waliokuwa wakipita hapo wakamtukana,+ huku wakitikisa vichwa vyao+ 40 wakisema: “Wewe uliyetaka kuliangusha chini hekalu na kulijenga kwa siku tatu,+ jiokoe mwenyewe! Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti wa mateso!”*+ 41 Vivyo hivyo, wakuu wa makuhani, waandishi, na wazee wakaanza kumdhihaki wakisema:+ 42 “Aliwaokoa wengine lakini hawezi kujiokoa mwenyewe! Yeye ni Mfalme wa Israeli;+ acheni sasa ashuke kutoka kwenye mti wa mateso* nasi tutamwamini. 43 Amemtegemea Mungu; acheni Mungu amwokoe ikiwa anamtaka,+ kwa maana alisema, ‘Mimi ni Mwana wa Mungu.’”+ 44 Vivyo hivyo, hata wezi waliotundikwa mtini kando yake walikuwa wakimshutumu.+
45 Kukawa na giza katika nchi yote kuanzia saa sita* mpaka saa tisa.*+ 46 Karibu saa tisa, Yesu akapaza sauti, akisema: “Eli, Eli, lama sabakthani?” yaani, “Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?”+ 47 Waliposikia hilo, baadhi ya wale waliokuwa wamesimama hapo wakaanza kusema: “Mtu huyu anamwita Eliya.”+ 48 Mara moja, mmoja wao akakimbia, akachukua sifongo akailowesha katika divai kali akaiweka kwenye utete akampa anywe.+ 49 Lakini wengine wakasema: “Mwacheni! Acheni tuone kama Eliya atakuja kumwokoa.” 50 Yesu akapaza tena sauti kisha akafa.*+
51 Na tazama! pazia la patakatifu+ likapasuka vipande viwili,+ kuanzia juu mpaka chini,+ dunia ikatetemeka, na miamba ikapasuka. 52 Makaburi* yakafunguka na miili mingi ya watakatifu waliokuwa wamelala usingizi ikainuliwa 53 (na watu waliokuwa wakitoka makaburini baada ya kufufuliwa kwake wakaingia katika jiji takatifu), nayo ikaonwa na watu wengi. 54 Lakini yule ofisa wa jeshi na wale waliokuwa pamoja naye wakimlinda Yesu walipoona tetemeko la ardhi na mambo yaliyokuwa yakitokea, wakaogopa sana na kusema: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”+
55 Na wanawake wengi ambao walikuwa wamemfuata Yesu kutoka Galilaya ili kumhudumia walikuwa wakitazama kwa mbali;+ 56 miongoni mwao kulikuwa na Maria Magdalene, Maria mama ya Yakobo na Yose, na pia mama ya wana wa Zebedayo.+
57 Sasa kwa kuwa ilikuwa jioni, akaja tajiri mmoja wa Arimathea, aitwaye Yosefu, ambaye pia alikuwa mwanafunzi wa Yesu.+ 58 Mtu huyu alienda kwa Pilato akaomba apewe mwili wa Yesu.+ Naye Pilato akaamuru apewe.+ 59 Yosefu akauchukua mwili huo, akaufunga kwa kitani bora kilicho safi,+ 60 akaulaza katika kaburi lake jipya,*+ alilokuwa amechimba katika mwamba. Kisha akaviringisha jiwe kubwa kwenye mwingilio wa lile kaburi,* akaondoka. 61 Lakini Maria Magdalene na yule Maria mwingine wakabaki hapo, wakiwa wameketi mbele ya kaburi.+
62 Siku iliyofuata, baada ya Matayarisho,+ wakuu wa makuhani na Mafarisayo wakakusanyika mbele ya Pilato, 63 wakisema: “Bwana, tumekumbuka mjanja huyo alipokuwa hai alisema, ‘Nitafufuliwa baada ya siku tatu.’+ 64 Kwa hiyo, amuru kaburi lilindwe mpaka siku ya tatu, ili wanafunzi wake wasije wakamwiba+ na kuwaambia watu, ‘Alifufuliwa kutoka kwa wafu!’ Kisha udanganyifu huu wa mwisho utakuwa mbaya zaidi kuliko ule wa kwanza.” 65 Pilato akawaambia: “Mnaweza kuweka walinzi. Nendeni mkalilinde jinsi mnavyotaka.” 66 Basi wakaenda na kulilinda kaburi kwa kulitia jiwe muhuri na kuweka walinzi.
28 Baada ya Sabato, kulipokuwa kukipambazuka siku ya kwanza ya juma, Maria Magdalene na yule Maria mwingine wakaenda kulitazama kaburi.+
2 Na tazama! tetemeko kubwa la ardhi lilikuwa limetokea, kwa maana malaika wa Yehova* alikuwa ameshuka kutoka mbinguni akaja na kuliviringisha lile jiwe, naye alikuwa amelikalia.+ 3 Alikuwa aking’aa kama radi, na mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji.+ 4 Ndiyo, wale walinzi wakatetemeka, wakawa kama wafu kwa sababu ya kumwogopa.
5 Lakini malaika akawaambia wale wanawake: “Msiogope, kwa maana ninajua mnamtafuta Yesu aliyeuawa kwenye mti.+ 6 Hayupo hapa, kwa maana amefufuliwa kama alivyosema.+ Njooni, tazameni mahali alipokuwa amelala. 7 Basi nendeni upesi mkawaambie wanafunzi wake kwamba alifufuliwa kutoka kwa wafu, na tazama! anawatangulia kwenda Galilaya.+ Mtamwona huko. Tazama! Nimewaambia ninyi.”+
8 Basi, wakaondoka upesi kwenye kaburi la ukumbusho wakiwa na hofu na shangwe kubwa. Wakakimbia kwenda kuwajulisha wanafunzi wake.+ 9 Na tazama! Yesu akakutana nao na kuwaambia: “Siku njema!” Wakamkaribia, wakamshika miguu na kumsujudia.* 10 Ndipo Yesu akawaambia: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu ili waende Galilaya, na huko wataniona.”
11 Walipoondoka na kwenda, baadhi ya walinzi+ wakaenda jijini na kuwajulisha wakuu wa makuhani mambo yote yaliyotokea. 12 Baada ya wakuu wa makuhani na wazee kukutana na kushauriana, wakawapa wale wanajeshi kiasi kikubwa cha fedha 13 wakawaambia: “Semeni, ‘Wanafunzi wake walikuja usiku wakamwiba tulipokuwa tumelala usingizi.’+ 14 Na gavana akisikia, sisi tutamwelezea jambo hilo,* nanyi hamtahitaji kuwa na wasiwasi.” 15 Basi wakachukua zile fedha na kufanya kama walivyoagizwa, na hadithi hiyo imeenea miongoni mwa Wayahudi mpaka leo hii.
16 Hata hivyo, wale wanafunzi 11 wakaenda Galilaya+ kwenye mlima ambao Yesu alikuwa amepanga kukutana nao.+ 17 Walipomwona wakasujudu,* lakini baadhi yao walikuwa na shaka. 18 Yesu akakaribia na kuwaambia: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.+ 19 Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,+ mkiwabatiza+ katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, 20 na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.+ Na tazama! mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”*+
Au “ukoo wa.”
Au “Masihi; Mtiwa-mafuta.”
Au “nguvu ya utendaji.”
Hii ndiyo mara ya kwanza, kati ya mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambapo jina la Mungu, Yehova, linapatikana katika toleo hili. Angalia Nyongeza A5.
Linafanana na jina la Kiebrania Yeshua, au Yoshua, linalomaanisha “Yehova Ni Wokovu.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Au “wataalamu wa nyota.”
Au “kumwinamia.”
Au “Masihi; Mtiwa-mafuta.”
Au “kumwinamia.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “wakiitafuta nafsi ya.”
Inaelekea ni kutokana na neno la Kiebrania “chipukizi.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “akawatumbukiza; akawazamisha.”
Au “nyoka-vipiri.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “ukuta wa ukingoni; sehemu ya juu zaidi.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Nyongeza A5.
Au “Eneo lenye Majiji Kumi.”
Au “walio na kiu au njaa ya kiroho; ombaomba wa kiroho.”
Au “watatoshelezwa.”
Au “kikapu cha kupimia.”
Mahali pa kuteketezea takataka nje ya Yerusalemu. Angalia Kamusi.
Tnn., “kwadrani ya mwisho.” Angalia Nyongeza B14.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Tnn., “maili moja.” Angalia Nyongeza B14.
Yaani, umkopeshe bila faida au riba.
Au “kamili.”
Au “unapowapa maskini zawadi.” Angalia Kamusi.
Au “litukuzwe; lionwe kuwa takatifu.”
Au “utuokoe.”
Au “hawatunzi sura au mwonekano wao.”
Aina ya wadudu.
Aina ya wadudu.
Au “linaona vizuri.” Tnn., “ni rahisi.”
Au “utajawa na nuru.”
Tnn., “ni bovu; lina uovu.”
Au “nafsi zenu.”
Au “nafsi.”
Angalia Nyongeza B14.
Aina ya maua.
Yaani, uadilifu wa Mungu.
Au “kumwinamia.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “ukingo wenye mteremko mkali.”
Au “machela.”
Au “akiwa ameketi mezani.”
Au “kuketi mezani.”
Au “kumwinamia.”
Au “Tuonyeshe rehema.”
Au “mwenye bidii.”
Au “vazi la ziada.”
Au “iweni wenye kujihadhari.”
Au “anayevumilia.”
Jina lingine la Shetani, mkuu, au mtawala, wa roho waovu.
Au “uhai,” yaani, tumaini la kuishi.
Angalia Kamusi.
Tnn., “kwa sarafu moja ya asarioni. ” Angalia Nyongeza B14.
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “uhai wake.”
Au “uhai wake.”
Au “mavazi bora.”
Tnn., “mbele ya uso wako.”
Au “hutetewa.”
Au “kwa matokeo yake.”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Au “kwa ajili ya nafsi zenu.”
Au “rahisi.”
Au “mikate iliyowekwa mbele za Mungu.”
Au “nafsi yangu imemkubali.”
Jina lingine la Shetani.
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “nyoka-vipiri.”
Au “kisicho na uaminifu.”
Angalia Kamusi, “Mfumo wa mambo.”
Au “hamira.”
Au “ukaumuka.”
Au labda, “kuumbwa kwa ulimwengu.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Tnn., “tetraki.”
Yaani, Herode Antipa. Angalia Kamusi.
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Tnn., “stadia nyingi.” Stadiamu moja ilikuwa sawa na mita 185 (futi 606.95).
Yaani, karibu saa 9 usiku hadi saa 12 asubuhi.
Au “wakamwinamia.”
Yaani, hawajisafishi kisherehe.
Au “anayesema mambo mabaya kumhusu.”
Wingi wa neno la Kigiriki porneiʹa. Angalia Kamusi.
Yaani, bila kujisafisha kisherehe.
Au “Nionyeshe rehema.”
Au “kumwinamia.”
Au “wamefunga.”
Au “kisicho na uaminifu.”
Au “hamira.”
Au “kwa sababu mwanadamu hakukufunulia.”
Au “Hadesi.” Angalia Kamusi.
Au “jitendee kwa fadhili.”
Angalia Kamusi, “Mti wa mateso.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “nafsi yake.”
Au “yakawa meupe.”
Au “mwonyeshe rehema.”
Angalia Nyongeza A3.
Angalia Nyongeza B14.
Au “kodi ya kichwa.”
Tnn., “sarafu ya stateri,” inadhaniwa kuwa ndiyo tetradrakma. Angalia Nyongeza B14.
Au “msipobadilika.”
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A3.
Au labda, “yenu.”
Tnn., “na umkaripie.”
Tnn., “kinywa cha.”
Talanta 10,000 za fedha zilikuwa sawa na dinari 60,000,000. Angalia Nyongeza B14.
Au “kumwinamia.”
Angalia Nyongeza B14.
Au “karibu na mipaka ya.”
Neno la Kigiriki, por·neiʹa. Angalia Kamusi.
Au “kamili.”
Angalia Nyongeza B14.
Yaani, karibu saa 3 asubuhi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Yaani, karibu saa 11 jioni.
Angalia Nyongeza B14.
Angalia Nyongeza B14.
Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “ni baya; lina uovu.”
Au “mkarimu.”
Au, “akamwinamia.”
Au “nafsi yake.”
Au “tuonyeshe rehema!”
Au “tuonyeshe rehema!”
Angalia Nyongeza A5.
Au “chanzo chake ni wanadamu?”
Au “mahali pa kukamulia zabibu.”
Tnn., “kichwa cha pembeni.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “wale waliokuwa wameketi mezani.”
Au “sawa.”
Au “kodi ya kichwa.”
Angalia Nyongeza B14.
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Angalia Nyongeza A5.
Au “wanapanua vibweta vyao.”
Au “bora.”
Au “Mwalimu.”
Angalia Nyongeza A3.
Angalia Kamusi.
Au “vitu vilivyoporwa.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “nyoka-vipiri.”
Angalia Kamusi.
Au labda, “Mmeachiwa nyumba yenu ukiwa.”
Angalia Nyongeza A5.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “anayevumilia.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “wakati gani wa usiku.”
Au “hekima.”
Au “hekima.”
Talanta ya Wagiriki ilikuwa sawa na kilogramu 20.4. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “fedha.”
Tnn., “fedha.”
Au “sikuwa na mavazi ya kutosha.”
Yaani, kutoka kwa uhai. Tnn., “kukata matawi; kupogolewa.”
Au “kwa ujanja.”
Au “alipokuwa ameketi mezani.”
Au “zaburi.”
Au “nafsi yangu inahuzunika.”
Au “inapenda.”
Au “maandiko.”
Au “lafudhi.”
Au “Utajua utakachofanya.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “Auawe kwenye mti!”
Au “Usifiwe.”
Angalia Kamusi.
Kinywaji kichungu.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Yaani, karibu saa 6 mchana.
Yaani, karibu saa 9 alasiri.
Tnn., “akaitoa roho yake.” Au “akakata pumzi.”
Au “makaburi ya ukumbusho.”
Au “kaburi lake jipya la ukumbusho.”
Au “kaburi la ukumbusho.”
Angalia Nyongeza A5.
Au “kumwinamia.”
Tnn., “tutamshawishi.”
Au “wakamwinamia.”
Angalia Kamusi.